22 Dec 2016

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.
IJUMAA iliyopita, kulijitokeza tukio ambalo hadi wakati ninaandika makala hii limezua utata. Usiku wa siku hiyo, Rais Dk. John Magufuli alitengua wadhifa wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.
Siku moja kabla, Dk. Mwele alizungumza na waandishi wa habari kuwaeleza kuhusu matokeo ya utafiti wa takriban mwaka mzima kati ya NIMR na Chuo Kikuu cha Bugando kuhusu ugonjwa huo na ilibainika kuwa kati ya sampuli za damu 533, 88 zilikutwa na virusi vya ugonjwa wa zika.
Hata hivyo, siku iliyofuata, serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto ilitoa taarifa kuwa ugonjwa huo haujaingia nchini, kana kwamba taarifa ya Dk. Mwele ilizungumzia kuingia kwa ugonjwa huo.
Pengine kabla ya kuingia kwa undani katika kujadili suala hili, ni vema niweke bayana ukweli kuwa Dk. Mwele ni dada-rafiki yangu, na nimesikitishwa sana na tukio hilo, hususan jinsi wadhifa wake ulivyotenguliwa.
Ni kwamba, wakati taarifa ya wadhifa wake kutenguliwa ilitolewa usiku wa Ijumaa iliyopita, saa chache baadaye, Jumamosi asubuhi, kukatangazwa uteuzi wa Profesa Yunus Mgaya kuchukua wadhifa ulioachwa wazi na Dk. Mwele.
Kama nilivyoeleza awali, hadi wakati ninaandika makala hii kuna utata unaoendelea kuhusu suala hilo. Hiyo imetokana na vitu kadhaa. Kwanza, taarifa ya Ikulu kuhusu uamuzi wa Rais Magufuli kutengua ukurugenzi wa Dk. Mwele haikueleza kwa nini rais alichukua uamuzi huo, tena usiku.
Kadhalika, utata huo unachangiwa na hisia kuwa huenda ‘siku za Dk. Mwele zilikuwa zinahesabika,’ kwani katika mazingira ya kawaida, sio rahisi mkurugenzi wa taasisi nyeti kama NIMR kuondolewa madarakani usiku kisha mbadala wake akapatikana asubuhi.
Hisia hizo zinachangiwa pia na ukweli kuwa Dk. Mwele ni mtoto wa Waziri Mkuu wa zamani, mzee John Malecela. Miezi minane iliyopita, familia ya mwanasiasa huyo mkongwe ilikumbwa na ‘balaa’ kama hili, ambapo Rais Magufuli alimwondoa madarakani mke wa mzee Malecela, mama Anne Kilango, aliyekuwa mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.
Tofauti na wadhifa wa Dk. Mwele ulivyotenguliwa bila maelezo, tukio la mama Kilango liliambatana na maelezo kwamba alitangaza kwenye vyombo vya habari kuwa mkoa wake hauna watumishi hewa jambo ambalo lilisababisha Ikulu kufanya uchunguzi wake na kubaini wafanyakazi hewa 45 katika awamu ya kwanza huku awamu ya pili ya uchunguzi bado ukiendelea.
Katika mazingira ya kawaida, huwezi kumlaumu mtu anayeweza kuhoji “tatizo lilikuwa utendaji kazi wa mama Kilango na Dk. Mwele au ‘mlengwa’ ni mzee Malecela?”
Wasomi kadhaa waliozungumzia hatua ya rais dhidi ya Dk. Mwele wameonyesha kushangazwa kwao, hasa ikizingatiwa kuwa rais naye ni miongoni mwa wasomi. Kwamba, alichofanya Dk. Mwele ni kuripoti tu matokeo ya utafiti husika, lakini kukajitokeza mkanganyiko katika tafsiri ya ripoti ya matokeo hayo.
Laiti busara ingetumika, basi Dk. Mwele angefahamishwa tu kuwa taarifa yake imezua mkanganyiko, na angeitisha mkutano na waandishi wa habari kutoa ufafanuzi. Ikumbukwe kuwa dada huyo ni mmoja wa wanasayansi wachache kabisa kutoka Afrika na hususan Tanzania wanaoheshimika mno kimataifa.
Japo sijapata idhini yake ‘kutoa siri hii,’ mwishoni mwa mwaka jana alinieleza kuwa anahitajiwa na taasisi moja ya kimataifa inayohusiana na masuala ya afya duniani, lakini akasema hayupo tayari kuacha kuwatumikia Watanzania wenzake. Binafsi nilimshauri akubali tu nafasi hiyo kwa vile atakapoitumikia dunia, atakuwa akiitumikia Tanzania pia. Hata hivyo, Dk. Mwele alikataa nafasi hiyo.
Vile vile, baada ya jina lake kutopitishwa kuwania kuteuliwa katika nafasi ya urais kwa tiketi ya CCM mwaka jana, Dk. Mwele alielekeza nguvu zake kumuunga mkono mgombea aliyepitishwa, Dk. Magufuli na kila jioni alitumia muda wake baada ya kazi kufanya ‘majukumu ya kisomi’ katika kampeni za chama chake. Na licha ya kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, baadhi ya vijana aliowakabidhi majukumu ya kampeni za Dk. Magufuli hawajalipwa stahili zao hadi leo (licha ya Dk. Mwele kufuatilia suala hilo kwa zaidi ya mwaka sasa). Linganisha hilo na makada ‘waliozawadiwa’ nafasi mbalimbali licha ya kampeni zao ndani au nje ya chama dhidi ya Dk. Magufuli alipokuwa mgombea.
Mwaka jana nilipata fursa ya kuandika wasifu wake kwenye blogu yangu. Pamoja na mengineyo mengi, alieleza kuwa tangu alipokuwa binti mdogo alikuwa na ndoto ya kuwa mtafiti wa maradhi. Na licha ya kuwa mtoto wa waziri mkuu, ambapo alikuwa na fursa ya ‘kufanya chochote atakacho,’ alifuata ndoto yake ya kitaaluma na kitaalamu, akatumia muda mwingi ‘vichakani na misituni’ kujifunza kuhusu maradhi mbalimbali ya binadamu. Kwa hakika, safari yake tangu utotoni hadi kupata shahada ya uzamivu na hatimaye kuwa mkurugenzi mkuu wa kwanza wa kike wa NIMR, inatoa hamasa kubwa.
Kuna wanaoona kuvuliwa madaraka kwa Dk. Mwele ni kama mwendelezo wa kile kilichomkumba aliyekuwa Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru, ambaye kutenguliwa kwa wadhifa wake hivi karibuni kunatafsiriwa kama matokeo ya yeye kutoa maoni yake ya kitaalamu kuhusu suala fedha za taasisi za serikali kuwekwa kwenye akaunti za muda maalumu (fixed deposits).
Nihitimishe makala hii kwa kumpa pole Dk. Mwele huku nikiamini kuwa muda si mrefu ataipatia fahari Tanzania kama mwanasayansi wa kimataifa. Kadhalika, inasikitisha kuona tukio hili ilhali majuzi tumeshuhudia teuzi za baadhi ya mabalozi zikifanywa kwa kigezo cha ukada

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.