14 Aug 2009


Kingunge Ngombale Mwiru ni mkingwe,kiumri,kisiasa na kimadaraka.Japo umri si kigezo muhimu cha kuwa na busara,ukongwe katika fani flani unatarajiwa kuambatana na busara.Lakini hali si hivyo kwa Kingunge.Kuna nyakati baada ya kifo cha Nyerere baadhi ya watu walitarajia kuwa Kingunge angefanikiwa kuendeleza mema ya Mwalimu hasa kwa vile tuliaminishwa kwamba mwanasiasa huyu (Kingunge) ana damu ya Ujamaa kiasi cha kuachana na mambo ya imani ya kidini.Tuliambiwa dini ya Kingunge ni Ujamaa.

Pamoja na mapungufu ya hapa na pale,Nyerere anaendelea kukumbukwa kwa jitihada zake za kujenga jamii yenye kukaribia usawa na kuchukia unyonyaji.Sijui Kingunge akifa tutamkumbuka kwa lipi zaidi ya kuzeekea kwake kwenye siasa pasipo tija na hili jukumu jipya alilojipachika la u-Baba wa Taifa wa Mafisadi.Kingunge ni mnafiki mkubwa kwa vile wakati anadai kuwa viongozi wa kanisa "wangeufyata" laiti Mwalimu angekuwa hai,sijui yeye Kingunge angemwambia nini anaposimama kidete kutetea mafisadi.

Haya ndio madhara ya kuviacha vikongwe madarakani hadi vinapoteza uwezo wa kufikiri.Na huyu ni mshauri wa kiongozi wa nchi!Kama uwezo wake binafsi wa kufikiri umefikia kikomo atawezaje kumshauri mtu mwingine,achilia mbali kiongozi wa nchi?

Kwanini adai waraka wa kanisa utawagawa Watanzania lakini akae kimya pale chama chake cha CCM kilipocheza karata-tatu ya kisiasa kilipoahidi (katika manifesto yake ya uchaguzi 2005) uanzishwaji wa mahakama ya kadhi kwa Waislam?Binafsi,sina tatizo na uanzishwaji wa mahakama ya kadhi iwapo mambo flani muhimu yatazingatiwa,lakini kwa uendeshaji wa mambo kwa mtindo wa zima moto,au pata potea,ni dhahiri uamuzi huo wa mahakama ya kadhi unaweza kulipeleka pabaya taifa.Narudia,tatizo sio uanzishwaji au kuwepo kwa mahakama hiyo,bali ni ubabaishaji wa viongozi wetu katika kushughulikia uanzishwaji na uwepo wake pasipo kuathiri umoja wa kitaifa.

Na kikongwe huyu (Kingunge) mbona yuko kimya hadi leo baada ya chama chake kusuasua katika utekelezaji wa ahadi hiyo ya uanzishwaji wa mahakama ya kadhi?Kama uamuzi wa CCM kutaja katika manifesto yake juu ya suala hilo ulikuwa hatari (kwa mujibu wa wanaodhani hivyo),kitendo cha chama hicho kurushiana mpira kila kinapoulizwa na waahidiwa (Waislam) kuhusu utekelezaji ni cha hatari zaidi.

Tatizo la Kingunge kuhusu waraka wa kanisa haliko kwenye kile anachodai "kuijua vizuri nchi yetu" bali wasiwasi wake kwamba pindi waraka huo ukitekelezwa kwa vitendo basi yeye na mafisadi anaowatetea watakuwa katika wakati mgumu.Kwa lugha nyingine,Kingunge anatetea maslahi ya tabaka alilomo na analoliwakilisha (mafisadi).

Hivi ni lini umewahi kumsikia Kingunge akikemea ufisadi?Hivi Kanisa lingetoa wapi wazo la kujana waraka huo laiti kikongwe hiki cha siasa kingesimama kidete kuendeleza harakati za Mwalimu kupambana na unyonyaji?Badala ya kutueleza yeye anafanya nini kuhakikisha nchi inakwenda vizuri anakimbil;ia kukosoa wengine kuwa wanataka kuipeleka nchi pabaya.

Halafu inakera zaidi kumskikia babu huyu akijifanya kama yeye ndio mwenye hatimili ya historia,mwelekeo na chochote kuhusu Tanzania.Eti anakemea wenzake "wanaodakia hoja pasipo kujua vema tumefikaje hapa..."Tumefika hapa tulipo kwa sababu ya watu kama Kingunge,wanafiki waliojifika kwenye ngozi wa kondoo wakati wa Mwalimu kumbe ni mbwa mwitu wa kifisadi waliokuwa wakisubiri Mwalimu aondoke kwenye ulingo wa siasa kisha watufisadi.

Kingunge ni mtu hatari sana,na asipodhibitiwa ataiingiza nchi katika machafuko.Kishajizeekea,hajali litakalotukumba kwa vile ashachuma vya kutosha na anamsubiri Muumba amrejeshe mbele ya haki (na huko atakuwa na maswali lukuki ya kujibu atapokutana na Mwalimu).Ni muhimu kwa wanaomlea kikongwe huyu wakamhurumia kwa kumpatia pumziko haraka,la sivyo "atazidi kulikoroga".

Mungu ibariki Tanzania na waangamize mafisadi na watetezi wao,hususan wale wanaotaka ligi
na wachunga kondoo wako.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.