14 Oct 2010


Profesa Nkunya na vyuo vya kutengeneza shahada.

Na Idd Amiri



Wiki iliyopita Profesa Mayunga Nkunya, Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania, aliongea na waandishi wa habari na baadaye akatoa tangazo juu ya kuwepo kwa vyuo vikuu visivyotambulika hapa nchini na huko nchi za nje vinavyotoa shahada za udaktari wa heshima wa falsafa kwa watu mbalimbali mashuhuri hapa nchini na kwingineko barani Afrika hususa ni kwa Wabunge, Mawaziri na hata Marais. Marais wetu wawili nao ni madaktari wa falsafa.

Katika tangazo lake kuhusu kuzuka kwa vyuo hivyo amebainisha kuwa kumekuwa na mbadilishano wa fedha kati ya wahusika na vyuo hivyo na hili ni kwa nia ya kujipa hadhi wasiyositahili waheshimiwa hao kwa wanajamii.

Profesa Nkunya amekuja na kauli hii baada ya Mheshimiwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi profesa Jumanne Maghembe, kutoa ufafanuzi juu ya kutolewa kwa shahada hizo kutoka katika vyuo hivyo ambavyo kwake yeye hakuviita visivyotambulika au vyuo vya kutengeneza shahada kama profesa Nkunya alivyoviita.

Profesa Maghembe alitoa ufafanuzi katika mkutano wa mwisho wa Bunge La Jamhuri ya Muungano wa Tanzania huko Dodoma, Waheshimiwa aliowataja Profesa Maghembe ni pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Kwera, Mheshimiwa Chrisant Mzindakaya na Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Amani Abeid Karume.

Katika kikao hicho cha Bunge wakati wa kuchangia mijadala mbalimbali Mheshimiwa Juma Ngasongwa, ambaye kwa kiwango cha elimu au usomi ni daktari wa falsafa alilalamika kuwa pamoja na kuwa na shahada nzuri ya udaktari wa falsafa katika uchumi lakini haiitwi Member of the learned brothers!. Mara nyingi wanasheria huiitwa hivyo ingawa binafsi sijui inakuwaje msomi mwenye shahada ya kwanza awe katika kundi hilo na madaktari wa falsafa katika fani nyingine wasiwe katika kundi hilo, Kwa leo hilo siyo sehemu ya mjadala wangu.

Profesa Maghembe alisema kuwa Mheshimiwa Mzindakaya amepewa shahada ya heshima ya udakatari wa falsafa kwa kutambua mchango wake katika upenzi, ujenzi na maendeleo ya viwanda na Mheshimiwa Karume alitunukiwa shahada yake kwa kufanikiwa kutokomeza malaria katika visiwa vya Zanzibar.

Lakini hii si mara ya kwanza kuhojiwa kwa shahada za heshima za watu mbalimbali, katika vikao vya Bunge miaka ya nyuma huko Mheshimiwa Dr. Hansy Kitine aliwahi kuongelea suala hilo na aliyekuwa Waziri wa Elimu ya Juu Sayansi na Teknolojia Dr. Pius Sabasi Ng’wandu alimjibu kuwa haoni kama kuna ubaya wowote kwani hakuna madhara kwa mtu kupewa hadhi hiyo. Lakini hoja ya Kitine ilikuwa zaidi kwa maprofesa wa mitishamba. 

Kwa wale waliowahi kutembelea makumbusho ya Bagamoyo watakuwa wanamfahamu Profesa Kejeli, huyu jamaa ni mahiri kwa kuelezea historia ya mji wa Bagamoyo tena kwa kasi ya ajabu, Kumbukumbu za watu, miaka na mahali alizonazo profesa Kejeli kwa kweli zinakuacha mdomo wazi anaposimulia. Nilibahatika kumwuliza ilikuwaje akaitwa profesa alinijibu kuwa alipewa hadhi hiyo na Marehemu Meshack Maganga aliyekuwa Mkuu wa Chuo Cha Uandishi wa Habari Tanzania (TSJ).

Miaka mitatu iliyopita nilikuwa nikifuatilia mwendelezo wa kipindi cha kweli (Reality show) cha kila mwaka cha runinga ya shirika la utangazaji la uingereza (BBC) katika BBC Two, kinachoitwa You’re Fired ambacho huongozwa na Milionea wa Kiingereza Sir Alan Sugar. Lengo la kipindi hiki huwa ni kutafuta mtu mmoja ambaye bila kuangalia kiwango cha elimu yake anaweza kuwa na mbinu za kijasiliamali na kimenejimenti kwa kuwaongoza wenzie katika kutafuta faidi iwe katika hoteli, kiwanda na mahali popote ambapo uzalishaji kwa lengo la kutafuta faidi unafanyika. Mshindi wa mchakato huo huajiriwa katika moja ya makampuni ya milionea huyo na kwa mwaka analipwa paundi za kiingereza laki moja (100,000). 

Ili kufanikisha mkakati wake huo Sir Alan Sugar, aliwagawa washiriki wake wapatao 20 katika makundi mawili ya kila upande watu kumi, akawagawia mtaji wa kuendesha biashara ya kufua nguo ambapo makundi yote mawili yalitakiwa kupita kwa wateja majumbani na kujitangaza na hatimaye wateja walikubali kuwapa nguo zao zikafuliwe na kunyooshwa kwa gharama walizokubaliana.

Hatimaye ikafika wakati wa kuangalia nani kapata nini na kapoteza nini, makundi yote mawili yalipata faidi lakini moja lilipata faidi ndogo na hapo Sir Alan akawa mbogo akitaka kujua nani kasababisha kutopatikana kwa faidi kubwa na kwa bahati mbaya nguo za mmoja wa wateja zilikwenda kwa mteja ambaye siye mwenye nazo!

Katika kutafuta uzembe ulikuwa wapi alijitokeza mshiriki mmoja katika kundi hilo akapaza sauti kuwa tatizo katika kundi lao kuna washiriki ambao siyo wasomi, ndipo Sir Alan akamwuliza kuwa ana elimu ya kiwango gani? mshiriki yule akajibu kuwa ana shahada ya uzamili katika uchumi. Swali la mwisho na ambalo lilimwondoa katika ushiriki ule lilikuwa ametumiaje elimu yake katika kuleta faida, mshiriki akawa kimya na Sir Alan hakuwa na la ziada ila kumfukuza huku akisema wale wafanyakazi wake ambao hawana shahada lakini wanamwingizia faida wana tatizo gani.

Mshiriki aliyekuja kushinda na hatimaye kuajiriwa kwa mshahara wa paundi 100,000 alikuwa ni yule aliyekaa chuo kikuu kwa miezi mitatu na kuacha kwa sababu alionyesha kuwa ana mbinu za kijasiliamali na kimenejimenti za kuweza kuzalisha faida katika kampuni.

Sasa nirejee kwenye usomi na shahada za bandia na za kweli, hapa najiuliza maswali mengi lakini kwa uchache ni inawezekana vipi kwa msomi ambaye ni profesa kuteuliwa kuwa waziri wa mawasiliano na uchukuzi na baada ya muda Fulani anapoondoka wizara ile mashirika karibu yote katika ile wizara yanakuwa taabani? Msomi mwingine ambaye ni profesa anaanzisha taasisi isiyokuwa ya kiserikali huku fedha zote za kuendeshea taasisi hiyo zikitoka nje kwa wahisani wake, anajenga jumba lake kubwa la kifahari, ananunua gari la kifahari pia na anasomesha watoto wake ughaibuni na katika kufanikisha mradi anaendesha utafiti ambao mara zote ni kuangalia kama mwanasiasa fulani anapendwa na watanzania au la? Fikra zangu duni ni kuwa baada ya kuwa mtu yeyote amesoma na kuwa na hadhi ya profesa na chuo kumkubali nadhani anatakiwa kuonyesha kwa vitendo thamani ya elimu aliyopata.

Kwahiyo unaweza kujiuliza kutokana na yale niliyoeleza hapo juu kuwa hii ndiyo gharama ya kodi za watanzania walizotumia kumlipia yeye wakati akisoma inasaidia nini kujua kuwa fulani anapendwa au hapendwi? Unakuwa na msomi mwingine ambaye ni daktari wa falsafa na waziri vilevile lakini hajui hata kutoka Mwenge jijini Dar es Salaam hadi jimboni kwake ni kilomita ngapi na huyu ndiye anayetakiwa kusimamia ujenzi wa barabara? Jambo linalonipa taabu ni kama kwa utashi wangu niwape heshima ya usomi waheshimiwa hawa? Upo mfano mmoja hivi inakuwaje kwa msomi kung’ang’ania kufanya kazi katika chuo kimoja tu wakati anaweza kusaidia mahala pengine hata kama siyo kwa kufundisha, kwanini msomi kama huyu asifanye kazi nyingine yoyote zaidi ya kufundisha na kufanya utafiti ambao matumizi yake ni yamkini?

Kwa bahati mbaya nimekuwa nikijikuta nawasilikiza au kuwatazama wasomi mbalimbali wakiongea katika runinga na redio na wengi ni wakosoaji wazuri, kuna wakati Mzee Ali Hassani Mwinyi alipokuwa rais wa Tanzania alikuwa na mshauri wa uchumi ambaye ni profesa na ni huyo huyo leo hii anasema kuwa serikali inategemea sana misaada katika bajeti yake na ijaribu kuja na mbinu za kujitegemea, lakini wote tunajua jinsi nchi hii ilivyopoteza viwanda na raslimali chungu mbovu wakati msomi huyu alipokuwa msahuri wa mzee ruksa.

Wakati Rais Jakaya Kikwete akitoa hutoba ya kulivunja Bunge, Mjini Dodoma kulikuwa na wasomi wawili ambao walialikwa na Runinga ya Taifa(TBC) ili watoe tathmini yao kutokana na hutoba ile na kwa kuwa ilikuwa na takwimu nyingi hapo ulikuwa ni uwanja wao. Kilichonishangaza ni moja wa wasomi wale alipokuwa akiunga mkono takwimu zile kwa kusema kuwa zinatokana na utafiti uliofanyika wakati hali halisi haiendani kabisa na yaliyokuwa yakitoka kwenye takwimu zile, hii ilinipa simanzi sana.

Kwa mfano, katika hotuba ile kulitajwa kuwa umasikini umeshuka kwa kiwango cha kuridhisha na kwa bahati mbaya wiki ile ile katika kituo kingine cha televisheni ilionyesha mama moja akiwa katika kijiji kimoja wilayani Kyela akiomba msaada wa kujengewa nyumba na wazungu waliokuwa katika ziara ya kujifunza maisha ya watu wa nchi hii. Mama yule ana watoto saba ambao bado hawajawa na uwezo wa kujitegemea, yeye mwenyewe ni mgonjwa, nyumba anayoishi ipo mbioni kudondoka, katika hali ile takwimu za Mheshimiwa zilizopata baraka za wasomi zilikuwa sahihi kweli?

Nirudi kwa kuuliza swali usomi wake umeisaidiaje nchi hii? Kuwa daktari wa falsafa, profesa kama hakuna ulichosaidia kupambana na matatizo ya watanzania na kwa bahati mbaya ukafanya mambo kama siyo msomi bado ni hasara kwa taifa.

Kwa wale tunaofuatilia mienendo ya hawa wote wawili naamini hatuna shaka kwa sababu zilizotolewa na vyuo hivyo kuamua kuwaenzi kwa kwatunuku shahada za falsafa za udaktari wa heshima kwani michango yao tumeiona na hata profesa Maghembe alikubaliana na vyuo hivyo kutoa shahada hizo.

Hivi Karume kuitwa daktari kwa kuwaondolea wazanzibari gonjwa linalotafuna maisha ya watu chungu mbovu katika nchi za kitropiki kuna ubaya? Wasomi wanaotambulika kwa kupitia vyuo vinavyotambulika mbona wameshindwa kuwaangamiza wale mbu pale Hospitali ya taifa Muhimbili? Mzindakaya kuanzia kwenye uanzishaji wa SIDO hadi kuwa na kiwanda chake mwenyewe hilo ni tatizo? Wasomi wangapi hatujui wameifanyia nini nchi hii?

Ninao mfano moja wa kijana aliyemaliza masomo yake kutoka chuo cha maji pale ubungo, jijini Dar Esa salaam, miaka ya mwanzo ya themanini aliporudi kijijini kwake mkoani Iringa alijaribu kufanya matembezi katika moja ya milima inayozunguka kijiji chake, kwa bahati nzuri alifanikiwa kuona chemchem ya maji katika moja ya milima ile, wazo likamjia akawasilisha serikalini na wanakijiji wakafanya harambee ya kuchimba mtaro wa kupitishia mabomba ya maji na yeye akatumia utaalamu wake kukinga maji yale ili yatiririke kuelekea vijiji vya karibu.

Kwa bahati nzuri serikali ilimsikia na kwa juhudi na maarifa aliyokuwa nayo mradi ule unatoa maji kwa vijiji zaidi ya 10 leo hii na hakuna hata siku moja maji yamekatika na wanachi wanaulinda mlima ule kama almasi yao.  Baada ya mradi ule kufanikiwa aliendelea kufanya kazi katika miradi ya maji sehemu mbalimbali nchini na kila alipokwenda na kuondoka wananchi walimlilia, je huyu akipewa shahada ya heshima ya udaktari wa falsafa kuna tatizo?

Kuna wakati niliwahi kuuliza swali kwa raia moja wa nchi za magharibi kuwa kwanini Waziri Mkuu wa Uingereza wakati huo Gordon Brown, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani, Condereza Rice hawapendi kuitwa kwa majina ya kisomi ya Daktari na profesa wakati wanasitahili hivyo kwa elimu zao, alinijibu kuwa siyo vizuri kuitwa msomi na kesho yake ukafanya mambo kama siyo mtu aliyekwenda shule.

Lakini hoja ya Profesa Nkunya ni kama hapendezwi na tunu wanazopata watu mbalimbali kutoka katika vyuo visivyotambulika na kwa hili yuko sahihi, angependa shahada hizi zitolewe zaidi kwa wale wanaosomea kwa kukaa vyuoni na kusimamiwa na wahadhiri na kwa vile huwezi kupata shahada ya udaktari wa falsafa bila kufanya utafiti kwa vigezo vilivyowekwa na chuo ni dhahiri ni lazima uhenyeke au utaabike kabla hujavaa joho hilo.

Kwangu mimi ambaye siyo msomi sioni tofauti yoyote kati ya viwanda vya kutengeneza shahada kama profesa Nkunya alivyoviita na vyuo vinavyotambulika. Lazima tukubali kuwa Vyuo vyetu ni mahali pa kwenda kuchukua vyeti ili kupata ajira kwa sababu hilo ndilo sharti kubwa kuwa na elimu ya shahada ya kwanza, ya pili, tatu hadi mwisho na hii yote inategemea mshahara atakaolipwa mtarajiwa kwa elimu yake na majukumu atakayopangiwa na ofisi inayomwajiri.

Hapa ni kama mashindano ya Bongo Star Search kwani aliyeshinda mwaka jana amefanya kazi yoyote ya muziki? Si ni fedha tu ndizo zinazotafutwa kipaji ni jambo la wengine, unaweza kuiga mwanamuzi unayempenda na kumudu vizuri ili watu wakupigie kura upate mahela! Na kwa upande wa shahada ni hivyo hivyo kinatafutwa cheti kwa gharama yoyote iwe kwa kuiba mitihani, kuhonga mwalimu kwa fedha na ngono, kukodi mtu akufanyie mtihani, kunakili utafiti wa mtu mwingine na hata kukodi mtu wa kufanya utafiti wenyewe suala ni maisha nani anabisha?

Siyo siri kuwa kupata shahada hakuendani na hadhi au muktadha na mantiki ya shahada hiyo, tujiulize wakati tuna wanasheria wenye shahada lukuki inakuwaje mikataba ya madini inakuwa kama ya akina Mangungo wa Msovelo? Taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali kuwa chafu na wahasibu wasomi ndiyo hao? Waandishi wa habari wanaofanya uandishi wa habari kama maofisa uhusiano wa makampuni na shahada zao? Makocha wa mpira wasioleta kombe hata moja la kimataifa huku wakitaka waitwe super coach? Wahandisi wa barabara zinazoharibika siku ya kwanza ya ufunguzi na shahada zao? Wahandisi wa maji wanaotandaza mabomba ya maji wakati wakijua kuwa hakuna maji yatakayotoka na shahada zao? Fani zote zina matatizo na ni wasomi wa vyuo vyetu tunavyovipenda sana na kuviita vinatambulika. Kutambulika kwa chuo bila ufanisi ni sifuri tu. Kama wasomi wetu wangekuwa wanaonyesha mifano kwa wasiosoma ingekuwa ni halali kuwanyooshea kidole wanaofanya ujanja wa kielimu. Msomi hawezi kutuonyesha jinsi alivyoweza kutumia elimu yake kuwa na shamba lenye mazao na mifugo iliyonona kila siku anafanya utafiti ili kiwe nini?

Kwa hapa nirudi miaka ya nyuma kwa upande wa Mahakama, kulikuwa na Mawakili ambao watu wengi walipenda kwenda kuwaona wakitoa hoja zao mahakamani kwa mfano, akina Murtaza Lakha, Ismail Mukhadam, Francis Uzanda na baadaye wakaja akina Abasi Mselem, Dr. Masumbuko Lamwai na Michael Wambali.

Wakati huo mashahidi walikuwa na wakati mgumu sana kwa waheshimiwa hawa kwa hoja na maswali waliyokuwa wakiwatupia wakati wakitoa ushahidi wao mahakamani nilitegemea leo tungekuwa na wanasheria wakali zaidi ya hawa lakini hilo halipo na bado tuendelea kuzalisha kundi la werevu ambao ni members of the learned brothers kila mwaka katika vyuo mbalimbali hapa ndani na nje ya nchi kwani sivinatambulika kwenye mafaili yetu!

Kwa waandishi wa habari ambao kwa kweli kwa wakati huo kulikuwa hakuna hata chuo kimoja ambacho kilikuwa kikitoa shahada za uandishi wa habari watawakumbuka akina Stanley Katabalo na John Rutayisingwa, hawa wote ni marehemu kwa sasa kwa jinsi walivyoweza kuandika habari za uchunguzi wa kikachero na kuwafanya wasomaji wa magazeti kufuatilia habari zao kila magazeti yalipokuwa yakitoka, naye Mnenge Suluja alivyokuwa akiandika habari za mahakamani na kumfanya msomaji ahisi kama alikuwepo mahakamani siku ya shauri. Leo tunao wenye shahada si ndiyo! Habari gani ambayo wameandika ikionyesha kuwa inaendana na usomi wao?

Nimeanzisha mjadala huu ili wachangiaji wengine wanisaidie kupata picha halisi ya viwanda vya kutengeneza shahada na vyuo vinavyotambulika kwani mimi siyo msomi na sina nia mbaya ya kuleta utetezi wa shahada za heshima tatizo langu ni ujinga na uelewa mdogo nilio nao, bado sielewi tofauti iko wapi na nini mchango wa wale tunaowaita wasomi waliobobea katika maendeleo ya nchi hii?


Waweza kunisaidia kwa hili kwa kuniandikia barua pepe kwa anwani hii [email protected]

ASANTE SANA MDAU IDD KWA MAKALA HII MWANANA.WADAU WENGINE PIA MNAKARIBISHWA KUTUMA MAKALA ZENU AU CHOCHOTE KILE CHA MANUFAA KWA JAMII.


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.