Showing posts with label PRO-UFISADI ALLIANCE. Show all posts
Showing posts with label PRO-UFISADI ALLIANCE. Show all posts

22 Apr 2012




JK alinda mawaziri
•  ASISITIZA WAACHWE, UPEPO HUU UTAPITA

na Mwandishi wetu

WAKATI taarifa ya Kamati ya wabunge wa CCM chini ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, juzi iliridhia mawaziri wote wanaokabiliwa na tuhuma za ubadhirifu kwenye wizara zao wajiuzulu, jana Rais Jakaya Kikwete aliwasili nchini akitokea Brazil akiwa na msimamo tofauti.

Taarifa zinasema kumekuwa na mazungumzo baina ya Rais Kikwete na Pinda yaliyolenga kunusuru serikali yao lakini walitofautiana kuhusu hatua inayopaswa kuchukuliwa dhidi ya mawaziri waliotakiwa kujiuzulu.

Msimamo wa Pinda inadaiwa kuwa anataka mawaziri wanaokabiliwa na tuhuma waondoke ili kuleta uwajibikaji serikalini, lakini Rais Kikwete amesema mawaziri hao waachwe waendelee na kazi zao, kwa kuwa suala hili ni la upepo tu, liachwe litapita.

Tanzania Daima Jumapili limeelezwa kuwa rais anakataa shinikizo hilo kwa madai serikali haipaswi kuyumbishwa yumbishwa.

Miongoni mwa mawaziri wanaopaswa kuondoka ni Waziri wa Fedha, Mustafa Mkullo; Waziri wa Viwanda na Biashara Dk. Cyril Chami na naibu wake, Lazaro Nyalandu; Waziri wa Tawala wa Mikoa na Serikali za Mitaa, George Mkuchika na naibu wake, Aggrey Mwanri; Waziri wa Afya, Dk. Haji Mponda na naibu wake, Lucy Nkya na Waziri wa Uchukuzi, Omari Nundu.
Wengine ni Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja na Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige.

Habari zinasema Rais Kikwete na Pinda walitofautiana juu ya hatua dhidi ya mawaziri hao, hivyo kuwafanya baadhi ya mawaziri kutamba mitaani kuwa hawang’oki madarakani kwa sababu tayari bosi wao ameonyesha kutounga mkono tuhuma zinazoelekezwa kwao na wabunge wa upinzani na CCM.

Habari hizi zinasema pia kwamba Pinda amekuwa hafurahishwi na msimamo wa ‘bosi’ wake, hasa katika kushindwa kutoa uamuzi mgumu.

Zinadai kuwa rais amekuwa na tabia ya kuacha upepo uchukue nafasi yake wakati Pinda anataka baadhi ya watu wawajibike bila kujali nyadhifa zao au ukaribu na kiongozi mkuu wa nchi ili kurejesha imani ya serikali kwa wananchi.

Pinda inadaiwa amekuwa akitaka maamuzi magumu yafanyike, kwakuwa yeye ndiye anayesulubiwa na maswali pamoja na hoja za wabunge wawapo bungeni.
Baadhi ya wabunge waliozungumza na Tanzania Daima Jumapili, wameweka wazi kuwa kama Rais Kikwete ataamua kuwalinda na kuwatetea mawaziri wake basi watawaondoa kwa mkakati tofauti utakaomlazimisha rais kukubaliana na hoja za wabunge.

Baadhi ya wajumbe waliozungumza na gazeti hili waliweka wazi hatua hiyo inahitaji muda na mipango madhubuti na wao wapo tayari kufanya hivyo, kwani nchi inazidi kudidimia kwenye umaskini huku watu wake wakikosa huduma muhimu za kijamii.

Walisema kwa muda mrefu wamekuwa wakiwalalamikia watendaji wa serikali na chama tawala lakini rais amekuwa mgumu wa kuyashughulikia matatizo hayo.

Wanasema rais ndiye kikwazo kikubwa cha maendeleo ya chama chao na serikali, hasa kwa kuwateua mawaziri, wakurugenzi na maofisa wengine bila kuangalia uwezo wao wa kiutendaji.

“Kaka kwenye Bunge la Februari kuna mbunge alitoa kauli kuwa kama tunaona mambo hayaendi serikalini tupige kura ya kutokuwa na imani na rais, watu walimshambulia. Sasa tunaona umuhimu wa kauli yake ile,” alisema mbunge mmoja.

Tanzania Daima Jumapili, limedokezwa makada wa CCM wameanza kuingiwa na hofu ya kubomoka kwa chama chao hasa baada ya makada wenzao kuanza kujiunga na vyama vya upinzani.
Wanasema wakati makada wa chama hicho wakiendelea kukihama uongozi wa CCM hauonekani kuchukua hatua zinazostahiki dhidi ya viongozi wanaochangia wananchi wakose imani na chama tawala.

Mbunge wa Ludewa, Deo Filikunjombe, aliweka wazi kuwa wabunge wa CCM ni lazima wakemee ubadhirifu kwakuwa Tanzania si mali ya CCM.

Mbunge huyo alikwenda mbali kwa kumtaja Waziri wa Fedha, Mustafa Mkullo, kuwa ni mwizi, mwongo na mbadhirifu wa mali za umma.

Mawaziri wasuasua kuwasilisha barua
Hadi jana Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema hajapokea barua ya kujiuzulu kutoka kwa waziri yeyote huku akiweka wazi kuwa kesho atatoa taarifa kamili juu ya jambo hilo.

Juzi vyombo vya habari vilipata taarifa kutoka kwenye kikao cha wabunge wa CCM kuwa baada ya wabunge kuzituhumu baadhi ya wizara kukithiri kwa ubadhirifu mawaziri wake wameamua kujiuzulu.

Taarifa hizo zilidokeza kuwa mawaziri hao walishinikizwa kuachia nyadhifa zao ili kukinusuru chama na serikali dhidi ya hasira za wananchi wanaokerwa na ufisadi.

Chami atoboa siri
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Cyril Chami, amejitetea kuwa wizara yake haimlindi Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Charles Ekelege, kama alivyotuhumiwa na baadhi ya wabunge.
Alisema amesononeshwa na taarifa ya ukaguzi wa CAG juu ya TBS iliyotolewa kwa waheshimiwa wabunge bila yeye mwenyewe au wizara kupewa nakala kwa kipindi cha wiki nzima.

Alisema kuwa baada ya kusikia kuwa waheshimiwa wabunge wengi wanayo taarifa hiyo na hata naibu wake kukiri bungeni kwamba taarifa imetoka wakati yeye hana nakala, alikwenda kwa Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashillilah na kuiomba nakala ya taarifa hiyo.

Alibainisha kuwa baada ya kufanya ufuatiliaji katika ofisi ya CAG ilikiri kuigawa kwa wabunge na kusahau kuipeleka kwa wizara hiyo ambayo ndiyo inayohusika.

“Hapa wasomaji wapime wenyewe. Inawezekanaje taarifa ya CAG iliyoandikwa kutokana na takwimu zilizotolewa na wizara yangu, iwafikie wabunge huku wizara yangu itakayotakiwa kuifanyia kazi taarifa yenyewe haipewi nakala, eti kwa kughafilika?

“Ni ukweli ofisi ya CAG walighafilikiwa, au jambo hili limesukwa ili kuniaibisha mimi mbele ya Watanzania, rais aliyeniteua na hasa wapiga kura wangu wa Moshi Vijijini?” alihoji.

Nundu ajitetea
Naye Waziri wa Uchukuzi, Omar Nundu, alisema tuhuma dhidi yake zilizoelekezwa na baadhi ya wabunge, hazina ukweli na zimelenga kumchafua.

Alisema kilichoelezwa na Kamati ya Miundombinu ni uongo na uzushi, kwani nyaraka walizozitumia kuorodhesha tuhuma dhidi yake si halali.

Kuhusu kuingilia utendaji wa Mamlaka ya Bandari kwa masilahi binafsi,  alisema si kweli, akaongeza kuwa kinachomponza ni kuipinga kampuni inayotetewa na menejimenti isipewe zabuni ya kufanya upembuzi yakinifu peke yake na kwenda kukopa na baadaye iruhusiwe kujenga gati namba 13 na 14.

“Wanasema namtaka mwekezaji  ambaye makubaliano yanaonyesha atamiliki gati hilo kwa miaka 45. Nachelea kusema ni uongo na uzushi,” alisema Nundu.

Mkuchika apata kigugumizi
Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Mkuchika, alipoulizwa juu ya suala hilo alishindwa kukubali wala kukataa iwapo ataandika barua ya kujiuzulu. Alimtaka mwandishi amuulize Katibu wa Kamati ya Uongozi.


CHANZO: Tanzania Daima

UPDATE:


 
Picture

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 

Gazeti la Tanzania Daima la leo Jumapili Aprili 22, 2012 lina habari katika ukurasa wake wa mbele yenye kichwa cha habari ‘JK alinda Mawaziri’, inayodai kumekuwa na mazungumzo baina ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Waziri MkuuMhe Mizengo Pinda kuhusu hatua inayopaswa kuchukuliwa dhidi ya mawaziri waliotakiwa kujiuzulu.

Habari hiyo imedai kuwa Mhe. Pinda anataka mawaziri wanaokabiliwa na tuhuma waondoke ili kuleta uwajibikaji serikalini, lakini, imeendelea  kudai habari hiyo, “Rais Kikwete amesema mawaziri hao waachwe waendelee na kazi zao, kwa kuwa suala hilini la upepo tu, liachwe litapita”.

Tunachukua nafasi hii kuweka bayana kwamba habari katika hilo gazeti la Tanzania Daima Jumapili si za kweli, bali ni za uzushi na upotoshaji mkubwa.

Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye alikuwa katika ziara ya kikazi nchini Brazil, amerejea jana Aprili 21, 2012 jioni. Hajaonana wala kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu, Mhe. Pinda.

Hivi sasa Mhe. Rais anasubiri kupata taarifa rasmi  kutoka Bungeni Dodoma.

Mhe Rais anawasihi wananchi wasiamini habari hizo za upotoshaji zilizomo kwenye gazeti hilo la Tanzania Daima Jumapili.

Pia ametoa rai kwa wanahabari wasitoke nje ya mstari wa weledi katika kutekeleza kazi zao ili kuendelea kulinda heshima zao binafsi, vyombo wanavyofanyia kazi pamoja na taaluma yenyewe.

Mwisho

Imetolewana:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
22 Aprili, 2012


Source: SUBI

20 Apr 2012

Mtalii akijaribu  souvenir huko Brazil


Nchi yetu inaelekea kubaya japo asilimia kubwa ya Watanzania bado wanalichukulia suala hili kama mzaha.Ukimya,upole na kutochukua hatua madhubuti dhidi ya majambazi wanaofilisi nchi yetu ni kama tumewapa ruhusa ya kufanya wapendavyo.

Moja ya makosa makubwa yaliyofanywa na Watanzania wenzangu ni pale walipoamua kuiweka nchi yetu rehani kwa kumkabidhi urais Jakaya Kikwete.Miaka yake mitano ilitawaliwa na matukio yaliyoashiria bayana kuwa TUMELIWA.Lakini makosa yakarejewa tena mwaka juzi na kwa kumpa dhamana ya 'kumalizia alipoishia.'

Kwanini ninamlaumu Kikwete?Yeye ndiye aliyewateua majambazi hawa wanaotafuna raslimali zetu kana kwamba kuna ligi ya ufisadi.Majuzi,Rais alikabidhiwa Ripoti ya Ukaguzi wa Mahesabu ya Serikali,ambapo ndani ya ripoti hiyo kuna maelezo yanayoweza kukupa ugonjwa wa moyo.Ni wizi wa hali ya juu.Lakini badala ya kuchukua hatua,Kikwete huyooo safarini.Amekwenda Brazil kwa ziara ya siku tano.Mzururaji huyu ni nadra kupitisha mwezi bila kwenda ng'ambo.

sINTOFAHAMU YAKE KATIKA UTEUZI WA MAJAMBAZI NA SINTOFAHAMU YAKE KATIKA KUCHUKUA HATUA KALI DHIDI YA WABABAISHAJI ALIOWAKABIDHI DHAMANA YA KUTUNGOZA NDIO CHANZO KIKUBWA CHA YOTE TUNAYOSHUHUDIA HIVI LEO.

Hebu soma habari ifuatayo ya kuchukiza.
Ufisadi wa mabilioni kila kona



Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo
NI KWENYE MAGARI YA SERIKALI,TANESCO,MALIASILI,MABILIONI YA JK,AFYA NA MISHAHARA HEWA
Daniel Mjema Dodoma na Fidelis Butahe
WABUNGE jana waliijia juu Serikali kwa matumizi mabaya ya fedha za umma na ufisadi ulijitokeza kwenye taasisi zake mbalimbali katika mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, mwaka jana.

Hasira za wabunge hao zilitokana na ripoti tatu za Kamati za Bunge; Mashirika ya Umma (POAC), Serikali za Mitaa (LAAC) na Hesabu za Serikali Kuu (PAC) kuonyesha upotevu wa mabilioni ya shilingi yaliyotumika katika nyanja mbalimbali ikiwemo mishahara hewa na mikataba mibovu.

Mbunge wa Longido (CCM), Michael Laizer alisema ni aibu kila mwaka kuwa na ripoti za wizi wa mali za umma lakini Serikali inakaa kimya.

Alisema katika Halmashauri ya Wilaya ya Longido, mmoja wa maofisa wake aliidhinisha Sh11 milioni kwa ajili ya matengenezo ya gari. “Labda Serikali imechoka sasa inafanya makusudi fedha za wananchi zinaliwa lakini yenyewe inakaa kimya. Serikali itujibu hizi fedha zinazopitishwa kila mwaka zinakwenda wapi?” alihoji Laizer

Mbunge wa Viti Maalumu (CUF), Magdalena Sakaya alisema Serikali inapaswa kuona aibu kwa kutekeleza pendekezo moja tu kati ya 12 yaliyotolewa na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita.

Alihoji suala la mishahara hewa kuendelea kujitokeza huku Serikali ikikaa kimya na kila mwaka CAG anatoa ripoti yake… “Kuna vitabu vya halmashauri za wilaya ambavyo CAG hakuvikagua kwa kuwa havikuonekana vilipo, sasa hapo tunakwenda wapi? Kuna Sh8 bilioni hazikufika katika halmashauri husika zimekwenda wapi? Wabunge tunatakiwa kuhoji na kupewa majibu sahihi.”

Mbunge wa Arumeru Mashariki (Chadema), Joshua Nassari alisema sasa Tanzania imekuwa kama Saccos kwa kuwa fedha za umma zinatafunwa bila utaratibu huku vielelezo vikitoweka kusikojulikana.

“Wakati wa uchaguzi wa wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki, mawaziri walijaa bungeni ila sasa tunajadili hatima ya Watanzania hawaonekani. Wabunge tuwe kitu kimoja tuibane Serikali itueleze hizi fedha zimekwenda wapi?” alisema Nassari.

Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Ester Bulaya alisema chama tawala kisipokuwa makini katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kitahukumiwa na vijana.

“Serikali ndiyo chanzo cha fedha kutafunwa… inakuwaje Naibu Waziri wa Maji anasimama na kuahidi mambo mengi wakati anajua wazi kuwa fedha za kutekeleza miradi hazipo?” alihoji.

Alisema mwaka 2015, utakuwa mgumu kwa CCM kwa kuwa wakati huo vijana watakuwa asilimia 85 na wanaweza kukinyima kura kutokana na Serikali yake kushindwa kusimamia masuala ya msingi ya maendeleo.

Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee aliwataka wabunge kuacha kulalamika kwa kuwa wao ndiyo wenye rungu la kuishikisha adabu Serikali: “Tukilalamika wananchi waliotuchagua nao watatushangaa kwa kuwa wametutuma kuwawakilisha na si kulalamika.”

Alisema umefikia wakati wa wabunge kuweka itikadi za vyama vyao pembeni na kuwashughulikia mawaziri wa wizara husika ambazo zinaonekana kuwa tatizo.

Mbunge wa Mwibara (CCM), Alphaxard Lugola alimlipua Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo akisema alihusika katika uuzaji wa mali ya Serikali katika Kiwanja namba 10 Barabara ya Nyerere na kwamba anaingilia utendaji wa mashirika ya Serikali.

Alisema kuwa kiwanja hicho awali, ilikuwa kiuzwe kwa Shirika la Tanzania Motors chini ya Kampuni ya Mashirika Hodhi ya Umma (CHC) kwa Sh1.3 bilioni lakini baadaye Mkurugenzi Mkuu wa CHC alipewa barua kusitisha uuzwaji wa jengo hilo na kumtaka kuitisha mazungumzo upya na Morad Sadik, ambaye alikuwa akitaka kununua eneo hilo awali.

“Inakuwaje wizara inaingia utendaji wa taasisi au kampuni zilizopo chini yake?” alihoji.

Awali, baada ya Kipindi cha Maswali na Majibu, Wenyeviti wa Kamati hizo za Bunge; Zitto Kabwe (POAC), John Cheyo (PAC) na Augustine Mrema (LAAC), waliwasilisha ripoti za kamati zao zinazoonyesha kukithiri kwa vitendo vya ufisadi serikalini na matumizi mabaya ya fedha za umma.

Kamati ya PAC
Cheyo alisema kamati yake imebaini kuwapo kwa matumizi ambayo hayakupitishwa na Bunge na kutaja Maonyesho ya Sabasaba, Nanenane na Utumishi kama sehemu ambako fedha hizo zilitumika.

Alisema mwaka 2009/2010 Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, ilitumia fedha za matumizi ya jumla ya Sh1.10 bilioni kwa ajili ya Maonyesho ya Nanenane ambazo hazikuwamo kwenye bajeti iliyopitishwa na Bunge.

Alisema hata matumizi ya Sh21.63 bilioni zilizotumika kuendesha Mfuko wa Kukwamua Wananchi kiuchumi maarufu kama ‘mabilioni ya JK’ hazikuwapo katika bajeti iliyopitishwa na Bunge. Alipendekeza kuwa ili kuondoa hali hiyo, mfuko huo unatakiwa kuwa na mtu au taasisi ya kuusimamia badala ya kuachwa bila usimamizi.

Alisema kuwepo kwa udanganyifu na ukwepaji kodi kumeisababishia Serikali hasara ya Sh15.4 bilioni na Dola 2.6 milioni za Marekani.

Alisema Wizara ya Maliasili na Utalii na ilipoteza Sh874,853,564 baada ya kufanya uamuzi wa upendeleo wa kutoa kiwango cha chini cha mrabaha kwa mazao ya misitu.
  
Kuhusu magari ya Serikali, Cheyo alisema kumekuwa na matumizi yasiyo ya lazima katika uendeshaji na ukarabati wa magari hayo. Hadi Juni 30, 2010 Serikali ilikuwa inamiliki magari yenye thamani ya Sh5 trilioni.

Alisema mwendelezo wa ununuzi wa magari unaofanywa na Serikali unaongeza gharama za uendeshaji na kusisitiza kwamba matumizi hayo si ya lazima kwa Serikali yenye uchumi mdogo uliozidiwa na madeni.

Kuhusu ukaguzi wa magari uliofanywa na wakala chini ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS), PAC imependekeza kuwajibishwa kwa ofisa masuuli wa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kuisababishia Serikali hasara ya Dola 18,343,540 za Marekani ambazo ni karibu Sh30 bilioni na kusisitiza: “Sh30 bilioni zilitumika kufanyia ukaguzi wa magari ambao haukuwepo.”

Alisema pia wamegundua kuwa Serikali inatumia fedha nyingi kwa ajili ya kukodi majengo ya wizara na kusisitiza kuwa moja inaweza kulipa kodi ya Sh485 milioni.

Alisema kuna watumishi hewa takriban 3,000 na kwamba Serikali haifahamu lolote kuhusu hali hiyo… “Kuna Sh1.8 bilioni ambazo hutumiwa na Serikali kwa ajili ya kulipa watumishi hewa. Pia imebainika kuwa Serikali haijui thamani ya majengo yake yaliyopo ndani na nje ya nchi.”

POAC

Zitto kwa upande wake, alielezea maeneo yenye matatizo sugu ya matumizi ya fedha ambayo yanahusisha ukiukwaji mkubwa wa Sheria ya Ununuzi wa Umma na kanuni zake.

Alitola mfano wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), ambalo kwa mwaka mmoja wa fedha linafanya ununuzi wenye thamani ya kati ya Sh300 bilioni hadi Sh600 bilioni.

Alisema kwa mwaka wa fedha 2009/2010, Tanesco  ililitumia Sh1.8 bilioni ukilinganisha na Sh65 milioni zilizokuwa zimepangwa katika bajeti ya ukarabati wa gati mojawapo katika Kituo cha Bwawa la Mtera. 

“Ongezeko hilo la gharama za ununuzi kwa ajili ya ukarabati, ni kiasi kikubwa na Kamati haikuridhika na majibu ya menejimenti hivyo kuagiza uchunguzi wa ndani ili kubaini uhalisia wa ununuzi huo,”alisema na kuongeza:

“Tumependekeza Tanesco ianze kutumia vyanzo vyake vya umeme na iache kununua umeme hasa wa kampuni ya IPTL kwani inatumia Sh62.4 kununua umeme katika kampuni hii kwa mwaka.”
  
Alisema Chuo Kikuu Kishiriki cha Mkwawa (MUCE) kilishindwa kuthibitisha kwa wakaguzi wa hesabu uwepo wa vifaa vya maabara vilivyonunuliwa ambavyo vina thamani ya Sh267 millioni.

Katika ripoti hiyo, Zitto alisema imebainika pia mkataba kati ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), na Kampuni ya Startimes unatakiwa kupitiwa upya ili uinufaishe TBC.

Pia aliugusia matumizi mabaya ya fedha katika Bodi ya Pamba ambako alisema kuwa kiasi cha Sh2 bilioni zilizotolewa na Serikali hazijulikani zilipo na wala hazikuwafikia wakulima wa zao hilo.

LAAC

Kwa upande wake, Mrema aliitaka Serikali ivunje mtandao wa wezi wa mali za umma na kuhoji inakuwaje inawakumbatia mafisadi?
Alihoji majalada ya watuhumiwa wa ufisadi kukaa zaidi ya miaka 10 katika Ofisi za Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka (DPP) na ile ya Makosa ya Jinai (DCI) wakati kesi za uchaguzi zimewekewa kikomo.

Alisema ripoti ya CAG kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2010, inaonyesha kuwa Sh583.2 milioni zililipwa kama mishahara hewa kiasi ambacho alisema kingetosha kujenga madarasa 194.

Mrema alisema katika ripoti hiyo, imebainika kwamba Sh8 bilioni zilitumika katika ununuzi usiokuwa na nyaraka na ama wenye nyaraka pungufu hali inayoashiria kuwapo kwa wizi.

Aliwataja watumishi wa Halmashauri ya Kishapu akisema ni vinara wa ubadhirifu wa Sh6 bilioni na kudai kuwa walishirikiana na baadhi ya watumishi wa Benki ya NMB Tawi la Manonga, Shinyanga kuiba fedha hizo za umma.

Aliwataja watumishi hao kuwa ni Mweka Hazina, Muhdin Mohamed, Mtunza Fedha wa Halmashauri hiyo, Walugu Mussa, Boniface Nkumiming na Mhandisi wa Halmashauri, Leonard Mashamba.

Alisema fedha hizo zilitafunwa kwa kutumia nyaraka feki, uhamisho wa fedha bila idhini na kuzitumia kinyume cha malengo, uhamisho wa fedha ambao haukufika kwenye akaunti husika na malipo kwa walipaji wasiofahamika.

Mrema aliilaumu Serikali kwa kuwahamisha kutoka halmashauri moja kwenda nyingine na Serikali Kuu, watumishi wanaotuhumiwa kwa ufisadi badala ya kuwachukulia hatua za kisheria.

Kamati hiyo imependekeza Bunge likubali kuitaka Serikali kutoa maelezo ya kuridhisha ni kwa nini ubadhirifu huo umeachwa ukishamiri kwa miaka mitatu mfululizo bila wahusika waliotajwa na CAG kuchukuliwa hatua.

“Shida iliyopo hapa ni Serikali kuonekana inawakumbatia wahusika kwa kisingizio cha uchunguzi unaendelea… nini kinachochunguzwa badala ya kupeleka watu mahakamani na kumuita CAG kama shahidi?”


CHANZO: Mwananchi

6 Mar 2012

Usiniite mnafiki,au mpindisha maneno.Uthibitisho kuwa hata Rais Jakaya Kikwete hana imani na TAKUKURU upo katika habari ifuatayo (ANGALIA MAANDISHI MEKUNDU)


Rungu la Kikwete lilimwokoa Siyoi
Monday, 05 March 2012 09:17

Rais Jakaya Kikwete
NAPE, WASSIRA WADAIWA KUSIMAMA KIDETE ATOSWE, JK AKATUMIA 'RUNGU' KUZIMA HOJA,WABUNGE WOTE CHADEMA KUHAMIA ARUMERU
Joseph Zablon, Dar na Moses Mashalla, Arusha 

USHINDI wa Siyoi Sumari kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki, unadaiwa kuitesa Kamati Kuu (CC) ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kukuna vichwa kuhusu mbinu na mikakati ya kutengua ushindi alioupata katika duru ya pili dhidi ya William Sarakikya.

Katika Mkutano Mkuu wa jimbo hilo uliofanyika, Februari 20 ulimchagua Siyoi ambaye ni mtoto wa aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, marehemu Jeremiah Sumari kwa kura 361, akifuatiwa na Sarakikya aliyepata kura 259. Hata hivyo, CC ya CCM iliyoketi Februari 27, iliagiza kurejewa kwa upigaji kura kati ya wagombea hao.
Katika duru hilo la pili la uchaguzi uliofanyika Machi Mosi mwaka huu, Siyoi alipata ushindi wa kishindo wa kura 761 na kumtupa mbali mpinzani wake, Sarakikya aliyepata kura 361. 

Juzi katika kikao hicho cha CC, ushindi huo wa mara ya pili wa  Siyoi uliipasua tena kamati hiyo kuu yenye mamlaka ya juu ya uamuzi ndani ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kudaiwa kutaka atoswe na apitishwe Sarakikya kutokana na tuhuma za matumizi makubwa ya fedha wakati wa kampeni.

Vyanzo vya habari vya kuaminika kutoka katika kikao hicho cha CC, vilifafanua kwamba waliosimama kidete kutaka Siyoi atoswe ni Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Nape alipinga Siyoi kurejeshwa akizingatia matukio mbalimbali ya tuhuma za matumizi makubwa ya fedha yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya watu ili wamchague mgombea huyo, kitu ambacho hakikupaswa kuvumiliwa. 

Hoja hiyo ya Nape iliungwa mkono na Wassira ambaye naye alitaka Siyoi atoswe kutokana na tuhuma hizo za matumizi makubwa ya fedha kutoka kwa baadhi ya wapambe wake waliotaka mgombea huyo achaguliwe.


Lakini inadaiwa kuwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete alisema kikao hicho kisingeweza kumkata Sumari kwa sababu tu ya tuhuma hizo za rushwa zilitolewa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), mkoani humo.


Chanzo kingine kilimnukuu mwenyekiti huyo akisema kwamba, Arusha ni mkoa wenye siasa za aina yake hivyo ni muhimu kuwa makini kwani siku za nyuma kuliwahi kuibuka tuhuma za rushwa kwa wabunge wa CCM kukamatwa lakini, mahakama ikawaachia huru.

Chanzo hicho kiliongeza kwamba, Rais Kikwete alisisitiza kuwa hata tuhuma za rushwa zilizotolewa zilikuwa zikigusa wengine kwani iliwahi kupendekezwa kwamba Elishalia Kaaya ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC), ndiye apitishwe na wengine wang'olewe. 

Katika kikao hicho, Rais Kikwete pia alinukuliwa akihoji kuwa endapo Siyoi angekatwa jina kungekuwa na uhakika wa chama kushinda kwa kumsimamisha Sarakikya? Hakupata jibu kama mgombea huyo wa pili angeweza kushinda kiti hicho.

Hata hivyo, chanzo hicho kilisema baada ya mwenyekiti kutumia rungu kumpitisha Siyoi alimpa angalizo: “Basi na wewe usiende kutamba huko mitaani kwamba umeangusha watu, fanya kampeni, ushinde jimbo tuangalie mambo mengine mbele.”

Ilielezwa zaidi kwamba Rais Kikwete aliungwa mkono na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, aliyeeleza kuwa haoni sababu ya kumwondoa Siyoi katika kinyang'anyiro hicho kwani ushindi wake ulikuwa mkubwa. 


Chanzo na Kwa habari Kamili: Mwananchi

31 Dec 2011

Kikwete's smile says it all
Vyombo mbalimbali vya habari leo vimebeba picha ya Rais Jakaya Kikwete akiwa na Katibu Mkuu Kiongozi mpya,Balozi Ombeni Sefue na mtangulizi wake Philemon Luhanjo ambaye amestaafu.Sidhani kama kuna Mtanzania asiyefahamu uhusika wa Luhanjo katika sakata la ufisadi uliofanywa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini,David Jairo.Bunge lilishamshauri Kikwete awawajibishe wahusika wote wa ufisadi huo,ikiwa ni pamoja na Jairo na Luhanjo.

Lakini kama ilivyokuwa katika sakata la ufisadi wa Richmond ambapo Bunge lilishauri wahusika wachukuliwe hatua,lakini tukaishia kuona watu kama aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Johnstone Mwanyika walistaafu kwa heshima (bila kusahau marupurupu ya kustaafu),Kikwete amerejea tena udhaifu wake kwa kumwogopa Luhanjo na hatimaye kumwokoa kwa kumruhusu astaafu badala ya kumwadhibu kwa ufisadi wake na Jairo.

Kwa vile leo ni siku ya mwisho kwa mwaka huu 2011,picha ya Kikwete na Luhanjo ni kama kuwakumbusha Watanzania jinsi Rais wao alivyo dhaifu na mbabaishaji wa hali ya juu katika kushughulikia ufisadi.Na japo wengi wenu mtajipa matimaini kuwa mwaka 2012 utakuwa wa matumaini,ukweli mchungu ni kwamba kwa mwenendo huu wa Kikwete kuwaogopa na kuwalea mafisadi,viumbe hao hatari watazidi kuzaliana kwani wanajua fika hakuna wa kuwadhibiti au kuwaadhibu.

Samahani Mheshimiwa Rais,lakini uzembe wako katika kuwashughulikia mafisadi ni sawa na tusi kwa taasisi takatifu ya Urais.Ni lini utaamka na kuyatumia madaraka yako ipasavyo kupambana na ufisadi?

Salama zangu za mwaka mpya kwako si za kupendeza kwani namwomba Mungu aharakishe siku ili umalize muhula wako na ubaki historia isiyo na manufaa kwa Watanzania.Can't wait to see you gone!

10 May 2011



Kwa walioamini usanii wa CCM kuwa imeamua kujivua magamba wahesabu wameliwa.Sio tu ukweli kwamba joka linalojivua magamba linakuwa hatari zaidi bali pia ufahamu wetu wengi kuwa joka likijivua magamba haligeuki kuwa mjusi.Na kama baadhi ya wanasiasa wa upinzani walivyoelezea suala hilo la magamba,tatizo la CCM ni mithili ya kansa ya damu.Dawa yake pekee ni kifo,and sure will CCM die,sio kwa vile kimezeeka vibaya bali kwa sababu ni mkusanyiko wa walafi,waroho,majambazi,matapeli na mabazazi wa kisiasa.Putting it bluntly,ushirika wa wachawi kamwe hauwezi kudumu.Let's wait and see!

VIONGOZI wakuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wameshindwa kuwaondoa katika chama hicho wale wanaowaita watuhumiwa wakuu wa ufisadi nchini, imefahamika.

Viongozi ambao waliotajwa kuwa wanatakiwa kujiondoa kwenye uongozi au chama ndani ya siku 90 kwa kuwa ni “mafisadi wanaochafua sura ya chama mbele ya jamii,” ni Edward Lowassa, Rostam Aziz na Andrew Chenge.

Kinyume na majigambo ya viongozi wa juu wa chama hicho, kuwa sharti watuhumiwa hao waondolewe kwenye vikao vya maamuzi, hadi sasa chama kimeshindwa kuwapa barua za kuwajulisha juu ya suala hilo.

Katibu Mkuu Wilson Mukama, katibu wa itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara, John Chiligati wamekuwa wakishindilia kuwa “mafisadi lazima waondoke.”

Hata hivyo, Mukama aliwaambia waandishi wa habari juzi Jumatatu, jijini Dar es Salaam, “…hakuna mahali popote katika maazimio ya NEC panapotaja siku 90.”

Alisema, “Kama ni muda basi ni pale mwenyekiti wetu aliposema NEC ijayo. NEC hukutana kila baada ya miezi minne na kwa hiyo kama ni siku, basi ni 120 na siyo 90,” alieleza Mukama akijibu swali la mmoja wa waandishi waliotaka kufahamu ni lini chama hicho kitaandika barua na kukabidhi watuhumiwa.

Kauli ya Mukama kwamba hakuna mahali ambapo NEC imeagiza Lowassa, Rostam na Chenge waondoke ndani ya chama katika muda wa siku 90 zijazo, imekuja wiki moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kukutana kwa faragha na Lowassa.

Taarifa za ndani ya chama na kutoka baadhi ya viongozi wa CCM, zinasema mazungumzo ya viongozi hao wawili yalijikita katika kile kilichoitwa “kujivua gamba” na kwamba Lowassa anamtuhumu Nape kusambaratisha chama chao kwa kuendeleza tuhuma katika mikutano ya hadhara.

Lowassa na Kikwete walikutana ikulu jijini Dar es Salaam, 25 Aprili 2011 baada ya kushindwa kukutana mjini Dodoma, 3 Aprili 2011 kama ambavyo Kikwete alikuwa ameahidi.

Katika mkutano wake na wahariri wa vyombo vya habari, Mukama alisema, “NEC ilitoka na maazimio 26. Azimio mojawapo linasema chama kiendelee na mapambano yake dhidi ya ufisadi na kwamba watuhumiwa wakitafakari, wajipime na kuchukua hatua.”

Alisema, “Sehemu ya hotuba ya mwenyekiti wakati akifunga mkutano ilisema tunatambua athari ya kukosekana maadili katika chama na tuendelee kupambana; na katika hili hakuna ajizi. Viongozi wanaotuhumiwa kwa ufisadi wajitafakari, wajipime na wachukue hatua,” alisema Mukama akinukuu kauli ya mweneykiti wa CCM, Rais Kikwete.

Alipoulizwa ni watuhumiwa gani wa ufisadi kwa kuwa chama hicho hakijawahi kuwa na orodha yake, badala yake orodha inayofahamika kwa wengi ni ile iliyotolewa na kiongozi mkuu wa upinzani nchini, Dk. Willibrod Slaa, Mukama alisema, “…CCM ni taasisi kubwa yenye mfumo wake na miongozo yake; hivyo haitegemei orodha ya CHADEMA.”

Mukama alikuwa akijibu swali la Manyerere Jackton wa New Habari House. Alitaka kufahamu vigezo vinavyotumika kutambua mafisadi; na iwapo wataweza kumwondoa Kikwete ndani ya chama hicho kwa vile naye ametajwa katika orodha ya Dk. Slaa ya tarehe 15 Septemba 2007.

Hata hivyo Mukama aliendelea kushikilia kuwa chama chake hakiwezi kufuata orodha za vyama vingine, hasa CHADEMA.

Kwa upande mwingine Lowassa amenukuliwa akimtaka Kikwete kumdhibiti Nape kwa kuwa “anakivuruga chama” kwa hatua yake ya kusisitiza kuwa NEC ilipitisha maamuzi ya kuwataka wajiuzulu, wakati akijua fika kwamba hilo si kweli.

“Mkutano kati ya Lowassa na rais ulikuwa mfupi sana. Lowassa alimueleza Bwana Mkubwa (rais Kikwete), jinsi asivyofurahishwa na mwenendo wa Nape hasa jinsi anavyowatuhumu ufisadi. Alimsihi Rais Kikwete kumweleza hilo katibu wake mwenezi, Nape…,” ameeleza mtoa taarifa.

Kikwete, taarifa zinasema, alimhakikishia Lowassa kuwa “…hakuna lolote litakalotokea,” kauli ambayo imethibitishwa na Mukama katika mazungumzo yake na wahariri.

“Yule bwana (Lowassa) alimuuliza Kikwete, mnataka kunipa barua kwa kosa lipi? Nimefanya nini? Nini ambacho wewe hukifahamu,” anasema mtoa taarifa wa MwanaHALISI.

Gazeti hili limejulishwa na vyanzo vyake vya ndani ya serikali kuwa uamuzi wowote utakaochukuliwa na Lowassa, unaweza kuzidisha mgawanyiko ndani ya CCM.

Mara baada ya Lowassa kukutana na Kikwete, taarifa zinasema mbunge huyo wa Monduli alikutana na kufanya mazungumzo marefu na Peter Kisumo, mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya chama hicho.

Katika mazungumzo yao, Lowassa alionya kuwa CCM kiko hatarini kupasuka kutokana na kauli za Nape na mwenzake John Chiligati juu ya ufisadi na watuhumiwa wake.

“Huyu bwana anaua chama. Nakuhakikishia mzee Kisumo, hawa watu wakiendelea kunishutumu bila sababu, nitatoka hadharani na kujibu mapigo,” anaeleza mtoa taarifa akimnukuu Lowassa katika mazungumzo yake na Kisumo.

Naye Kisumo anaripotiwa kumhoji Lowassa, “Mbona ninyi marafiki wawili mnataka kusambaratisha chama?” Naye Lowassa alijibu, “Kheri iwe hivyo…”

Mwandishi wa gazeti hili alimtafuta Lowassa ili kuthibitisha walichojadili na Kikwete, lakini simu yake iliita bila kupokelewa.



8 Jan 2011







Mbunge wa zamani kutoka chama cha Labour hapa Uingereza,David Chaytor (pichani juu),leo amelala usiku wa kwanza akiwa jela kama mfungwa baada ya kuhukumiwa kifungo cha miezi 18 kutokana na kukutwa na hatia ya ubadhirifu wa fedha za umma takriban pauni 20,000 (takriban shilingi 45 milioni za Tanzania).Ubadhirifu wa fedha hizo za umma ni kutokana na matumizi mabaya ya fedha za posho kwa wabunge.


Wakati hayo yakijiri hapa,huko nyumbani Waziri wa Nishati na Madini,William Ngeleja alivunja mzizi wa fitina kwa kutangaza hadharani kuwa hatimaye serikali italipa shilingi 95,000,000,000 (bilioni tisini na tano) kwa kampuni ya kifisadi ya Dowans kufuatia hukumu ya kiini macho iliyotoa ushindi kwa kampuni hiyo licha ya rundo la utata linaloendelea kuizunguka.



Ngeleja,bila haya wala uoga,alieleza kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (Frederick Werema) ameridhia hukumu hiyo ya miujiza kabisa na ushauri wake wa kitaalam (ya sheria) ni kuilipa kampuni hiyo.

Wote,Ngeleja na Werema ni wateuliwa wa Rais Jakaya Kikwete,ambaye kwa makusudi kabisa aliepuka kuzungumzia suala la Dowans katika hotuba yake ya kukaribisha mwaka mpya 2011.Ni dhahiri kuwa Kikwete ameridhia Dowans ilipwe na ndio maana Ngeleja na Werema wanatoa maamuzi yao bila hofu wala aibu. Na kama umesahau,ni Kikwete huyuhuyu aliyeahidi wakati wa kampeni zake kuwa ana dhamira ya kuboresha maisha ya Watanzania.Nadhani labda alichomaanisha ni kuboresha akaunti za mafisadi kwa mgongo wa walalahoi.

Napata shida kutumia lugha ya kistaarabu kushangazwa na uwendawazimu huu!Hivi hawa viongozi wetu wamerogwa na mafisadi au ni matokeo ya kupokea fadhila za mafisadi kupita kiasi kwamba sasa wanalazimika kulipa fadhila hizo kwa gharama yoyote ile?Hizi sio tamaa za kawaida tulizozowea kuziona kwa watawala wetu.Hiki ni kichaa hatari ambacho pasipo hatua za haraka kinaweza kupelekea nchi nzima kuuzwa,kisha akina Werema wakaja kutuambia gharama za kuzuia kuuzwa kwa nchi yetu ni kubwa kuliko uamuzi wa kukubali nchi iuzwe.

Blogu hii ilifanya kila ilichoweza kuhamasisha wapiga kura waiepuke CCM na mgombea wake Kikwete.Sio kwamba blogu hii ilifanya utafiti wa kina kubaini athari za kuirejesha CCM madarakani bali taarifa kuhusu uhuni wa chama hicho,sambamba na kilivyojipa jukumu la kuwa kichaka cha kuhifadhi mafisadi,zilikuwa bayana kwa kila mwenye macho.Hivi kuna Mtanzania asiyefahamu kuwa ujio wa kampuni ya kijambazi ya Richmond (iliyopelekea ujambazi mwingine wa Dowans) ulikuwa na baraka za Kikwete pamoja na swahiba wake Lowassa na "kubwa la maadui" Rostam Aziz?





Ndio maana majuzi baada ya aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema,Dkt Wilbroad Slaa,kurejea kauli yake kuwa Kikwete ni mmiliki wa Dowans,hasira za mkuu huyo zikaishia kwa kuamuru polisi wake kutoa kipigo kwa raia wasio na hatia huko Arusha na kupelekea vifo kadhaa (Polisi wanadai wameua watu watatu tu lakini tangu lini wauaji wakaaminika?).


Na kama adhabu ya Kikwete kwa Chadema na wana-Arusha haijatosha,kaamua kuwadhihaki Watanzania wote kwa kuidhinisha Dowans ilipwe mabilioni hayo,huku swahiba wake Rostam akidhihaki Watanzania kwa kudai hizo bilioni kadhaa ni fedha kiduchu tu kwake.Huwezi kumlaumu kwani kaiweka serikali mfukoni na anaendesha nchi kwa remote control.

Blogu hii iliwaasa wapiga kura kuhusu madhara ya kumpatia Kikwete miaka mitano mingine baada ya awamu yake ya kwanza kugubikwa na ufisadi wa kutisha.Lakini hata kwa viwango vilivyozoeleka vya ufisadi hakuna aliyetarajia kuwa hata kabla miezi mitatu haijapita tangu arejee madarakani,Kikwete angediriki kuruhusu Watanzania wenzie wabakwe kiuchumi kwa mtindo huu wa Dowans.Lakini kwa vile Katiba tuliyonayo inampa madaraka mithili ya mungu-mtu,na kwa vile anafahamu fika kuwa Watanzania ni wepesi wa kusahau na ndio maana wengi wao wakampigia kura licha ya maumivu aliyowasababishia tangu aingie madarakani Desemba 2005,ameruhusu ujambazi huu wa mabilioni ya fedha za walipa kodi pasi soni.

Tusipochukua hatua za haraka tutashtukia tumefikishwa mahala ambapo hatutokuwa na namna ya kurekebisha mambo.Kama less than three months tangu Kikwete arejee madarakani tumeshashuhudia Dowans ikizawadiwa mabilioni kama asante ya kututapeli,na tumeona hasira za Kikwete kwa ukatili na mauaji yaliyofanywa na polisi wake (kisa kasutwa kuwa analea ufisadi),ni wazi kuwa hali itazidi kuwa mbaya na yawezekana ikawa ya kutisha kabla Kikwete hajamaliza muda wake hapo 2015 (assuming hatachakachua Katiba kutaka aongezewe muda).

Moja ya hatua inayoweza kuzaa matunda ni kufikisha kilio chetu kwa nchi wahisani.In addition to malezi anayotoa Kikwete kwa mafisadi,sasa tuna jambo jingine zito ambalo linaweza kuvuta hisia za wahisani,nalo ni ukiukwaji wa haki za binadamu kama ilivyodhihirika huko Arusha.



Kwa kuanzia,blogu hii inamwomba kila mzalendo anayeishi katika nchi mfadhili kwa Tanzania,kuwasiliana na mbunge wake na kumwomba afikishe kilio cha wanyonge wa Tanzania.Toa chapa ya picha za matukio ya Arusha pamoja na habari zinazobainisha ukiukwaji wa haki za binadamu,na ufisadi,kisha mfahamishe mbunge huyo kuwa hii ndio hali halisi ya Tanzania chini ya utawala wa Kikwete.Kama utahitaji maelezo zaidi ya namna ya kuwasilisha ujumbe wako kwa mbunge wa sehemu unayoishi,usisite kuwasiliana nami.

KWA USHIRIKIANO WETU,TUNAWEZA KUPAMBANA NA UTAWALA DHALIMU AMBAO LICHA YA KUUA RAIA WASIO NA HATIA HUKO ARUSHA,UNATOA ZAWADI YA SHILINGI BILIONI 95 KWA DOWANS KANA KWAMBA HIYO NDIO RAMBIRAMBI KWA WALIOUAWA NA POLISI HUKO ARUSHA.

5 Jan 2011

Picha Hii Inatoa Maelezo Alfu Kidogo.Ukiangalia kwa Makini Utamwona Rostam Kama Kalizimishwa Kuinua Mkono,huku Kikwete Akiwa as if Anampigia Debe Bosi Wake...na Tabasamu Juu!Lol,Ama Kweli Rais Tunaye,Si Mchezo

Dk. Slaa: Kikwete ajiuzulu
• Asisitiza anahusika na Dowans, aahidi kutoboa siri
na Janet Josiah

KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Wilibrod Slaa, sasa amekuja na hoja mpya ya kumtaka Rais Jakaya Kikwete ajiuzulu kutokana na kuhusika moja kwa moja na sakata la Dowans iliyorithi mikoba ya Richmond.

Dk. Slaa ametoa kauli hiyo nzito jana katika mahojiano maalumu na Tanzania Daima Jumatano, ikiwa ni siku moja baada ya Ikulu kutoa taarifa ya kejeli na vijembe vya mitaani dhidi yake kuhusu sakata hilo.

Akizungumza kwa utulivu na umakini mkubwa, Dk. Slaa alisema Rais Kikwete alipaswa kujiuzulu kabla ya aliyekuwa Waziri Mkuu na swahiba wake mkubwa, Edward Lowasa, kuchukua hatua hiyo Februari 7, mwaka 2008, mjini Dodoma.

Yaani Kikwete Mpaka Kaikamata Mic Kuhakikisha Kuwa Debe Analompigia Swahiba Wake ni La Nguvu Kweli Kweli!Kama Alivyowahi Kusema Lowassa,Wawili Hawa Hawakufahamiana Mtaani.Wametoka Mbali.BIRDS OF A FEATHER..
Mawaziri wengine waliojiuzulu kutokana na sakata la Richmond lililozua mjadala mkali nchini ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini wakati huo, Nazir Karamagi na Ibrahim Msabaha ambaye alikuwa waziri wa wizara hiyo kabla ya kuhamishiwa Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki (EAC).

Akitoa ufafanuzi wa taarifa ya Ikulu iliyotolewa juzi na Kurugenzi ya Mawasiliano, Dk. Slaa alisema mkuu huyo wa nchi hawezi kukwepa kuhusishwa na sakata la Dowans, kwani alilijua hata kabla mitambo yake haijaingizwa nchini.

"Nataka niwatoe Watanzania wasiwasi kwamba ingawa kurugenzi ya mawasiliano imetoa taarifa ya kumsafisha Rais Kikwete na kunikashifu mimi kwa lugha ya mtaani, nawaambia alipaswa kujiuzulu kabla na anatakiwa ajiuzulu sasa, kwani anahusika moja kwa moja na uingiaji wa mkataba wa Kampuni ya Richmond na baadaye na Dowans" alisema Dk. Slaa.

Alimtaka Rais Kikwete kutambua kuwa hawezi kukaa kimya kwa kisingizio cha kuhatarisha amani na utulivu wakati wananchi wanaibiwa mabilioni ya fedha na mafisadi wachache kupitia kampuni feki ya Dowans.

Akirejea historia ya vita dhidi ya ufisadi aliyoiasisi bungeni, Dk. Slaa aliwataka wananchi wakumbuke kuwa taifa lilipokumbwa na tatizo la umeme kabla ya mitambo ya Richmond kuingia nchini, Rais Kikwete alikwenda Marekani kwa ziara ya kikazi.

Alisema aliporejea nchini, alizungumza na waandishi wa habari kuhusu tatizo hilo na kuahidi kuwa serikali yake inalifanyia kazi na siku chache baadaye, rafiki yake wa karibu, Rostam Azizi, Mbunge wa Igunga (CCM), naye alikwenda Marekani.

"Rostam aliporejea kutoka Marekani baada ya siku chache tukaanza kusikia mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura kutoka Kampuni ya Richmond inatarajiwa kuwasili. Kweli ilitua nchini katika Uwanja wa Mwalimu Nyerere na shughuli nyingine zilifungwa uwanjani hapo kupisha ushushaji wa mitambo ya Richmond" alisema Dk. Slaa.

Kwanini Rostam Asiwe na Furaha?Kuendesha Nchi ya Watu Takriban Milioni 50 kwa Kutumia Remote Control si Jambo Dogo Ati!

Huku akisisitiza kuwa ana ushahidi wa anachokisema, Dk. Slaa alisema hata baada ya Richmond kushindwa kuzalisha umeme na kusababisha mawaziri kujiuzulu, serikali ya Kikwete iliamua kuingia mkataba na Dowans iliyorithi shughuli za Richmond na hatua hiyo Rais Kikwete pia aliijua.

"Dowans nayo ikashindwa kuzalisha umeme, mwisho Bunge katika moja ya maazimio yake liliridhia uamuzi wa kuvunja mkataba huo, lakini leo Serikali inadaiwa fidia ya sh bilioni 185, je, Rais Kikwete anaweza kukwepa kwamba hana mkono wake hapo?" alihoji.

Kutokana na hayo, Dk. Slaa alimtaka Rais Kikwete amtaje mmiliki halali wa Dowans ili kuwatoa kiu Watanzania wanaohitaji kumjua.

"Sitaacha kuzungumzia masuala yanayowagusa Watanzania na mali, hasa katika kipindi hiki ambacho Watanzania wanataka kuibiwa fedha zao, wakati wa kukaa kimya umekwisha" alisema Dk. Slaa.

Alisema hashangazwi na kejeli za Ikulu na kuwataka Watanzania kukumbuka alipoanza kuwalipua mafisadi, Rais Kikwete aliwahi kutamka kwamba kelele za mlango haziwezi kumnyima mwenye nyumba usingizi na kamwe kelele za chura hazimzuii ng ombe kunywa maji.

Kaaazi Kweli Kweli
"Lakini baada ya sisi kuamua kupambana na Richmond, Rais Kikwete alikiri linamnyima usingizi na hili la Dowans litamnyima usingizi zaidi katika kipindi hiki cha mwisho cha uongozi wake" alisema Dk. Slaa.

Ili kumaliza kelele za Dowans, Dk. Slaa alimtaka Rais Kikwete kumtaja mmiliki wake ambaye anataka kuwaibia Watanzania mabilioni ya fedha.


 
Wakati Dk. Slaa akimkaba koo Rais Kikwete, mjadala wa Dowans hivi sasa umewavuruga hata viongozi wa serikali tangu ilipoamriwa ilipwe sh bilioni 185.

Aliyekuwa Spika wa Bunge lililopita, Samuel Sitta, hivi karibuni alikaririwa akiitaka serikali iache kuilipa Dowans kwa madai kuwa ni mradi wa mafisadi watatu.

Kauli hiyo ilipingwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye alisema kuwa suala la malipo ya Dowans lipo kisheria na ikithibitika serikali haiwezi kukata rufaa, italazimika kulipa mabilioni hayo.

Juzi Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu imeelezea kukerwa kwake na hatua ya Dk. Slaa kumtaja Rais Kikwete kuwa alihusika katika uzembe uliosababisha taifa kutakiwa kuilipa Kampuni ya Dowans sh bilioni 185 kama fidia.

Taarifa hiyo kali ya Ikulu iliyobeba ujumbe wenye maneno ya kebehi na ya mitaani ya kumwita Dk. Slaa mtu aliyechanganyikiwa na mzabinazabina ilisainiwa na Salvatory Rweyemamu, ambaye kabla ya kwenda Ikulu alikuwa mmoja wa wahariri watendaji, aliyekuwa akiheshimika kwa kutumia lugha fasaha na ya staha.

Rweyemamu katika taarifa yake hiyo iliyoonyesha waziwazi kuandikwa na mtu mwenye hasira, chuki na dharau ama kwa Dk. Slaa, CHADEMA na Tanzania Daima, alikwenda mbali na kumwita kiongozi huyo wa kisiasa kuwa ni mtu hatari.

Katika mahojiano maalumu na gazeti la Tanzania Daima Jumapili, mwishoni mwa wiki, Dk. Slaa alikaririwa akisema chanzo cha suala la Dowans kutakiwa kulipwa fidia limetokana na uzembe wa serikali na Rais Kikwete mwenyewe anahusika kuileta Kampuni ya Richmond ambayo baada ya kuonekana ya kitapeli iliamua kurithisha kazi zake kwa Dowans.

VYANZO: Habari kwa Mujibu wa Tanzania Daima.Picha Kutoka Vyanzo Mbalimbali Mtandaoni.

29 Dec 2010



Takriban kila jambo kinaweza kutizamwa kwa sura mbili,au zaidi,hasa kwa minajili ya kuangalia faida na hasara.Ni katika mantiki hiyo,baadhi yetu tunaweza kuthubutu kuangalia "upande wa pili wa shilingi" kuhusu umoja wa Watanzania.Naomba nisisitize kuwa hoja hapa sio kudharau jitihada za waasisi wa taifa letu waliofanya kazi kubwa kujenga mshikamano miongoni mwa makabila zaidi ya 120 na kuzaa Utanzania uliogubika ukabila,udini,nk (angalau kwa kipindi kirefu cha uhai wa Tanzania).

Lakini moja ya athari zinazosababishwa na umoja huo ni uwezekano wa watu wasio na damu ya Kitanzania kujificha kwenye kivuli hicho cha "umoja wetu".Na ukichanganya na udhaifu,let alone ufisadi uliokubuhu,wa Idara ya Uhamiaji,yayumkinika kuamini tuna "Watanzania wenzetu" kadhaa tu ambao kimsingi hawapaswi kuwepo nchini mwetu.Kadhalika,kwa vile teuzi zinazofanywa na Rais Jakaya Kikwete (kama ilivyokuwa enzi za Mwinyi na baadaye Mkapa) hazizingatii kujiridhisha kuhusu u-Tanzania halisi ( as opposed to u-Tanzania wa kufoji), baadhi ya viongozi wanaoteuliwa kushika nyadhifa nyeti wanaweza kabisa kuwa sio Watanzania.

Kuongeza ugumu katika suala hilo la u-Tanzania ni makabila ambayo yametapakaa zaidi ya mipaka ya nchi.Hapa nazungumzia makabila ambayo yapo zaidi ya nchi moja.Kwa mfano,Kenya kuna Wamasai,Wameru,Wajaluo,nk kama ilivyo Tanzania.Simaanishi kila Mtanzania anayetoka katika makabila ya aina hiyo anaweza kuwa na utata katika u-Tanzania wake bali kilicho wazi ni ukweli kwamba ni rahisi kwa asiye Mtanzania (lakini anatoka kabila kama la Kitanzania) kujificha nchini ndani ya kivuli cha umoja wetu.

Tutamtambuaje mtu wa aina hiyo?MATENDO YAKE (including KAULI zake).Na ni katika mstari huo wa fikra nimefika mahali nikalazimika kujiuliza iwapo Mwanasheria Mkuu wa Serikali,Jaji Werema ni Mtanzania kweli au ni walewale wanaotumia umoja wa Tanzania (licha ya wingi wa makabila)+udhaifu na ufisadi Idara ya Uhamiaji,kuwepo Tanzania isivyo halali,na kupewa madaraka makubwa pasipo watoa madaraka hayo kujiridhisha kuhusu u-Tanzania wa mteuliwa.

Simtuhumu Werema kuwa si Mtanzania kwani sina nyaraka za kuthibitisha hilo.Hata hivyo,nalazimika kupata hisia za walakini katika u-Tanzania wake kutokana na mlolongo wa kauli zake za kihuni na zisizoendana na wadhifa mkubwa aliokabidhiwa.Wakati takriban kila Mtanzania halisi anazungumzia umuhimu wa Katiba mpya,mbabaishaji Werema akakurupuka na kudai hakuna haja ya Katiba mpya (kana kwamba Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyesema atashughulikia suala hilo ni mdogo kimadaraka kwa Werema).

Mpuuzi huyu ambaye ni dhahiri kuteuliwa kwake tena kuwa Mwanasheria Mkuu kunathibitisha matatizo makubwa ya kimaamuzi yanayomwathiri Rais Kikwete alifikia hatua ya kusifia rushwa ndani ya CCM kuwa ni sehemu ya demokrasia (rejea gazeti la Uhuru,Agosti 6,2010 habari yenye kichwa AG Asifu Demokrasia CCM).Yani kichwa maji huyu mwenye jukumu la usimamizi wa sheria ikiwa ni pamoja na kupambana na rushwa alijifanya kupofu kwenye rushwa za wazi zilizotawala mchakato wa CCM kupata wagombea wake katika uchaguzi mkuu uliopita.Basi bora angekaa kimya,lakini mropokaji huyu akaona ni vme atuthibitishie how good msema ovyo he is.

Tunakumbuka pia ubabaishaji wake kuhusu muswada wa kizushi wa Sheria ya Gharama za Uchaguzi.Ofisi ya mbabaishaji huyu pasipo aibu iliwasilisha madudu huko Bungeni ambapo haikuchukua muda kwa watu makini kama Dr Wilbroad Slaa kubaini uhuni uliofanyika.Na kwa vile ni rahisi zaidi kwa Kikwete kufanya teuzi kuliko kutimua wababaishaji,Werema hakuguswa.In fact,amezawadiwa tena Uanasheria Mkuu.

Ilikuwa rahisi kwa Werema kupandwa na muku katika kipindi cha kampeni za uchaguzi na kutishia kuishtaki Chadema kwa sababu anazojua yeye lakini sasa badala ya kuungana na Watanzania halisi kuonyesha hasira zao kuhusu hukumu ya Dowans ambapo serikali inatakiwa kuwalipa matapeli hao shilingi BILIONI MIA MOJA THEMANINI NA TANO (Tshs185,000,000,000/=)!!!!Badala ya angalau kuonyesha uchungu kwa nchi yetu na kuelezea suala hilo kistaarabu,jitu hili linakurupuka na kudai "..The matter is as good as closed...let's use our resources on important issues..." (mjadala huo umefungwa,tuangalie mambo mengine ya msingi).Yaani kwa mzembe huyu wa kufikiri,malipo ya shilingi bilioni 185 kwa matapeli wa Dowans sio suala muhimu (ambao laiti Werema na ofisi yake wangewajibika ipasavyo mmiliki wa Dowans angekuwa jela muda huu).Je cha muhimu ni kipi Mista Jaji?

Kwanini Watanzania wabebeshwe mzigo uliosababishwa na ufisadi katika serikali ya Kikwete?Yes,Kikwete anahofia kumuudhi swahiba wake anayemiliki Dowans,na ataendelea kuwa mateka wa fisadi huyo mpaka anamaliza urais wake 2015.Ni katika mazingira haya ya kubebana na kulindana ndipo wababaishaji kama Werema wanapata nafasi za kupewa madaraka (kulinda maslahi ya mafisadi) na kwa vile anafahamu fika kuwa Kikwete hana ubavu wa kumtimua (Werema) anaropoka kadri misgipa ya mdomo wake inapowashwa.Huyu mtu ana kauli chafu na zilizojaa ngebe.Si mlevi wa madaraka (kama walivydai Chadema) bali ni teja la madaraka.Uanasheria wake Mkuu haukamiliki pasipo kuwadharau Watanzania wenye nchi yao.Hajioni mheshimiwa mpaka aongee maneno mawili matatu ya "kutunyooshea kidole cha kati" (middle finger in the air)

Ndio maana nimepatwa na wazo la kujiuliza kuhusu iwapo Werema ni Mtanzania kweli au ndio walewale wanaojificha kwenye umoja wetu licha ya wingi wa makabila yetu?Nimeeleza hapo awali kuwa katika mchanganyiko huu wa makabila ni rahisi kwa wasio Watanzania kujichanganya nasi kana kwamba ni wenzetu.Kuwatamvua si rahisi lakini kwa bahati nzuri baadhi ya watu hawa wanaweza kutambulika,sio kwa mwonekano wao,bali KAULI ZAO ZINAZOONYESHA BAYANA HAWANA UCHUNGU WALA UPENDO KWA TANZANIA.

Nimalize kwa kumlaumu tena Rais Kikwete kwa kuzidi kuipeleka Tanzania shimoni.Teuzi zake za rapid fire na zinazoelemea zaidi kwenye kulindana badala ya sifa na/au uzalendo ndio sababu ya kupata watu wa ajabu kama huyu Werema.Najua Chadema wamemtaka kichwa maji huyu ajiuzulu,lakini hiyo ni ndoto mbaya.Werema ajiuzulu achekwe?Na akishajiuzulu nani atasimamia maslahi ya mafisadi hapo kwa Mwanasheria Mkuu?Nani atasimamia malipo kwa mafisadi kama wa Dowans?Nani atahakikisha mikataba ya kiuendawazimu inaendelea kusainiwa na kulindwa kwa nguvu zote?Werema ajiuzulu ili Kikwete aonekane a total fraud katika uongozi na teuzi zake?

26 Aug 2010

Rostam Aziz
Katika kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005,mfanyabiashara controversial Rostam Aziz alitumia raslimali zake nyingi kuhakikisha mgombea wa nafasi ya urais kwa tiketi ya CCM,Jakaya Kikwete,anashinda kwa gharama yoyote ile.Na kutokana na utajiri mkubwa alionao pamoja na mbinu zake mbalimbali,mchango wake ulimsaidia sana Kikwete kuingia Ikulu,na sasa ni Rais wetu anayeomba tena ridhaa ya kutuongoza kwa miaka mitano ijayo.

Kati ya mwaka 2005 (baada ya Kikwete kuingia Ikulu) na sasa,Rostam ameibuka kuwa kiumbe mwenye nguvu za kutisha sio tu ndani ya CCM bali kwenye siasa za Tanzania kwa ujumla.Lakini kubwa zaidi katika kipindi hicho ni kwa mfanyabiashara huyo kuhusishwa na tuhuma mbalimbali za ufisadi na Kikwete na serikali yake kushindwa kuwaridhisha Watanzania kwamba "hamkumbatii swahiba wake huyo".Haihitaji kurejea namna Rostam alivyohusishwa na ufisadi wa EPA (Kagoda) na ujambazi wa Richmond.
Jakaya Kikwete

Mwaka 2010,yaani mwaka huu,Rostam anaelekea kurejea tena ulingoni japo si kwa wazi sana.Ushahidi wa kimazingira unaonyesha kuhusika kwa mfanyabiashara huyo katika kampeni za Kikwete.Vyombo vya habari vinavyomilikiwa na Rostam vimekuwa vikiendesha kampeni ya chuki dhidi ya mgombea urais kwa tiketi ya Chadema,Dokta Wilbroad Slaa,mwanasiasa anayeonekana kuwa  tishio kwa mfanyabiashara huyo na vitendo vyake dhidi ya maslahi ya taifa.
Magazeti yanayomilikiwa na Rostam

Na kama hilo la vyombo vya habari vya Rostam kumuandama Dkt Slaa halitoi mwangaza wa kutosha basi taarifa kwamba mwandishi mwandamizi wa kampuni ya Habari Corporation (inayomilikiwa na Rostam),Muhingo Rweyemamu,anatajwa kuwa mratibu wa kampeni za Kikwete.Itakumbukwa kuwa mwaka 2005,waliokuwa waandishi waandamizi wa Habari Corporation,Salva Rweyemamu na Dokta Gideon Shoo walitumika sana kwenye kampeni hizo.Baada ya kuingia Ikulu,Kikwete "alimzawadia" Salva ukurugenzi wa habari wa Ikulu,nafasi anayoshikilia hadi sasa.
Muhingo Rweyemamu

Kama alivyo Salva,Muhingo anasifika kwa uwezo wake wa hali ya juu wa kujenga hoja.Kwa bahati mbaya au makusudi,uwezo huo pia unatumika ipasavyo kutengeneza fitna.Wengi watakumbuka namna Dokta Salim Ahmed Salim,mmoja wa wana-CCM waliokuwa wanawania kuchuana na Kikwete,alivyoundiwa zengwe kubwa na kumhusisha na kundi la Hizbu la huko Zanzibar.Inaelekea kuwa mbinu hizohizo zimeanza kutumika dhidi ya Dokta Slaa,na kuna kila sababu ya kuamini kuwa kuna mengi yatakayoibuliwa dhidi yake.
Salva Rweyemamu  (kushoto) na Gideon Shoo

Yayumkinika kuamini kuwa waandishi wa habari wanaotumiwa kumchafua Dokta Slaa na Chadema kwa ujumla wanafanya hivyo kwa minajili ya "kupeleka mkono kinywani".Kubwa zaidi ni sapoti ya Rostam kwa Kikwete.Wakati mwaka 2005 alijibidiisha ili kufanikisha maslahi yake binafsi ya kibiashara (na amenufaika kweli-kwa kuangalia ishu za Kagoda na Richmond/Dowans) safari hii Rostam anahaha kumzuia Dokta Slaa kwa vile anafahamu fika kwamba laiti mwanasiasa huyo wa Chadema anayesifika kwa msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi akiingia Ikulu,zama za mafisadi kutumia jeuri yao ya fedha "kuendesha serikali kwa remote control" itakuwa imefikia kikomo.

Kwahiyo,Dokta Slaa na Chadema kwa ujumla wanapaswa kuelewa kuwa safari hii Rostam ana "special mission" ya kuhakikisha "survival (kusalimika) yake.Atatumia kila raslimali aliyonayo kuhakikisha Dokta Slaa haingii Ikulu.Anafanya hivyo akifahamu wazi kuwa rais yeyote mwenye kujali maslahi ya nchi yake "atamkalia kooni" mfanyabisahara huyo na washirika wake.

Hata hivyo,kwa vile si fedha za Rostam au wanahabari wake zitakazopiga kura kwenye uchaguzi mkuu,bali mimi na wewe pamoja na kila Mtanzania aliyechoshwa kuona nchi yetu ikigeuzwa "shamba la bibi",ni muhimu kwa wapiga kura kusema HAPANA.Tusitoe fursa kwa watu wenye maslahi binafsi kuipeleka nchi yetu kwenye maangamizi.Na ni muhimu zaidi kutambua kuwa baadhi ya watu hao wana utata wa kutosha tu kuhusu asili ya mahali walipozaliwa.Hiyo inamaanisha kuwa "wakishaiingiza Tanzania kwenye mtaro",watakuwa na sehemu ya kukimbilia.

KILA MTANZANIA MWENYE KUITAKIA MEMA NCHI YETU ANAPASWA KUPAMBANA NA WAHUNI WA KISIASA WANAOTAKA KUTUWEKEA MADARAKANI VIONGOZI WANAOWAMUDU NA HIVYO KUENDELEA KUTUFISADI KAMA ILIVYOKUWA KATIKA KIPINDI CHA MIAKA MITANO ILIYOPITA.


INAWEZEKANA,TIMIZA WAJIBU WAKO

10 Aug 2010





Miongoni mwa mambo yanayoipa kiburi CCM ni imani ilishamiri miongoni mwa viongozi wa chama hicho kuwa Watanzania hawana kumbukumbu,hawajui kutofautisha zuri na baya,wavumulivu kupita kiasi,na ni viumbe wa kupelekeshwa tu.Yayumkinika kuhitimisha kwamba imani hiyo ya viongozi hao inasababishwa na mambo makuu mawili:Kwanza,dharau,kiburi,ubinafsi,na kubwa zaidi ya yote,ufisadi.Sababu ya pili,ni namna Watanzania wengi wanavyoendelea kukiamini chama ambacho kilishawatelekeza miaka kadhaa iliyopita.

Katika sababu hii ya pili,mfano mzuri ni ule wa mume anayemnyanyasa mke kupindukia lakini mapenzi ya mke huyo yanazidi kudumu akitarajia mumewe atapatwa na akili au huruma.Kwa bahati mbaya,utiifu huo wa mke kwa mume mnyanyasaji huishia kutafsiriwa na mume huyo kuwa mkewe “amenasa kwenye zege”,hana ujanja wa kuomba talaka au kukabiliana na manyanyaso ya mume huyo.

Ni katika mantiki hiyo ndipo leo tunasikia kioja cha mwaka ambapo “msema chochote” wa CCM,Tambwe Hizza (ambaye bado anaugulia maumivu ya kubwagwa kwenye kura za maoni huko Temeke) akikurupuka na kudai Rais Jakaya Kikwete hajawahi kutamka kuwa “hataki kura za wafanyakazi”.

Huyu Tambwe ni mhuni,hana nidhamu kwa Watanzania (kama alivyokuwa mhuni kwa kuapa kumtukana mama yake mzazi),na anafikiri bado tunaishi katika zama zile ambapo kama mwananchi hakuhudhuria mkutano uliohutubiwa na kiongozi husika,basi tegemeo pekee ni magazeti ya CCM ya Uhuru na Mzalendo au “midomo ya serikali” yaani Radio Tanzania na Daily News.Na vyombo vyote hivyo vya habari vilikuwa na unyenyekevu wa kuchefua kwa namna vilivyokuwa vikifanya kila liwezekanalo kupendezesha hotuba au kauli za watawala wa enzi hizo.

Japo vyombo vya habari vya serikali (Habari Leo,Daily News na TBC) bado vimeendelea kukumbatia siasa za chama kimoja kwa kuipendelea CCM waziwazi na kupuuza kuwa vinaendeshwa kwa fedha za walipakodi (ambao takriban milioni 35 kati yao sio wanachama wa CCM) lakini angalau siku hizi tuna vyombo binafsi vya habari pamoja na social media (blogs,youtube,facebook,twitter,nk) na hiyo inasaidia kwa kiasi kikubwa “kutofautisha mchele na pumba”.

Lakini kutokana na dharau zao na kutojali,Tambwe na CCM wanajifanya hawajui kuwa hotuba ya Kikwete kuhusu tishio la mgomo wa wafanyakazi ipo mtandaoni.Mtandaoni kuna video zenye hotuba hiyo,na uzuri wa mtandao ni kwamba unahifadhi kumbukumbu vyema sana.Kwahiyo hata kama CCM wangetaka “kufuta maneno hayo ya JK” bado wangekabiliwa na kigingi katika kufuta kumbukumbu zilizozagaa mtandaoni.Pengine wanafahamu sana kuhusu hilo lakini wanajipa matumaini kwa kuamini kuwa “Watanzania ni wanyonge sana na hawaweza kusaka kumbukumbu za kauli hiyo ya Kikwete”.Au pengine ni jeuri tu ya madaraka na imani kwamba kiongozi ana ruhusa ya kuahidi chochote,kusema lolote na kufanya chochote na asihukumiwe na umma.

Leo Tambwe anasema Kikwete hajawahi kutamka kuwa hahitaji kura za wafanyakazi.Je atakanusha pia kuwa Kikwete hajawahi kusema mimba za wanafunzi wa kike ni kiherehere chao?Au hakuwahi kutamka kuwa hajui kwanini Tanzania ni masikini?Au hajawahi kutamka kuwa anawafahamu wala rushwa lakini anawapa muda wa kujirekebisha?Au hakuwahi kuahidi kuwa maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana?Au Tambwe pia atakabusha kuwa Kikwete hakutumia mfano wa MBAYUWAYU?

Kwani Tambwe au CCM,au hata JK mwenyewe,hawakukanusha habari zilizoandikwa na gazeti la Mwananchi chapisho la mtandaoni Mei 3, 2010 na kupewa kichwa cha habari "JK: Nipo Tayari Kukosa Kura Zenu" na kumnukuu "(Kikwete) alifafanua kuwa kima cha chini cha mshahara cha Sh315,000 kwa mwezi kinachopigiwa debe na Tucta, serikali haiwezi kukitekeleza na kama hilo ni shinikizo kwake ili wafanyakazi wampatie kura kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, hahitaji kura zao". (BONYEZA HAPA KUSOMA HABARI HIYO)

Ni dhahiri hili zoezi la kukanusha kauli halitafanikiwa.Liliwezekana katika zama ambapo Watanzania uhuru na access ya habari ilikuwa kwa ridhaa ya watawala lakini sio sasa ambapo blogs,webforums,facebook,twitter,youtube,nk zinapatikana kila kona ya dunia alimradi kuna internet connection.

Dharau na jeuri ya CCM iliwafanya wajisahau kwenye usingizi wa pono huku JK akitoa baadhi ya kauli zisizotarajiwa kutoka kwa mwanasiasa anayetarajia kuomba tena ridhaa ya wananchi kuwaongoza tena.Wakati huo walikuwa na uhakika wa asilimia zaidi ya 100 kuwa JK na CCM yake kurejea madarakani ni suala la muda tu na sio “if watarejea”.Lakini ghafla,baada ya Chadema kumtangaza Dkt Wilbroad Slaa kuwa mgombea wake wa nafasi ya urais,CCM wametahayari.Hawakuona umuhimu wa kukanusha kauli hiyo ya JK mpaka baada ya kumsikia Dkt Slaa akiwaeleza wafanyakazi kuwa “anahitaji kura ambazo Kikwete hazihitaji”.Ghafla,CCM wanakugundua kuwa kauli hiyo haikuwa mwafaka,lakini kwa dharau zao badala ya kuomba radhi au kutafuta suluhu wanakimbilia kukanusha.

Nimeandika makala kadhaa katika blogu yangu kuhusu umuhimu wa CCM kuwaomba radhi Watanzania kwa madudu mbalimbali waliyotufanyia badala ya wao kuendelea kujigamba kuhusu “mafanikio yaliyopatikana katika utawala wao”.Yani wanataka kutuambia kuwa hata kushamiri kwa ufisadi ni mafanikio?Kwanini wasingetumia busara ya kutueleza “mafanikio” yao kisha wakaonyesha uungwana kwa kueleza maeneo ambayo kimsingi “wametuangusha”?Hawawezi kufanya hivyo kwa vile wanatudharau,wanatuona wajinga tusiojua kutenganisha mema na mabaya,wasahaulifu tusiokumbuka hata mahitaji yetu muhimu.

Tayari chama hicho tawala kimeshaonyesha “mchecheto” kwa kukacha kushiriki mdahalo wa wagombea urais kabla ya “kulialia” kuwa Chadema inacheza rafu “kwa kuanza kampeni kabla ya muda wake”.Ukichanganya na songombingo linaloendelea ndani ya chama hicho katika mchakato wa kupata wagombea wa nafasi mbalimbali katika uchaguzi ujao ni dhahiri kuwa kwa mara ya kwanza CCM inaanza kuona dalili za kung’olewa madarakani.Na huenda moto mkubwa zaidi ukawaka ndani ya chama hicho baada ya mchujo wa wagombea baadaye mwezi huu.

Tahayari iliyowakumba CCM inaweza kuwa silaha nzuri kwa Dokta Slaa na Chadema kwa ujumla.Kwa kauli kama hizi za akina Tambwe,ni rahisi kwa Chadema kuwaonyesha Watanzania namna gani chama hicho kinavyowadharau.Ndio!Kwani kama si dharau ni nini basi pale mtu anapokutukana halafu baada ya kitambo akaibuka na kukanusha kuwa hajakutukana japo ushahidi upo bayana?CCM inajikaanga kwa mafuta yake yenyewe.Dharau na jeuri yao inaweza kuwa mtaji mzuri wa anguko lake.

Kwa wale wote wenye uchungu wa dhati kwa nchi yetu na waliochoka kufisadiwa na CCM,kitendo cha chama hicho kukanusha kuwa JK hajawahi kukataa kura za wafanyakazi kinapaswa kutafsiriwa kama namna Watanzania “watakavyoingizwa mkenge tena kama mwaka 2005” ambapo chama hicho kiliahidi mambo chungu mbovu lakini badala yake matokeo ni kushamiri kwa ufisadi.Kama mwenyekiti wa chama hicho anaweza kutoa kauli hadharani kisha chama chake kikaibuka kudai kuwa hajatoa kauli hiyo,je kwanini tusiamini kuwa mgombea urais wa chama hicho (JK) ataishia kupuuza ahadi anazotoa sasa na wakati wa kampeni,na CCM ikiulizwa ikaishia kukanusha kuwa hajwahi kuahidi hivyo?

Watanzania sasa tumepatiwa nafasi adimu ya kuondokana na CCM.Katika chaguzi zilizotangulia tulikuwa hatuna uhakika na wagombea waliosimamishwa kuchuana na mgombea wa CCM lakini safari hii tumebahatika kupata mtu ambaye rekodi yake inajidhihirisha bayana.Na kwa namna ambayo haijawahi kutokea katika historia ya chaguzi nchini mwetu ambapo CCM inaonekana ikianza kutahayari waziwazi baada ya mwamko ulioletwa na Chadema na Dkt Slaa,huo ni uthibitisho tosha kuwa mafisadi wamegundua kuwa siku zao zinahesabika.

Tusirejee makosa ya huko nyuma ya kujaa kwenye mikutano lakini kura zinakwenda CCM.Safari hii,acha watoe rushwa zao (na mzipokee tu kwa vile ni fedha walizowafisadi) lakini kura ziende kwa Dkt Slaa.Dawa ya kung’oa ufisadi ni kung’oa mmea unaolea ufisadi,na mmea huo ni CCM.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.