22 Aug 2007

Asalam aleykum,

Nianze na habari “nyepesi nyepesi.” Kwa mujibu wa utafiti ambao matokeo yake yalinukuliwa na gazeti la Daily Mail la hapa Uingereza,kioo kinaweza kuwa na majibu kuhusu hali ya afya ya binadamu.Inaelezwa kwamba “kujishangaa” kwenye kioo kwa muda flani kunaweza kukupatia tetesi kuhusu dalili za matatizo ya kiafya katika mwili wako.Pengine hii itakuwa habari njema zaidi kwa baadhi ya akinamama ambao,kama wengi wetu tujuavyo,huweza kutumia hata nusu saa wakijiangalia kwenye vioo,hususan kabla ya kufanya “mtoko” (kwenda kwenye harusi,kitchen party,ubarikio,nk).Mie ni miongoni mwa “wazembe” ambao naweza kupitisha hata siku tatu bila kujiangalia kwenye kioo (na pengine siko peke yangu).Lakini kwa mujibu wa utafiti huo,kujiangalia kwenye kioo japo kwa muda michache kunaweza kubainisha matatizo ya kiafya kama vile maambukizo ya bacteria,kupanda kwa “cholesterol”, “anaemia”, “arthritis”,upungufu wa Magnesium mwilini,mshtuko wa moyo na hata kubaini ujauzito.Kwa mfano,ukijitazama kwenye kioo na kubaini kuwa macho yamekuwa meupe kuliko kawaida,basi hiyo inaweza kuwa dalili ya kuzidi kwa “cholesterol” mwilini;macho yakiwa yamevimba pasipo sababu inaweza kuwa dalili ya maambukizo ya bacteria au pengine “arthritis”;kope (“eyelids”) zinazoonekana kama zinataka kunyonyoka zinaweza kuashiria dalili za “anaemia”;jicho linalozunguka bila kuzungushwa (“myokymia”) linaweza kuashiria upungufu wa Magnesium;kupauka kwa rangi ya mwili kunaweza kumaanisha dalili za homa ya manjano au matatizo ya maini;fizi zinazotoka damu zinaweza kuashiria “leukaemia” au ujauzito;na mipasuko kwenye “lips” kunaweza kuashiria kisukari.Hata hivyo,kama yalivyo matokeo ya tafiti nyingi,matokeo ya utafiti huu kuhusu “faida za kioo katika kubaini hali ya mwili” hayamaanishi kuwa kila dalili utakayoiona kwenye kioo (kati ya hizo zilizotajwa) basi lazima inaashiria ugonjwa flani.Ni dhahiri kwamba mtu “akilamba” mzinga mzima wa “Mzaramo” (Konyagi) basi siku inayofuatia anaweza kuwa na macho yaliyovimba,na wala si dalili za “arthritis” au maambukizo ya bacteria (sidhani kama bacteria wana jeuri ya kumudu makala ya Konyagi.,,natania tu!).Lakini nadhani licha ya kujiangalia kwenye kioo kwa madhumuni ya kujua kama “reception” (sura) iko maridhawa,kujitazama mwenyewe kwenye kioo kunaweza kukusaidia kujisuta kama umefanya jambo baya,kujipongeza kama umefanya jambo zuri na hata kujishauri pale unapokuwa njia panda kutokana na matatizo au ugumu wa kutoa maamuzi.

Na utafiti mwingine kwa mujibu wa jarida la Saikolojia ya Uchumi (the Journal of Economic Psychology) watu wenye sura nzuri wana uhakika wa kipato kizuri zaidi kushinda wale wenye “sura mbaya.” Wachumi James Andreoni na Ragan Petrie wanaeleza kwamba katika kuangalia mafanikio ya kipato kati ya watu wenye sura nzuri na wale wasio na sura nzuri wamebaini kuwa hata pale watu wa makundi hayo mawili wanapofanya jitihada zinazolingana,wengi wa wenye sura nzuri “wanaibuka kidedea”.Watafiti hao wanaamini kwamba kinachowasaidia wenye sura nzuri kuwa na mafanikio ni ukweli kwamba watu wa aina hiyo huwa na matarajio makubwa ambayo wangependa yawe na matokeo mazuri yatakayoshabihiana na sura zao nzuri.Pia walibaini katika utafiti huo kwamba watu wenye sura nzuri wakizembea “kulinda uzuri wao” (kwa mfano kutojiweka “sopu-sopu” au kuongezeka “nyama za uzembe”) basi wale wanaonekana “wabaya” kwa sura wanapata nafasi ya “kuwapiga bao” (kuchukua nafasi za) hao wenye sura nzuri.Swali nililobaki nalo baada ya kusoma taarifa hizo ni kwamba nani ana mamlaka ya kusema flani mzuri au flani mbaya,pengine kwa kuzingatia msemo wa Kiswahili kwamba “apendae,chongo huona kengeza” au hata pengo kuitwa mwanya.

Pia,siku chache zilizopita wanafunzi kutoka nje ya Uingereza tulipata habari iliyowaacha baadhi ya “wenyeji” wetu wakiwa wamenuna.Kwa mujibu wa Dokta Bernard Lamb,msomi (reader) wa “genetics” kutoka Imperial College London,wengi wa wanafunzi wa kigeni wanaonekana kukimudu vema Kiingereza kuliko wanafunzi wazawa (Waingereza),ambapo wageni hao huwa na makosa machache wanapoandika au kuongea lugha hiyo ulinganisha na hao wenye lugha yao.Dr Lamb alieleza kwamba wanafunzi kutoka nchi za Singapore na Brunnei ndio wanaoongoza kwa ubora wa Kiingereza japokuwa lugha hiyo sio yao ya asili (ni second language).Amesema kwamba sio jambo gani kwa wanafunzi wazawa kuandika kwenye insha zao maneno kama “there” pale inapopaswa kuwa “their” au “bean” pale inapopaswa kuwa “been,” au kutamka “effect” badala ya “affect” na “sun” badala ya “son,” au badala ya wingi (plural) ya “tomato” kuwa “tomatoes” wao wanachapia “tomatos” na badala ya “theories” kama wingi wa “theory” wao wanaibuka na “theorys.” Msomi huyo anadai kuwa udhaifu mkubwa uko kwenye sarufi (grammar) na vituo (punctuation),na sasa anaandaa kitabu cha kuziumbua mamlaka za elimu kwa kuzembea kuweka mkazo kwenye kuboresha somo la Kiingereza mashuleni.

Kadhalika,moja ya mambo yaliyotawala anga za siasa za ndani za Marekani ni tangazo la mpanga-mikakati mkuu (“chief political strategist”) wa rais Bush,Karl Rove,kuwa anajiuzulu mwishoni mwa mwezi huu.Huyu jamaa ana akili sana,tena sana.Tayari wapo wanaodai kuwa hakuna mtu mwenye uwezo wa kuziba pengo lake hapo White House baada ya kuondoka kwake.Inategemea unazungumza na mtu aliye upande gani wa mjadala,kwani kuna watu wanaomtuhumu Rove kwa “kumpotosha” Bush katika maamuzi mbalimbali,na wanadai kuwa kupungua kwa umaarufu wa urais wa Bush (huko Marekani kila baada ya muda flani huwa zinatolewa “ratings” za utendaji kazi wa rais, “congress”,nk na kwa sasa wanaorodhishwa na utendaji kazi wa Bush ni asilimia 32.9 tu huku asilimia 62.4,yaani zaidi ya nusu ya Wamarekani,hawaridhishwi na utendaji kazi wake) kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na swahiba huyo wa Bush.Lakini,mpende au mchukie,mwanamikakati huyu ni mtu mwenye kipaji cha hali ya juu katika kuhakikisha ushindi unapatikana kwa kila aina ya mbinu.Na ndio maana haishangzi kuona baadhi ya watu wakijiuliza kama kutatokea mtu mwenye kipaji kama cha Karl Rove.Yayumkinika kusema kuwa kujiuzulu kwake kumekuja wakati mbaya kwani ripoti inayosubiriwa kwa hamu kutoka kwa kamanda wa majeshi ya Marekani huko Irak,Jeneral David Petraeus,kuhusu mwenendo mzima wa vita ya Irak inatarajiwa kuwasilishwa katikati ya mwezi ujao,na wapo wanaodhani kwamba kukosekana kwa Rove katika kipindi hicho muhimu kunaweza kuwa ni tatizo kwa Bush iwapo ripoti hiyo itakuwa siyo nzuri.Rove ambaye anaelezwa kama mtu atakayengia kwenye vitabu vya historia kama kiumbe asiye na huruma (ruthless) linapokuja suala la kufanikisha matakwa ya kisiasa ya bosi wake,na ambaye alipachikwa jina la utani la “the Architect” (msanifu) kutokana na ufanisi wake kwenye sanaa ya kupanga mikakati,alimsaidia Bush kupata ugavana wa jimbo la Texas mwaka 1994,kabla ya lutoa mchango wa hali ya juu katika ushindi wa Bush kwenye chaguzi za urais za mwaka 2000 na 2004.Japo naweza kuwa miongoni mwa wale wanaoamini kuwa kuna maeneo ambayo “alimpotosha” Bush,na ukweli kwamba tofauti na nguli huyo,mrengo wangu kisiasa ni wa kati ya kushoto (Centre-Left),nimetokea kumhusudu sana Karl Rove (na nadiriki kumwita “role model” katika malengo yangu ya mbeleni).Ukipata nafasi ya kusoma kitabu kiitwacho “Boy Genius: Karl Rove, the Brains Behind the Remarkable Political Triumphs of George W Bush” au “Bush's Brain: How Karl Rove Made George W. Bush Presidential” unaweza kuungana nami “kumkubali” huyu jamaa.

Mwisho,napenda kuwapongeza watani wetu wa jadi Yanga kwa kunyakua kombe la Tusker.Nimesikia “rambirambi” zao kwamba fedha inayotolewa na waandaaji wa mashindano hayo haikidhi gharama halisi walizoingia hadi kufikia hatua ya fainali,lakini nadhani walipaswa kutafakari suala hilo kabla ya kuanza mashindano hayo.Licha ya “kuukosa ubingwa” (haituumi kwa vile hatukufungwa bali tulijitoa) wana Msimbazi tunafarijika na hilo “contract” la nguvu la kuitangaza “chata” ya kimataifa ya “ADDIDAS.” Simba ina bahati na wadhamini,pengine kutokana na rekodi yake nzuri kwenye mechi za kimataifa,lakini ni muhimu kwa Kaduguda na wenzie kuhakikisha kuwa udhamini huo unasaidia katika kutimiza ndoto ya Watanzania kuona vikombe vya michuano mikubwa ya vilabu barani Afrika vinatua nchini.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.