Showing posts with label KIKWETE. Show all posts
Showing posts with label KIKWETE. Show all posts

18 Feb 2018


Nianze makala hii kwa kutoa salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daniel John, ambaye hadi alipouawa kinyama alikuwa Katibu wa Chadema kata ya Hananasifu, na pia kwa familia, ndugu,jamaa na marafiki wa marehemu Acqulina Akwilin (samahani kama nimekosea jina).

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, mwili wa marehemu Daniel uliokotwa kwenye ufukwe wa Coco jijini Dar es Salaam ukiwa na majeraha. Alieleza kuwa awali marehemu alichukuliwa na Land Rover nyeupe na watu waliohifanya askari polisi, lakini tangu wakati huo Polisi hawakuwa na taarifa zozote za kiuchunguzi, na hata jitihada za kupatikana mwili huo zilifanywa na Chadema wenyewe.




Kwa upande wa marehemu Acquilina, kifo chake kilisababishwa na kasumba hatari inayozidi kuzoeleka kwa watumishi wa vyombo vya dola kufanya mzaha katika matumizi ya silaha za moto, ambapo katika tukio husika, polisi waliokuwa wakizuwia maandamano ya wafuasi wa Chadema, walitumia risasi za moto,na moja kati ya risasi hizo ilipelekea kifo cha binto huyo, ambaye hadi mauti yanamfika alikuwa mwanafunzi katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) akisomea shahada ya ununuzi na ugavi.
Ni muhimu kutambua kuwa vifo vyote hivi viwili vingeweza kuepukika laiti utu na ubinadamu wetu ungewekwa mbele ya chuki za kisiasa. Huhitaji kuwa mjuzi wa uchunguzi wa mauaji kufahamu kuwa vifo hivyo ni matokeo ya chuki, hujuma, uonevu na kila aina ya baya dhidi ya chama kikuu cha upinzani, Chadema, kuhusiana na kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Kinondoni, ambalo kama ilivyo kwa jimbo la Siha, ni "piga ua" kwa CCM ishinde. Yaani chama hicho tawala kilitarajiwa kutumia kila mbinu kuhakikisha inashinda katika majimbo hayo mawili.

Lakini kabda sijaingia kwa undani katika mada hii - ambayo lazima nikiri kwamba inanipa wakati mgumu sana kuiandika kwa sababu nimebanwa na mchanganyiko wa majonzi na hasira, sambamba na hofu ya kuona taifa langu likisukumwa kuelekea kwenye upotevu wa amani na mshikamano wetu – naomba kuweka wazi masuala matatu ya msingi kunihusu mie mwandishi wa mwakala hii.

Kwanza, mimi licha ya kuwa na makazi nje ya Tanzania kwa takriban miaka 15 sasa bado no Mtanzania. Utanzania wangu ni haki nilioirithi kutoka kwa wazazi wangu, na itabaki hivyo milele. Naeleza hili kwa sababu kuwa wabaguzi wanaopenda kutuhukumu Watanzania tunaoishi huku ughaibuni, na kutaka tuonekane kama Utanzania wetu sio kamili. Kwa mantiki hiyo, kama Mtanzania, nina kila haki ya kutoa maoni yangu kuhusu mustakabali wa taifa letu, hususan katika nyakati hizi ambapo kuna dalili za wanaotaka kulipeleka kubaya taifa letu.

Pili, mwaka 2015 nilishiriki kikamilifu katika kampeni zilizomwingiza madarakani Rais John Magufuli. Kwa upande mmoja nililazimika kumkampenia Magufuli kwa vile nilikuwa nina "sababu binafsi" dhidi ya aliyekuwa mpinzani wake mkuu, mgombea urais wa tiketi ya UKAWA, Edward Lowassa. Wanasema "adui ya adui yako ni rafiki yako."Kwa upande mwingine, nililipwa kutoa huduma ya ushauri wa kitaalamu (usadi, yaani consultancy kwa kimombo) hususan kwenye mitandao ya kijamii. Natanabaisha hili ili asije akakurupuka mtu na kusema "ah ulishiriki kutupigia kampeni kwa vile tulikupa pesa."

Tatu, huko nyuma nilikuwa mtumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa. Na kabla ya kuanza utumishi katika taaluma hiyo muhimu na nyeti, nilikula kiapo kwa nchi yangu, kiapo ambacho nitaishi nacho hadi ninaingia kaburini. Kiapo hicho sio cha kukitumikia chama flani au viongozi wake bali Tanzania yetu. Nchi ni muhimu  kuliko vyama vya siasa au wanasiasa.

Mtu aliyepikwa na kuiva kwenye taaluma ya uafisa usalama wa taifa, katika nchi yoyote ile, anapaswa kubaki kuwa mtiifu kwa nchi yake bila kujali yupo ndani au nje ya ajira ya taasisi inayohusika na usalama wa taifa wa nchi husika.

Wanasema hata nje ya ajira rasmi, kila mtu aliyewahi kuwa afisa usalama wa taifa anaendeshwa na "sense of public duty born in their previous lives" yaani wajibu kwa umma uliozaliwa katika maisha yao huko nyuma. Jasusi mmoja mstaafu anaeleza “...I have obligations, professional obligations. If there’s a national security emergency or possible national security issue, I should report it."


Kwahiyo, hata kama "maafisa wenzangu wa zamani" wataamua kukaa kimya kwa sababu moja au nyingine – wengi wanahofia usalama wa maisha yao – sie wengine hatuwezi kukaa kimya, hasa kwa vile baadhi yetu tumeshalipa gharama kubwa kwa kelele zetu. Kukaa kimya ni sawa na kuafiki uhuni unaoendelea ambao ni tishio kwa usalama wa taifa.

Lakini licha ya wajibu huo unaotokana na utumishi wetu kwa nchi huko nyuma, Rais Magufuli amefanikiwa kuvifunga mdomo vyombo vya habari kiasi kwamba haviwezi kusema lolote kuhusu "mabaya" yake, na amefanikiwa kuvijengea nidhamu ya uoga vyombo hivyo vya habari kiasi kwamba habari pekee zenye umuhimu kwao ni za kumtukuza na kumpamba "mungu-mtu" huyo. Kwahiyo na sie tuliopikwa na kuiva kuhusu ujasiri, kujitoa mhanga na kutokuwa waoga tukiufyata na kukaa kimya - ilhali media zetu ndio zishapigwa kufuli - hali itazidi kuwa mbaya.


Baada ya kuweka wazi nafasi yangu, sasa tuangalie kwa kina kinachoendelea huko nyumbani hasa kuhusiana na uchaguzi mdogo kwenye jimbo la Kinondoni na Siha na kuuawa kwa Daudi na Acquiline.

Ni muhimu kutambua kwamba ukandamizaji dhidi ya vyama vya upinzani sio kitu kilichoanza chini ya utawala wa Magufuli bali hali hiyo imedumu mfululzo tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1992. Labda kilicho tofauti kwa zama hizi ni "ujasiri" wa Magufuli kutoficha chuki yake dhidi ya vyama vya upinzani. Yaani angalau akina Mwinyi,Mkapa na Kikwete walikuwa "wanauma na kupuliza." Kwamba angalau walikuwa na "mshipa wa aibu" na walijitahidi japo kutowaonea Wapinzani waziwazi.

Kwa wanaojua "yanayojiri nyuma ya pazia" watakwambia kuwa hujuma dhidi ya vyama vya upinzani ni miongoni mwa vipaumbele vikubwa kwa CCM na serikali zake, na hiyo imepelekea kujengeka "symbiotic relationship" kati ya chama hicho tawala na taasisi za dola, ambapo kila mmoja anategemea uhai wa mwenzie.

Lakini kama kuna kitu kinachokera zaidi kuhusu hujuma dhidi ya demokrasia ni pale CCM na taasisi zake hasa za dola wanapoweka mbele maslahi yao mbele ya utu na uhai wa Watanzania. Na hili halijaanza jana au katika kampeni za chaguzi ndogo katika majimbo ya Kinondoni na Siha.

Uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995 ulihusisha matukio mengi tu ambayo kwa makusudi hayapo kwenye kumbukumbu za wazi (japo yamehifadhiwa mahala flani).

Lakini kama wanavyosema "amekula asali sasa anachonga mzinga," baada ya hujuma za kimyakimya za mwaka 1995 kuzaa matunda, CCM na taasisi zake ikanogewa, na matokeo yake ni kwamba uchaguzi mkuu uliofuata, mwaka 2000 uliweka doa kubwa kwa historia ya Tanzania yetu ambapo kwa mara ya kwanza nchi yetu ilizalisha wakimbizi kufuatia unyama uliofanyika huko Zanzibar na kupelekea vifo kadhaa (idadi halisi ya vifo haijawahi kuwekwa hadharani japo "wenyewe" walisema zaidi ya watu 19 ndio waliokufa kwenye machafuko hayo. Wasichosema pia ni idadi ya watu waliobakwa, kuteswa na kuwekwa kizuizini.

Kwamba hujuma hizo za CCM dhidi ya demokrasia zilipelekea vifo na majeruhi ni kitu kibaya kabisa. Lakini kitu kingine kibaya ni ukweli kwamba hakuna mtu hata mmoja aliyechukuliwa hata kutokana na unyAma waliofanyiwa Wazanzibari hao.

Kwa namna ya kipekee, CCM ikawa kama imepewa ruhusa ya kutumia vyombo vyake vya dola kufanya lolote itakalo ili ifanikishe hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla, kisha iibuke na ushindi.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 ulikuwa na "uchafu kupindukia." Kundi lililofahamika kama "mtandao" lilijipenyeza katika kila sekta, kuanzia kwenye vyombo vya habari, taasisi za dola hadi kwenye taasisi za dini. Yayumkinika kabisa kuhitimisha kwamba yaliyojiri wakati "mtandao unafanya jitihada za kumwingiza mtu wao Ikulu" ni mabaya zaidi ya haya tunayoshuhudia sasa tangu Magufuli aingie madarakani.

Kwanini basi hayo yaliyojiri kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 hayajulikani? Jibu ni kwamba, wakati mbinu iliyotumika mwaka 1995 na 2000 ilitegemea zaidi vyombo vya dola, uchaguzi wa mwaka 2005 na 2010 ulitegemea zaidi nguvu ya fedha, nyingi zikiwa fedha haramu. Na sehemu ya fedha hiyo ilitumika "kununua ukimya" wa wanahabari wengi tu. 

Lakini si fedha tu bali pia kuna hujuma mbalimbali – nyingine chafu na za kuchefua – zilizotawala safari za ushindi wa chama tawala kwenye chaguzi hizo.


Image result for lowassa kikwete 2005

Labda tofauti nyingine kuhusu mwaka 2005 na 2010 ni ukweli kwamba wakati chaguzi hizo zilihusisha "kikundi binafsi" yaani hicho cha wanamtandao ambacho hakikuwa taasisi ya serikali au chama.

Lakini muda wote huo, CCM ilikuwa kama imepwa ruhusa na Watanzania kuendeleza hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla. Hakujawahi na utashi miongoni mwa Watanzania kutaka kukabiliana kwa dhati za uhuni/uhalifu wa kisiasa. Na kwa bahati mbaya, kwa vile vipaumbele vya Watanzania wengi ni kwenye "ubuyu" na "kubeti/mkeka" basi habari mbaya ni uwezekano wa CCM kuendelea kufanya itakavyo kwa muda mrefu sana.

Sio kama kwa kubashiri kuwa unyanyasaji wa CCM utaendelea muda mrefu sana ninamaanisha kuwa nimekata tamaa. Hapana. Ninakuwa mkweli tu. Tatizo ni zaidi ya CCM na uhuni wake. Watanzania wenyewe ni sehemu ya mfumo unaowezesha CCM kufanya uhuni/uhalifu huo.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ulihusisha pia matuki kadhaa yaliyojiri "nyuma ya pazia." Na ukitaka kufahamu kuwa Tanzania yetu haijawahi kuhangaishwa na mauaji ya kisiasa – kuanzia yale ya mwaka 2001 huko Zanzibar hadi haya ya Daudi wa Hananasifu na dada Acquilina – ni kifo cha Mchungaji Christopher Mtikila.


Kwahiyo, na ninaandika haya kwa uchungu mkubwa uliochanganyika na hasira, kuuawa kwa Daudi na Acquilina kutaishia kuwa moja tu ya matuko yaliyowahi kutokea katika Tanzania yetu. Tutawasikia wanasiasa wetu wa vyama vya upinzani wakiongea kwa hisia kubwa. Tutashuhudia pia wanafiki wengi tu miongoni mwa wasanii wetu nao wakijifanya kuguswa na vifo hivyo, lakini wakiwa makini kuepuka kumuudhi "Bashite na baba yake" au kuitibua CCM. Tutashuhudia pia kundi la wanafiki hatari ndani ya CCM wakijifanya kuumizwa na mauaji hayo, na kutaka uchunguzi ufanyike, ilhali nao ni kondoo waliojivika ngozi ya mbwa mwitu.



Kama ambavyo "mauaji mengine ya kisiasa" yalivyoruhusiwa kupita kimyakimya, ndivyo unyama huu uliofanywa dhidi ya Daudi na Acquilina utakavyoruhusiwa uishe kimyakimya.

Kwa upande mmoja tusitarajie Rais Magufuli awajibike – sio kwa yeye binafsi kujiuzulu kwa sababu hilo litakuwa kutarajia zaidi ya muujiza – kwa kumtimua Waziri husika na watendaji katika jeshi la polisi. Kwa upande mwingine, hakuna wa kumshinikiza Rais Magufuli achukue hatua stahili dhidi ya wahusika.

Na nisingependa kuuma maneno hapa. Yeye Magufuli mwenyewe ni chanzo muhimu cha siasa hizi za uhasama zinazoendelea kuitafuna Tanzania yetu. Huyu ni mtu ambaye wala hapati shida kuonyesha chuki zake za waziwazi dhidi ya Wapinzani, Upinzani na demokrasia kwa ujumla.


Kama ilivyo kwa madikteta wengine duniani, Magufuli amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutumia ajenda yake ya ufisadi kama kisingizio cha kusigina haki za binadamu nchini Tanzania, na kubinya kila fursa ya haki za kidemokrasia na uhuru wa habari. Kama nilivyoeleza awali, amefanikiwa kuviziba midomo vyombo vya habari na ndio maana hata habari za kusikitisha kuhusu mauaji ya Daudi na Acquiline hazijaripotiwa vya kutosha.

Kwa kuviziba midomo vyombo vya habari Magufuli amefanikiwa kuzuwia "habari asizozipenda" na ndio maana hadi muda huu ni Watanzania wachache tu wanaofahamu kilichojiri huko MKIRU katika kilichoitwa "operesheni dhidi ya ugaidi." Kuna siku yaliyojiri huko – na ambayo yamechangia "kupotea" kwa mwandishi wa gazeti la Mwananchi Azory Gwanda – yatajulikana hadharani. Haijalishi itachukua miaka mingapi.


Lakini "yaliyojiri MKIRU" ni uthibitisho mwingine wa hicho nilichoeleza hapo juu kuwa Watanzania wenyewe ndio wanaopaswa kubeba lawama nyingi katika kasumba ya CCM kutojali uhai katika harakati zake za kukandamiza demokrasia. Kwamba kama yaliyojiri MKIRU yameachwa yaishe kienyeji, kwanini tutegemee hali tofauti kwa vifo vya Daudi na Acquiline?

Kama ndugu zetu wa Chadema (na kila mpenda haki) "wamekubali yaishe" kuhusu kifo cha Kamanda Mashaka, "kupotea" kwa kada Ben Saanane (hata zile kampeni za #BringBackBenAlive zimejifia kifo cha asili), na hawasumbuliwi na serikali ya Magufuli kupuuzia jaribio la mauaji dhidi ya Tundu Lissu, kwanini tutarajie jipya katika mauaji yaliyofanywa dhidi ya Daudi na Acquiline?

Yaani Mnadhimu Mkuu wa upinzani anamwagiwa risasi hadharani wakati mkutano wa bunge unaendelea huko Dodoma, na tunaambiwa kuwa tukio hilo lilitokea katika eneo lenye ulinzi mkubwa na lenye CCTV, kwanini basi wanaosumbuliwa na tukio hilo wasitafute njia stahili za japo kuifanya serikali ione aibu na kufanya japo "uchunguzi wa kizushi"?

Kuhusu hujuma "za kawaida" za uchaguzi, kama kila aina ya uhuni uliofanywa na CCM kwenye chaguzi ndogo za madiwani katika kata 43 uliofanyika Novemba mwaka jana uliruhusiwa upite "kimya kimya" – kwa maana kwamba hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi ya uhuni huo – kwanini basi chaguzi hizi ndogo katika jimbo la Siha na Kinondoni zilitarajiwa kuwa tofauti?

Na katika hili, inapaswa wana-Chadema wajiulize kuhusu busara za viongozi wao kuamua kushiriki katika chaguzi hizo ndogo Siha na Kinondoni ilhali mazingira yaliyokuwepo yalikuwa yaleyale yaliyopelekea chama hicho kususia chaguzi nyingine ndogo tatu katika majimbo ya Longido, Singida Kaskazini na Songea Mjini uliofanyika mwezi uliopita.

Hadi wakati ninaandika makala hii, tayari Tume ya Uachaguzi ilikuwa imeshamtangaza mgombea wa CCM jimbo la Siha, Godwin Mollel kuwa mshindi kwa tofauti kubwa tu ya kura dhidi ya mgombea wa Chadema. Hata kama CCM wameiba kura, ukubwa wa tofauti kati ya kura za mgombea wao na huyo wa Chadema zinaashiria kuwa chama hicho kikuu cha upinzani kilipitisha mgombea fyongo.


Na kama ilivyotarajiwa mgombea wa CCM jimbo la Kinondoni, Maulid Mtulia, naye ametangazwa mshindi.


Mie mtumishi wako nilishabashiri mapema tu kuwa chama hicho tawala kingeshinda majimbo hayo, "iwe isiwe."

Ushindi kwa wagombea hao wa CCM ulipaswa kupatikana kwa gharama yoyote kwa sababu laiti wangeshindwa, kinachoelezwa kama "mkakati wa Magufuli kuua upinzani kwa kununua wabunge na madiwani wa Upinzani"  kingemfanya achekwe hata huko kwenye chama chake.

Na kwa vile hadi sasa wabunge na madiwani waliohama upinzani na kujiunga na CCM wamefanikiwa kurudi madarakani baada ya chama hicho tawala kuwapa fursa ya kuwa wagombea wake kwenye chaguzi ndogo, na kuwasaidia kwa hali na mali washinde, tutarajie wabunge na madiwani wengin zaidi kuhama vyama vya upinzani na kujiunga na CCM. Kisa? "Dili hilo linalipa," kwa CCM na kwa wanasiasa hao wanaohama.

Na unadhani mbunge au diwani "mwenye moyo mwepesi" akiona jinsi chama chake "kilivyochukulia poa" yaliyowasibu akina marehemu Mashaka na Daudi, na yaliyowasibu Ben Saanane na Lissu, kwanini iwe ngumu kwake kushawishika kuhama?

Ningetamani sana kuhitimisha makala hii kwa kushauri nini kifanyike lakini itakuwa kupoteza muda wangu na muda wako msomaji. Ni vigumu mno kuwashauri watu waliokubali kwamba mgao wa umeme ni stahili yao kwa zaidi ya miaka kumi sasa, na ambao kila mara umeme unaporudi wanashangilia kana kwamba wamepewa upendeleo flani.

Kama Watanzania wameshindwa kuilazimisha Tanesko iache mgao wa umeme, wataweza kweli kuilazimisha CCM iache hujuma dhidi ya vyama vya upinzani na demokrasia kwa ujumla? Ndio maana bila utu wala aibu, chama hicho tawala kinapata ujasiri wa kukifanyia mzaha kifo cha Acquiline ambapo kwa kudai polisi (haohao waliomuua binti huyo) wachukue hatua dhidi ya Mbowe. Utterly disgusting!


Na kama mauaji mbalimbali ya kisiasa huko nyuma yameachwa yapite na kusahaulika, kwanini tutarajie miujiza kwenye mauaji haya ya sasa dhidi ya wapendwa wetu Daudi na Acquline?

Na ukweli mchungu ni kwamba Magufuli ataendelea kuwapelekesha Watanzania atakavyo ka sababu si watangulizi wake -Mwinyi, Mkapa na Kikwete – wenye jeuri ya kumwambia "Ee bwana ee, huku unakoipeleka nchi siko." Hawawezi kwa sababu nao ni kama "mateka." Madhambi waliyofanya kwenye tawala zao yanawafanya wahofie hatma yao pindi wakimkosoa "mungu-mtu" aliyepo madarakani.

Na wakati wastaafu au watumishi wa zamani wa Idara za Usalama wa Taifa kwenye nchi kama Marekani wamekuwa mstari wa mbele kukemea kila tendo linalotishia usalama wa nchi hiyo – kwa mfano 'ndoa' kati ya Rais Donald Trump na Russia – wastaafu wetu sie hawana jeuri ya kufungua mdomo sio tu kwa vile wanahofia kuathiri posho na marupurupu yao bali kwa vile nao ni mateka wa "madudu" waliyofanya walipokuwa madarakani. Ukiwa mchafu unajinyima uhuru wa kukemea uchafu.


Basi niishie hapa kwa kurejea tena salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daudi na Acquiline. Ni vigumu kuwaambia maneno yanayotosha kuwaliwaza lakini la muhimu ni kuendelea kuzikumbuka roho za marehemu hao, hasa katika kipindi hiki cha Kwaresma ambapo sisi Wakristu tunaadhimisha mateso ya Bwana Yesu Kristo. Pumziko la Milele awape Bwana, na Mwanga wa Milele awaangazie, wapumzike kwa amani. Amen


10 Oct 2014

Kwanza soma taarifa ifuatayo kutoka Ikulu kisha tuijadili pamoja
Kweli Tanzania yetu haina uhaba wa mazingaombwe. Lakini hilo dogo, kubwa ni 'akili' za baadhi ya wasaidizi wa Rais. Binafsi nimekuwa mpinzani sana wa hoja kuwa 'tatizo si JKI bali wasaidizi/ watendaji wake,' kigezo changu kikubwa kikiwa 'kwani walimshikia mtutu wa bunduki awateue na kisha kumtahadharisha kuwa akiwatimua pindi watapoboronga watamdhuru'?

Lakini ukiangalia mlolongo wa 'makanusho' yanayotolewa na wasaidizi wa Rais, unaweza kukubaliana na wanaosema kuwa 'wasaidizi/ watendaji wa JK wanamwangusha' (japo siafiki wanaotaka kutumia sababu hiyo kama excuse ya kumsafisha JK mwenyewe.)


Hebu tuichambue kauli hiyo ya Ikulu hatua kwa hatua. Kwanza, Ikulu haikuwahi kukanusha lundo la picha (kama hiyo inayoambatana na kichwa cha habari hii) zilizowekwa mtandaoni zikimwonyesha Rais Kikwete akipokea zawadi ya saa, huku maelezo yakibainisha waziwazi kuwa 'Rais Jakaya Kikwete akipokea zawadi ya saa..." Najua kwanini hawakuhangaika na taarifa hizo za awali: hazikuhusiana na 'utata' unaomkabili mwekezaji aliyetoa zawadi hiyo.
Lakini baada ya gazeti la Raia Mwema kueleza bayana kuwa mwekezaji wa mradi wa treni ya kisasa Dar ndiye huyo alompa zawadi ya saa Rais Kikwete, na kutanabaisha maswali kadhaa yanayouzunguka mradi husika na wasifu wa mwekezaji huyo, Ikulu ikakurupuka na kanusho hili. WALIKUWA WAPI MUDA WOTE HUO?

Mwandishi wa taarifa hiyo ameonyesha ni mtovu wa nidhamu wa kutokana na matumizi ya maneno yasiyopaswa kutoka ofisi iliyopo sehemu 'tukufu' kama Ikulu. Matumizi ya maneno kama "ni habari ya uzushi na UPUUZI..." na  "...kumhusisha Rais na zawadi ya KIPUUZI kama saa..."Huwezi kuita upuuzi habari inayohoji suala la msingi, ambapo logically, mfanyabiashara anaonekana akitoa zawadi kwa Rais (iwe saa au suti), kisha siku chache baadaye mfanyabiashara huyo anatangaza 'mradi wa utata'...Kwanini wananchi (waandishi wa gazeti hilo ni sehemu ya wananchi hao) wasihoji suala hilo ambalo mwandishi wa Ikulu anaona ni la kipuuzi?

Na kwa kinachoweza kuelezwa kama uhuni na si ubabaishaji, taarifa hiyo ya Ikulu imekwepa kabisa kuzungumzia maswali lukuki yanayoiandama kampuni inayomilikiwa na mfanyabiashara huyo, wasifu wa mfanyabiashara mwenyewe, sambamba na 'sintofahamu' lukuki kuhusu uwekezaji huo.

Kimsingi, habari Ikulu 'imejishtukia' tu inapodai "Ni habari ya uzushi na upuuzi. Ni habari inayolenga kumdhalilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwamba amepokea zawadi kutoka kwa mtu ambaye anajaribu kupewa kandarasi ya kujenga ya usafiri wa treni jijini DSM na ambaye pia anahusishwa kwenye shughuli nyingine za kibiashara zenye utata huko kwao Marekani."

Kwa wapambe hao wa Rais ni upuuzi na kumdhalilisha Rais kupokea zawadi kutoka kwa mtu ambaye WANAKIRI BAYANA kuwa anahusishwa na shughuli nyingine za kibiashara ZENYE UTATA huko Marekani. 

Kwanini taarifa hiyo isingewekeza nguvu katika 'kumsafisha' Rais kwa 'kujihusisha' na mtu huyo wanayekiri kuwa na shughuli zenye utata, badala ya kung'ang'ania hoja moja tu 'ya kipuuzi' kuhusu 'zawadi ya kipuuzi' ya saa?

Kilicho bayana ni kasumba iliyoota mizizi kwenye utawala wa Kikwete wa kudhani Watanzania wanaishi karne ya 18, hawana access na internet kufuatilia masuala mbalimbali yanayoihusu nchi yao, na hata wakifuatilia na kupatwa na hofu basi wakae kimya!

Suala la msingi si Rais kupewa zawadi, iwe ni Rolex au 'souvenir watch' nyingine, bali ni utata unaozunguka kampuni inayotaka kuwekeza katika mradi wa treni za kisasa, na inayomilikiwa na mtu ambaye anazungukwa na habari zenye utata, na ambaye alimzawadia Rais saa (iwe halisi au souvenir' tu) siku chache kabla ya kutangazwa taarifa za uwekezaji huo. Surely huu sio upuuzi bali ni kuihoji serikali yetu ambayo ina historia 'nzuri tu' ya kuingia mikataba ya 'ajabu ajabu' kama ule wa kitapeli wa Richmond.

Nihitimishe makala hii kwa kuwakumbusha wasaidizi wa Rais Kikwete kwamba Watanzania wana haki ya msingi kuuliza maswali kuhusu masuala yanayohusu taifa lao. Kadhalika, wanahabari wana haki ya kuhoji utata unapojitokeza katika mahusiano ya serikali au viongozi wake (hususan Rais) na watu au taasisi mbalimbali.

By the way, ajira ya mwandishi wa taarifa hiyo inategemea kumtetea bosi wake, na hakuna cha ajabu katika kujitokeza kwake kwa ukali kukanusha taarifa hiyo. Lakini kama wana ujasiri, basi wajibu maswali haya tuliyomuuliza mwekezaji huyo badala ya kung'ang'ania 'hoja ya kipuuzi ya "SIO ROLEX" au kutuhadaa kuwa "saa aliyopewa Rais Kikwete ni mali ya Watanzania" (mbona hawakutangaza kuwa Rais amekabidhiwa saa ambayo ni mali ya Watanzania hadi walipoona habari hiyo kwenye gazeti la Raia Mwema?)

Rais Kikwete amekuwa ajitianabaisha kama muumini wa dhana ya 'open goverment' inayopigia mstari haja ya wananchi kufahamu utendaji kazi wa serikali yao. Lakini wakati huohuo, wasaidizi wake huwa wakali kweli pindi wananchi wanapotaka kufuata dhana hiyo na kuhoji 'maswali magumu' kama hayo yanayouzunguka mradi wa treni za kisasa Dar.

Ni muhimu kwa watendaji wa serikali yetu kutambua kwamba Rais wanayemtumikia ni mwajiriwa wa Watanzania, na kila mwajiriwa anatambua haki ya mwajiri wake kuhoji masuala mbalimbali yanayomtatiza. Tanzania ni yetu sote na si ya kikundi kidogo cha miungu-watu wasiotaka kuuliza 'kulikoni?' hata katika masuala yanayohitaji 'akili ndogo' tu ya ku-Google kuhusu mtu au taasisi flani (kama ilivyo kwa ishu ya 'M/S Shumoja a.k.a Shumake Rails.'


20 Jan 2012


Dk Slaa: Kwa nini sikumsalimia JK 


Thursday, 19 January 2012 20:42
Fredy Azzah 
KATIBU Mkuu wa Chadema Dk Willibrod Slaa  amesema kuwa, hakuweza kusalimiana na Rais Jakaya Kikwete kutokana na Jiografia ya eneo la makaburini lilivyopangwa na watu wa usalama wa taifa pamoja na kamati ya mazishi kutomruhusu kufanya hivyo.

 
Hata hivyo Dk Slaa alisisitiza kuwa, kwa upande wake, kwenye msiba siyo sehemu ya kwenda kwa ajili ya kusalimiana na watu ama kurekebisha mambo yaliyoharibika bali ni sehemu ya kumwombea marehemu.

 “Siyo hulka ya Dk Slaa kutumia misiba kama sehemu ya kusalimiana, wala kutengeza mambo yaliyoharibika, mimi huwa naenda kwenye msiba kwa lengo moja tu la kumwombea marehemu, huwa simtazami hata mtu aliyekaa pembeni yangu,” alisema Dk Slaa alipozungumza kwa njia ya simu  jana.  

Alifafanua kuwa, katika eneo la makaburi kulikuwa na mabanda matano ambayo yalipangwa kwa ajili ya Askofu, Rais, Viongozi wa vyama vya siasa, mwili wa marehemu  na familia na banda jingine lilikuwa la watu wengine waliohudhuria mazishi hayo. 

“Sasa kutoka alipokuwa amekaa Rais mpaka kwenye banda nilipokuwa mimi, kulikuwa na umbali wa karibu  mita 20, sasa mlitaka nikimbie kumsalimia Rais nivunje protokali kisha nikamatwe na usalama wa taifa,” alisema Dk Slaa. Alisema alikuwa mtu wa kwanza kufika makaburini kwa lengo la kuangalia jinsi kaburi la mbunge wa chama chake lilivyochimbwa kisha akaonyeshwa sehemu ya kukaa na watu wa usalama wa taifa.

 Alisema kuwa, hata katika wakati wa kuaga mwili wa Marehemu Regia Mtema, katika ukumbi wa Karejee, kulikuwa na utaratibu kama huo ambapo ilitengwa sehemu ya kukaa Makamu wa Rais, Spika wa Bunge, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Makamu wake na yeye Dk Slaa akawekewa sehemu yake kama Katibu wa Chama alichokuwa akikitumika marehemu.

 “Mimi sipendi kuweka siasa kwenye mambo kama ya msiba, Dk Slaa siyo kichaa siyo kichaa aanze kukimbia kumsalimia Rais. Katika sehemu kama ile Rais huwa anakuja baada ya watu wote wakiwa wameshakaa, yeye ndiye hupita na kuanza kusalimia watu na hamjaona hata sehemu moja aliponyoosha mkono kunisalimia nikamkwepa,” alisema Dk Slaa:

 “Msiba siyo mahali pa kutengeza urafiki, au kutengeza mambo yaliyo haribika, pale ni ibada tu na kumuombea marehemu siyo sehemu ya kufanya siasa” alisisitiza Dk Slaa. Jana baadhi ya vyombo vya habari viliripoti kuwa, Dk Slaa alishindwa kusalimiana na Rais Jakaya Kikwete katika mazishi ya Regia Mtema yaliyofanyika kijijini kwao Ipangalala Morogoro juzi.Regia alifariki dunia Januari 14 kwa ajali ya gari iliyotokea katika eneo la Ruvu mkoani Pwani.  


CHANZO: Mwananchi

8 Jun 2011






Mafisadi CCM wageuka mbogo

Na Jabir Idrissa - Imechapwa 01 June 2011

SASA ni piga ni kupige ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Wanaotuhumiwa kwa ufisadi, wanakataa kujiuzulu, MwanaHALISI limeelezwa.

Taarifa zinasema walipoitwa mbele ya viongozi wakuu wa chama hicho – makamu mwenyekiti Pius Msekwa na katibu mkuu, Wilson Mukama - wanaoitwa na CCM kuwa “watuhumiwa wakuu wa ufisadi nchini,” walishikilia msimamo kuwa hawawezi kujiuzulu kwa kuwa hawana hatia.

Wanaotakiwa kujiuzulu na viongozi wakuu wa CCM ni Edward Lowassa, Rostam Aziz na Andrew Chenge. Mkutano wa kuwashawishi wajiuzulu, ulifanyika Alhamisi na Ijumaa wiki iliyopita katika ofisi ndogo za chama hicho zilizopo Lumumba, Dar es Salaam.
Taarifa zinasema katika mkutano huo, Msekwa na Mukama waliomba Lowasa ajiuzulu ili kukiokoa chama hicho, lakini yeye alipinga kwa hoja kuwa hana hatia.

MwanaHALISI lilipowasiliana na Msekwa kutaka kufahamu kilichojadiliwa katika mkutano wake na viongozi hao, haraka alisema, “…Umetoa wapi habari hizo?”

Alipoelewa ni vyanzo vya ndani ya chama na serikali, Msekwa alisema, “Hayo ni mambo ya ndani ya chama. Hatuwezi kuyaleta magazetini.”
Lowassa alipoulizwa juu ya kuwapo kwa kikao hicho, alisema ni kweli wamekutana. Hata hivyo, alisema hawezi kueleza walichojadili kwenye vyombo vya habari.

Rostam hakupatikana kueleza upande wake. Hata hivyo, MwanaHALISI limeelezwa na mtoa taarifa wake kuwa mbunge huyo wa Ingunga alitoka kwenye ukumbi wa mkutano akiwa amenuna na kuvurumisha “maneno makali.”

Anasema Rostam alitoka pale akiwa amenuna na kusema yeye hana hatia yoyote na kwa hiyo hastahili kushambuliwa. Amesema yote yanayotokea sasa yanatokana na uadui wa siasa za urais wa mwaka 2005 na ule wa 2015.


Hili linatokea wakati uongozi wa juu wa chama hicho ukishindwa kukabidhi barua ya kuwataka watuhumiwa hao wajiuzulu.
Kuchelewa kwa utekelezaji wa maazimio ya kuwawajibisha Lowassa, Rostam na Chenge kumezaa majungu na umbeya. Hivi sasa taarifa zinasema, Mukama anadaiwa kugoma kuandika barua ya kuwataka watuhumiwa hao kuachia nafasi zao za ujumbe wa Halmashauri Kuu ya taifa (NEC) wanazozishikilia.

Baada ya Mukama kugoma kuandika barua hizo kwa hoja kuwa kilichoamuriwa na NEC hakifahamu kwa kuwa alikuwa hajateuliwa, ndipo Nape Nnauye, katibu wa itikadi na uenezi alipoandika barua hizo na kuzipeleka kwa Msekwa.

Naye Msekwa alizipokea barua na kuzirekebisha. Akazirejesha kwa Nape ili azipeleke kwa Mukama kuzisaini. Mukama akagoma. Zikapelekwa kwa mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, ambaye taarifa zinasema, “amezifungia kabatini.”

Kwa mujibu wa taarifa za ndani ya kikao hicho, Lowassa alifika Lumumba saa nne asubuhi. Mazungumzo kati yake, Msekwa na Mukama inakadiriwa yalichukua takribani saa moja.

Katika mazungumzo hayo, Msekwa ananukuliwa akimweleza Lowassa “unatakiwa ujiuzulu nyadhifa zako za uongozi katika chama ili kutekeleza maagizo ya NEC na falsafa ya chama ya kujivua gamba.”

Akijibu hoja hiyo, mtoa taarifa anasema Lowassa alijibu, “Kuhusu Richmond (kampuni feki ya kufua umeme wa dahurula), ukweli unafahamika…Katika hili, mimi sina makosa. Rais anafahamu hilo na kila mmoja anajua hivyo.”

Anasema Lowassa alisema kama kuwajibika kwa makosa yaliyotokana na Richmond tayari amefanya hivyo kwa niaba ya chama chake na serikali pale alipoamua kujiuzulu wadhifa wake wa uwaziri mkuu.
Anasema mbali na kueleza hilo, Lowassa alisikika akisema, “nilikutana na Rais Kikwete. Aliyonieleza si haya.”

Alisema Rais Kikwete alimweleza kuwa hakuna maazimio yoyote ya NEC yaliyomtaka kujiuzulu. Akahoji, “Sasa nimwamini nani, ninyi mnaotaka nijiuzulu au rais aliyesema hakuna azimio kama hilo?”

Habari zinasema mara baada ya Lowassa kuwaeleza viongozi wake msimamo juu ya mazungumzo yake na Kikwete, ndipo Msekwa aliposikika akisema, “Lowassa acha mbio za urais.”

Naye Lowassa hakumkawiza Msekwa. Alijibu, “Lini nimetangaza kugombea urais? Lakini hata kama ninataka kufanya hivyo, ni haramu kugombea nafasi hiyo? Je, kuna mliowaandaa?”

Ni kauli hiyo ya Lowassa, iliyomshutua Msekwa na kusema, “Hapana. Hapana. Hakuna tuliyemuandaa…Haya mambo ya urais yatatuvuruga.”
Akihitimisha hoja zake kabla ya kumalizika kwa mkutano huo, mtoa taarifa anasema Lowassa alikitaka chama chake kuisaidia serikali kutekeleza wajibu wake kwa wananchi, badala ya kufanyia kazi kile alichoita, “majungu ya wanasiasa.”

Naye Chenge taarifa zinasema aliwaambia viongozi aliokutana nao kuwa yeye si fisadi na hafahamu maana ya ufisadi. Akataka kama tuhuma wanazomtuhumu wanaweza kuzithibitisha wamfikishe mahakamani ili aweze kujitetea. Hakuna maelezo ya ziada.

Hata hivyo, watu waliokaribu na kiongozi huyo wanasema, Chenge amejipanga kuhakisha kwamba hang’oki katika kiti chake cha NEC; ikibidi kuondolewa kwa nguvu ametishia kuondoka CCM na kujiunga na upinzani.

Kwa upande wa Rostam Aziz, taarifa zinasema alitakiwa kujiuzulu ujumbe wa NEC kwa tuhuma za kuingiza nchini kampuni feki ya Richmond na baadaye Dowans.

Mtoa taarifa anasema, mara baada ya kuelezwa tuhuma hizo, Rostam alihoji, “Haya ni maamuzi ya NEC?” Naye Msekwa akajibu, “NEC imetaka chama kijivue gamba kuanzia ngazi ya taifa hadi chini kwa kuondoa watu wote wanaotuhumiwa ufisadi.”

Habari zinasema, katika mazungumzo kati ya viongozi hao na Rostam, hakuna mahali popote ambapo Msekwa na Mukama walitaja ushiriki wa mbunge huyo wa Igunga, katika wizi wa fedha za umma kupitia kampuni ya Kagoda Agriculture Limited.

Kampuni ya Kagoda ni miongoni mwa makampuni 22 yaliyothibitika kuchota mabilioni ya shilingi kwenye akaunti ya madeni ya nje (EPA) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Gazeti hili limeshindwa kufahamu mara moja kilichosababisha Msekwa na wenzake kushindwa kumweleza Rostam ushiriki wake katika Kagoda. Hata hivyo, kwa zaidi ya miaka minne sasa, CCM imekuwa ikituhumiwa kunufaika na fedha za EPA hasa Sh. 40 bilioni zilizoibwa na Kagoda.

Wakati suala hilo likichukua sura hiyo, taarifa zilizofikia gazeti hili zinasema baadhi ya vigogo wa chama hicho wamepanga kupeleka hoja katika vikao vijavyo vya (CC) na (NEC) kushinikiza kufukuzwa ndani ya chama hicho wanaoitwa, “wasaliti ndani ya chama.”

Wanaopangiwa mkakati wa kufukuzwa ni spika wa zamani wa Bunge, Samwel Sitta na mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe wanaotuhumiwa kuanzisha Chama cha Jamii (CCJ) wakati wakiwa bado wanachama na viongozi wa CCM.

Wengine ni Nape Nnauye, Victor Mwambalaswa na Daniel Porokwa.
Habari kutoka ndani ya CCM zinawanukuu makada mawili; rais mstaafu, na mjumbe mmoja wa NEC wakitaka chama chao kuwafukuza waasisi wa CCJ kwa kukosa uaminifu.

MwanaHALISI limeelezwa na aliyekuwa naibu katibu mkuu wa CCJ, Dickson Ng’hily kwamba Sitta na Mwakyembe waliokuwa waanzilishi wa chama hicho, walimkatiza masomo yake nchini Afrika Kusini ili kusaidia kupatikana usajili wa chama hicho.

Ng’hily ambaye mahojiano yake yatachapishwa kikamilifu katika toleo lijalo amesema, aliyemwingiza yeye CCJ ni Sitta na Dk. Mwakyembe na anasikitishwa na hatua ya viongozi hao kutaka kuficha ukweli.

“Hawa watu ndio waanzilishi hasa wa CCJ. Mimi na Makonda tulipewa jukumu la kutafuta usajili wa chama. Lakini naona wenzangu wameamua kuficha ukweli kwa maslahi binafsi. Hii si sahihi,” ameeleza.

Ng’hily anaonyesha nyaraka za muhtasari wa vikao walivyoshiriki viongozi wakuu wa CHADEMA, John Mnyika, Anthony Komu na Tundu Lissu kuwa ni miongoni mwa watu walioshiriki katika majadiliano ya kuunganisha nguvu kati ya CCJ ya Sitta na CHADEMA.

“Tulikubaliana kama CCJ itakosa usajili, basi mheshimiwa Sitta atagombvea urais kupitia CHADEMA. Lakini kama tutafanikiwa kusajili chama chetu, basi Sitta angegombea urais kupitia CCJ na CHADEMA wangetuunga mkono,” anaeleza Ng’hily.

Kuibuka kwa Ng’hily kuelezea ushiriki wa Sitta na Dk. Mwakyembe katika kuanzisha na kusimamia usajili wa CCJ kumekuja wiki tatu baada ya Fred Mpendazoe kumtaja Nape Nnauye kuwa ni miongoni mwa waanzilishi wa kwanza wa CCJ.

Mpendazoe aliuambia mkutano mkubwa wa hadhara mjini Njombe kuwa yeye, Sitta na Mwakyembe ndio walianzisha CCJ; bali yeye alitangulia kutoka CCM ili kurahisisha usajili wa chama hicho. Wenzake walikuwa wamfuate baadaye.

CHANZO: Mwanahalisi

4 Apr 2011


Magufuli atamba mbele ya Rais
• Atoa onyo la bomoabomoa kwa wakazi Dar

na Bakari Kimwanga

SIKU chache baada ya Rais Jakaya Kikwete kumtaka Waziri wa Ujenzi, John Magufuli, aache ubabe katika kutekeleza zoezi la bomoabomoa, jana waziri huyo alitoa onyo mbele yake akiwataka wakazi wa Tegeta jijini Dar es Salaam hasa waliokuwa katika hifadhi ya barabara ya Mwenge hadi Tegeta, wahame wenyewe kabla hajachukua hatua za kuwaondoa kwa nguvu.

Magufuli aliyasema hayo jijini Dar es Salaam jana huku Rais Kikwete mwenyewe akiwa pembeni yake, wakati wa sherehe za uzinduzi wa mradi wa upanuzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 12.9 inayojengwa kwa msaada wa serikali ya Japan kupitia shirika lake la maendeo (JICA).

Waziri huyo makeke alisema katu hataacha kusimamia sheria namba 18 ya mwaka 2007 ambayo ilisainiwa na Rais mwenyewe ambayo inakataza watu kuingilia eneo la hifadhi ya barabara kwa kujenga makazi au kufanya biashara.

“Mheshiwa Rais, hata wakileta malalamiko kwako usiwasikilize, kwani sheria namba 18 uliyoisaini inakataza….naahidi kuisimamia na kuwepo kwa Makatapila katika eneo la Tegeta sasa ni ishara tosha kwa wakazi waliovamia hifadhi ya barabara kuondoka wenyewe kabla sijaanza kuwaondoa kwa nguvu!”

“Mradi huu utachukua miezi 27 kuanzia mwezi Februari na unatarajiwa kukamilika Mei, 2013 na utagharimu shilingi bilioni 88 na fedha zote ni msaada toka serikali ya Japan,” alisema Magufuli.

Barabara hiyo inapanuliwa kwa kiwango cha lami na itakuwa na njia nne na vituo rasmi vya mabasi 22.

Aidha, alieleza kuwa hatua ya Rais Kikwete kumteua kushika wadhifa huo ni msukumo tosha kwa yeye na wasaidizi wake kuhakikisha wanasimamia sheria na ikiwa kutatokea utata Naibu Waziri wake, Harrison Mwakyembe, kwa kushirikiana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Hebert Mrango, wanaweza kuutatua kwani wao ni wanasheria kitaaluma.

Awali akizindua mradi huo, Rais Kikwete aliiagiza wizara hiyo kukishughulikia mara moja kile alichokiita “genge la watu waliojipanga kuidhulumu serikali na wananchi” kwa kuwalipa mabilioni ya fedha makandarasi ambao ujenzi wao wa barabara ni wa kiwango hafifu na cha chini.

Pia aliiagiza Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuacha mara moja kugawa maeneo ya wazi na badala yake iyasimamie ipasavyo maeneo hayo yakiwamo yale ya watoto kuchezea kwa kuzuia kabisa ujenzi katika maeneo hayo.

Hata hivyo agizo hilo la Rais Kikwete linaonekana limechelewa sana kwani tayari kuna tuhuma na malalamiko mengi yanayoonyesha kuwa tayari maeneo mengi ya wazi yamekwishagawiwa kwa watu binafsi wenye uwezo kinyume cha taratibu, huku ikielezwa kuwa wahusika bado hawajachukuliwa hatua.

“Tumejitahidi kupandisha bajeti ya barabara mwaka 2006; ilikuwa bilioni 470 na hivi sasa tumepanda hadi trilioni 1.3 ili kuimarisha miundombinu ya barabara za ndani.”

“Wizara na Tanroads sasa msifanye malipo kwa watu ambao ujenzi wao ni wa kiwango cha chini na msipokee barabara ambayo iko chini ya kiwango ili kuongeza ufanisi wa barabara zetu jamani,” alisema Rais Kikwete.

Alisema kukamilika kwa upanuzi wa barabara ya Mwenge hadi Tegeta kutapunguza msongamano jiji la Dar es Salaam ambao kila mara umekuwa ukisumbua wakazi wa jiji.




5 Mar 2011


Tunaposema kuna ombwe la uongozi kwenye Serikali ya Rais Jakaya Kikwete baadhi ya vichwa panzi wanatuita wachochezi.Sasa unapoona Waziri anauchapa usingizi kwenye mkutano wa kimataifa,huku bosi wake akiwa kando,basi sijui tusemeje!!!

Na tunaposema Kikwete ni kiongozi dhaifu sio kama ni uchochezi,majungu au chuki binafsi.Hivi kama Rais anashindwa kumkemea Waziri wake kwa kulala kwenye mkutano tunaoambiwa una umuhimu mkubwa kwa nchi yetu (hadi imelazimu mkuu wa nchi aende mwenyewe badala ya kuwakilishwa na Makamu wake,Waziri Mkuu au Waziri wa Nishati na Madini)atamudu vipi kukemea wabaka uchumi ambao baadhi yao ni watu wake wa karibu waliochangia harakati zake za kuukwaa Urais?

Na kuna umuhimu gani kwa fedha ya walipa kodi kugharamia safari ya Ngeleja ambaye anaishia kulala mkutanoni badala ya kutuwakilisha?Au Kikwete amelazimika kwenda mwenyewe badala ya kumwacha Ngeleja pekee kwa vile alijua kuwa waziri wake huyo ataishia kuuchapa usingizi mkutanoni?

Kutegemea watu wa aina hii wanaweza kumsaidia Mtanzania kuondokana na umasikini wa kutupa ni sawa na kutegemea kugema damu kwenye jiwe.Na ukiona waziri mzima pasi haya anachapa usingizi huku Rais wake akiwa kando basi ujue wazi kuwa si akina Richmond na Dowans tu waliomudu kutuingiza mkenge bali tutarajie mengi zaidi.Unadhani kama Ngeleja anathubutu kuuchapa usingizi katika mkutano wa kimataifa unaouhusu maslahi ya nchi,hali inakuwaje wakati anashughulikia maslahi ya nchi ofisini mwake?Sintoshangaa kusikia kuna mikataba ya kuhamisha madini yetu ikisainiwa huku waziri yuko fofofo usingizini

Au Ngeleja ameanzisha mashindano ya kuchapa usingizi dhidi ya Mbunge wa CCM Kapteni John Komba,ambaye kama inavyoonekana pichani chini,alifumwa akiwakilisha wapiga kura wa jimbo lake kwa kuchapa usingizi Bungeni Dodoma



Picha kwa hisani ya Jamii Forums

24 Feb 2011


Katika harakati zake duni za kujinasua uhusika wake katika suala la ujambazi wa Dowans,Rais Jakaya Kikwete alijaribu kuwahadaa Watanzania kwa kudai,pamoja na mambo mengine,kuwa "hawajui wamiliki wa Dowans".

Na kwa bahati nzuri kwake,vyombo vyetu vya habari vikaishia kumnukuu tu.Lakini kwa minajili ya kufupisha makala hii(na kupunguza maumivu yanayotokanayo) tuweke kando kuangalia namna Kikwete alivyotengeneza mazingira ya ujio wa Dowans kupitia majambazi wengine wa Richmond.Hapa namaanisha kauli yake kuwa tatizo la umeme lingekuwa historia baada ya ujio wa mitambo ya kuzalisha umeme kutoka Marekani (na tukaishia kuletewa mitambo garasa)

Hatimaye mwarabu Adawi aliyekimbia ukombozi wa Mzanzibari,amediriki kuja na kutufanyia kila aina ya vituko (kukataa kupigwa picha,nk) na kutangaza hadharani kuwa yeye ndio mmiliki wa Dowans.Na kama kututukana Watanzania,akadai kuwa anaweza kuangalia uwezekano wa kupunguza FIDIA ANAYOPASWA KULIPWA KWA KUTUIBIA (yale yale ya vibaka wanaomkaba mtu kisha kumpigia ukelele wa "mwizi,mwizi...")

Adawi ambaye Kikwete anadai hamjui (japo anamjua sana kwani wana mahusiano ya "kifamilia")ameweza kutia mguu Ikulu na kuongea na Makamu wa Rais Gharib Bilali (anayekaimu urais katika kipindi hiki ambacho Kikwete yuko kwenye mizunguko yake).

Japo tunajua kuwa Ikulu yetu imegeuzwa kijiwe cha mafisadi ambao wana uhuru wa kutembelea mahala hapo patakatifu kila wanapojisikia lakini kwa Adawi kupewa nafasi ya kukutana na Rais (kwa maana ya anayekaimu nafasi hiyo),na mkutano huo kufanywa siri,inaashiria kuwa Kikwete na serikali yake sio tu anamjua Adawi bali pia anamtumikia.

Sintashangaa kusikia kuwa Kikwete aliamua kwenda Mauritania ili kumwezesha Adawi afanye uhuni wake kisha ahitimishe ziara yake kwa maongezi na kaimu wa Kikwete (Gharib Bilali).Na sintoshangaa kusikia kwamba kabla ya kurejea Tanzania,maswahiba hao wawili (Kikwete na Adawi) wakakutana faragha kujadili kuendeleza ujambazi wa Dowans.

Na hata tukiweka kando ujio wa Adawi,kauli ya Kikwete kuwa hawajui wamiliki wa Dowans ilhali majina ya wamiliki hao yapo BRELA (na Waziri Ngeleja alishayaweka hadharani kabla Kikwete hajatoa utetezi wake feki) inatosha kuwafahamisha Watanzania kuwa Rais wao ameshindwa kazi.How come Waziri ajue kile ambacho Rais hakijui?Je kama anashindwa kujua jambo dogo tu kama rekodi ndogo tu iliyopo BRELA atawezaje kujua na hatimaye kushughulikia matatizo ya Watanzania takriban milioni 50?

Tusipofumbuka macho kama wenzetu wa Tunisia,Misri,Libya na kwingineko wanakopambana na tawala dhalimu tunaweza kuishia kuwa koloni la Adawi,yaani mwarabu huyo kuongoza nchi yetu kwa kutumia remote control in the form of Kikwete.

24 Dec 2010


Majuzi,msomaji mmoja wa blogu hii alinitumia maoni ambapo pamoja na mambo mengine aliashiria kuwa nina chuki dhidi ya Rais Jakaya Kikwete.Msomaji huyo aliyejitambulisha kuwa mkazi wa hapa Glasgow alidai (namnukuu) "...I know you hate JK because whatever happens to him you have a negative view, even a tyre puncture...",yaani kwa Kiswahili,"najua unamchukia JK kwa vile chochote kinachotokea kwake wewe una mtizamo hasi,hata pancha ya tairi".Hii ndio mitizamo ya Watanzania wenzetu ambao licha ya kubahatika kuwa nje ya nchi,hususan nchi zilizoendelea kama hapa Uingereza,bado wana mitizamo mgando ambayo kwa kiasi kikubwa imechangia kutufanya hata miaka 49 baada ya uhuru kutamani mkoloni arejee.

Yah,huwezi kuwalaumu wanaotama mkoloni arejee japo mie si mmoja wao.Hivi tunawezaje kuelezea namna Watanzania wanavypelekeshwa kama watoto wadogo tena yatima siku chache tu baada ya Kikwete na CCM yake kupita huku na kule kuahidi neema,only for madudu and more madudu kuibuka kila kukicha?Unajua,angalau mkoloni alipotupelekesha alikuwa na excuse (japo isiyokubalika) kwamba yeye hakuwa Mtanganyika,na hakuwa na uchungu na nchi yetu.Na kwa wanaokumbuka vizuri somo la historia wanafahamu bayana kuwa ujio wa mkoloni ulikuwa kwa minajili ya kuendeleza nchi zao za asili,yaani kukwapua raslimali zetu kwa ajili ya viwanda vyao,kupata masoko ya bidhaa zao na eneo la makazi kwa nguvukazi ya ziada katika nchi hizo za wakoloni.Sasa ondoa neno mkoloni kisha weka neno FISADI,na yayumkinika kuhitimisha kuwa angalau mkoloni alikuwa na ajenda ya maendeleo huko kwao japo at our expense.Mafisadi nao wana ajenda za maendeleo pia,ila ni katika kutunisha akaunti zao kwenye mabenki ya hukohuko kwa wakoloni,kuongeza idadi ya nyumba ndogo zao (isomeke ufuska au uzinzi),kuongeza idadi ya mahekalu yao na magari ya kifahari,na sasa ajenda mpya ya kuimarisha himaya zao kwa kutumbukiza kila mwanafamilia na ndugu wa karibu kwenye siasa ili pindi baba akiondoka madarakani basi mwana amrithi kuzuia uwezekano wa baba mtu kukaliwa kooni kwa madudu aliyofanya akiwa madarakani.

Nimelazimika kuandika makala hii sio kwa minajili ya kumjibu huyo msomaji wangu wa hapa Glasgow bali ni baada ya kusoma toleo la mtandaoni la gazeti la Mwananchi ambapo kuna habari kuwa Tanesco wametangaza tena mgao wa umeme nchi nzima.Hivi sio majuzi tu shirika hilo lilitangaza mwisho wa mgao wa umeme?Tuwe wakweli,hivi uhuni huu wa Tanesco,ambao mie natafsiri kuwa ni uhuni wa serikali iliyopo madarakani,utaendelea hadi lini?So far,hakuna taarifa za wazi kuhusu athari za mgao wa umeme lakini haihitaji sayansi ya roketi au dissertation ya quantum physics kumaizi kwamba mgao huo una madhara makubwa mno kwa uchumi wa taifa na kwa maisha ya walalahoi kwa ujumla (vigogo licha ya kunufaika na ufisadi unaowawezesha kuuza jenereta kila mgao unapotangazwa lakini pia hawaathiriki kwa vile majumbani na maofisini kwao kuna jenereta zinazoendeshwa na fedha za kodi za walalahoi).

Hatuwezi kuilaumu Tanesco pekee kuhusiana na uhuni huu kwani ni siri ya wazi kuwa shirika hilo na sekta ya nishati kwa ujumla vimegeuzwa kitegauchumi kizuri kwa mafisadi.Majuzi tu tumesikia majambazi wa Richmond wakijiandaa kurejeshewa fedha walizotuibia ambapo watalipwa fidia ya mabilioni kwa mgongo wa binamu zao wa Dowans.Hatuwezi kumwepusha Kikwete na CCM yake na ufisadi huu kwa vile licha ya madudu hayo kushika hatamu wakati wa utawala wake,sasa tunafahamu kuwa amekuwa akiwakingia kifua mafisadi wasichukuliwe hatua za kisheria (thanks to nyaraka za siri za kidiplomasia zilizovujishwa na mtandao wa WikiLeaks).Kwa wale ambao hawajabahatika kusoma habari hizo,kuna nyaraka kutoka ubalozi wa Marekani hapo Dar zilizobeba maongezi kati ya bosi wa Takukuru Edward Hoseah na afisa ubalozi wa Marekani ambapo Hoseah alinukuliwa akieleza bayana kwamba Kikwete alishinikiza baadhi ya mafisadi wasichukuliwe hatua.Japo bosi huyo wa Takukuru amejaribu kuruka kimanga na kukana tuhuma hizo,kila mwenye akili timamu anafahamu kuwa ufisadi unashamiri Tanzania kwa vile Kikwete ameshindwa kuwachukulia hatua mafisadi papa licha ya madaraka lukuki aliyorundikiwa na Katiba.

Baadhi yetu tuliwaasa Watanzania wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita majuzi kwamba kuirejesha tena madarakani serikali ya Kikwete ni sawa na kumwaga chumvi kwenye kidonda kibichi,na matokeo yake ndio haya.Wakati tunaelekea mwezi wa pili tangu Kikwete atangazwe mshindi,hakuna lolote la maana lililokwishafanyika kuashiria kuwa kiongozi huyo ana ajenda mpya tofauti na zile zilizotawala miaka mitano iliyopita,kubwa ikiwa na kushamiri kwa ufisadi na uimarishaji himaya za mafisadi huko nyumbani.

Sawa,makosa yameshafanyika kwa kumrejesha Kikwete na CCM yake madarakani lakini hiyo isiwe sababu ya kuendelea kunung'unika kimoyomoyo huku nchi yetu ikizidi kuteketea.Umefika wakati Watanzania wasikubali kupelekeshwa namna hii.Kwanini Kikwete asibanwe kuhusu tatizo la umeme licha ya ahadi zake za mara kwa mara kuwa tatizo hilo lingekuwa historia?Au alimaanisha kuwa tatizo hilo litaendelea kuwa la kihistoria?

Nimesikia taarifa za mpango wa Chadema kuandaa maandamano ya nchi nzima kupinga kuongezwa bei ya umeme.Yaani licha ya mgao wa kila kukicha bado Tanesco wanataka kuongeza bei?Yayumkinika kuhisi kuwa wazo hilo la ongezeko la bei ya umeme ni la kifisadi lenye lengo la kupata fedha za kuwafidia mafisadi wa Richmond/Dowans.Ni muhimu kwa kila Mtanzania mzalendo kuunga mkono mpango huo wa maandamano ya amani ili kufikisha ujumbe kwa Kikwete na serikali yake kuwa Watanzania wamechoka kupelekeshwa.Hata hivyo,kama maandamano ya kuwapongeza wabunge wa upinzani yalizuiliwa na polisi,sidhani kama serikali itaridhia maandamano hayo ya kupinga ongezeko la bei ya umeme.

Mwisho,tuna choices mbili tu:kuchukua hatua sasa kabla hatujafika mahala ambapo hata tukichukua hatua itakuwa sawa na kutwanga maji kwenye gunia,au tusubiri kusoma rambirambi kuhusu nchi yetu hapo 2015.

5 Sept 2010


Inaudhi na kukasirisha kuona gazeti la serikali,Habari Leo,likijipachika jukumu la kumuua kisiasa mgombea wa Chadema Dokta Wilbroad Slaa kama ambavyo imekuwa ikifanywa na magazeti ya Habari Corporation na Changamoto,na mengineyo yanayofadhiliwa na mafisadi.

Gazeti hilo limeandika kwa kirefu kuhusu anayedaiwa kuwa mume wa mwenza wa sasa wa Dkt Slaa,Josephine Mushumbusi.Ungetegemea gazeti hilo linaloendeshwa kwa fedha za walipa kodi wa Kitanzania pasipo kujali itikadi zao za kisiasa,lingetafakari kwa makini madhara ya habari hiyo.Wanajua sana wanachofanya,na yayumkinika kuamini kuwa serikali inayoongozwa na mgombea wa CCM,Jakaya Kikwete,imeridhia uchapishaji wa habari za aina hiyo.

Kuna msemo wa busara unaoasa "WANAOISHI KWENYE NYUMBA ZA VIOO WASIRUSHE MAWE".Mantiki ya msemo huo ni kwamba kama una wasifu wenye mawaa ya aina moja au nyingine then si wazo jema kuwachafua watu wengine.Wengi wetu tunafahamu "ishu binafsi" za viongozi wa CCM ikiwa ni pamoja na Kikwete mwenyewe.Hazizungumzwi hadharani kwa kuwatunzia heshima viongozi hao lakini inaelekea katika kutapatapa kwao baada ya kugundua hawamwezi Dokta Slaa kwa hoja,wameamua kuhamia kwenye character assassination.

Majukwaani,Kikwete na CCM yake wanajifanya kuhubiri umuhimu wa kampeni za kistaarabu lakini pembeni wanaruhusu raslimali za umma zitumike kumchafua Dokta Slaa.Kikwete alichukua hatua za haraka pale mtandao maarufu wa Ze Utamu ulipochapisha picha zinazomhusu lakini anaruhusu gazeti la serikali litumike kumwandama Dkt Slaa.

Na kwa kuonyesha unazi,kuna mahala katika habari hiyo ambapo pasi aibu wameandika (nanukuu) "Na wakati Mahimbo akiwa njia panda akishindwa kujua hatima ya ndoa yake, Dk. Slaa, Padri msomi `amelitangazia’ taifa mbele ya mikutano ya kampeni ya chama chake cha Chadema kuwa Josephine ndiye mke wake mtarajiwa..." 

Hivi Mhariri wa Habari Leo hafahamu kuwa Dkt Slaa sio Padri bali aliwahi kushika nafasi hiyo na kuiacha?

Blogu hii inamshauri Kikwete akemee mkakati huu mufilisi wa character assassination.Wengi wanafahamu kwa undani maisha ya Kikwete tangu akiwa Waziri,na wanajua vema maisha yake binafsi ndani na nje ya nchi.Asijivunie vyombo vya dola kumlinda pindi kibao kitapogeuzwa upande wake.Ni bora Dokta Slaa anayetangaza hadharani kuhusu uhusiano wake na Josephine kuliko kashfa lukuki zinazohifadhiwa kuhusu viongozi wa CCM kwa vile tu tunawaheshimu na tuna mambo muhimu zaidi ya kuzungumzia kuliko maisha binafsi ya viongozi wetu.

I repeat: Those who live in glass houses shouldn't throw stones!!!



22 Aug 2006

KULIKONI UGHAIBUNI-21

Asalam aleykum,

Leo nina jambo muhimu sana kuhusiana na maslahi ya Taifa letu.Nawaomba wasomaji wapendwa tuwe pamoja kwa makini ili tusipoteane njiani na hatimaye kuleta tafsiri potofu ya ninachotaka kuzunguzia.Natanguliza rai-au niite tahadhari-kwa vile mada yangu ya leo ni nyeti,na ni kuhusu suala ambalo mara nyingi limekuwa likikwepwa na watu wengi.Lakini kabla sijaingia kwa undani,nielezee uzoefu wangu mimi mwenyewe katika suala hilo.

Kwa wafuatiliaji wa makala hii watatambua kwamba mara zote huwa naanza na asalam aleykum.Nimezowea sana kuwasalimia ndugu zangu kwa namna hiyo.Pengine ni kwa vile nimewahi kukaa miji ambayo salamu hiyo inatumika sana,au pengine wengi wa marafiki zangu ni Waislam.Robo ya elimu yangu ya msingi niliipata mkoani Kigoma katika kitongoji cha Ujiji.Nakumbuka kuna wakati flani katika darasa nililokuwa nasoma tulikuwa Wakristo watatu tu na waliosalia (nadhani zaidi ya silimia 90) walikuwa Waislam.Niliwahi kufundisha sekondari flani mjini Tanga na takribani robo tatu ya wanafunzi wangu walikuwa Waislam pia.Na nikipiga hesabu ya harakaharaka,katika marafiki zangu kumi bora saba ni Waislam.Hata siku moja,tangu nikiwa Kigoma,Tanga,Dar na kwengineko sikuwahi kujiona nimezungukwa na watu tofauti nami ambaye ni Mkristo Mkatoliki.Wanafunzi wenzangu,wanafunzi niliowafundisha na marafiki zangu walinichukulia kama Mtanzania mwenzao japo tulikuwa tunatoka madhehebu tofauti.Na hivi karibuni nilipokuja huko nyumbani kwa utafiti wa PhD nayosoma,wengi wa niliohojiana nao walikuwa Waislam.Sikuwahi kupata matatizo yoyote hata pale nilipokutana na wanaoitwa mujahidina.Katika levo ya familia,kaka-binamu yangu mmoja ambaye ni Mkatoliki wa kwenda kanisani kila Jumapili ana mke ambaye ni Mwislam wa swala tano.Uzoefu wangu huo mdogo unatoa picha moja muhimu:Watanzania tumekuwa tukijichanganya sana bila kujali tofauti zetu za kidini.Nikisema kujichanganya namaanisha kujumuika pamoja na sio vinginevyo.

Kuanzia kwenye miaka ya 80 kulianza kujitokeza dalili zilizoashiria kwamba mambo si shwari sana katika eneo la dini nchini.Tunakumbuka uvunjaji wa mabucha ya nguruwe,matukio kwenye msikiti wa Mwembechai,mihadhara ya kidini,suala la Ustaadh Dibagula na mengineyo.Wapo waliosema kwamba kulikuwa na kikundi cha watu wachache kilichokuwa kinachochea vurugu za kidini kuganga njaa zao.Wapo pia waliokuwa wanadai kuwa vurugu za kidini zilikuwa na sura ya kisiasa huku mara kadhaa chama cha CUF kikibebeshwa lawama.Yayumkinika kusema kuwa japo viongozi wetu walikuwa wakikemea vurugu hizo hakukuwa na jitihada za makusudi za kubaini chanzo hasa ni nini.Wanataaluma wetu nao kwa namna flani wamekuwa wakilikwepa suala hili pengine kwa vile linagusa hisia za wengi au pengine kutokana na hisia kwamba matokeo ya tafiti zinahusu migogoro ya kidini huweza kuchangia kuleta utata zaidi badala ya ufumbuzi wa matatizo.Mwalimu wangu wa zamani katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,Dr John Sivalon alichapisha kitabu ambacho kilitokana na thesis yake kuhusu mahusiano kati ya Kanisa Katoliki na Serikali ya Tanzania.Bila kuingia kwa undani kujadili kitabu hicho cha mhadhiri huyo wa Kimarekani ambaye pia ni Padre,ukweli ni kwamba kimekuwa ni nyenzo muhimu katika mihadhara na mijadala ya kidini nchini,japo sina hakika kama kimesaidia katika kuwa sehemu ya utatuzi wa matatizo yaliyopo.

Hebu sasa niingie kwenye ishu yenyewe.Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na mijadala inayoendelea kwenye forums mbalimbali za Watanzania kwenye internet.Suala hilo ambalo limegusa hisia zangu ni madai kwamba Rais Jakaya Kikwete amekuwa akiwapendelea Waislam katika teuzi mbalimbali anazoendelea kuzifanya tangu aingie madarakani.Na pengine kinachotajwa zaidi ni ule uteuzi wake wa kwanza wa mabalozi wa mwanzo (akina Adadi na wengineo) ambao kwa mujibu wa majina yao wote ni Waislam.Pengine bila kudadisi sifa za walioteuliwa,wanaolalamika wakaangalia dini zao.Teuzi nyingine nazo zimeendelea kuzua mijadala isiyo rasmi japo sina uhakika kama na huko nyumbani nako hali ni kama hii niliyoiona kwenye mtandao.Ila niliona kwenye mtandao makala mbili tofauti ambazo nadhani zilitolewa kwenye magazeti ya huko nyumbani ambapo mwandishi mmoja mkongwe alikuwa akijibu hoja za mwanasiasa flani ambaye nadhani pia ni kiongozi wa kidini,na mada yenyewe ilikuwa ni hiyohiyo eti Kikwete anawapendelea Waislam.

Mimi siamini kabisa kwamba yeyote kati ya aliyeteuliwa-iwe kwenye uwaziri,unaibu waziri,wakuu wa mikoa,wakurugenzi na kadhalika-wamepewa dhamana zao kutokana na Uislam au Ukristo wao.Unajua kwa miaka mingi sisi tumekuwa Watanzania kwanza halafu ndio vinafuatia vitu kama Ukristo au Undamba wangu.Na ndio maana kule Ujiji,Tanga,Dar na kwingineko nilikokuwa sikuwahi kupata matatizo na waliokuwa karibu nami kwa vile cha muhimu kwetu haikuwa dini au kabila bali urafiki au mahusiano yetu kikazi.Na naamini kabisa kuwa Kikwete ni Mtanzania kwanza,na anaongoza Watanzania kwa misingi ya umoja wao na sio tofauti za kidini,na kwa mantiki hyo hata anapochagua viongozi haangalia dini bali sifa za wateuliwa.

Hata hivyo,kuna matatizo kadhaa yanayohusiana na suala la dini nchini.Tusijidanganye kwamba hatufahamu kuwa kumekuwa na manung’uniko miongoni mwa Waislam kuhusu usawa katika sekta ya elimu na ajira.Iwapo chanzo cha tatizo hilo ni sera za kibaguzi za wakoloni au kuna mbinu za makusudi za kuchochea matatizo hayo,hiyo sio muhimu sana kama ilivyo kwa umuhimu wa serikali,taasisi mbalimbali,wanataaluma na wananchi kwa ujumla kulitafutia ufumbuzi tatizo hilo.Matokeo ya awali ya utafiti wangu unaohusu harakati za Waislam nchini yanathibitisha kwamba matatizo yapo na yanajulikana ila kinachokosekana ni jitihada za makusudi za kupata ufumbuzi wa kudumu.Habari nzuri ni kwamba,hilo (la kupata ufumbuzi) linawezekana iwapo busara zitatumika na wadau kujumuishwa kwa karibu.Namalizia kwa kusisitiza kwamba wanaoleta madai ya udini wanatumia haki yao ya kikatiba kutoa mawazo yao,japo siafikiani nao.Hivi mtu anapooa au kuolewa na mtu anayetoka naye dini moja anaitwa mdini?Hapana.Kitakachojadiliwa hapo ni sifa za huyo mume au mke.Hivyohivyo,Jakaya hawezi kuitwa mdini pindi akichagua Muislam kama yeye alimradi ana sifa zinazostahili.

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.