Showing posts with label Modestus Kipilimba. Show all posts
Showing posts with label Modestus Kipilimba. Show all posts

29 Feb 2020


Somo: Kuvuliwa uanachama Bernard Membe, Waziri Wa Zamani wa Mambo ya Nje, Mbunge wa zamani, kada mkongwe na mmoja wa wana CCM walioingia "tano bora" ya kutafuta mgombea urais kwa tiketi ya CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015

Key subject(s)

  1. Bernard Kamilius Membe
  2. John Pombe Magufuli
  3. Jakaya Mrisho Kikwete
  4. Modestus Kipilimba
Dhana ya kwanza: Membe "anakubali matokeo," anaamua kuachana na siasa. 

Dhana ya pili: Membe "anafanyiziwa."

Dhana ya tatu: Membe "anakubali matokeo," anaamua kujiunga na chama cha upinzani

Dhana ya nne: Membe hakubali matokeo, anaamua "kutafuta haki yake" CCM.

Dhana ya tano: Membe hakubali matokeo, anaamua "kutafuta haki yake" nje ya CCM

Ushahidi: Hadi muda huu Membe hajatoa tamko rasmi kuhusu mustakabali wake. Kwahiyo dhana zote nne zinasimama kama zilivyo kwa vile hakuna ushahidi wa kupelekea kuziondoa.

Kipimo/Vipimo: Haipo muda huu mpaka Membe atoe tamko rasmi. Dhana zote zinaendelea kubaki hai.

Mchujo: Kwa kuzingatia kuwa Membe hakuomba msamaha alipoitwa kwenye vikao husika, na kwa kuzingatia "damu mbaya" (bad blood)kati yake na Rais John Pombe Magufuli, tangu mwanzo wa Awamu ya Tano, yayumkinika kuamini kuwa uwezekano wa Membe "kutafuta haki yake" CCM ni hafifu.
Vigezo hivyo vinafanya uwezekano wa Dhana Ya Nne kutimia kuwa ni hafifu. Kwa mantiki hiyo, dhana hiyo inaondoshwa (yaweza kurejeshwa huko mbeleni)

Walakini: Hakuna

Unyeti: upo katika maeneo yafuatayo
  1. Membe ni mmoja wa makada zaidi ya 40 wa CCM waliojitokeza kuwania kupitishwa na chama hicho kwenye nafasi ya urais wa JMT.
  2. Membe alikuwa mpinzani mkuu wa Edward Lowassa kada aliyekuwa anapewa nafasi kubwa ya kuwa mrithi wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, na ambaye baada ya kutopitishwa CCM alihamia Chadema, japo baadaye alirudi tena CCM.
  3. Membe alikuwa miongoni mwa "tano bora" pamoja na Magufuli, January Makamba, Amina Ali na Asha Rose Migiro
    Migiro
  4. Membe ni swahiba mkubwa wa Rais mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete
  5. Membe ni mwanachama wa kwanza wa CCM "mwenye hadhi ya kitaifa"kufukuzwa uanachama.
Uchambuzi:

Uzito wa dhana ya kwanza kwamba Membe atakubali matokeo na kuachana na siasa upo kwenye hoja kwamba kutokana na uzoefu wake ndani ya CCM, anafahamu kuwa jaribio lolote la kuendelea na "maisha ya kisiasa" litakumbwa na upinzani na vikwazo vingi kutoka kwa Magufuli na CCM kwa ujumla.

Kadhalika, kama shushushu wa zamani, Membe anafahamu kuwa yeye sasa ni "high value target" huko Idara ya Usalama wa Taifa, ambapo kila nyendo yake sio tu itafuatiliwa kwa karibu bali pia anaweza "kuchanganywa akili" kwa kufanyiwa "overt surveillance" (kumfuatilia mlengwa bila kificho, lengo likiwa kumjulisha kuwa anafuatiliwa. Mbinu hii hutumika zaidi "kumchanganya akili" mlengwa).

Mapungufu ya dhana ni ukweli kwamba Membe ni "high value target" pia kwa vyama vya upinzani, na kwa kuzingatia kuwa huu ni mwaka wa uchaguzi, anaweza kupewa fursa ya "kulipa kisasi dhidi ya Magufuli kwa kupitishwa kuwa mgombea wa chama cha upinzani."

Mapungufu mengine katika dhana ya kwanza  ni "dalili za awali" kuwa "huu sio mwisho wa Membe kisiasa."

Uzito wa dhana ya pili upo katika ukweli kwamba Magufuli " hana mshipa wa aibu." Kama aliweza "kuamuru Lissu afanyiziwe," hashindwi kutoa maagizo kama hayo dhidi ya Membe.

Uzito mwingine upo kwenye ukweli kwamba shushushu wa zamani Membe nje ya CCM anabaki kuwa tishio kuliko alipokuwa mwanachama "anayebanwa na taratibu za chama."

Uzito mwingine ni ukweli kwamba Membe ni swahiba na watu wawili muhimu kwenye siasa za Tanzania, na ambao huenda wakawa na influence kwenye uchaguzi mkuu ujao, Rais Mstaafu Kikwete na Mkurugenzi wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa, na sasa balozi wa Tanzania Namibia, Dkt Modestus Kipilimba. Japo watu hawa wawili, kama ilivyo kwa Membe sasa, nao ni "high value targets" ambao sio tu wanafuatiliwa na mawasiliano yao kusikilizwa (uwepo wa walinzi unarahisisha zoezi hilo), lakini wanaweza kuwa nguzo muhimu kwaMembe "kulipa kisasi."

Kwa vile Kipilimba yupo nje ya nchi, na Kikwete huwa safarini mara kwa mara, kuwafuatilia kwa utimilifu wa asilimia 100 ni kugumu, na ikizingatiwa kuwa Membe ni shushushu wa zamani, anaweza kufanikisha mawasiliano nao na kuepa "surveillance" (kufuatiliwa) na "bugging" (kunasa mawasiliano).

Mapungufu ya dhana yapo kwenye ukweli kuwa japo "Magufuli hana mshipa wa aibu," na hivyo anaweza "kumfanyizia" Membe, lolote litakalomtokea Membe kati ya sasa na Oktoba litatafsiriwa moja kwa moja kuwa ni "mkono wa Magufuli." Na hilo linaweza kuwafanya "mabeberu kumrukia kama mwewe."

Na ikumbukwe kama Waziri wa Mambo ya Nje kwa miongo miwili, Membe atakuwa na "connections" kubwana nzito huku ughaibuni. Akidhuriwa na Magufuli, yawezekana kabisa "mabeberu" wakaamua kuharakisha utekelezaji wa mkakati wa kumng'oa kiongozi huyo.

Uzito wa dhana ya tatu ni ukweli kwamba kujiunga na chama cha upinzani sio tu kunaweza kumpatia fursa ya "kulipa kisasi kwa Magufuli, kwa kuwa mpinzani wake kwenye uchaguzi mkuu ujao (kwa kuamini kuwa atapitishwa kuwa mgombea urais katika chama chochote atakachohamia)," pia itakuwa nafasi adimu kwake kufanya jaribio jingine la kuwania urais wa Tanzania.

Uzito mwingine wa dhana hii ni kauli za Kiongozi Mkuu wa chama cha Wazalendo (ACT),Zitto Kabwe baada ya tangazo kuhusu kufukuzwa kwa Membe huko CCM, Kauli hizo zilikuwa na harufu ya "karibu kwetu."




Mapungufu ya dhana hii yapo kwenye ukweli kwamba hata kama Membe ataamua kujiunga na chamacha upinzani, vikwazo na usumbufu kutoka kwa Magufuli kupitia Idara ya Usalama wa Taifa vinaweza kumfanya "atamani ardhi immeze."

Kingine ni ukweli kwamba "Membe sio msafi kihivyo," na hiyo inaweza kumrahisishia Magufuli "kumzulia kesi ya utakatishaji fedha na/au uhujumu uchumi." 

Vivilevile, Idara ya Usalama wa Taifa inaweza kumshurutisha Membe asijiunge na chama kingine, hasa ikizingatiwa kuwa Magufuli amekuwa akiitumia taasisi hiyo kuwatisha na kuwahujumu wapinzani wake au/na wakosoaji/wanaharakati.

Kadhalika, licha ya Zitto kuonyesha dalili za awali za uwezekano wa "Membe kuhamia ACT-Wazalendo," kwa kuwa hatujui Maalim Seif na "ACT-Zanzibar" wana mtazamo gani kuhusu "ujio wa Membe," na ukweli kuwa wanaweza kumkataa, yawezekana Membe kuhamia chama hicho kusitokee.

Uzito kwenye dhana ya tano upo kwenye ukweli kwamba endapo atatumia vema ujuzi wake kama shushushu mstaafu, na endapo atapata sapoti kutoka kwa Kikwete na Kipilimba, Membe anaweza kuwa tishio nje ya CCM bila hata kujiunga na chama kingine cha siasa. 

Ukweli kwamba kuna wana-CCM wengi tu wanaotamani Magufuli aondoke hata kesho unaweza kumsaidia Membe kupata "marafiki" wengine muhimu ndani ya chama hicho, ambao pamoja nao wanaweza kuanzisha harakati za kumng'oa Magufuli.

Mapungufu ya dhana hii ukweli kwamba kwa nchi ambayo "ili nguvu za kisiasa shurti uwe mwanasiasa," uwezekano wa Membe kuwa na "nguvu" nje ya mfumo wa kisiasa ni mdogo.

Mchanganuo: Kwa upande mmoja, uamuzi wa Magufuli kumfukuza Membe unaelezea zaidi kuhusu yeye kuliko kilichompata Membe. Ukweli kwamba jina la Membe limekuwa likitajwa mara kadhaa kuhusiana na kinyang'anyiro cha urais mwaka huu, uamuzi huo wa Magufuli unatafsiriwa kuwa ni UOGA. Kwa kifupi, Magufuli amemuogopa Membe akiwa ndani ya CCM na ndio maana akashinikiza afukuzwe chamani.

Hofu ya Magufuli kwa Membe haina mashiko. Membe hakupaswa kushika nafasi ya tano kwenye "tano bora" ya kumtafuta mgombea urais kwa tiketi ya CCM, huku akiambulia kura 120 tu, nyuma ya JanuaryMakamba (124), Migiro (280),Amina Ali  (284) na Magufuli (290). Hakupaswa kushika nafasi hiyo kwa sababu kuu mbili. Kwanza, yeye ndiye alikuwa "front runner," kwa kuzingatia kuwa ndiye alikuwa mpinzani mkuu wa Lowassa.Na pili ni uswahiba wake na Kikwete na familia yake. Kingine cha kuongezea hapo ni ukaribu wake na maafisa mbalimbali wa Idara ya Usalama wa Taifa ambayo aliwahi kuitumikia huko nyuma.

Membe hakuwa na sababu moja ya msingi ya kutoibuka mshindi kwenye kinyang'anyiro hicho. Sasa sijui hiyo hofu ya Magufuli inatoka wapi. 

Ubashiri: Endapo Magufuli "hatomfanyizia" Membe, kuna uwezekano mwanasiasa huyo akajiunga na ACT- Wazalendo. Lakini kujiunga huko kutategemea endapo Maalim Seif na "ACT - Zanzibar) wataridhia. Hata hivyo, intelijensia sio sayansi timilifu, na matokeo ya ubashiri huu yanaweza kuwa tofauti.

Hitimisho: Suala hili lina sura mbili. Moja ni ukweli kwamba udikteta wa Magufuli sasa umepiga hodi ndani kabisa ya CCM.Pili, mpira upo mikononi mwa Membe. Akipanga karata zake vizuri, anaweza kutoa upinzani japo kidogo kwa Magufuli hapo Oktoba. Anaweza kuwa Rais ajaye wa Tanzania? Uwezekano huo ni hafifu japo wanasema "never say never in politics."

Uchambuzi huu ni endelevu. Utakuwa updated kadri kunapotokea maendeleo mapya.









21 Apr 2018


Jana ilitolewa taarifa kwa vyombo vya habari  kuwa Rais John Magufuli amemteua "Msalika Robert Makungu kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora." Hata hivyo, kwa makusudi, taarifa haikueleza kabla ya uteuzi huo, Makungu alikuwa na wadhifa gani, japo ilieleza kuwa anakwenda mkoani Tabora kuchukua nafasi ya Dokta Thea Ntara ambaye amestaafu.



"Kilichofichwa" kwenye taarifa hiyo ni ukweli kwamba Makungu alikuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa (DDGIS) ambaye aliteuliwa wakati mmoja na Mkurugenzi Mkuu wa Idara hiyo, Dokta Modestus Kipilimba, Agosti mwaka jana.

Japo taarifa husika haikutumia neno "kutumbuliwa," lakini haihitaji ufahamu wa mfumo wa utawala wa Idara ya Usalama wa Taifa kumaizi kwamba kutoka u-Naibu Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo nyeti hadi u-Katibu Tawala wa Mkoa ni kushushwa cheo (demotion). 

Kwa mujibu wa vyanzo vyangu vya kuaminika ndani ya taasisi hiyo, kilichopelekea hatua hiyo inayoelezwa kuwa ngumu kwa  Magufuli ni tofauti kati ya watendaji hao wakuu wa taasisi hiyo, yaani Makungu na aliyekuwa bosi wake, yaani Kipilimba.

Inaelezwa kuwa tofauti kati yao ilikuwa kubwa kiasi cha Kipilimba kutishia kujiuzulu iwapo Magufuli asingechukua hatua dhidi ya Makungu.

Hata hivyo, Makungu alikuwa "mtu wa Magufuli" kwa sababu ni wote wanatoka Kanda ya Ziwa, na ni miongoni mwa "circle ya karibu ya Magufuli" ambayo pamoja na watu wengine, inayojumuisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Katibu Mkuu wa Hazina Dotto James, na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga.

Kwahiyo wakati  ingetarajiwa Magufuli "angemkumbatia poti wake Makungu" lakini kwa mujibu wa vyanzo vyangu, umuhimu wa Kipilimba kwa Magufuli ni mkubwa zaidi. 

Tukio hilo ambalo halikuvuta hisia za wengi hasa kwa vile lilitokea muda mfupi baada ya kupatikana taarifa za kifo cha mlimbwende maarufu Agnes Masogange aliyefariki jijini Dar jana.

Japo wadhifa wa "Naibu Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa" (DDGIS) sio wa muda mrefu tangu uanzishwe (Makungu alikuwa mtu wa pili kushika wadhifa huo baada ya Jack Zoka kuwa wa kwanza), kitendo tu cha Mkurugenzi katika taasisi hiyo kutolewa na kupelekwa mkoani ni cha kushangaza na kinaingia moja kwa moja kwenye kumbukumbu za kihistoria.

Hata hivyo, kabla ya Makungu "kutumbuliwa" tayari kuna Mkurugenzi mwingine ambaye aliondolewa kwenye wadhifa wake kama  nilivyoripoti kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana wakati huo, kuondoka kwa mwanamama huyo kulichangiwa na mtazamo wake wa kutaka mabadiliko ndani ya taasisi hiyo ambao ulikinzana na wahafidhina wasiotaka mabadiliko yoyote kwa taasisi hiyo.

Wakati hayo yanatokea, Zoka, aliyekuwa Balozi wa Tanzania huko Canada nae alitolewa katika wadhifa huo hivi karibuni. Nilieleza kwa kirefu kuhusu tukio hilo katika makala HII

Kama ambavyo Zoka aliandamwa na lawama kwamba alikuwa akiongoza mkakati wa kuhujumu vyama vya upinzani, Makungu pia ametoka katika nafasi hiyo akikabiliwa na lawama kama hizo.


Kwa upande wangu binafsi kama afisa wa zamani katika taasisi hiyo, wakati fulani nililazimika kumwandikia barua Makungu kutokana na taarifa flani zilzonikera. Na katika barua hiyo nilimkumbusha kuwa cheo ni dhamana, na hakina mwamana.


Tatizo kwa wenzetu wengi wanaposhika madaraka ni ile hali ya kujisahau wakidhani watafia wakiwa kwenye madaraka. Hupuuzia ukweli kuwa ipo siku watatoka katika nafasi zinazowapa jeuri na kujikuta "mtaani." Maisha hayatabiriki, leo unalala ukiwa DDGIS kesho unaamka ukiwa RAS.



Kuhusu iwapo hatua hiyo ya Magufuli kuwa na atahri zozote, kwa sasa ni mapema mno kubashiri. Baadhi ya maafisa waliopo kazini na wastaafu  wa Idara ya Usalama wa Taifa walidokeza kwamba taarifa hiyo ya kuondolewa kwa Makungu imewashtua wengi

 Kwa upande mwingine, wakati yote haya yanatokea, haijafahamika hali ikoje kwa "Idara ya Usalama wa Taifa nje ya Idara ya Usalama wa Taifa," yaani kile kikosi kilicho chini ya Daudi Alabert Bashite.



Kwamba Kipilimba ameweza kumn'goa "poti wa Magufuli" Makungu, basi huenda pia akawezesha kung'oka kwa Bashite, mtu anayeutia doa utawala wa Magufuli kwa kila hali.



Ni muhimu pia kujumuisha tweet ya mtu mmoja ambaye hujitambulisha kama Gavana wa zamani wa Benki Kuu, Daudi Balali.


Nimalizie makala hii kwa kukushauri uwe ukiitembelea blogu hii mara kwa mara upate fursa adimu ya kusoma uchambuzi exclusive kama huu wa leo.

27 Aug 2016

Tarehe 24 mwezi huu, Rais Dokta John Magufuli alimteua Dokta Modestus Kipilimba kuwa Mkurugenzi Mkuu (DGIS) wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS). Uteuzi huo umefanyika kufuatia kustaafu kwa mkurugenzi aliyemaliza muda wake, Othman Rashid.

Makala hii inajikita katika uchambuzi wa uteuzi huo kwa kuangalia changamoto na fursa zinazomkabili kiongozi huyo mkuu wa taasisi hiyo nyeti kabisa. Kwa mtizamo wangu, kama kuna kitu ambacho kinaweza kuzua maswali kuhusu uteuzi huo basi ni wadhifa wa Director of Risk Management alioshikilia Dokta Kipilimba huko nyuma alipokuwa mtumishi wa Benki Kuu ya Tanzania.

Sote twafahamu jinsi Benki Kuu yetu imekuwa ikiandamwa na matukio mfululizo ya ufisadi, kuanzia EPA hadi Tegeta Escrow. Kwa wadhifa wake katika taasisi hiyo, kuna uwezekano wa bosi huyo mpya wa mashushushu kuonekana ‘sehemu ya mfumo ulioshindwa kudhibiti ufisadi.’ Hata hivyo, utetezi unaweza kuwa huenda yeye alitekeleza majukumu yake vema lakini walio juu yake hawakuchukua hatua stahili.

Kadhalika, huko mtandaoni kuna ‘tuhuma’ kadhaa kuhusu Dokta Kipilimba, lakini itakuwa sio kumtendea haki yeye, blogu hii na mie mwenyewe kujadili tuhuma ambazo hazina ushahidi wowote. Ni muhimu kutambua kuwa Tanzania yetu licha ya kuwa kisiwa cha amani pia ni kisiwa cha majungu, uzandiki, fitna, umbeya na uzushi.

Changamoto kubwa kwa Dokta Kipilimba ni pamoja na kurejesha hadhi na heshima ya Idara ya Usalama wa Taifa. Katika miaka ya hivi karibuni, taasisi hiyo muhimu kabisa imekuwa ikishutumiwa kuwa inachangia ustawi wa ufisadi, ujangili, biashara ya madawa ya kulevya, nk.

Wanaoilaumu taasisi hiyo hawamaanishi kuwa watumishi wake wanahusika katika matukio hayo ya kihalifu as such bali kushindwa kwa Idara hiyo kukabiliana na kushamiri kwa matendo hayo ya kihalifu, ambayo kimsingi ni matishio kwa usalama wa taifa, na kazi kuu ya Idara hiyo ni kukabiliana na matishio kwa usalama wa taifa la Tanzania.

Ninaamini kuwa Dokta Kipilimba anafahamu kanuni muhimu kuhusu ufanisi au mapungufu ya idara ya usalama wa taifa popote pale duniani, kwamba “kushamiri kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa lolote lile ni kiashiria cha mapungufu ya idara ya usalama wa taifa ya nchi husika, na kudhibitiwa kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa popote pale duniani ni kiashiria cha uimara wa idara ya usalama wa taifa ya nchi husika.”

Kwahiyo, kwa kuzingatia kanuni hiyo, kushamiri kwa biashara ya madawa ya kulevya, ujangili, rushwa, na ufisadi mwingine ni viashiria vya mapungufu ya Idara yetu ya Usalama wa Taifa.

Changamoto nyingine kwa Dokta Kipilimba ni tuhuma za mara kwa mara dhidi taasisi hiyo muhimu kabisa kuwa katika utendaji kazi wake imegeuka kuwa kama ‘kitengo cha usalama cha chama tawala CCM.’ Idara hiyo imekuwa ikituhumiwa kuwa kwa kiasi kikubwa imeweka kando taaluma ya ushushushu (tradecraft) na kutekeleza majukumu yake kisiasa.

Madhara ya muda mfupi ya kasoro hiyo ni taasisi hiyo kujenga uhasama na vyama vya upinzani na kwa namna flani kupoteza heshima na uhalali wake. Lakini la kuogofya zaidi ni madhara ya muda mrefu, ambapo watu wanaoweza kuwa ni matishio kwa usalama wa taifa letu wanaweza kutumia ‘urafiki’ unaodaiwa kuwepo kati ya Idara ya Usalama wa Taifa na CCM, wakitambua bayana kuwa ‘Idara haina muda na makada wa chama tawala,’ na hatimaye kufanikiwa kutimiza azma zao ovu.

Baadhi ya watumishi wa zamani wa taasisi hiyo walijikuta matatizoni kwa vile tu walitekeleza majukumu yao dhidi ya wanasiasa wa chama tawala, na wakaishia kuonekana kama wahaini.

Changamoto nyingine kwa Dokta Kipilimba ni tuhuma zinazoikabili taasisi hiyo kuhusu mfumo wa ajira ambapo inadaiwa kuwa zimekuwa zikitolewa kwa upendeleo kwa ndugu na jamaa za ‘vigogo.’ Tatizo kubwa hapa ni kwamba utiifu wa ‘ndugu na jamaa hao wa vigogo’ haupo kwa taifa bali kwa vigogo hao waliowaingiza Idarani. Pengine sio vibaya kufikiria ‘utaratibu wa wazi’ katika ‘recruitment’ kama inavyofanywa na wenzetu wa CIA, NSA, MI5, MI6, HGCQ, nk wanaotangaza nafasi za ajira kwenye vyombo vya habari.

Pia kuna tatizo la baadhi ya maafisa usalama wa taifa ‘kujiumbua’ kwa makusudi kwa sababu wanazojua wao wenyewe, kubwa ikiwa kutaka sifa tu, au waogopwe ‘mtaani.’ Hii inaathiri sana ufanisi wa maafisa wa aina hiyo kwani ni vigumu kutekeleza majukumu yao ipasavyo pasi usiri.

Sambamba na hilo ni kasumba ya muda mrefu ambapo baadhi ya maafisa wa Idara hiyo waliopo kwenye vitengo mbalimbali kuwepo huko kwa muda mrefu mno kiasi cha kuathiri utendaji wao. Miongoni mwa maeneo hayo ni pamoja na ‘vituo muhimu’ na kwenye ofisi za balozi zetu nje ya nchi. Ikumbukwe kuwa unless afisa ametengeneza deep cover, uwepo wake kwa muda mrefu katika sehemu aliyokuwa ‘penetrated’ au kituo chake cha kazi kwingineko (mfano ubalozini) unaweza kupelekea ‘akaungua’ (burned).

Changamoto nyingine kubwa ni uwepo wa majasusi kibao nchini mwetu, hususan kutoka nchi moja jirani, huku wengi wa majasusi hao wakiwa wameajiriwa katika taasisi za umma na binafsi. Hili ni tishio kubwa kwa usalama wa taifa wa Tanzania yetu.

Kwa upande fursa kwa Dokta Kipilimba, licha ya kuwa ‘mwenyeji’ katika taasisi hiyo muhimu, wasifu wake kitaaluma unamweka katika nafasi nzuri sana kukabiliana na changamoto za karne ya 21 ambayo imetawaliwa zaidi na teknolojia ya kisasa.

Dokta Kipilimba ni msomi aliyebobea kwenye teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) na yayumkinika kuamini kuwa anaweza kutumia usomi wake kuibadilisha Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwenda na wakati, kufanya kazi kama taasisi ya kishushushu ya karne ya 21, ambayo licha ya kutegemea HUMINT inaweza pia kutumia njia nyingine za kukusanya taarifa za kiusalama kwa kutumia teknolojia (GEOINT, MASINT, SIGINT, CYBINT, FININT na TECHINT kwa ujumla)

Na katika kwenda na teknolojia ya kisasa, basi pengine si vibaya iwapo Idara yetu ikafikiria haja ya uwepo wake kwenye mtandao, kwa kuwa na tovuti yake kamili na pia kufungua akaunti kwenye mitandao ya kijamii, hususan Twitter na Facebook. Hii sio tu inaweza kusaidia kutengeneza "human face" ya intel service bali pia yatoa fursa nzuri katika OSINT.

Fursa nyingine kwa Dokta Kipilimba ni matarajio ya sapoti ya kutosha kutoka kwa Rais Dokta Magufuli ambaye kama alivyoahidi wakati wa kampeni za kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka jana, mapambano dhidi ya ufisadi yamepewa kipaumbe cha hali ya juu kabisa. Kama ‘sponsor’ na ‘consumer’ wa taarifa za kila siku usalama, inatarajiwa kuwa Dokta Magufuli atatekeleza ushauri wa Idara katika kukabiliana na matishio mbalimbali ya usalama wa taifa letu.

Dokta Kipilimba ana fursa ya kuleta mageuzi kwa Idara ya Usalama wa Taifa kwa kuangalia uwezekano wa kuwafikia watu walio nje ya taasisi hiyo, hasa pale uwezo wa Idara yetu unapokuwa limited. Nitoe mfano. Katika kupata taarifa mwafaka wa kudumu kuhusu, kwa mfano, mgogoro wa kisiasa huko Zanzibar, Idara inaweza ku-reach out wanazuoni wa historia ya taifa letu walipo ndani na nje ya nchi yetu.

Ikumbukwe kuwa sio rahisi kwa taasisi hiyo kuwa na maafisa au watoa habari katika kila eneo. Wenzetu wa nchi za Magharibi wamekuwa wakikabiliana na hali hiyo kwa kufanya kazi na ‘makandarasi’ (contractors), ambao of course, wamekidhi taratibu kama vile vetting.

Sambamba na hilo ni Idara hiyo kuangalia uwezekano wa kutumia hazina kubwa tu ya maafisa wake wa zamani, hususan wastaafu. Ikumbukwe kuwa wengi wao ni watu wanaowindwa na ‘subjects’ mbalimbali wanaolenga kulihujumu taifa letu.

Nimalizie makala hii kwa kutoa pongezi za dhati kwa Dokta Kipilimba na Naibu wake (DDGIS) Robert Msalika, sambamba na kumtakia mapumziko mema Mkurugenzi mstaafu Othman, na kumkaribisha ‘uraiani.’

MUNGU IBARIKI TANZANIA, MUNGU IBARIKI IDARA YETU YA USALAMA WA TAIFA




Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.