21 Apr 2018


Jana ilitolewa taarifa kwa vyombo vya habari  kuwa Rais John Magufuli amemteua "Msalika Robert Makungu kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora." Hata hivyo, kwa makusudi, taarifa haikueleza kabla ya uteuzi huo, Makungu alikuwa na wadhifa gani, japo ilieleza kuwa anakwenda mkoani Tabora kuchukua nafasi ya Dokta Thea Ntara ambaye amestaafu.



"Kilichofichwa" kwenye taarifa hiyo ni ukweli kwamba Makungu alikuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa (DDGIS) ambaye aliteuliwa wakati mmoja na Mkurugenzi Mkuu wa Idara hiyo, Dokta Modestus Kipilimba, Agosti mwaka jana.

Japo taarifa husika haikutumia neno "kutumbuliwa," lakini haihitaji ufahamu wa mfumo wa utawala wa Idara ya Usalama wa Taifa kumaizi kwamba kutoka u-Naibu Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo nyeti hadi u-Katibu Tawala wa Mkoa ni kushushwa cheo (demotion). 

Kwa mujibu wa vyanzo vyangu vya kuaminika ndani ya taasisi hiyo, kilichopelekea hatua hiyo inayoelezwa kuwa ngumu kwa  Magufuli ni tofauti kati ya watendaji hao wakuu wa taasisi hiyo, yaani Makungu na aliyekuwa bosi wake, yaani Kipilimba.

Inaelezwa kuwa tofauti kati yao ilikuwa kubwa kiasi cha Kipilimba kutishia kujiuzulu iwapo Magufuli asingechukua hatua dhidi ya Makungu.

Hata hivyo, Makungu alikuwa "mtu wa Magufuli" kwa sababu ni wote wanatoka Kanda ya Ziwa, na ni miongoni mwa "circle ya karibu ya Magufuli" ambayo pamoja na watu wengine, inayojumuisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Katibu Mkuu wa Hazina Dotto James, na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga.

Kwahiyo wakati  ingetarajiwa Magufuli "angemkumbatia poti wake Makungu" lakini kwa mujibu wa vyanzo vyangu, umuhimu wa Kipilimba kwa Magufuli ni mkubwa zaidi. 

Tukio hilo ambalo halikuvuta hisia za wengi hasa kwa vile lilitokea muda mfupi baada ya kupatikana taarifa za kifo cha mlimbwende maarufu Agnes Masogange aliyefariki jijini Dar jana.

Japo wadhifa wa "Naibu Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa" (DDGIS) sio wa muda mrefu tangu uanzishwe (Makungu alikuwa mtu wa pili kushika wadhifa huo baada ya Jack Zoka kuwa wa kwanza), kitendo tu cha Mkurugenzi katika taasisi hiyo kutolewa na kupelekwa mkoani ni cha kushangaza na kinaingia moja kwa moja kwenye kumbukumbu za kihistoria.

Hata hivyo, kabla ya Makungu "kutumbuliwa" tayari kuna Mkurugenzi mwingine ambaye aliondolewa kwenye wadhifa wake kama  nilivyoripoti kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana wakati huo, kuondoka kwa mwanamama huyo kulichangiwa na mtazamo wake wa kutaka mabadiliko ndani ya taasisi hiyo ambao ulikinzana na wahafidhina wasiotaka mabadiliko yoyote kwa taasisi hiyo.

Wakati hayo yanatokea, Zoka, aliyekuwa Balozi wa Tanzania huko Canada nae alitolewa katika wadhifa huo hivi karibuni. Nilieleza kwa kirefu kuhusu tukio hilo katika makala HII

Kama ambavyo Zoka aliandamwa na lawama kwamba alikuwa akiongoza mkakati wa kuhujumu vyama vya upinzani, Makungu pia ametoka katika nafasi hiyo akikabiliwa na lawama kama hizo.


Kwa upande wangu binafsi kama afisa wa zamani katika taasisi hiyo, wakati fulani nililazimika kumwandikia barua Makungu kutokana na taarifa flani zilzonikera. Na katika barua hiyo nilimkumbusha kuwa cheo ni dhamana, na hakina mwamana.


Tatizo kwa wenzetu wengi wanaposhika madaraka ni ile hali ya kujisahau wakidhani watafia wakiwa kwenye madaraka. Hupuuzia ukweli kuwa ipo siku watatoka katika nafasi zinazowapa jeuri na kujikuta "mtaani." Maisha hayatabiriki, leo unalala ukiwa DDGIS kesho unaamka ukiwa RAS.



Kuhusu iwapo hatua hiyo ya Magufuli kuwa na atahri zozote, kwa sasa ni mapema mno kubashiri. Baadhi ya maafisa waliopo kazini na wastaafu  wa Idara ya Usalama wa Taifa walidokeza kwamba taarifa hiyo ya kuondolewa kwa Makungu imewashtua wengi

 Kwa upande mwingine, wakati yote haya yanatokea, haijafahamika hali ikoje kwa "Idara ya Usalama wa Taifa nje ya Idara ya Usalama wa Taifa," yaani kile kikosi kilicho chini ya Daudi Alabert Bashite.



Kwamba Kipilimba ameweza kumn'goa "poti wa Magufuli" Makungu, basi huenda pia akawezesha kung'oka kwa Bashite, mtu anayeutia doa utawala wa Magufuli kwa kila hali.



Ni muhimu pia kujumuisha tweet ya mtu mmoja ambaye hujitambulisha kama Gavana wa zamani wa Benki Kuu, Daudi Balali.


Nimalizie makala hii kwa kukushauri uwe ukiitembelea blogu hii mara kwa mara upate fursa adimu ya kusoma uchambuzi exclusive kama huu wa leo.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.