13 Nov 2006

KULIKONI UGHAIBUNI-31

Asalam aleykum,

Moja ya mambo ambayo yalikuwa magumu kwangu baada ya kuwasili hapa nilipo ni namna ya kuendana na aina ya chakula kilichozoeleka hapa.Mie ni Mndamba,na kule kwetu Ifakara hadithi ni wali,wali na wali sana.Asubuhi ni chai na kiporo cha wali,mchana ni wali,na usiku hadithi ni hiyohiyo ya wali.Nilipokuwa nawakaribisha rafiki zangu pale Ifakara mama alihakikisha kuwa lazima wapate wali,na japo ugali pia ni mlo lakini kwa tabia za Kindamba kumlisha mgeni ugali ni kama kutompatia makaribisho mazuri.

Sasa nilipokuja hapa Uingereza nikakutana na mambo ya chips samaki,burgers,pizza na kadhalika.Sio kwamba huko nyumbani hakuna vitu hivyo katika zama hizi za utandawazi (kuna Steers,Subway,Nando’s,nk) lakini makoronya hayo kwangu ilikuwa ni ya anasa na pia ladha yake haikuwa sawa na ile ya wali nilouzowea Ifakara.Ukienda huko kwenye mwezi Juni au Julai unakutana na harufu ya mchele mpya ambao unanukia utazani umemwagiwa pafyumu bila kusahau habari za pepeta.

Majuzi nilikuwa naongea na baba yangu mdogo Mzee Magungu ambaye makazi yake ni Kiberege.Alinipa habari ambazo kwa hakika ni za kusikitisha.Labda kwanza niwapatie jiografia ndogo ya bonde la mto Kilombero,eneo ambalo lina rutuba ya asili ambayo kimsingi ndio chemchem ya utajiri wa mpunga na hatimaye mchele kwa maeneo hayo.Sio hadithi za kusifia sehemu ninayotoka lakini ni ukweli usiopingika kwamba kwa namna flani Mungu ameijalia sana wilaya ya Kilombero.Kuna vijito na mito lukuki ambayo mingi yao inaishia Mto Kilombero.Michache kati ya hiyo ni Mto Lwipa,Mpanga,Ruhuji,Mwatisi,Furua,Misima na Kihansi.Kulingana na kitabu cha maeneo yenye unyevunyevu ambayo yana umuhimu wa kimataifa (Directory of Wetlands of International Importance) bonde la Mto Kilombero ni la kipekee kitaifa na kimataifa kwa vile licha ya ardhi yake nyenye rutuba ya mwaka mzima kuna utajiri mkubwa wa misitu, wanyama na ndege asilia.Ndio maana enzi hizo majangili kutoka sehemu mbalimbali walikuwa wakimiminika huko “milima ya Golan” kuwinda tembo na faru,na hadi leo naamini kuwa nyama za nyati,mbawala,swala na nyinginezo bado si adimu.Takwimu zinaonyesha kuwa Bonde la Mto Kilombero ni makazi ya asilimia 75 ya swala waliopo duniani kote.Pia eneo hilo lina takribani aina 20,000 ya ndege wanaopenda maji (water birds) sambamba na aina tofauti 23 za samaki (hapo ndipo kuna akina “mlamu kaliandili”,”perege”,”kitoga”,“mbufu”,nk…nadhani Wandamba wakisikia hivi mate yanawachuruzika).Kuna utani mmoja kwamba Wandamba,Wambunga,Wabena,nk wana uhodari sana wa kula samaki wenye miiba sana halafu wana teknolojia ya kutenganisha nyama ya samaki na miiba hiyo mdomoni,yaani unakuta miiba ya samaki inatoka kwenye pembe ya mdomo kana kwamba kuna mashine inayotenganisha nyama na miiba.Ardhi yenye rutuba ya bonde hilo ndio inayomudu ustawi wa miwa ya sukari (Kilombero Sugar),miti ya mitiki,na mazao lukuki.Pia kutokana na utajiri huo wa maliasili,eneo hilo limekuwa kivutio kwa watalii (kwa mfano kingo za hifadhi ya Udzungwa) japokuwa inasikitisha kuona eneo hilo haliendelezwi ipasavyo.

Kilio cha wakazi wa maeneo yaliyopo kwenye Bonde la Mto Kilombero ni uvamizi wa jamii ya wafugaji ambao wengi wao wanatoka Kanda ya Ziwa na Arusha.Hawa jamaa wana ukorofi wa namna flani.Unajua mgeni sharti uwe na heshima kwa mwenyeji wako,lakini hawa “waungwana” wamekuwa wakitumia siasa za ubabe kulisha mifugo yao,ambapo kimsingi chakula cha mifugo hiyo ni mazao ya wakazi halisi wa maeneo hayo.Licha ya uvamizi huo kwenye mazao,jamii hiyo ya wafugaji inaelekea kutishia vyanzo vya mito vinavyolirutubisha Bonde la Mto Kilombero sambamba na kuathiri mito kadhaa iliyopo maeneo hayo.

Kwa mujibu wa Mzee Magungu,kilio cha wakazi wa maeneo hayo sio cha hivi karibuni bali kimekuwepo kwa muda mrefu.Ngazi husika katika serikali zimefahamishwa lakini hadi sasa hakuna dalili ya utatuzi wa tatizo hilo.Naomba nisisitize kwamba mimi binafsi nimeshuhudia uharibifu wa mazao na mzingira unaofanya na jamii hizo za wafugaji katika safari zangu tatu nilizofanya nilipokuwa huko nyumbani kwa ziara ya kimasomo.Yaani ukifika Morogoro mjini ukiwa unaelekea Ifakara unakutana na kundi kubwa la jamii za wafugaji wakijiandaa kwenda kulisha mifugo yao maeneo hayo.Na humo njiani unakutana na mifugo lukuki ambayo haichagui kati ya majani na mpunga au mahindi.Sawa,Tanzania ni ya Watanzania wote lakini kuna watu wana maeneo yao binafsi pamoja na mashamba na mito wanayoitegemea kwa kilimo na uvuvi.Sasa uhuru wa kikatiba wanaopatiwa watu wa kwenda popote wanapotaka usitumiwe vibaya kiasi cha kuwaathiri wenzao.

Ombi kubwa la wakazi wa maeneo hayo ni kwa Mheshimiwa Jakaya Kikwete kwa vile wanaamini kuwa walimchagua kutokana na sifa zake za kuwajali wananchi wake.Wanamwomba awabane watendaji wake ambao wanaelekea kulea matatizo hadi pale yanapolipuka.Kama filamu ya mapanki ilimchukiza Rais kwa vile ilikuwa inachafua jina la nchi yetu huku nje basi wanamwomba afahamu kuwa uvamizi wa jamii ya wafugaji sio tu unachafua mahusiano kati ya wakazi wa maeneo hayo na wafugaji bali pia unaathiri jitihada zao halali za kumudu maisha kwa njia ya kilimo na uvuvi.Makala hii inaomwomba Rais Kikwete kuangalia njia za kutatua mgogoro huu ambao ukiachiwa unaweza kuwa mbaya kuliko ile inayotokea huko mkoani Mara.Ardhi ni haki ya kila Mtanzania lakini pia ni muhimu kukumbuka kuwa hakuna haki bila wajibu,na wajibu wa jamii za wafugaji wanaovamia Bonde la Mto Kilombero ni kuelewa kuwa wanawakosea heshima wenyeji wao na vitendo vyao vinaa thri ustawi wa eneo hilo lenye umuhimu si kwa wakazi wake tu bali pia Taifa kwa ujumla.

Alamsiki.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.