15 Jun 2007

Asalam aleykum,

Enzi za Ujamaa na Kujitegemea tulikuwa tukiambiwa kuwa ubepari ni unyama.Bado naamini kuwa kauli hiyo ni sahihi hadi kesho.Nimeikumbuka kauli hiyo baada ya kuona kipindi cha “Witness” kwenye kituo cha runinga cha Aljazeera English ambapo mada ilikuwa maendeleo ya sekta binafsi ya afya nchini India.Nchi hiyo inasifika hivi sasa kwa kutoa huduma bora za afya hasa kwa wageni ambao wanakimbia gharama za afya kwenye nchi zao ili kupata unafuu huko India.Lakini wakati “watalii” hao wa afya wananufaika na unafuu huo,maelfu kwa maelfu ya Wahindi wasio na uwezo wanaishia kukodolea tu majengo ya hospitali hizo kwa vile hawana uwezo wa kumudu gharama za tiba.Kibaya zaidi,jitihada za hospitali hizo za kisasa kutoa “msaada wa kibinadamu” kwa wagonjwa wasio na uwezo wa kumudu gharama zinaishia mikononi mwa wajanja wachache ambao badala ya msaada huo kuwafikia walengwa,wengi wa wanaonufaika ni wale wenye mahusiano na watawala ambao ndio wanaopendekeza nani apatiwe msaada wa tiba ya bure.Wamiliki wa hospitali hizo wanatetea uamuzi wao wa kutoza gharama za juu kwenye tiba wanazotoa kwa kigezo kwamba gharama za uendeshaji ni za juu sana na wanategemea zaidi teknolojia kutoka nje ya nchi hiyo ambayo pia ni ghali.

Niliona taarifa nyingine Skynews kuhusu kushamiri kwa biashara ya mafigo ya binadamu huko Pakistani. “Watalii” wa afya (watu wanaosafiri kutoka nchi moja kwenda nyingine kutafuta huduma nafuu za afya) wamekuwa wakimiminika katika hopsitali moja nchi humo kwenda kununua mafigo ya bei rahisi.Gharama ya matibabu ni pauni za Kiingereza 3,500 lakini wanaouza mafigo hayo huambulia pauni 800 tu.Hicho ni kiwango kikubwa sana kwa watu hao kwani inakadiriwa kuwa kwa baadhi yao itawachukua zaidi ya miaka kumi kufikisha kiwango hicho cha fedha iwapo watategemea vipato vyao kiduchu katika kazi zao za kila siku,nyingi zao zikiwa ni mithili ya utumwa.Lakini fedha hizo wanazolipwa ambazo kwa wengi ni kama kushinda bingo flani huishia kwenye matibabu zaidi kwani sote tunafahamu kuwa mwili ni kama gari,ukishakongoroa kifaa kimoja basi unakuwa ushaharibu “balansi” ya mwili mzima.Matokeo yake ni mzunguko usioisha.Baba anauza mafigo yake,anapata fedha ambazo mwanzoni zinaonekana kama ukombozi kwa familia,lakini muda si mrefu afya inaanza kudhoofika,fedha iliyopatikana kwenye kuuza mafigo inaanza kurejea hospitali alikouza mafigo,hatimaye inalazimu mama au mtoto naye auze mafigo ili kumuda gharama za matibabu ya baba,na hadithi hiyo inaendelea mithili ya Isidingo (hivi imeshafikia mwisho?).Mmiliki wa hospitali hiyo ya kipekee nchini Pakistan anatetea uamuzi wake wa kununua mafigo akidai kuwa anatoa huduma kwa jamii mara mbili:kuokoa maisha ya watalii wa afya ambao wanahitaji mafigo kwa udi na uvumba,na kuwakwamua watu walio hohehahe ambao mtaji wao ni mafigo yao.Alipoulizwa kuwa anachofanya sio sawa na “kumwibia Pita ili kumlipa Paulo” mmiliki huyo alidai kuwa yeye anajiona ni mkombozi kwa makundi yote mawili:wanaohitaji mafigo na wanaohitaji hela.

Napopata mapumziko baada ya “kubukua” kwa nguvu huwa napendelea kuiangalia dunia kupitia macho ya runinga.Na “hobi” yangu hiyo inanikutanisha na habari za aina mbalimbali,za kuchekesha na za kuhudhunisha,za kufundisha na za kutia ghadhabu.Iliyonipa ghadhabu hivi karibuni ni taarifa ya kiuchunguzi ya BBC kuhusu makampuni yajulikanayo kama “vulture fund companies” (makampuni yanayozengea mizoga).Haya ni makampuni yaliyoshamiri sana kwenye nchi za magaharibi na walengwa wake wakuu ni nchi masikini za dunia ya tatu.Makampuni haya yanaishi kwa kununua madeni ya nchi masikini kwa bei nafuu halafu katika yanaishia kutengeneza mamilioni ya dola.Yule “mtu mfupi” wa Zambia,Frederick Chiluba, ambaye tulikuwa tukiambiwa kuwa ni mlokole, amejikuta akiumbuka baada ya kubainika kuwa alikula dili na “vulture fund company” flani ya Marekani ambapo kampuni hiyo ilinunua madeni ya nchi hiyo na kisha kutoa teni pasenti ya nguvu kwa Chiluba.Yaani wanachofanya wenye kampuni hizo ni hivi:wewe una deni la shilingi laki moja lakini huna uwezo wa kulilipa au unasuasua kulilipa.Mie nalinunua deni hilo kwa anayekudai,bei ya kulinunua deni hilo ikiwa ni poa.Kwa hiyo mie nageuka kuwa ndie naekudai.Hadi hapo hakuna tatizo,lakini ujanja uko kwenye ukweli kwamba mengi ya makampuni hayo yanafanya biashara zake kwa siri na shughuli zake haziko wazi sana kisheria.Na hapo ndipo “dili za kuuza nchi” zinapojitokeza.Unajua kuna tofauti kati ya kudaiwa na taasisi “ya kueleweka” kama benki na kudaiwa na “mjanja” flani wa mtaani.Kibaya zaidi ni kwamba hao wadaiwa hawatoi fedha zao mfukoni,bali ni fedha za walipa kodi (wananchi).Kwahiyo,kwa upande mmoja kuna kampuni ya kiujanjaujanja ambayo haijali taratibu za kisheria za madeni na ulipwaji wake na kwa upande mwingine ni mdaiwa ambaye anatumia nafasi kudili na “mdai poa” kujitengenezea fedha kadhaa,ambapo mwisho wa dili pande zote mbili zinanufaika,huku walipa kodi wakizidi kuumia.

Unaweza kujiuliza kwanini makampuni haya hayadhibitiwi ilhali yanaendesha shughuli zao katika nchi tunazoamini kuwa zinafuata utawala wa sheria.Jibu ni jepesi:sheria za kuyabana makampuni hayo ziko “luzi” sana kiasi kwamba ni sawa na hakuna sheria kabisa.Pia kuwepo kwa makampuni hayo kunayanufaisha sana mashirika ya kimataifa katika kupata fedha zao walizokopesha kwa nchi masikini.Kadhalika,mengi ya makampuni hayo yana mahusiano ya karibu na mashirika ya kimataifa yanayotoa mikopo kwa nchi masikini.Kadhalika,baadhi ya viongozi wa nchi masikini wamekuwa wakihusishwa na umiliki wa makampuni haya.Hiyo ndio dunia tunayoishi ambayo mwenye nacho anataka zaidi ya alichonacho na asiyenacho ananyang’anywa hata kile kidogo kabisa alichonacho.

Huko nyumbani nako kuna mambo.Nilisoma sehemu flani kwamba Wizara ya Miundombinu inaanda utaratibu wa kuwa na teknolojia ya kufuatilia matumizi ya magari ya serikali.Wazo zuri kama lingekuwa halihusishi fedha,tena mamilioni ya fedha.Hivi jamani namna bora ya kufuatilia matumizi ya mali yako si kuhakikisha sheria zilizopo zinafuatwa?Unadhani kuna dereva ambaye akielezwa bayana kwamba atatimuliwa kazi pindi gari la umma analoendesha likionekana mtaani saa 2 usiku atathubutu kukiuka amri hiyo?Unadhani jeuri ya madereva hao inatoka wapi?Mjuzi mmoja wa udereva wa magari ya umma aliwahi kuninong’oneza kuwa madereva na masekretari ni “wasiri” muhimu sana kwa mabosi.Hao ndio wanaojua nyumba ndogo za mabosi wao,ndio wanapokea meseji na kupeleka mizigo na hata kwenye madili ya mabosi wao huwa wanahusika kwa namna moja au nyingine.Leo utabuniwa mradi wa kudhibiti magari ya umma kesho utabuniwa mradi wa kuhakikisha wafanyakazi wanaripoti ofisini muda stahili.Yote ni mawazo mazuri kama malengo ni kuongeza tija na sio kuongeza matumizi yasiyo ya lazima.Jamani,tuionee huruma nchi yetu!

Mwisho,ni bajeti ya mwaka ujao wa fedha.Kwa kuongeza kodi kwenye mafuta inamaanisha kuwa bei za bidhaa na huduma kadhaa zitapanda,kuanzia nyanya magengeni hadi usafiri wa daladala na mikoani.Mikakati ya kupambana na umasikini inaweza kuwa na wakati mgumu kufanikiwa pale gharama za maisha zinazidi kupaa.Cha muhimu hapa sio kulaumiana bali kuangalia nini cha kufanya.Bajeti imeshasomwa na matokeo yake yanafahamika (mfano,uwezekano wa kupanda kwa bei ya bidhaa na huduma).Cha kufanya ni kuhakikisha kuwa walafi wa faida hawatumii mwanya huo kuwaminya walalahoi.Wananchi wataumia vya kutosha tukiwaachia wafanyabiashara wajipangie bei za bidhaa na huduma au tukitegemea nguvu ya soko katika kudhibiti bei. “To hell with” (ifie mbali) hekaya za soko huria.Iwe hivi,mamlaka husika zitamke bayana kuwa bei ya kitu flani isidhidi kiasi flani,kama hutaki tunafunga biashara yako.Sema huo ni udikteta,lakini kuna dhambi gani ya kuwa dikteta kwa maslahi ya wengi wasiojiweza?Udikteta usiokubalika ni ule wa dhidi ya watu wengi na sio huo naoshauri ambao ni kwa manufaa ya watu wengi.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.