Showing posts with label UTAFITI. Show all posts
Showing posts with label UTAFITI. Show all posts

22 Aug 2007

Asalam aleykum,

Nianze na habari “nyepesi nyepesi.” Kwa mujibu wa utafiti ambao matokeo yake yalinukuliwa na gazeti la Daily Mail la hapa Uingereza,kioo kinaweza kuwa na majibu kuhusu hali ya afya ya binadamu.Inaelezwa kwamba “kujishangaa” kwenye kioo kwa muda flani kunaweza kukupatia tetesi kuhusu dalili za matatizo ya kiafya katika mwili wako.Pengine hii itakuwa habari njema zaidi kwa baadhi ya akinamama ambao,kama wengi wetu tujuavyo,huweza kutumia hata nusu saa wakijiangalia kwenye vioo,hususan kabla ya kufanya “mtoko” (kwenda kwenye harusi,kitchen party,ubarikio,nk).Mie ni miongoni mwa “wazembe” ambao naweza kupitisha hata siku tatu bila kujiangalia kwenye kioo (na pengine siko peke yangu).Lakini kwa mujibu wa utafiti huo,kujiangalia kwenye kioo japo kwa muda michache kunaweza kubainisha matatizo ya kiafya kama vile maambukizo ya bacteria,kupanda kwa “cholesterol”, “anaemia”, “arthritis”,upungufu wa Magnesium mwilini,mshtuko wa moyo na hata kubaini ujauzito.Kwa mfano,ukijitazama kwenye kioo na kubaini kuwa macho yamekuwa meupe kuliko kawaida,basi hiyo inaweza kuwa dalili ya kuzidi kwa “cholesterol” mwilini;macho yakiwa yamevimba pasipo sababu inaweza kuwa dalili ya maambukizo ya bacteria au pengine “arthritis”;kope (“eyelids”) zinazoonekana kama zinataka kunyonyoka zinaweza kuashiria dalili za “anaemia”;jicho linalozunguka bila kuzungushwa (“myokymia”) linaweza kuashiria upungufu wa Magnesium;kupauka kwa rangi ya mwili kunaweza kumaanisha dalili za homa ya manjano au matatizo ya maini;fizi zinazotoka damu zinaweza kuashiria “leukaemia” au ujauzito;na mipasuko kwenye “lips” kunaweza kuashiria kisukari.Hata hivyo,kama yalivyo matokeo ya tafiti nyingi,matokeo ya utafiti huu kuhusu “faida za kioo katika kubaini hali ya mwili” hayamaanishi kuwa kila dalili utakayoiona kwenye kioo (kati ya hizo zilizotajwa) basi lazima inaashiria ugonjwa flani.Ni dhahiri kwamba mtu “akilamba” mzinga mzima wa “Mzaramo” (Konyagi) basi siku inayofuatia anaweza kuwa na macho yaliyovimba,na wala si dalili za “arthritis” au maambukizo ya bacteria (sidhani kama bacteria wana jeuri ya kumudu makala ya Konyagi.,,natania tu!).Lakini nadhani licha ya kujiangalia kwenye kioo kwa madhumuni ya kujua kama “reception” (sura) iko maridhawa,kujitazama mwenyewe kwenye kioo kunaweza kukusaidia kujisuta kama umefanya jambo baya,kujipongeza kama umefanya jambo zuri na hata kujishauri pale unapokuwa njia panda kutokana na matatizo au ugumu wa kutoa maamuzi.

Na utafiti mwingine kwa mujibu wa jarida la Saikolojia ya Uchumi (the Journal of Economic Psychology) watu wenye sura nzuri wana uhakika wa kipato kizuri zaidi kushinda wale wenye “sura mbaya.” Wachumi James Andreoni na Ragan Petrie wanaeleza kwamba katika kuangalia mafanikio ya kipato kati ya watu wenye sura nzuri na wale wasio na sura nzuri wamebaini kuwa hata pale watu wa makundi hayo mawili wanapofanya jitihada zinazolingana,wengi wa wenye sura nzuri “wanaibuka kidedea”.Watafiti hao wanaamini kwamba kinachowasaidia wenye sura nzuri kuwa na mafanikio ni ukweli kwamba watu wa aina hiyo huwa na matarajio makubwa ambayo wangependa yawe na matokeo mazuri yatakayoshabihiana na sura zao nzuri.Pia walibaini katika utafiti huo kwamba watu wenye sura nzuri wakizembea “kulinda uzuri wao” (kwa mfano kutojiweka “sopu-sopu” au kuongezeka “nyama za uzembe”) basi wale wanaonekana “wabaya” kwa sura wanapata nafasi ya “kuwapiga bao” (kuchukua nafasi za) hao wenye sura nzuri.Swali nililobaki nalo baada ya kusoma taarifa hizo ni kwamba nani ana mamlaka ya kusema flani mzuri au flani mbaya,pengine kwa kuzingatia msemo wa Kiswahili kwamba “apendae,chongo huona kengeza” au hata pengo kuitwa mwanya.

Pia,siku chache zilizopita wanafunzi kutoka nje ya Uingereza tulipata habari iliyowaacha baadhi ya “wenyeji” wetu wakiwa wamenuna.Kwa mujibu wa Dokta Bernard Lamb,msomi (reader) wa “genetics” kutoka Imperial College London,wengi wa wanafunzi wa kigeni wanaonekana kukimudu vema Kiingereza kuliko wanafunzi wazawa (Waingereza),ambapo wageni hao huwa na makosa machache wanapoandika au kuongea lugha hiyo ulinganisha na hao wenye lugha yao.Dr Lamb alieleza kwamba wanafunzi kutoka nchi za Singapore na Brunnei ndio wanaoongoza kwa ubora wa Kiingereza japokuwa lugha hiyo sio yao ya asili (ni second language).Amesema kwamba sio jambo gani kwa wanafunzi wazawa kuandika kwenye insha zao maneno kama “there” pale inapopaswa kuwa “their” au “bean” pale inapopaswa kuwa “been,” au kutamka “effect” badala ya “affect” na “sun” badala ya “son,” au badala ya wingi (plural) ya “tomato” kuwa “tomatoes” wao wanachapia “tomatos” na badala ya “theories” kama wingi wa “theory” wao wanaibuka na “theorys.” Msomi huyo anadai kuwa udhaifu mkubwa uko kwenye sarufi (grammar) na vituo (punctuation),na sasa anaandaa kitabu cha kuziumbua mamlaka za elimu kwa kuzembea kuweka mkazo kwenye kuboresha somo la Kiingereza mashuleni.

Kadhalika,moja ya mambo yaliyotawala anga za siasa za ndani za Marekani ni tangazo la mpanga-mikakati mkuu (“chief political strategist”) wa rais Bush,Karl Rove,kuwa anajiuzulu mwishoni mwa mwezi huu.Huyu jamaa ana akili sana,tena sana.Tayari wapo wanaodai kuwa hakuna mtu mwenye uwezo wa kuziba pengo lake hapo White House baada ya kuondoka kwake.Inategemea unazungumza na mtu aliye upande gani wa mjadala,kwani kuna watu wanaomtuhumu Rove kwa “kumpotosha” Bush katika maamuzi mbalimbali,na wanadai kuwa kupungua kwa umaarufu wa urais wa Bush (huko Marekani kila baada ya muda flani huwa zinatolewa “ratings” za utendaji kazi wa rais, “congress”,nk na kwa sasa wanaorodhishwa na utendaji kazi wa Bush ni asilimia 32.9 tu huku asilimia 62.4,yaani zaidi ya nusu ya Wamarekani,hawaridhishwi na utendaji kazi wake) kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na swahiba huyo wa Bush.Lakini,mpende au mchukie,mwanamikakati huyu ni mtu mwenye kipaji cha hali ya juu katika kuhakikisha ushindi unapatikana kwa kila aina ya mbinu.Na ndio maana haishangzi kuona baadhi ya watu wakijiuliza kama kutatokea mtu mwenye kipaji kama cha Karl Rove.Yayumkinika kusema kuwa kujiuzulu kwake kumekuja wakati mbaya kwani ripoti inayosubiriwa kwa hamu kutoka kwa kamanda wa majeshi ya Marekani huko Irak,Jeneral David Petraeus,kuhusu mwenendo mzima wa vita ya Irak inatarajiwa kuwasilishwa katikati ya mwezi ujao,na wapo wanaodhani kwamba kukosekana kwa Rove katika kipindi hicho muhimu kunaweza kuwa ni tatizo kwa Bush iwapo ripoti hiyo itakuwa siyo nzuri.Rove ambaye anaelezwa kama mtu atakayengia kwenye vitabu vya historia kama kiumbe asiye na huruma (ruthless) linapokuja suala la kufanikisha matakwa ya kisiasa ya bosi wake,na ambaye alipachikwa jina la utani la “the Architect” (msanifu) kutokana na ufanisi wake kwenye sanaa ya kupanga mikakati,alimsaidia Bush kupata ugavana wa jimbo la Texas mwaka 1994,kabla ya lutoa mchango wa hali ya juu katika ushindi wa Bush kwenye chaguzi za urais za mwaka 2000 na 2004.Japo naweza kuwa miongoni mwa wale wanaoamini kuwa kuna maeneo ambayo “alimpotosha” Bush,na ukweli kwamba tofauti na nguli huyo,mrengo wangu kisiasa ni wa kati ya kushoto (Centre-Left),nimetokea kumhusudu sana Karl Rove (na nadiriki kumwita “role model” katika malengo yangu ya mbeleni).Ukipata nafasi ya kusoma kitabu kiitwacho “Boy Genius: Karl Rove, the Brains Behind the Remarkable Political Triumphs of George W Bush” au “Bush's Brain: How Karl Rove Made George W. Bush Presidential” unaweza kuungana nami “kumkubali” huyu jamaa.

Mwisho,napenda kuwapongeza watani wetu wa jadi Yanga kwa kunyakua kombe la Tusker.Nimesikia “rambirambi” zao kwamba fedha inayotolewa na waandaaji wa mashindano hayo haikidhi gharama halisi walizoingia hadi kufikia hatua ya fainali,lakini nadhani walipaswa kutafakari suala hilo kabla ya kuanza mashindano hayo.Licha ya “kuukosa ubingwa” (haituumi kwa vile hatukufungwa bali tulijitoa) wana Msimbazi tunafarijika na hilo “contract” la nguvu la kuitangaza “chata” ya kimataifa ya “ADDIDAS.” Simba ina bahati na wadhamini,pengine kutokana na rekodi yake nzuri kwenye mechi za kimataifa,lakini ni muhimu kwa Kaduguda na wenzie kuhakikisha kuwa udhamini huo unasaidia katika kutimiza ndoto ya Watanzania kuona vikombe vya michuano mikubwa ya vilabu barani Afrika vinatua nchini.

Alamsiki

10 Aug 2007


Further Updates: "Majibu" ya Mrisho na Tulizo Kilaga.USIKOSE KUSOMA COMMENTS MBALIMBALI MWISHO WA MAKALA HII NA KWENYE BLOGU YA MRISHO

Latest Updates: Baada ya "washtaki" kuwa judge,jury and prosecutor,hatimaye mtuhumiwa apewa nafasi ya kujieleza

Updates: Mashambulizi yaendelea

Updates: Kaazi kweli kweli

Mtanzania huyu kumponza Mengi

Ni mropokaji, anayeandika bila kufanya utafiti
Na Mwandishi Wetu
Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Aberdeen, Scotland, Evarist Chahali huenda akamponza Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, ambaye pia ni mmiliki wa gazeti la Kulikoni, kufuatia habari potofu aliyoiandika kwenye gazeti hilo dhidi ya gazeti la Risasi.

Kwa mujibu wa habari hiyo, mwandishi huyo ambaye ni Mtanzania anayedai kuchukua kozi ya Udaktari wa Falsafa (PhD) katika chuo hicho, aliandika makala ya kuyashutumu magazeti ya Udaku kuwa yanaandika habari feki na kutolea mfano gazeti la Risasi.

Katika makala yake ya Jumatano Agosti 8, mwaka huu, Chahali alidai kuwa habari zilizoandikwa kwenye gazeti la Risasi ambalo ni dada la hili, zilizoambatana na picha hazikuwa na ukweli wowote.

Chahali alitolea mfano wa habari iliyochapwa kwenye gazeti hilo la Julai 18-20 iliyokuwa na kichwa cha habari 'Warembo wa TZ wapiga picha za X tupu'.

Habari hizo ambazo chanzo chake ni mtandao, zilieleza kuwa wasichana hao ni Watanzania waliopiga picha wakiwa watupu kwa nia ya kutangaza biashara ya kuuza miili ambapo waliweka bayana mawasiliano yao.

Hata hivyo, Chahali alidai kuwa habari hiyo ni ya uongo (feki), kwani picha zilizotumika ni za nyota wa sinema za ngono (porn star) wa Marekani na si Watanzania.

Mwandishi huyo alieleza katika makala yake hiyo kuwa, aliamua kuandika hivyo baada ya kuambiwa na rafiki yake anayeishi Marekani.

Akiongea na gazeti hili, Meneja Mkuu wa Kampuni inayochapa gazeti hilo, Abdallah Mrisho, alisema kuwa amesikitishwa na makala ya gazeti la Kulikoni ambayo haikufanyiwa utafiti wa kutosha.

"Habari iliyoandikwa na gazeti la Risasi ni ya kweli, hatujawahi kuandika wala haturuhusu wahariri wetu kuandika habari za uongo ndani ya magazeti yetu, ila Chahali ameropoka.

"Kimsingi mwandishi wa makala hayo, (Chahali) ameonyesha udhaifu mkubwa kwa kuandika habari bila kufanya utafiti na kufikia uamuzi wa kushambulia gazeti letu bila kuwa na uhakika na alichokiandika", alisema Mrisho.

Mrisho aliendelea kusema ana wasiwasi hata na shahada alizonazo Chahali, kwani mtu mwenye elimu kama yake hawezi kuandika habari za kuambiwa bila kufanyia utafiti, hivyo kuupotosha umma na anaweza kumponza mmiliki wa kampuni inayochapisha gazeti hilo, ambaye anaheshimika sana.

"Chahali hakupaswa kutoa shutuma nzito kama zile kwa maneno ambayo hakuyafanyia uchunguzi na kuchapa kwenye gazeti, kwani anaweza kumponza mmiliki wa kampuni hiyo tunayemuheshimu, anapaswa kuona aibu (shame on him)," alisema Mrisho.

Kuthibitisha kuwa habari iliyoandikwa ni ya kweli, wahariri wa gazeti la Risasi wamelazimika kutaja anuani ya tovuti ambako wasichana hao wanapatikana, ili umma kwa ujumla uelewe nani mkweli kati ya Chahali na gazeti la Risasi, ingawa haikuwa kusudio lao kufanya hivyo.

Anuani hiyo ni http://swallowmyjuice.hi5.com ambako picha zilizotumika, mahali wanakoishi na utambulisho wa wasichana hao vinapatikana.

Aidha, kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari cha kuaminika kilichoko ndani ya chuo cha Aberdeen, Chahali ni miongoni mwa wanafunzi wasiofanya vizuri sana katika masomo yao.

"Chahali sio miongoni mwa wanafunzi wanaofanya vizuri sana chuoni," kilisema chanzo hicho.

Baadhi ya wanafunzi wanaosoma kozi moja na Chahali katika chuo hicho ni pamoja na Timofei Agarin, Gordon G. Davidson, Joyleve Elliat, Anna Gustavon, Jeremy Lamoreaux, Giseong lee, Yang Lia, Khristus Vassis, Lortraine Whitty na Anna Zawak.

Mrisho alimtahadharisha mhariri wa gazeti hilo kuwa asipokuwa makini na waandishi wanaoandika makala zao kwa chuki binafsi kama Chahali, wanaweza kujikuta kwenye matatizo makubwa.

Akiongea na mwandishi wetu kwa simu juzi, Mhariri Mtendaji wa magazeti ya This Day na Kulikoni, Evarist Mwitumba alisema kuwa hana habari kuhusu makala hayo.

"Nipigieni kesho asubuhi, kwa sasa niko barabarani naendesha gari na sijasoma gazeti lililoandika habari hiyo," alisema Mwitumba.


HAYA NI MAONI YA WATU MBALIMBALI KATIKA BLOGU YA IJUMAA/RISASI http://abdallahmrisho.blogspot.com KUHUSU MASHAMBULIZI DHIDI YANGU


mkandamizaji said...
Mrisho

Mimi sio mtaalam wa masuala ya mtandao, lakini hakuna mtandao ambao unavurugwa sana na watumiaji kama hi5.com. Kama hichi ndo chanzo chako pekee cha hiyo habari, nasikitika kuwa nitakuwa upande wa chahali kukusuta kuwa picha zile ni za Wamarekani na kuwa nyie mmedanganya watanzania.

Tupe mitandao yenye URL zinazoeleweka sio hi5.com. Mtu anaweza kuweka picha ya mtu yeyote kwenye hi5.com. Na kama nakumbuka kuhusu maelezo ya ile habari, ulisema kuwa kuna namba za simu, eno wanakopatikana hao wadada na mambo kama hayo. Lakini kwa hi5.com ambayo ni mtandao wa marafiki tu, bado hajani conivnce kuwa ulikuwa na source nzuri ya habari.

Najua unaweza kuamua kutotundika hii comment, lakini ujumbe utakuwa umeupata.

Asante

August 9,:53 PM
================================================================
Anonymous said...
Nyote mnahitaji kuwa makini.Mbona hakuna cha ajabu katika hizo picha mnazozizungumzia?Bikini ni nguo za kawaida tu jamani..tuache ushamba na ushambenga watanzania.

August 10, 2007 1:02 AM
===================================================================
kichuguu said...
Nimeangalia picha zile pale Hi5, nina wasiwasi kuwa naweza kukubaliana na chahali kuwa wale ni pornstar wa kimarekani. mambo matatu yanawezekana:

(a)wasichana wa kitanzania wametumia picha za mastar hao.

(b) mastar wameamua kudanganya kuwa wako Tanzania.

(c) mastar hao ni watanzania.

Picha hizo hazikupigwa katika mazingira ya Tanzania. Baadaye nitakutafutia picha nyingine za yule anayejiita Melanie ndipo utakapogundua kuwa siyo za kutoka mazingira ya Tanzania.

August 10, 2007 6:40 AM
===================================================================
mzalendo said...
tumesikitishwa sana kuona vyanzo vyetu vya habari havina uhakika na habari zao. hiyo website iliyotolewa na gazeti la ijumaa inaonyesha moja kwa moja kuwa hao watu mmoja ni MGANDA na wote ni GAYS/ LESBIANS!
mbili ni kuwa hamkuhakikisha kama hizo picha ni za hao MNAOWAITA WAREMBO wa KIBONGO na MMEWASILIANA NAO. Mnauhakika gani kama ni picha za wabongo???? mpaka mkaamua kuandika gazetini?? ....au ndo mnafanya chochote kuuuza magazeti yenu?

August 10, 2007 7:59 AM
===================================================================
Anonymous said...
website mliyotupatia inahakikisha kuwa muandishi wa RISASI hana uhakika na alichokisema, kwa vile website hiyo inaonyesha kuwa wale ni GAYS/LESBIANS na pia HAILAZIMISHI kuwa zile picha ni za hao walioziweka na wala hamkutupa ushahidi kuwa mlihakikisha hao mlowapigia simu ndio wenye picha zile.

August 10, 2007 8:02 AM
====================================================================
Anonymous said...
na kwa vile hakuna uhuru wa kujielezea , na jua nilichokiandika hutokipublish

August 10, 2007 8:04 AM
===================================================================
Anonymous said...
nyote hapo juu nahisi mnamiss point, chahali aliamua kuwakandia wenzake bila kujua kama zile picha kweli zipo na wahusika wamejitambulisha kama wabongo, hivyo ishu sio kama ni wabongo au sio wabongo, ila ishu iliyopo hapa ni kwamba kwa nini Chahali amewakandia jamaa wa risasi na kudai wanaandika habari feki? kwa nini, wakati vitiu hivyo vipo? kama jamaa angefanya utafiti kidogo, angekuwa na ishu tofauti ya kuwabana.. hapa nawaunga mkono jamaa wa risasi..

August 10,:27 AM
===================================================================
Anonymous said...
Mimi naungana na Chalali kuwa magazeti hayo mara nyingi wanaandika habari za uongo ili watu wanunu e magazeti, utakuta mtu anaandika eti kapigiwa simu na mtu wanaandika habari kwenye gazeti je hii ni sawa??? unatunia uongo kupata pesa za watu???? I think tuungane watanzania tuanzishe kampeni za kutonunu magazeti ya udaku!!! Hongera chalali, najua unaweza usitoe hii lakini msg will be sent

August 10, 2007 1:10 PM
===================================================================
Anonymous said...
kwanza hii habari mbona imepindishwapindishwa jamani, kichwa cha habari cha muhusu Mengi, Ndani ya habari main content gazeti la Risasi.Mambo tofauti tofauti.

Simtetei Chalali...ila swala la kutofanya vizuri darasani linawahusu nini hasa, au linahusika vipi na habari yenyewe?...Huo ni mpindisho tosha na ni kupakana matope. Hatuelewi huyu jamaa anasoma katika mazingira gani, isitoshe level anayosoma Phd. haijadiliwi tena kama anafanya vizuri au vibaya darasani. Watanzania tuangalie cha kuandika.
Last point, magazeti ya udaku yapo hata Ulaya, ila cha muhimu ni kuandika mambo ambayo kweli yapo, au yametokea, si kubahatisha ili kuuzisha gazeti.

August 10, 2007 1:19 PM
===================================================================
mkereketwa said...
kama hiyo website ya porn iliyowekwa , chahali alikuwa na haki ya kupinga maelezo ya RISASI kwa vile hao watu hawapo TZ bali wanafanya kazi ya porn Marekani.
tusingefurahi kudanganywa na magazeti kwa kutofuatilia vyanzo vyao vya habari kikamilifu.
kosa la RISASI ni kutokufuatilia kikamilifu hao waliotowa namba zao na wapi wanapatikana kama ni sawa na hao walioweka picha za uchi kwenye Hi5. ushahidi mkubwa unaonyesha kuwa walitumia picha za hao watu tu kujipa umaarufu na kinachoshangaza ni kuona RISASI haikusema kuwa haikutuambia kuwa kuna uwezekano kuwa zile picha si zao.

August 10, 2007 2:45 PM


PIA NIMEONA MAONI HAYA HUKO JAMBO FORUMS

Vyanzo vya Habari vya Magezeti Mengine
Mimi ni msomaji sana wa blogu ya Abdallah Mirosho ya http://www.abdallahmrisho.blogspot.com. Blogu hii hunipatia udaku safi sana kutoka mitaa mbali mbali ya Dar es Salaam. Habari niliyonukuu hapa ilinishtua sana kwamba badala ya wao kukubali kuwa magaxeti yao ni ya udaku, wakaamua kumtukna mwandishi aliyewasema kuwa habari waluyokuwa wameandika haikuwa sahihi.

Quote:

Mtanzania huyu kumponza Mengi

Ni mropokaji, anayeandika bila kufanya utafiti

Na Mwandishi Wetu

Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Aberdeen, Scotland, Evarist Chahali huenda akamponza Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, ambaye pia ni mmiliki wa gazeti la Kulikoni, kufuatia habari potofu aliyoiandika kwenye gazeti hilo dhidi ya gazeti la Risasi......Kwa mujibu wa habari hiyo, mwandishi huyo ambaye ni Mtanzania anayedai kuchukua kozi ya Udaktari wa Falsafa (PhD) katika chuo hicho, aliandika makala ya kuyashutumu magazeti ya Udaku kuwa yanaandika habari feki na kutolea mfano gazeti la Risasi.Katika makala yake ya Jumatano Agosti 8, mwaka huu, Chahali alidai kuwa habari zilizoandikwa kwenye gazeti la Risasi ambalo ni dada la hili, zilizoambatana na picha hazikuwa na ukweli wowote......Chahali alitolea mfano wa habari iliyochapwa kwenye gazeti hilo la Julai 18-20 iliyokuwa na kichwa cha habari 'Warembo wa TZ wapiga picha za X tupu'.....Hata hivyo, Chahali alidai kuwa habari hiyo ni ya uongo (feki), kwani picha zilizotumika ni za nyota wa sinema za ngono (porn star) wa Marekani na si Watanzania................Kuthibitisha kuwa habari iliyoandikwa ni ya kweli, wahariri wa gazeti la Risasi wamelazimika kutaja anuani ya tovuti ambako wasichana hao wanapatikana, ili umma kwa ujumla uelewe nani mkweli kati ya Chahali na gazeti la Risasi, ingawa haikuwa kusudio lao kufanya hivyo.Anuani hiyo ni http://swallowmyjuice.hi5.com ambako picha zilizotumika, mahali wanakoishi na utambulisho wa wasichana hao vinapatikana....Aidha, kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari cha kuaminika kilichoko ndani ya chuo cha Aberdeen, Chahali ni miongoni mwa wanafunzi wasiofanya vizuri sana katika masomo yao...."

Nilipoangalia picha zilizosemekana za watanzania pale http://swallowmyjuice.hi5.com, nilikuta mwanadada mmja anayejiita Melanie ambaye kwa bahati mbaya ninadhani namfahamau vizuri na picha hiyo imepigwa zaidi ya miaka saba iliyopita. Mwanadada yule alikuwa mmoja wa ma-hooker wazuri sana pale South Beach Miami na nadhani kuwa alikuwa damu mchanganyiko mwasia na mwafrika. Nimeweza kupata baadhi ya picha zake nyingine kwenye websites chafu kama hii hapa. (ONYO: PICHA HIZO NI CHAFU SANA USIZIFUNGUE MBELE YA WATOTO NA WATU WA HESHIMA.)


Swali, je mwandishi wa Risasi kweli alifanya haki kumtolea matusi ya kashfa mwandishi wa Kulikoni kuhusu uhalali wa picha zile kama kweli zilikuwa za akina dada wa kitanzania?
__________________
Kichuguuu: Nyumba inayohifadhi mchwa na nguchiro kwa pamoja bila mkwaruzo

22 Aug 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum wasomaji wapendwa wa gazeti hili maridhawa.

Leo nina mada nzito na nakuomba msomaji uifatilie kwa makini kwa manufaa ya Taifa letu.Labda kabla “sijaivaa” mada hiyo nitoe mfano mmoja wa hapa Uingereza.Miongoni mwa matatizo makubwa ya kijamii yanayoikabili nchi hii ni suala la matumizi ya madawa ya kulevya hususan miongoni mwa vijana.Watu wanabwia unga kama hawana akili nzuri.Kipindi hiki cha summer nacho kinasaidia kupata “jeshi jipya la wabwia unga" hasa kwa vile baadhi ya vijana huenda mapumzikoni (summer holiday) nje ya nchi wakiwa mbali na wazazi wao.Ukisimuliwa vituko vinavyotokea pwani za sehemu kama Hispania (kwa mfano Ibiza,Majorca na kwingineko) utabaki mdomo wazi.Hata hivyo,serikali na taasisi nyingine zimekuwa zikifanya jitihada kubwa kupambana na tatizo hilo japokuwa mafanikio si makubwa sana.

Kwa huko nyumbani tatizo naliona kubwa sana zaidi ya kubwia unga ni matumizi ya bangi.Sijui ni kwa vile madhara ya bangi ni ya polepole zaidi ya kubwia unga,au sijui kwa vile bangi imezoeleka sana,ukweli unabaki kuwa hatua madhubuti dhidi ya uvutaji bangi hazijatiliwa mkazo sana na vyombo husika.Kwa bahati mbaya sijaona utafiti wowote rasmi uliofanywa kuonyesha ukubwa wa tatizo hili,lakini naamini pindi utapofanyika matokeo yake yatakuwa ya kutisha.

Kuna kundi maalumu nitalolizungumiza hapa:wasanii hususan wale wa Bongofleva.Nilipokuwa huko nyumbani nilijaribu kufanya utafiti usio rasmi kujua msanii gani anatumia bangi na nani hatumii.Kwa kuwa utafiti huo haukuwa rasmi naomba nisitoe “takwimu” zangu lakini ukweli ni kwamba bangi imekuwa ina wafuasi wengi sana miongoni mwa wasanii wetu.Unajua tatizo mojawapo la uvutaji bangi ni kwamba huwezi kujificha iwapo ni mtumiaji.Kuna vitu flani-flani huwa havifichiki pindi mtu akishapuliza majani hayo haramu.Ilinishtua nilipogundua kuwa karibuni robo tatu ya wasanii wa kundi flani maarufu huwa hawawezi kutumbuiza jukwaani bila kupata misokoto kadhaa ya bangi.Jamani,hii sio hadithi ya kutunga au Isidingo bali ni hali halisi.Kwa bahati mbaya,watu hawajali sana.Na ndio maana hata kwenye tungo za baadhi ya wasanii maarufu wa Bongoflava unasikia bangi ikitajwa kwa namna ya kusifiwa utadhani imekuwa chai.Sintotaja majina ya watu hapa lakini kwa harakaharaka nimesikia nyimbo tatu,mbili kati ya hizo zikiwa zimeimbwa na msanii mmoja ambapo baadhi ya maneno ni kama “mimi nina kijiti cha…na wewe leta kijiti cha …” (kijiti ni bangi,na ukisikia kijiti cha mwanza basi inamaanisha bangi inayotoka mwanza),nyingine kuna maneno “…nitembezee chata…” (kutembeza chata ni kupasiana bangi) na msanii mwingine hakuona aibu kusema waziwazi “…pobe nakunywa,bangi navuta…”Wahusika wanaweza kujitetea kwamba hizo ni nyimbo tu na wao hawatumii kilevi hicho lakini haihitaji PhD kujua kwamba mtu hawezi kusifia kitu kibaya kama hakitumii au kukipenda.

Miongoni mwa hofu zangu kuhusu matumizi ya bangi kwa baadhi ya wasanii ni kwamba mara nyingi (kwa mujibu wa utafiti wangu usio rasmi) baada ya kuvuta bangi na kutumbuiza,msanii husika hujikuta “akizidishiwa ulevi” kwa ofa za pombe kutoka kwa mashabiki au wapambe.Lakini pia kuna watu wanaoitwa “groupies” ambao mara nyingi ni akinadada ambao wanamwandama msanii na wako tayari kufanya lolote kumridhisha msanii huyo.Sasa mtu akishakuwa na “cocktail” ya bangi na pombe,je akipewa ofa ya tendo la ndoa na “groupie” kondom inakumbukwa kweli?Lakini hilo ni tatizo dogo ukilinganisha na lile la “utaahira”.Najua ni vigumu kumshawishi mvuta bangi aamini kuwa bangi inachangia katika kuleta madhara kwenye ubongo,lakini ukweli ndio huo.

Naomba ieleweke kwamba simaanishi kuwa wasanii wote ni wavuta bangi bali pointi yangu ni kwamba ulevi huo haramu umepata wafuasi wengi kwenye fani kama wanavyosema wenyewe.Nawajua wasanii kadhaa ambao wanajiheshimu ambao wanaelewa kuwa licha ya bangi kuwa ni kitu haramu pia ina madhara kwa afya ya mvutaji.Kwenye utafiti wangu “bubu” niligundua kwamba miongoni mwa sababu zinazowafanya baadhi ya vijana kujiingiza kwenye utumiaji wa bangi ni hoja ya kipuuzi kwamba “inaleta kujiamini na hisia za ubabe!!!”Nilidokezwa na rafiki yangu mmoja aliewahi kufanya “shooting” ya video ya tangazo flani lililokuwa limemhusisha msanii mmoja wa “mkoani” kwamba nusura amwombe bosi wake atafute mtu mwingine wa kutokea kwenye tangazo hilo kwa vile msanii huyo alibugia misokoto kama minane hivi siku waliyokuwa wanajiaandaa na shooting hiyo.

Sasa nyie vijana,na hasa baadhi ya wasanii,mnaoendekeza uvutaji bangi mkae mkielewa kwamba mnajitafutia matatizo kwenye maisha yenu.Lakini pia wakati umefika sasa kwa uvutaji bangi kuonekana kama tatizo sugu linalohitaji kutupiwa jicho kali.Wale wanaovuta bangi kwa kisingizio cha “imani zao za kidini” (ndio,wapo wanaodai kuwa wao ni marastafari na bangi ni majani matakatifu) watambue kwamba wanavunja sheria na wakati huohuo wanatuletea uwezekano wa kuwa na mataahira siku za mbeleni.Watambue kuwa nchi yetu ni masikini na wakati huu ambao jitihada zinaelekezwa katika kupambana na majanga kama ya ukimwi wao wanatuongezea mzigo mwingine wa kukabiliana na tatizo la uchizi unaosababishwa na weed (bangi).

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.