2 Jul 2007

Asalam aleykum,

Kifo ni kitu cha ajabu sana.Achilia mbali ukweli kwamba kifo hakitabiriki,isipokuwa kwa wale wanaojihusisha na matendo ambayo mwisho wake ni kifo (kwa mfano wanaobwia unga),kifo kina tabia ya kuelezea namna gani binadamu alikuwa muhimu kwa jamii au namna watu walivyokuwa wakimpenda wakati wa uhai wake.Mfano hai wa ninachoongelea ni kifo cha mwanasiasa aliyekuwa akija juu huko nyumbani,Marehemu Amina Chifupa.Yaani hata kuanza jina lake na neno “marehemu” inakuwa vigumu kwani najiskia kama sio kweli vile.Lakini kama baadhi ya watoa rambirambi walivyosema “wengi walimpenda Amina lakini Mungu alimpenda zaidi,na ndio maana akamwita.” Pia sie Wakristo tunaamini kuwa Bwana ndiye mtoaji na Bwana ndiye mchukuaji,sie waja wake tunapaswa kuendelea kulihimidi jina la Bwana.

Moja ya salamu za rambirambi zilizonigusa sana ni zile zilizotolewa na Mbunge mwingine kijana kutoka Chadema,Mheshimiwa Zitto Kabwe.Katika salamu zake alizozitoa katika gazeti la Tanzania Daima,Kabwe alikuwa kama anaongea na Marehemu Amina alipokuwa hai.Ni rambirambi zenye kugusa hisia sana,na kwa kiasi kikubwa zinaelezea Amina alikuwa mtu wa namna gani.Sehemu iliyonigusa zaidi ni pale Kabwe aliposema (nanukuu) “Niseme kweli, hata mimi nilikuwa najiuliza utafanya nini bungeni wewe, nikijisemea kuwa wewe ni kilaza tu.Rafiki yangu, na pia rafiki yako kipenzi, Omar…alinitahadharisha nisiwe kama watu wengine wanaokutafsiri kwa ujumla.” Nami nilijiskia dhambi ya namna flani kwani wakati Amina anaukwaa ubunge nilikuwa mingoni mwa wengi tuliokuwa tukifikiri kuwa asingeweza kufanya lolote la maana.Hata alipoanza vita yake dhidi ya biashara ya madawa ya kulevya,nilikuwa na mawazo kuwa huo ni utani tu.Kumbe nilikuwa “wrong” kwani Amina aliamua kwa dhati kupambana na biashara hiyo haramu ambayo kila kukicha inapoteza maisha ya vijana lukuki huku ikichangia sana matukio ya uhalifu.

Nikiri kwamba baadaye niliamini kuwa Amina alikuwa “serious” katika vita hiyo dhidi ya wauza unga.Na ni kutokana na “seriousness” hiyo ndio tukaanza kusikia kuwa wahusika walikuwa wakimtolea vitisho.Kwa mara nyingine tena,watu wengi walidhani vitisho hivyo ni haditihi tu lakini kadri siku zilivyozidi kwenda baadhi yetu tulianza kuhisi kuwa kuna ukweli katika madai hayo.Amina alijua bayana kuwa vita aliyokuwa anaianzisha ni ngumu na kubwa pengine zaidi ya “Vita ya Tatu ya Dunia” (kama itatokea).Binti wa watu hakujali madhara ambayo yangeweza kumkumba na akaamua kusimama kidete kutetea kile alichokuwa akikiamini.Aliitumia vyema nafasi yake kama Mbunge kijana kwani ujana unasaidia sana kufahamu nini kinatokea kwenye kona mbalimbali na vijiwe vilivyotapakaa sehemu kama Dar es Salaam..Unajua ukitaka kujua mapishi basi shurti usikae mbali na jiko,na ukitaka kuwa kinyozi mzuri basi usikose kuitembelea saluni.Na kwa kutumia “utoto wa mjini” wake na ukaribu wake na wanaolijua jiji,Amina aliweza kupata taarifa za ndani kabisa kuhusu wahusika kwenye biashara hiyo haramu.Kimsingi,mtu yeyote makini anaweza kupata taarifa za namna hiyo hasa ikizingatiwa kuwa wauza unga tunaishi nao mitaani,tunafahamu lini wanaenda “shamba” (wanakonunua dawa hizo),lini wanarudi na “mzigo” na hata mawakala wanaotumika kusambaza madawa hayo.Alichofanya Amina ni kuwa makini zaidi na kuongeza jitihada za dhati katika harakati zake za kupambana na biashara ya unga.

Wapo wanaosema kuwa Amina hakupewa msaada wa kutosha katika mapambano yake hiyo.Pengine kwa vile bado tunaomboleza,huu sio wakati mzuri wa kunyoosheana vidole.Hata hivyo,hali halisi ilikuwa ikionyesha bayana kuwa vita aloanzisha Amina ilikuwa ya “binafsi” zaidi,utadhani kwamba ilikuwa inamgusa yeye pekee.Hakuna anayefahamu kama orodha ya wauza unga aliyowasilisha kwenye mamlaka husika ilifanyiwa kazi,lakini yayumkinika kusema kuwa marehemu hakupewa sapoti ya kutosha kwenye mapambano hayo.Hata hivyo,bado mamlaka husika zinaweza kutoa “ubani” mkubwa zaidi wa kumuenzi Amina kwa kuendelea pale alipoishia.Hao waliokabidhiwa orodha ya wauza unga wamuenzi marehemu kwa kuanza kuifanyia kazi orodha hiyo haraka iwezekanavyo.Ikumbukwe kuwa marehemu alikuwa akifanya hivyo kwa ajili ya kizazi hiki kilichopo na hivyo vijavyo.Biashara ya unga ikiachwa ishamiri kana kwamba ni halali ni jambo la hatari sana.

Nirejee nilipoanzia.Kifo cha Amina kimeonyesha ni namna gani alivyokuwa akipendwa na Watanzania.Na hapo sizungumzii huko nyumbani pekee bali hata huku ughaibuni.Dakika chache baada ya habari za kifo chake kufahamika,nilipata sms zaidi ya kumi kuhusu habari hiyo,na zote zilikuwa na sura mbili: kutoamini na majonzi.Wengi bado hatuamini kuwa Amina ametutoka,hasa pengine kutokana na ukweli kuwa taarifa kuwa alikuwa akiumwa hazikuonyesha kuwa hali yake ni mahututi.Tovuti mbalimbali zinazowakutanisha Watanzania walioko huku ughaibuni na wenzao wa huko nyumbani bado zinaendelea na mjadala kuhusu kifo cha Mbunge huyo aliyekuwa kijana zaidi ya wote.Ofkozi, wapo wanaojenga “conspirancy theories” kwamba kifo hicho kina mkono wa mtu au watu,lakini wengi wamekuwa wakionyesha mshtuko wao kuhusu kifo hicho na kutoa salamu zao za rambirambi kwa famili ya marehemu badala ya kusaka mchawi.Yanasemwa na yatasemwa mengi kuhusiana na kifo hicho,lakini japo sioni ubaya wa kujibidiisha kujua “ukweli” (kama upo zaidi ya ule wa kawaida kuwa kifo ni mapenzi ya Mungu) nadhani la muhimu zaidi kwa sasa ni kuiombea roho ya marehemu ipate pumziko na raha ya milele,na kuyaendeleza yale yote mema aliyoyaanzisha ikiwa ni pamoja na mapambano yake dhidi ya biashara ya unga.

Niseme kuwa hizo “conspirancy theories” kuhusu kifo cha Amina zinaweza kuwa zinachochewa na ukweli kwamba yeye mwenyewe alitamka wakati wa uhai wake kuwa alikuwa akipewa vitisho na hao aliokuwa akiwalenga kwenye mapambano yake dhidi ya biashara ya unga.Sasa,hata mimi nikisema kuwa kuna mtu ananitishia uhai wangu halafu kwa bahati mbaya nikafa katika mazingira ya kutatanisha,ni dhahiri kuwa watu watanyoosha vidole na kusema “hapa kuna namna.” Ikumbukwe kuwa hata alipofariki mwandishi mahiri kabisa,Marehemu Stan Katabalo,watu walinyoosha vidole na kusema kuwa “kuna namna.” Kimantiki,wanaonyoosha vidole wanaweza kuwa na hoja ya msingi kwani sote tunafahamu namna majambazi wa uchumi wetu,kama walivyo wauza unga,walivyo tayari kufanya lolote kuhakikisha wanaongeza idadi ya mahekalu,mashangingi na nyumba ndogo zao.Naposema wako tayari kufanya lolote namaanisha kuwa wako tayari hata kutoa roho ya mtu pale wanapoona “vitumbua vyao vinatiwa mchanga.” Hivi unadhani mtu anayeingiza madawa ya kulevya ambayo madhara yake ni vifo vya maelfu ya vijana atashindwa kutoa uhai wa mtu mmoja?Nielewe kwa makini hapo.Sisemi kuwa wauza unga ndio waliomuua Amina bali naelezea namna gani “conspirancy theories” kuhusu kifi chake zinavyotengeneza mantiki.

Mwisho,wakati tunaendelea na maombolezo ya kifo cha Amina,napenda kuna tuhuma nzito dhidi ya gavana wa BOT,na tunaambiwa kuwa kuna tenda imetangazwa kupata kampuni ya nje kuja kuchunguza tuhuma hizo na pengine kampuni hiyo itakuwa imepatikana na kuanza kazi mwishoni mwa mwaka huu.Nisichoelewa ni kwamba je hatuna kabisa wataalamu wazalendo wa kuchunguza tuhuma hizo hadi tutangaze tenda?Lakini zaidi ya hapo,ikumbukwe kuwa pande mbili zinazohusika katika tuhuma hizo,yaani gavana na umma wa Watanzania wanataka haki itendeke mapema,kwani inavyocheleweshwa ni sawa na kuiminya justice delayed is justice denied).Lakini tukienda mbali kidogo tunaweza kuona kuwa gavana bado anaendelea na kazi zake katika kipindi hiki ambacho tunajizungusha kama shere kutafuta namna ya kujua ukweli.Kwa kuwa kwake ofisini,inawezekana kabisa kuwa hata hiyo kampuni itakapoanza uchunguzi tayari ushahidi wote utakuwa umeyeyuka.Hivi hata ungekuwa wewe,ukiwa na mke wa mtu,na unapata taarifa kuwa fumanizi litafanyika baada ya masaa manne,utaendelea kusubiri au utayeyuka?Mfano huo unaweza kuonekana wa kizinzi lakini hoja ni kwamba kwa mtuhumiwa mkuu kwenye tuhuma zinazohusu ufujaji wa mabilioni ya shilingi kuendelea kuwepo ofisini “akiwasubiri” wachunguzi waje kumtia hatiani (au kumsafisha) ni uamuzi mbovu.Kwani gavana akiambiwa apumzike hadi “asafishwe” (au kutiwa hatiani) na wachunguzi (iwe wa nje au wa ndani) itaathiri nini?Au shilingi yetu itaporomoka thamani ghafla zaidi ya inavyoporomoka kila siku?Haya,kama ni lazima kuleta wachunguzi kutoka nje,ushauri wangu wa bure ni huu:wahusika waende Ubalozi wa Uingereza kuomba msaada wa kuletewa wataalamu kutoka Scotland Yard au SFO (Serious Fraud Office) badala ya kutangaza tenda ambayo inaweza kutuletea kampuni kama Richmond.

Alamsiki


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.