Showing posts with label NDUGAI. Show all posts
Showing posts with label NDUGAI. Show all posts

25 Jun 2011

Kabla ya kuwaletea habari na picha kuhusu ziara ya wabunge kadhaa waliokuja hapa Uingereza kufuatilia malipo ya fedha za rada,ninaomba kuweka bayana mtizamo wangu katika suala hili.Kwanza,naona kilichofanywa na wabunge hao ni mithili ya kuuza ng'ombe kwa ajili ya kesi ya kuku.Nilitamani walioongea na wabunge hao kuwauliza umuhimu wa wao kuwepo Uingereza muda huu ambapo kikao cha Bunge la Bajeti kinaendelea huko Dodoma.Kuna dharura gani kwa wao kuja hapa muda huu badala ya kusubiri kikao hicho cha Bunge kimalizike?Je wanawatendea haki wapiga kura wao?Na nani anawawakilisha wapiga kura wao wakati huu?

Nimesema hii ni sawa na kuuza ng'ombe kwa ajili ya kumudu kesi ya kuku kwa vile kila mbunge aliyekuja analipwa mamilioni ya fedha kama posho za kujikimu.Waheshimiwa hawa wanadai fedha za rada zitatumika kuendeleza elimu ya watoto huko nyumbani.Swali la kwanza,kwanini wasingeokoa fedha zinazotumika kama posho zao kwa muda wote watakapokuwa hapa Uingereza,kisha fedha hizo zikaelekezwa kwenye elimu ya watoto wetu huko nyumbani?Binafsi,nadhani suala hilo lingeweza kabisa kushughulikiwa na ubalozi wetu hapa Uingereza unless watuambie kuwa hawana imani na utendaji kazi na Balozi wetu Peter Kallaghe (ambaye ninamfahamu vizuri kuwa ni mchapa kazi mahiri tangu alipokuwa huko Foreign Affairs na Ikulu--nimefanya nae kazi pasipo kufahamiana,just in case you doubt my assessment of him).

Lakini la muhimu zaidi ni ukweli kwamba historia inatufundisha kwamba fedha za aina hii husihia mifukoni mwa wajanja wachache.Sana sana zitawezesha kumalizika kwa ujenzi wa mahekalu ya vigogo,kama sio kuongeza idadi ya nyumba ndogo zao na misururu ya magari yao ya kifahari.Hivi waheshimiwa hawa wanaweza kutuambia kwanini wanatolea macho hayo mamilioni ya rada ilhali wameshindwa kuhoji kuhusu marejesho ya fedha za EPA?Vipi kuhusu zile fedha za mfuko wa pembejeo?Vipi kuhusu "stimulus package" yetu ya kizushi?

Let's be honest,na nilitegemea sana wanahabari waliotuwakilisha kwenye press conference ya wabunge hao wangeibua hoja hizi,waheshimiwa hawa wamekuja Uingereza kutalii tu.Period!So far,katika habari husika hawatuelezi namna gani ujio wao utawezesha fedha hizo kupatikana,na kutuhakikishia kuwa kweli zitaelekezwa kwenye elimu ya watoto wetu.Remember,kamwe tatizo la viongozi wetu halijawahi kuwa kwenye upungufu wa maneno matamu bali utekelezaji wa ahaid wanazojiwekea wao wenyewe.

Anyway,naomba kuwasilisha habari husika kama nilivyotumiwa na Miss Jestina

Wabunge wanne waliokuja Uingereza kuzungumzia mgogoro wa pesa za kampuni inayouza vifaa vya ulinzi –BAE Systems wamefafanua namna zitakavyotumiwa. Wakiongea katika Ubalozi wetu Uingereza mjini London, Ijumaa mchana, viongozi hao walihimiza wanachofanya ni kufuatilia matokeo ya mahakama ya sheria inayochunguza rushwa (Serious Fraud Office-SFO) maana kadri muda unavyokwenda ndivyo riba inaongezeka.
Wabunge walikutana na House of Lords ambao ni maofisa na viongozi wa ngazi za juu sana wenye usemi mzito katika masuala ya kisisiasa Uingereza.

Mwezi Desemba mwaka jana SFO iliiamuru kampuni ya BAE kulipa faini paundi laki tano na kuipa serikali ya Tanzania paundi 29.5 milioni sawa na shilingi 75.3 bilioni za kitanzania kama pesa za kujisafisha uso. Toka tamko hilo litokee miezi sita iliyopita imezuka migogoro kadhaa.
Upande mmoja BAE system wanataka fedha zisipewe serikali ya Tanzania bali kwa mashirika ya fadhila toka nchi za nje upande mwingine uongozi wa Tanzania unasisitiza serikali inao mfumo imara utakaohakikisha fedha zitawafikia wahusika.

Mgogoro ulianza mwaka 1999 wakati Tanzania ilipotaka kununua vifaa vya kusaidia ulinzi wa viwanja vya ndege toka kampuni ya BAE. Ilidaiwa kuwa mfanya biashara Shailesh Vithlani wa kampuni ya Merlin aliyefanya dili kati ya BAE na Tanzania alipewa asilimia 30 ya pesa ya mauzo kama hongo. Pesa hizo ziliwekwa katika akaunti yake ya benki Uswisi. Wahusika wengine ni aliyekuwa Wakili wa Serikali, Andrew Chenge na Gavana wa benki kuu, Idriss Rashid. Wote hawajashtakiwa na Vithlani anadaiwa kujificha Uswisi, ilhali SFO imetoa tamko afikishwe mahakamani.

Akijibu swali kuhusu kutokuelewana huku, mwenyekiti wa msafara Mbunge Job Ndugai ambaye ni Naibu Spika wa Bunge la Taifa, alisema si vizuri BAE kutuingilia au kutueleza nini cha kufanya na pesa hizo ambazo ni maslahi yetu .
“Sisi tunafahamu mfumo gani utakaohakikisha pesa hizo zinatumika sawasawa, zikienda kwa mashirika ya ufadhili ni kama zimetolewa kwa watu wa nje.”

Mbunge mwingine, John Momose Cheyo ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya Bunge inayohusika na Hesabu za Umma, aliwahakikishia wanahabari kwamba katika miaka kumi toka tukio hilo la 1999 vyombo vya serikali dhidi ya rushwa vimebadilika na kuimarika. “Matumizi halali ya fedha yatakahakikisha pesa zitatumika kujenga elimu,” alisema Mbuge huyo wa Bariadi Mashariki.

Toka SFO ilipoamuru BAE Systems ilipe faini kwa mahakama na fidia kwa Tanzania yametokea pia madai kwamba wapo walioandikia BAE barua pepe kuwa wasiilipe serikali ya Tanzania pesa hizo.
Wabunge wanasisitiza pesa zitaendeleza elimu.

Mbunge Maalum, Angellah Kairuki ambaye ni pia Naibu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Haki na Utawala, alielezea kwamba ingawa pesa hizo zinaonekana nyingi lakini hazitasuluhisha matatizo yote ya elimu nchini, mathalan, kuongeza mishahara ya waalimu.
Alitoa mifano ya ukosefu wa madaftari, vyoo na vitabu vya kusaidia waalimu kufundisha. Mifano hiyo inayolenga shule za msingi na sekondari inatokana na matizo makubwa ya wanafunzi kujisaidia porini na kukosa vifaa muhimu vya elimu.

Mbunge Mussa Zungu wa Ilala, na vile vile Naibu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge inayohusika na Ulinzi, Usalama na Mambo ya Nje, alikumbusha kwamba tatizo halikuanzwa na Watanzania. “Ni suala lililoamuliwa na mahakama ya Uingereza; sisi tuchohitaji ni kuendeleza elimu.”

Habari imeandikiwa na Freddy Macha akishirikiana Jestina George pamoja na
URBAN PULSE CREATIVE

MUNGU IBARIKI AFRIKA, MUNGU IBARIKI TANZANIA

Na kwa kumalizia,tuache kumchosha Mungu kwa kutaka aibariki nchi yetu ilhali sie wenyewe hatujibidiishi kuifanya Tanzania kuwa lulu ya Afrika na pengine dunia kwa ujumla.Au tunamtaka Mungu aibariki nchi yetu ili mambo yakizidi kwenda mrama tumlaumu yeye badala ya kujilaumu kwa uzembe wetu?

Pia naomba kutoa wito kwa wanahabari wenzangu (hoping hamto-mind kukosolewa),let's go beyond the "photo-op" cancer inayowasumbua wengi wa wanahabari wenzetu huko nyumbani.Picha ni muhimu lakini la muhimu zaidi ni kuwabana viongozi wababaishaji kila wanapojipendekeza kuleta porojo zao.Mtakumbukwa kwa kuuwakilisha umma vyema na sio picha.Sorry guys,I think you could have done better than just reporting what they said.You just gave them a free pass na pengine bado hawaamini kama wamesalimika kuulizwa maswali magumu na Watanzania waliopo "dunia ya kwanza".

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.