20 Jun 2007

Asalam aleykum,

Kwanza napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa wote wanaotembelea blogu yangu.Nina furaha kusema kuwa wakati naandaa makala hii blogu hiyo ilikuwa imeshatembelewa na watu 1015 kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni.Inanipa moyo sana kupata idadi hiyo ya wageni na napenda kuwakaribisha wale wote ambao hawajawahi kuitembelea blogu hiyo.Pamoja na hayo,nakaribisha maoni,mijadala na hata kunikosoa pale ambapo msomaji anadhani haafikiani nami.Pamoja na kupata nafasi ya kusoma makala mpya na za nyuma,blogu hiyo ina viunganishi (links) kadhaa vya tovuti mbalimbali za Kitanzania kuhusu habari na burudani.Karibuni sana.

Hivi karibuni serikali ya Uingereza imetangaza nia yake ya kuwaadhibu ipasavyo wale wote wanaopatikana na hatia ya kuwadhalilisha watoto kijinsia (paedophiles).Ni kwamba mtu atakaekutwa na hatia hiyo atadungwa kemikali flani ambayo itampunguzia tamaa ya kuwamendea watoto wadogo.Kwa “kizungu” wanaita “castration” ila tafsiri ya Kiswahili nayoifahamu sio mwafaka kuiandika hapa,ila nachoweza kusema ni kuwa kemikali hiyo inatarajiwa kuwafanya wahalifu hao kuwa kama wanaume wasio na uwezo wa kufanya tendo la ndoa.Nadhani msomaji wangu mpendwa unajua msamiati gani ni mwafaka hapo.Habari hii imenikumbusha mchapo mmoja niliopewa miaka kadhaa iliyopita kwamba katika maeneo flani ya mwambao wajuzi wa “teknolojia asili” (ndumba) wana mbinu ya kuhakikisha kuwa “vyao haviguswi na atakayethubutu kuvigusa atalijua jiji.”Ni kwamba katika kuhakikisha kuwa “mali zake” haziibiwi,mume “anamfunga” mkewe,yaani anamfanyia utaalam flani wa asili ambapo pindi mtu akitembea na mwanamke huyo anaathirika kwa namna flani (kwa mfano,sehemu zake za siri “zinaingia mitini” au mwizi huyo na mwanamke husika wanagandana kama gundi hadi wanafumaniwa).Hadi naondoka sehemu hiyo sikuweza kuthibitisha ukweli wa habari hiyo ila nachokiri ni kwamba utaalamu wa asili upo sana ila tu mara nyingi unatumika ndivyo sivyo.Pengine wakati nasi huko nyumbani tunasubiri teknolojia ya kemikali mamlaka zinazohusika na kuhakikisha kuwa watoto hawaangukii mikononi mwa “paedophiles” zinaweza kuomba msaada wa wataalamu hao wa asili ili kuwalinda watoto wetu.Hiyo ni nyepesi nyepesi,usidhani nimeishiwa na hoja za msingi.

Katika kupitapita kwenye magazeti ya hapa nilikutana na habari moja iliyonifanya niwashangae wanaopanga baadhi ya sera za nje za Marekani.Hivi msomaji mpenzi unafahamu kuwa mtu anayemnyima usingizi Joji Bushi na serikali yake,gaidi nambari wani Osama bin Laden,“alitengenezwa” na Wamarekani haohao?Ni stori ndefu ila kwa kifupi ni kwamba wakati wa “Vita Baridi” kati ya Marekani (na washirika wake) dhidhi ya wafuasi wa Ukomunisti wakiongozwa na Urusi (enzi hizo USSR),Marekani ilikuwa ikitoa sapoti kwa watu na vikundi kadhaa kwa lengo la kuzuia Ukomunisti usienee zaidi.Miongoni mwa watu hao ni Osama bin Laden ambaye pamoja na kundi la Taliban walipewa misaada ya hali na mali na Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) kwa ajili ya kufanikisha ushindi kwenye vita kati ya mujahidina wa Afghanistan na Urusi.Katika kuidhibiti Urusi,washirika wake na Ukomunisti kwa ujumla,CIA ilikuwa tayari kufanya lolote lile wakati mwingine pasipo kutafakari nini kitatokea iwapo matokeo yatakuwa tofauti na matarajio ya plani zao.Na ndivyo ilivyokuwa huko Afganistan.Baada ya majeshi ya Urusi kushindwa vita hiyo na baada ya “Vita Baridi” kumalizika,Marekani haikuwahitaji tena Osama,Taliban na vikundi vingine vya mujahidina,na kwa upande mwingine Osama na washirika wake nao walisharidhika na ushindi wao dhidi ya Urusi na walishakuwa na nyenzo za kutosha kuanzisha ngwe nyingine ya mapambano dhidi ya “wafadhili” wao Marekani na wale wote waliowaona kuwa ni maadui wa Uislam.

Ungedhani kuwa Marekani ingejifunza kutokana na maamuzi yake ya “kuangalia leo pasipo kufikiria kesho itakuwaje”.Majuzi nimesoma gazeti la Guardian la hapa Uingereza na kukuta taarifa kuwa Marekani imeandaa mpango wa kuvisaidia vikundi vya madhehebu ya Sunni nchini Iraki ili vipambane na wapiganaji wa Al-Qaeda waliojazana nchini humo.Matarajio ni kwamba vikundi hivyo vya Wa-Sunni vitaweka mbele maslahi ya taifa lao la Iraki dhidi ya wapiganaji wa Al-Qaeda ambao wengi wao wametoka nje ya nchi hiyo kuja kupambana na Wamerekani.Wasiwasi wa baadhi ya wachambuzi wa mambo ya usalama ni kwamba hata kama mpango huo utafanikiwa,hali itakuwaje iwapo misaada ya kifedha na silaha kwa vikundi hivyo itavipa jeuri vikundi hivyo kuanzisha “mtanange” mwingine dhidi ya Wa-Shia au Wa-Kurd iwapo Al-Qaeda wataondoka Iraki?Na kuna uhakika gani kuwa baada ya kupata misaada ya kutosha vikundi hivyo vya Wa-Sunni havitawageuka wafadhili wao na kuungana na makundi mengine kupambana na Wamarekani?

Kana kwamba hiyo hazitoshi,kuna taarifa kwamba CIA imekuwa inaendesha mkakati wa siri kuwarubuni baadhi ya Wasudan kuingia kwenye mpango ambao watapatiwa mafunzo ili baadaye wapenyezwe kwenye vikundi vya Kiisalam vyenye jitihada kali hususan Al-Qaeda.Dada mmoja anayefanya utafiti kuhusu hali ilivyo huko Darfur anadai kuwa Marekani inahusika kwa namna moja au nyingine katika machafuko yanayoendelea huko ambapo kwa mujibu wa utafiti wake,licha ya Marekani kuwa na uwezo wa kusaidia kudhibiti vikundi vinavyoendesha unyama katika eneo hilo imeamua kutofanya lolote kwa inavihitaji vikundi hivyo kuisaidia Marekani kudhibiti tishio la ugaidi kutoka vikundi visivyodhibitiwa katika nchi ya jirani ya Somalia.Nchi hiyo ambayo kwa miaka nenda rudi imekuwa ikiendeshwa kiholela na vikundi vya “mabwana vita” (warlords) inahesabiwa na Marekani kuwa ni tishio kubwa kwa vile ni rahisi kwa Al-Qaeda na wafuasi wake kupata hifadhi pasipo bughudha yoyote ile.

Kuhusu huko nyumbani,nimeshtushwa na mpango uliotangazwa na Waziri wa Fedha,Zakia Meghji,ambapo katika utekelezaji wake,baadhi ya waagizaji bidhaa kutoka nje wataweza kuingiza mizigo yao nchini pasipo mizigo hiyo kufanyiwa ukaguzi.Mpango huo unaweza kusababisha balaa kubwa kwa sababu zilizo wazi kabisa.Sote tunafahamu kuwa pamoja na sheria zilizopo bado kuna watumishi wasio waadilifu ambao kwa kuthamini matumbo yao wamekuwa wakizembea kukagua bidhaa zinazoingia nchini na hivyo kufanya nchi yetu kujaa bidhaa kadhaa kutoka nje ambazo hazina ubora unaostahili.Sasa kwa mpango huu wa Meghji kuna hatari kubwa zaidi ya hofu ya bidhaa zisizostahili kwani upo uwezekano wa wajanja flani kuingiza unga (sio wa ugali bali madawa ya kulevya) na hata silaha kwa kutumia mwanya huo wa kutokaguliwa bidhaa zinazoingizwa nchini.Hivi kuna uhakika gani kuwa utaratibu huo utawahusu wanaodaiwa kuwa na rekodi nzuri ya kulipa kodi au wawekezaji wa dhati?Tunafahamu kuwa baadhi ya wawekezaji wamekuwa wakichuma chapchap wakitumia msamaha wa kodi (tax holiday) halafu wanaingia mitini.Sasa wawekezaji wa namna hiyo wakipewa fursa nyingine ya kuingiza bidhaa pasipo ukaguzi hawawezi kutumia fursa hiyo kuingiza visivyofaa kuingizwa nchini?Kwa uchungu gani hasa walio nao kwa nchi yetu?Maana kama wangekuwa na uchungu basi wasingekimbia nchini au kubadili majina ya biashara zao baada ya kumalizika kwa “tax holidays” wanazopewa kwa nia nzuri tu ya kuwatengenezea mazingira mazuri ya uwekezaji.Hivi kweli kuna mfumo thabiti (fool proof) wa kuhakikisha kuwa watu wenye nia mbaya na nchi yetu hawatawatumia wafanyabishara wanaodaiwa kuwa na rekodi nzuri ya kulipa kodi kuingiza mizigo hatari kwa mfano silaha?

Mwisho,wakati naungana na Watanzania wenzangu kuipongeza Taifa Stars kwa mafanikio yake,napenda kumpongeza Mheshimiwa Anne Kilango kwa kilio chake ambacho naamini ni cha kila Mtanzania mwenye mapenzi na nchi yetu kuhusu hao wanaofanya maamuzi ambayo matokeo yake yanaiathiri nchi yetu.Maamuzi hayo ambayo unaweza kabisa kudhani kuwa yamefanyikia baa huku mtu akiwa “matingas” ni pamoja na kuingia mikataba ya ajabu kuliko ile aliyofanya Karl Marx na machifu wetu ambao hawakuwa na ujuzi wowote kuhusu suala la mikataba.Mama Kilango anawaomba viongozi wa namna hiyo wamuogope Mungu na kuionea huruma nchi yetu,mie nakwenda mbali zaidi ya hapo kwa kuwaombea mabaya wale wote ambao wanathamini sana matumbo yao na nyumba ndogo zao kuliko maisha ya Watanzania wenzao.Mungu awalaani na ikiwezekana wapate adhabu yao hapahapa duniani ili iwe funzo kwa wengine.

Alamsiki

1 comment:

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.