Showing posts with label MWELE MALECELA. Show all posts
Showing posts with label MWELE MALECELA. Show all posts

23 Dec 2016

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.


  • Virusi vya Zika viligundulika kuwepo Tanzania mwaka 1952
  • Dkt Mwele na wanasayansi wenzie 'wanakuna vichwa' wakisumbuliwa na swali la kitafiti je, virusi vya Zika vilivyoko kwenye nchi za Afrika mashariki vina madhara sawa na vile vya Brazil?
  • Alichowasilisha ni ripoti ya utafiti kuhusu virusi vya Zika, na sio kutangaza mlipuko wa ugonjwa huo.
  • Sheria iliyoanzisha NIMR ilimpa ruhusa/ mdaraka ya kutoa taarifa husika.
  • Waziri husika alikabidhiwa ripoti  (kumbukumbu namba NIMR/HQ/D13) MIEZI MINNE kabla Dokta Mwele hajatoa ripoti hiyo hadharani.


ANGALIZO: Japo ninafahamiana na Dokta Mwele Malecela (kama dada-rafiki), makala hii ya kiuchunguzi ni jitihada zangu binafsi kupata undani na usahihi kuhusu hatua iliyochukuliwa na Rais Magufuli wiki iliyopita kutengua wadhifa wa Dkt Mwele wa Ukurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR). Ikumbukwe sasa tunaishi katika zama za 'post truth politics' (siasa za hadaa/uongo) ambapo moja ya tabia muhimu ni kupingana na ukweli na kuugeuza uwe uongo, na uongo uwe ukweli. Ni jukumu la kila mmoja wetu kupambana na janga hili ambalo limetawala mno mwaka huu 2016 na kupelekea 'balaa' la Brexit (Uingereza kujitoa katika Umoja wa Ulaya) na Donald Trump kushinda Urais huko Marekani. 

Dokta Mwele Malecela ni nani?

Kwa faida ya wasiomjua vizuri Dkt Mwele, historia yake kwa kifupi ni kama ifuatavyo: Amekuwa mtumishi wa NIMR kwa miaka 30 mfululizo, ambapo alianza ngazi ya awali kabisa kama mwanasayansi 'wa ngazi ya mwanzo' (junior scientist). Yaani kama jeshini basi tungesema alianza kama 'private' na kupanda ngazi hadi kuwa Jenerali. Hili linaweza kuonekana ni jambo dogo lakini ukweli ni kwamba dunia ina mahitaji makubwa ya wansayansi, hususan katika nchi zilizoendelea. Mahitaji hayo ni makubwa zaidi kwa wanasayansi wa kike ambao kwa hakika ni wachache mno. Kuitumikia NIMR kwa miaka 30 mfululizo licha ya vishawishi mbalimbali vya ajira bora zaidi kama mwanasayansi wa kimataifa, Dokta Mwele aliweka mbele maslahi ya nchi yake Tanzania.

Lakini pengine kubwa zaidi kuhusu mwanasayansi huyo ni ndoto yake ya tangu utotoni ya kuwa mwanasayansi mtafiti. Kwa kuzingatia kwamba wakati anakua, baba yake, Mzee John Malecela alikuwa katika nyadhifa mbalimbali kitaifa na kimataifa, kubwa zaidi ikiwa Uwaziri Mkuu. Kwa wadhifa huo wa baba yake, Dkt Mwele angeweza 'kupata chochote,' pengine hata kujikalia tu nyumbani na 'kula maisha.' Hata hivyo, aliwekeza nguvu zake katika kufikia malengo yake ya kuwa mtafiti. 

Kielimu, alifanikiwa kuhitimu shahada ya kwanza chuo kikuu cha Dar es Salaam (BSc in Zoology) na baadaye kupata shahada ya uzamili (MSc) na ya Uzamifu (PhD) katika stadi kuhusu parasitolojia (Medical parasitology) katika taasisi maarufu ya London School of Hygiene and Tropical Medicine ya chuo kikuu cha London, hapa Uingereza.



Watanzania wengi wamemfahamu Dokta Mwele katitka kazi yake kubwa ya kutokomeza magonjwa yasiopewa kipuambele hususan matende na mabusha. Katika sehemu nyingi za Tanzania kama Pangani na Mtwara alijulikana kama mama matende. Kazi hii ilimpatia nishani ya kutambulika kwa kazi hii muhimu kutoka seriakli ya marekani (Neglected Tropical Disease Champion Award). Hivi sasa takwimu za Mtwara zinaonyesha kushuka kwa ugonjwa wa matende na mabusha kutoka asilimia 60-80 mwaka 2002 hadi asilimia 0 mwaka 2014. Juhudi hizi zimeendeshwa na Watanzania wakiongozwa na Mtanzania.

Wasifu mfupi wa Dokta Mwele upo HAPA na maelezo yake mwenyewe kuhusu safari yake hadi kuwa mwanasayansi wa kimataifa yapo HAPA 

Ni kutokana na ueledi wake mkubwa kitaaluma na kitaalamu, kitaifa na kimataifa, watu wengi wamepatwa na mshtuko mkubwa kufuatia uamuzi wa Rais Magufuli kumwondoa Dokta Mwele madarakani.



Japo taarifa ya Ikulu kuhusu uamuzi huo wa Rais haikutoa sababu yoyote, ni siri ya wazi kuwa ulitokana na taarifa aliyoitoa Dkt Mwele kwa waandishi wa habari kuhusu utafiti wa virusi vya ugonjwa wa Zika. Kwamba taarifa yake ilitafsiriwa vibaya au kulikuwa na mpango wa makusudi kumwondoa katika nafasi hiyo, ni jambo ambalo kwa sasa tunaishia kuhisi tu. Kilicho bayana ni kwamba hakutangaza MLIPUKO wa ugonjwa wa Zika bali aliripoti tu kuhusu MATOKEO ya utafiti uliofanywa na taasisi ambao ulibani kuwa sampuli 88 za damu kati ya 533 zilikuwa na virusi vya ungonjwa huo.

Historia ya Zika na uwepo wake Tanzania


Kabla ya kuingia kwa undani zaidi, ni muhimu kujielimisha vya kutosha kuhusu ugonjwa wa Zika na 'mahusiano yake na Tanzania yetu.' Kwa kifupi ugonjwa huu sio mgeni na uko katika kanda za tropiki zenye mbu na uligunduliwa kwa mara ya kwanza katika msitu zika (zika forest) Uganda mwaka 1947. Swali ambalo liko kwenye vichwa vya watafiti wa virolojia wa Afrika mashariki ni kuwa je, virusi vya zika vilivyoko kwenye nchi za Afrika mashariki vina madhara sawa na vile vya Brazil? 

Ifuatayo ni historia fupi ya Zika na uwepo wake Tanzania [Tafsiri ya Kiswahili katika maandishi mekundu]

Historia ya ZIKA

Kuanza kusambaa kwa virusi vya Zika kuliambatana na hali ya watoto kuzaliwa wakiwa na vichwa vidogo isivyo kawaida kunakohusiana na kutokamilika maendeleo ya ubongo (kwa kitabibu, 'microcephaly') na ugonjwa unaofahamika kama 'Guillain-Barre syndrome.' Baada ya kugundulika katika nyani nchini Uganda mwaka 1947, virusi hivyo viligundulika katika binadamu mwaka 1952. Mlipuko wa kwanza wa maradhi yanayotokana na maambukizo ya Zika uliripotiwa katika kisiwa cha Yap mwaka 2007. Hivi sasa kuna nchi kadhaa ambazo zimekumbwa na mlipuko wa  virusi vya Zika.

Zika: Asili na kusambaa kwa virusi hivyo vinavyosambazwa na mbu

Maelezo yafuatayo yanatoa muhtasari wa kusambaa kwa maambukizi ya Zika tangu yalipogunduliwa mwaka 1947 hadi mwezi Februari mwaka huu 2016 



1947: Wanasayansi waliokuwa katika uchungui wa kawaida wa homa ya manjano katika msitu wa Zika nchini Uganda wanabaini virusi vya Zika katika nyani.

1948: Virusi (vya Zika) vyatambuika katika mbu aina ya Aedes Africanus, kwenye msitu wa Zika


1969 - 1983 Uwepo wa Zika unasambaa hadi Asia ya Ikweta, ikiwa ni pamoja na India, Indonesia, Malaysia na Pakistani, ambapo virusi vya Zika vyagundulika katika mbu. Kama ilivyokuwa Afrika, maambukizi ya virusi hivyo yabainika lakini pasipo milipuko, na maradhi kwa binadamu yaendelea kuonekana adimu na ya wastani.

2007: Zika yasambaa kutoka Afrika na Asia na kusababisha mlipuko mkubwa wa kwanza katika binadamu katika kisiwa cha Yap kilichopo kwenye Bahari ya Pasifiki, Shirikisho la Mikronesia. Kabla ya tukio hili, hakukuwahi kuwepo mlipuko wa Zika na kesi 14 tu za uwepo wa Zika zilikuwa zimeripotiwa dunia nzima.

2013 - 2014: Milipuko ya Zika katika visiwa vingine vinne katika Bahari ya Pasifiki; French Polynesia, Kisiwa cha Easter, Visiwa vya Cook, na New Caledonia. Mlipuko katika Kisiwa cha French Polynesia wapelekea hofu ya maelfu ya maambukizi ya Zika, na uchunguzi wa kina waanza.Matokeo ya uchunguzi yaripotiwa kwa Shirika la Afya Duniani (WHO) Novemba 24, 2015 na Januari 27, 2016.

Machi 2, 2015 Brazili yaifahamisha WHO kuhusu ripoti ya maradhi yanayoambatana na vipele kwenye ngozi katika majimbo ya Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo. Kuanzia mwezi Februari 2015 hadi tarehe 29 Aprili 2015, takriban kesi 7000 za maradhi yanayoambatana na vipele kwenye ngozi yaripotiwa. Kesi zote hizo ni za wastani na hakuna taarifa za vifo. Hakukuwa na hisia kuhusu Zika wakati huu na wala hakukufanyika vipimo vya kugundua maambukizi ya virusi hivyo. 

Februari Mosi 2016: WHO yatangaza rasmi kuwa mahusiano ya hivi karibuni kati ya maambukizi ya Zika na dalili za 'microcephaly' na matatizo  megine ya ki-nyurolojia ni janga la afya kimataifa.

Historia hiyo inatufundisha nini?

Kwahiyo, kwa kuangalia tu historia ya virusi vya ugonjwa wa Zika, ni dhahiri kuwa taarifa ya Dokta Mwele, ambayo wala haikuwa yake binafsi bali ya taasisi za NIMR na Chuo Kikuu cha Bugando, haikukiuka kanuni au utaratibu wowote, kitu ambacho kinazua maswali kuhusu uamuzi wa Rais Magufuli kutengua wadhifa wa mwanasayansi huyo wa kimataifa.

Uamuzi wa Rais Magufuli kutengua ukurugenzi Mkuu wa Dkt Mwele NIMR:

Lakini kinachoashiria kuwa 'kuna namna' katika hatua hiyo ya Rais ni masuala yafuatayo:

Kwanza, taarifa iliyotolewa na Dokta Mwele ilishawasilishwa kwa Waziri husika kwa kufuata taratibu zilizopo, tarehe 12 mwezi Agosti 2016 na kupokelewa wizarani tarehe 16 mwezi huohuo. (kumbukumbu namba NIMR/HQ/D13) Kwa maana hiyo, sio kwamba Waziri husika alikuwa hana taarifa kuhusu matokeo ya utafiti huo. 

Na kwa vile alishawasilisha taarifa ya utafiti huo kwa Waziri, Dokta Mwele alikuwa na wajibu wa kutoa matokeo ya utafiti kwa watafiti na umma wa Watanzania wote. Sheria ya bunge namba 23 ya mwaka 1979 ya kuundwa kwa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (www.nimr.or.tz) kipengele cha "vi" kinaitaka taasisi kutoa matokeo ya utafiti wote unaofanyika ndani ya Tanzania. 

Dokta Mwele amekuwa akitoa taarifa hii kwa miaka saba ambayo amekuwa mkurugenzi mkuu. Ni lazima ieleweke kuwa hakuwa anatangaza MLIPUKO wa Zika - kazi ambayo ni ya Waziri/wizara - bali ripoti ya utafiti kuhusu Zika, na hivyo ni vitu viwili tofauti. Yayumkinika kuhisi kwamba tatizo hapa ni siasa kuwekwa mbele ya utaalamu na taaluma.

Kadhalika, wakati macho yameelekezwa kuhusu Zika pekee, Dokta Mwele siku hiyo aliongelea pia kuhusu utafiti wa magonjwa ya chikungunya, dengue na virusi vya West Nile.

Kumekuwa na nguvu kubwa inayotumika kujenga picha kuwa Dokta Mwele amekuwa insubordinate kwa Waziri husika. Lakini ukweli ni kwamba ramani hizo hapo juu zimethibitisha uwepo wa virusi vya Zika nchini Tanzania kwa muda mrefu. Kadhalika, utafiti uliofanywa na NIMR umesaidia kuongeza kile kiutafiti kinachofahamika kama 'body of evidence' ya kuelewa zaidi kuhusu kuenea kwa virusi vya ugonjwa huo na ugonjwa wenyewe.

Pili, Dokta Mwele aliongea na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) Alhamisi Desemba 15, 2016 kueleza alichosema kuhusu utafiti huo wa Zika. Kipindi hicho kilirushwa na BBC saa 12 asubuhi ya siku iliyofuata, Ijumaa Desemba 16, 2016. Sio kweli kwamba Dokta Mwele 'alifanya utovu wa nidhamu kwa kuongea na waandishi wa habari baada ya Press conference ya Waziri.' Ukweli ni kwamba aliongea kabla ya Waziri. Jitihada zinazofanyika kujenga picha ya 'utovu wa nidhamu' zaweza kutafsiriwa tu kama mbinu ya kuhalalisha hatua 'ya kionevu' iliyochukuliwa dhidi ya mwanasayansi huyo.

Pili, Dokta Mwele aliongea na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) Alhamisi Desemba 15, 2016 kueleza alichosema kuhusu utafiti huo wa Zika. Kipindi hicho kilirushwa na BBC saa 12 asubuhi ya siku iliyofuata, Ijumaa Desemba 16, 2016. Sio kweli kwamba Dokta Mwele 'alifanya utovu wa nidhamu kwa kuongea na waandishi wa habari baada ya Press conference ya Waziri.' Ukweli ni kwamba aliongea kabla ya Waziri. Jitihada zinazofanyika kujenga picha ya 'utovu wa nidhamu' zaweza kutafsiriwa tu kama mbinu ya kuhalalisha hatua 'ya kionevu' iliyochukuliwa dhidi ya mwanasayansi huyo.

Wakati uchunguzi huu unafanyika, ilibainika kuwa kuna jitihada za makusudi zinazoendelea mitandaoni 'kumchafua' Dokta Mwele. Kwa 'macho ya juu juu,' ni kama wananchi tu wanatoa maoni yao kuhusu suala hilo, lakini kwa yeyote atakayeangalia kwa 'jicho la tatu,' hatoshindwa kubaini kuwa kuna co-ordinated efforts' za kumchafua mwanasayansi huyo. Kwa bahati nzuri, juhudi hizo zinagonga mwamba kutokana na wananchi wengi kuonekana kumuunga mkono Dokta Mwele huku baadhi wakiamini kuwa ameonewa tu.

Kwa muda mrefu kulikuwa na kile kilichohisiwa kuwa jitihada za makusudi kuhakikisha Dokta Mwele anang'oka katika wadhifa huo. Miongoni mwa jitihada hizo ni pamoja na kuvujishwa hadharani mawasiliano ya kiofisi (yaliyopaswa kubaki ndani ya NIMR pekee) na tuhuma za ufisadi ambazo uchunguzi uliofanyika ulibaini kuwa hazikuwa na ukweli.

Mwaka jana, wakati Dokta Mwele alipochukua fomu za kuwania kuteuliwa kuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya CCM, zilifanyika jitihada za kudukua mawasiliano yake, na uchunguzi ulibaini uhusika wa mwanasiasa mmoja maarufu wa chama hicho ambaye pia anahusishwa na jitihada za muda mrefu 'kuhakikisha Dokta Mwele anang'oka NIMR.' 

Hitimisho: 

Ripoti hii ya kiuchunguzi inaonyesha bayana ukweli kuhusu Dokta Mwele ameondolewa madarakani bila ya hatia yoyote. HAKUFANYA KOSA LOLOTE. Sheria ya NIMR inamruhusu kuripoti kuhusu tafiti mbalimbali kama hiyo ya kuhusu virusi vya Zika. Pia Waziri husika alipewa ripoti ya utafiti huo miezi minne kabla ya Dokta Mwele kuitangaza hadharani. 


Katiba inampa nguvu Rais kuteua na kutengua viongozi wa taasisi mbalimbali za umma. Rais Magufuli alitumia nguvu hiyo ya Kikatiba kuchukua uamuzi huo dhidi ya Dokta Mwele. Hata hivyo, pengine Rais atapata wasaa wa kujiuliza kwanini waziri husika alikuwa na taarifa za utafiti huo tangu mwezi wa Agosti mwaka huu lakini hakuziwasilisha kwake?  Kadhalika, kama Waziri husika hataki kuona ripoti za tafiti mbalimbali zikitangazwa na 'watu walio chini yake' basi na awasilishe muswada bungeni ili sheria iwezeshe hilo.

Mara kadhaa Rais Magufuli amekuwa akiwakumbusha Watanzania kuwa msema kweli ni mpenzi wa Mungu. Basi itakuwa vema asiishie kwenye kuhubiri tu kuhusu usemwa kweli bali sasa atekeleze kwa vitendo na kutafakari upya ukweli kuwa Dokta Mwele hajatendewa haki. Licha ya Dokta Mwele kuwa mchapakazi, kitu ambacho NIMR inajua, Watanzania wanajua na ulimwengu unajua, pia hana kosa katika suala hili. Hii haimaanishi kumfundisha kazi Rais au kumwekea shinikizo bali kushauri haki itendeke.

Kwa upande mwingine, japo ni dhahiri kuwa kutakuwa na nafasi luki za kimtaifa zinazomsubiri Dokta Mwele, hatua iliyochukuliwa dhidi yake inaweza kuwa na athari kubwa katika namna watafiti wanafanya kazi nchini Tanzania. Ikifika mahala watafiti kuhofi kutangaza matokeo ya tafiti zao hata kama wamefuata taratibu zote, watakaoathirika zaidi ni Watanzania.

Na mwisho, kwa vile tumebahatika kuwa na Rais msomi na mwanasayansi basi ni matarajio yetu kuwa ataweka kipaumbele kwenye ukweli kuliko majungu, maana sayansi is all about ukweli na sio hisia. Kadhalika, ni matarajio ya Watanzania kuwa Rais hatoruhusu siasa kuingilia utaalam na/au taaluma. Ikumbukwe kuwa moja ya vikwazo vikubwa vya maendeleo yetu ni siasa kuingilia kila eneo. Ili azma za Tanzania, kwa mfano sera ya 'Tanzania ya viwanda' zitimie, ni lazima tuwasikilize watafiti. Na linapokuja suala la afya ambalo ndio uhai wetu, hatuna hiari wala uchaguzi kuwapuuza wataalamu katika sekta hiyo kama Dokta Mwele.

MUNGU IBARIKI TANZANIA



22 Dec 2016

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.
IJUMAA iliyopita, kulijitokeza tukio ambalo hadi wakati ninaandika makala hii limezua utata. Usiku wa siku hiyo, Rais Dk. John Magufuli alitengua wadhifa wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.
Siku moja kabla, Dk. Mwele alizungumza na waandishi wa habari kuwaeleza kuhusu matokeo ya utafiti wa takriban mwaka mzima kati ya NIMR na Chuo Kikuu cha Bugando kuhusu ugonjwa huo na ilibainika kuwa kati ya sampuli za damu 533, 88 zilikutwa na virusi vya ugonjwa wa zika.
Hata hivyo, siku iliyofuata, serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto ilitoa taarifa kuwa ugonjwa huo haujaingia nchini, kana kwamba taarifa ya Dk. Mwele ilizungumzia kuingia kwa ugonjwa huo.
Pengine kabla ya kuingia kwa undani katika kujadili suala hili, ni vema niweke bayana ukweli kuwa Dk. Mwele ni dada-rafiki yangu, na nimesikitishwa sana na tukio hilo, hususan jinsi wadhifa wake ulivyotenguliwa.
Ni kwamba, wakati taarifa ya wadhifa wake kutenguliwa ilitolewa usiku wa Ijumaa iliyopita, saa chache baadaye, Jumamosi asubuhi, kukatangazwa uteuzi wa Profesa Yunus Mgaya kuchukua wadhifa ulioachwa wazi na Dk. Mwele.
Kama nilivyoeleza awali, hadi wakati ninaandika makala hii kuna utata unaoendelea kuhusu suala hilo. Hiyo imetokana na vitu kadhaa. Kwanza, taarifa ya Ikulu kuhusu uamuzi wa Rais Magufuli kutengua ukurugenzi wa Dk. Mwele haikueleza kwa nini rais alichukua uamuzi huo, tena usiku.
Kadhalika, utata huo unachangiwa na hisia kuwa huenda ‘siku za Dk. Mwele zilikuwa zinahesabika,’ kwani katika mazingira ya kawaida, sio rahisi mkurugenzi wa taasisi nyeti kama NIMR kuondolewa madarakani usiku kisha mbadala wake akapatikana asubuhi.
Hisia hizo zinachangiwa pia na ukweli kuwa Dk. Mwele ni mtoto wa Waziri Mkuu wa zamani, mzee John Malecela. Miezi minane iliyopita, familia ya mwanasiasa huyo mkongwe ilikumbwa na ‘balaa’ kama hili, ambapo Rais Magufuli alimwondoa madarakani mke wa mzee Malecela, mama Anne Kilango, aliyekuwa mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.
Tofauti na wadhifa wa Dk. Mwele ulivyotenguliwa bila maelezo, tukio la mama Kilango liliambatana na maelezo kwamba alitangaza kwenye vyombo vya habari kuwa mkoa wake hauna watumishi hewa jambo ambalo lilisababisha Ikulu kufanya uchunguzi wake na kubaini wafanyakazi hewa 45 katika awamu ya kwanza huku awamu ya pili ya uchunguzi bado ukiendelea.
Katika mazingira ya kawaida, huwezi kumlaumu mtu anayeweza kuhoji “tatizo lilikuwa utendaji kazi wa mama Kilango na Dk. Mwele au ‘mlengwa’ ni mzee Malecela?”
Wasomi kadhaa waliozungumzia hatua ya rais dhidi ya Dk. Mwele wameonyesha kushangazwa kwao, hasa ikizingatiwa kuwa rais naye ni miongoni mwa wasomi. Kwamba, alichofanya Dk. Mwele ni kuripoti tu matokeo ya utafiti husika, lakini kukajitokeza mkanganyiko katika tafsiri ya ripoti ya matokeo hayo.
Laiti busara ingetumika, basi Dk. Mwele angefahamishwa tu kuwa taarifa yake imezua mkanganyiko, na angeitisha mkutano na waandishi wa habari kutoa ufafanuzi. Ikumbukwe kuwa dada huyo ni mmoja wa wanasayansi wachache kabisa kutoka Afrika na hususan Tanzania wanaoheshimika mno kimataifa.
Japo sijapata idhini yake ‘kutoa siri hii,’ mwishoni mwa mwaka jana alinieleza kuwa anahitajiwa na taasisi moja ya kimataifa inayohusiana na masuala ya afya duniani, lakini akasema hayupo tayari kuacha kuwatumikia Watanzania wenzake. Binafsi nilimshauri akubali tu nafasi hiyo kwa vile atakapoitumikia dunia, atakuwa akiitumikia Tanzania pia. Hata hivyo, Dk. Mwele alikataa nafasi hiyo.
Vile vile, baada ya jina lake kutopitishwa kuwania kuteuliwa katika nafasi ya urais kwa tiketi ya CCM mwaka jana, Dk. Mwele alielekeza nguvu zake kumuunga mkono mgombea aliyepitishwa, Dk. Magufuli na kila jioni alitumia muda wake baada ya kazi kufanya ‘majukumu ya kisomi’ katika kampeni za chama chake. Na licha ya kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, baadhi ya vijana aliowakabidhi majukumu ya kampeni za Dk. Magufuli hawajalipwa stahili zao hadi leo (licha ya Dk. Mwele kufuatilia suala hilo kwa zaidi ya mwaka sasa). Linganisha hilo na makada ‘waliozawadiwa’ nafasi mbalimbali licha ya kampeni zao ndani au nje ya chama dhidi ya Dk. Magufuli alipokuwa mgombea.
Mwaka jana nilipata fursa ya kuandika wasifu wake kwenye blogu yangu. Pamoja na mengineyo mengi, alieleza kuwa tangu alipokuwa binti mdogo alikuwa na ndoto ya kuwa mtafiti wa maradhi. Na licha ya kuwa mtoto wa waziri mkuu, ambapo alikuwa na fursa ya ‘kufanya chochote atakacho,’ alifuata ndoto yake ya kitaaluma na kitaalamu, akatumia muda mwingi ‘vichakani na misituni’ kujifunza kuhusu maradhi mbalimbali ya binadamu. Kwa hakika, safari yake tangu utotoni hadi kupata shahada ya uzamivu na hatimaye kuwa mkurugenzi mkuu wa kwanza wa kike wa NIMR, inatoa hamasa kubwa.
Kuna wanaoona kuvuliwa madaraka kwa Dk. Mwele ni kama mwendelezo wa kile kilichomkumba aliyekuwa Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru, ambaye kutenguliwa kwa wadhifa wake hivi karibuni kunatafsiriwa kama matokeo ya yeye kutoa maoni yake ya kitaalamu kuhusu suala fedha za taasisi za serikali kuwekwa kwenye akaunti za muda maalumu (fixed deposits).
Nihitimishe makala hii kwa kumpa pole Dk. Mwele huku nikiamini kuwa muda si mrefu ataipatia fahari Tanzania kama mwanasayansi wa kimataifa. Kadhalika, inasikitisha kuona tukio hili ilhali majuzi tumeshuhudia teuzi za baadhi ya mabalozi zikifanywa kwa kigezo cha ukada

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.