18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI

Asalam aleykum,

Siku za nyuma niliahidi kwamba iko siku nitawaletea stori kuhusu “mateja” wa huku Ughaibuni.Ndio,tatizo la matumizi ya madawa ya kulevya linawaumiza vichwa watu kadhaa huku Ughaibuni.Kuna vijana wadogo kabisa ambao wanashawishika kujiingiza katika kubwia unga.Ni vigumu kutabiri mafanikio ya jitihada za serikali na taasisi mbalimbali katika mapambano yao dhidi ya ulevi huo haramu na hatari.

Hivi karibuni nilipewa habari za kusikitisha sana.Kijana mmoja mwenye umri usiozidi miaka 18 alikutwa amekufa huku sindano aliyoitumia kujidungia adawa ya ulevya ikiwa inaning’inia kwenye mkono wake.Huyo kijana namfahamu vizuri kwa vile siku moja aliwahi kufika hapa ninapoishi akiwa ameongozana na rafiki yangu mmoja mwenye asili ya Afrika Mashariki.Kilichonivutia zaidi kuhusu kijana huyo ni kauli zake ambazo lazima nikiri kuwa mara nyingi kwa hapa zinatolewa na wanasiasa kuliko wananchi wa kawaida.Alikuwa akionyesha kuchukizwa kwake na watu wanaowabagua wenzao kwa vile tu ni wageni au wana rangi tofauti na wao.Kimsingi,alikuwa akilaani suala zima la ubaguzi.Kwa umri wake mdogo,nilimwona kama ni mtu mwenye upeo mkubwa sana.Kwa wakati huo sikujua kabisa kuwa pamoja na busara zake,kijana huyo alikuwa akiweka rehani roho yake kwa kubwia unga.Pengine lishe bora na huduma mbalimbali zinazopatikana kirahisi ndizo zilikuwa zinamsaidia kuficha “uteja” wake,kwani kama tujuavyo wengi si vigumu kumtambua m-bwia unga kwa kumwangalia tu.

Alienisimulia kuhusu mauti yaliyomkumba kijana huyo alinijulisha kwamba aliemletea marehemu madawa hayo ya kulevya alikuwa ni rafiki yake ambae walikuwa wanasoma darasa moja.Kwa lugha nyingine,wawili hao walishirikiana katika kuleta mauti ya mmoja wao.Huo ni ushirika wa mauti,na hilo ndio linanipeleka kwenye mada yangu ya pili kuhusu ujambazi uliotokea hivi karibuni pale Ubungo uliopelekea vifo na majeraha kwa waliosalimika.

Kuonyesha yeye ni kiongozi anaewajali mno wananchi wake,matra baada ya kurejea nchini akitoka ziarani kusini mwa Afrika,Rais Jakaya Kikwete alikwenda kuwajulia hali waliojeruhiwa na majambazi katika tukio hilo la Ubungo.Mheshimiwa Kikwete alinukuliwa na vyombo vya habari akisema kwamba anaamini kuwa kulikuwa na njama ndani ya benki iliyoibiwa fedha hizo kwa vile isingekuwa rahisi kwa majambazi hayo kuvamia tu gari lenye fedha bila kuwa na taarifa sahihi.Wafanyakazi waliohusika kuvujisha taarifa za fedha hizo kwa majambazi watakuwa hawana tofauti na yule kijana aliempelekea unga rafiki yake na hatimaye kumsababisha mauti.Waliovujisha taarifa hizo walikuwa na ushirika wa mauti na majambazi waliofanya unyama huo.Hivi tunapokuwa kazini si huwa tunaunda kitu kama undugu kwa vile muda mwingi tunautumia tukiwa pamoja na pengine kushirikiana katika mambo ya nyumbani kama vile harusi na misiba?Sasa unapotoa taarifa kwa majambazi wenye silaha za moto ili kuwawezesha kuvamia gari ambalo mfanyakazi mwenzio yupo humo si ni kama unamtengenezea mauti mwenzio?Jamani,hivi fedha zinatupeleka kupoteza utu wetu na kutothamini uhai wa wenzetu!Kwa hakika walioshiriki kwa namna yoyote katika kufanikisha uporaji huo wanastahili kusakwa kwa udi na uvumba na hatimaye kupatiwa kibano wanachostahili.Kwa “waliouza ishu” hiyo kwa majambazi wanakuwa wametenda dhambi kuu mbili:kuwasaliti wafanyakazi wenzao ambao aidha waliuawa au kujeruhiwa,na pia walishiriki katika ujambazi huo kwa vile wao ndio hasa waanzilishi wa mpango mzima.Hiyo si kusema kwamba majambazi waliohusika hawana hatia,lakini iwapo waliotoa taarifa hizo wasingewajulisha majambazi kwamba siku flani,muda flani,katika gari flani kutakuwa na shilingi bilioni moja ni dhahiri kwamba tukio hilo lisingetokea.

Kwa upande mwingine,ni muhimu kwa taasisi zetu za fedha kuwa makini zaidi wanaposafirisha fedha kutoka sehemu moja kwenda nyingine.Hivi kweli benki kama NMB inashindwa kununua gari moja ambalo ni maalumu kwa ajili ya kusafirishia fedha?Uzuri wa magari kama hayo ni kwamba licha ya kutoa usalama mkubwa kwa mali inayosafirishwa,maisha ya wanaosafirisha mali hiyo nayo yanakuwa salama zaidi ukilinganisha na magari ya kawaida.Natambua kuwa yapo makampuni binafsi ya ulinzi ambayo yanamiliki magari ya aina hiyo.Lakini siwezi kuilaumu NMB moja kwa moja kwa kutokodi huduma hiyo kwa vile kumbukumbu zinaonyesha kuwa siku za nyuma walinzi wasio waadilifu walishawahi kuingia mitini na mamilioni ya fedha wakiwa katika gari maalumu la kusafirishia fedha.

Hata hivyo,kuwa na gari maalumu la kusafirishia fedha bila kuwa na watumishi waadilifu ni sawa na kulala ukiwa kwenye chandarua chenye dawa lakini kimekufunika kuanzia kichwani hadi kiunoni tu,na hapohapo kuamini kuwa unawadhibiti mbu.Uaminifu,uadilifu na kuthamini maisha ya wenzetu ni vitu muhimu sana na lazima kwa kila Mtanzania.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.