13 Nov 2006

KULIKONI UGHAIBUNI-34

Idd Mubarak (japo nimechelewa kutoa salamu hiyo,nategemea kusikia “minal faidhina” kutoka kwako msomaji mpendwa wa safu hii).

Katika mojawapo ya makala zangu za nyuma niliwahi kuahidi kuwazungumzia jamaa flani ambao ndio kama uti wa mgongo wa uongozi wa Rais George W Bush.Hawa jamaa wanafahamika kama “neoconservatives” au kwa kifupi “neocons.”Msamiati huu uliibuka kwenye miaka ya 60 na 70 na ukapata umaarufu zaidi wakati wa utawala wa Rais Bush mkubwa,Ronald Reagan na sasa kwenye utawala wa huyu Bush mdogo ambaye anaonekana kuwategemea mno jamaa hao kiasi cha watu wengine kuamini kuwa wao ndio wanaendesha nchi hiyo kwa kumtumia Rais huyo.

Wengi wa hawa neocons ni watu ambao “shule imepanda” kweli (ni wasomi).Kwa kiasi kikubwa mafanikio yao ya kisiasa yametokana na elimu yao na sio mbinu chafu za kupata uongozi.Na kama ilivyo kwenye nchi nyingine za magharibi,wengi wa jamaa hawa wako ndani ya vivuli vya taasisi ambazo aidha ni za kitaaluma,ushauri au zile ambazo zinatetea maslahi flani (interest groups) lakini zilizo maarufu zaidi ni hizo zinazoitwa “think-tanks” (nadhani kwa lugha yetu ya taifa tunaweza kuziita “visima vya fikra” japo BAKITA wanaweza kuwa na msamiati bora zaidi).Think-tanks nyingi ni taasisi zinazosikilizwa na kuheshimika hasa kwa vile huwa zinakusanya wasomi waliobobea,wanasiasa wastaafu na watu wengine maarufu kwenye maeneo kama uchumi,sayansi na teknolojia,jamii,nk.Zilizo maarufu miongoni mwa nyingi zinazomsapoti Bush ni “American Enterprise Institute” (AEI) na “Project for the New American Century (PNAC)”.Neocons maarufu ni pamoja na Makamu wa Rais Dick Cheney,Waziri wa Ulinzi Donald Rumsfield,Rais wa Benki ya Dunia Paul Wolfowitz,Balozi wa Marekani kwenye Umoja wa Mataifa John Bolton,Balozi wa Marekani huko Irak Zaymal Khalilzad,Profesa wa siasa-uchumi ya kimataifa katika chuo kikuu cha John Hopkins Francis Fukuyama ,Mkurugenzi wa zamani wa CIA James Woolsey,Gavana wa Florida Jeb Bush (mdogo wake George Bush),Mhariri wa gazeti la Weekly Standard na mchangiaji kwenye kituo cha televisheni cha Fox News Bill Kriston na Naibu wa zamani wa Ulinzi na mtetezi maarufu wa siasa za Israel Richard Perle,na wengineo wengi ambao haiwezekani kuwataja wote kwenye makala moja kama hii.

Kimsingi hawa jamaa ndio waasisi wa vita dhidi ya Iraq na wamekuwa wakitumia ujuzi,elimu,umaarufu na nafasi zao kutetea sera za Bush ambazo kimsingi wao ndio vinara wake.Miongoni mwa imani zao ni pamoja na kuimarisha na kutumia “ipasavyo” nafasi ya Marekani kama taifa lenye nguvu zaidi ulimwenguni,kushambulia taifa lolote linaloonekana tishio kwa ustawi wa Marekani,kuisapoti Israel kwa nguvu zote (wengi wao wana asili ya Israel),kubadili “jiographia” ya nchi za Mashariki ya Kati kulingana na matakwa ya Marekani na hili la vita dhidi ya ugaidi.

Nadhani hadi hapa umeshaanza kuchoshwa na maelezo yangu kuhusu jamaa hawa na siasa zao.Tulia kidogo,nataka kujenga hoja muhimu hapa ambayo inawafananisha hawa jamaa na kikundi flani ambacho kinaelekea kushika hatamu kwenye siasa za huko nyumbani.Hapa nawazungumzia wanaoitwa “WANAMTANDAO.”Unajua hadi hivi karibuni nilikuwa naamini kuwa nazifahamu sana siasa za nchi yangu hadi nilipokutana na “mtaalam” flani wa siasa halisi (japo hazionekani waziwazi) za Tanzania.Huyo jamaa yangu aliniambia kuwa kwa sasa kundi la wanamtandao limeshika vilivyo hatamu ya siasa za Bongo,na wanamtandao wamekuwa sehemu muhimu ya maamuzi mbalimbali ya CCM na serikali yake (ya Bara,kwa vile nguvu za wanamtandao huko Visiwani hazijulikani sana japo zinaweza kuwa zipo).Mtaalam huyo alinidokeza kuwa wanamtandao wako kila kona:ndani ya serikali na taasisi zake,vyombo vya habari,taasisi za elimu,mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali,biashara binafsi (mambo ya fedha) na hata kwenye jobless kona za mitaani.Pia alinijulisha kuwa wanamtandao wana nguvu kweli na wametandaa hasa.Hapo ndio nikamkumbuka nilipokuwa huko nyumbani kulikuwa na jamaa mmoja aliyekuwa “akimwaga bia ovyo” kwenye baa flani maeneo ya Kinondoni huku akitamba kwamba “wao wanamtandao ndio wamekamata nchi kwa sasa.”Kwa wakati huo nilidhani huyo jamaa alikuwa anatafuta “ujiko” (sifa) tu,lakini sasa nakiri kwamba pengine alikuwa anaongea ukweli.

Mimi sina ugomvi na wanamtandao alimradi wanayofanya hayaipeleki nchi yetu kusikoeleweka.Wasiwasi wangu mkubwa ni ukweli kwamba ndani ya kundi hilo kuna watu safi na wengine wana sifa zenye walakini.Hawa wa kundi la pili ndio nawahofia zaidi kwa vile inawezekana wakawatumia wenzao walio katika nafasi za kutoa maamuzi kuhakikisha maslahi yao binafsi yanatekelezwa.Kinachoogopesha zaidi ni ukweli kwamba kundi hili limekuwa la siri kwa muda mrefu na karibu wahusika wake wote ni watu ambao tunawahisi tu kwa vile hawatamki hadharani uanamtandao wao.Pia inajulikana kuwa baadhi yao si viongozi wa chama tawala japokuwa wanaweza kufanya matakwa yao kutekelezwa bila ya wao wenyewe kuhudhuria vikao vya chama hicho.

Pengine ni wakati mwafaka kujiuliza hivi hatma ya hawa jamaa ni nini.Wajuzi wa mambo wanasema kuwa hawa jamaa ndio waliotengeneza timu ya ushindi wa Jakaya,kazi ambayo wameifanya kwa zaidi ya miaka 10.Leo wamefanikiwa kumuingiza Jakaya madarakani na pia baadhi yao wamefanikiwa kushika hatamu ndani ya serikali na chama tawala.Na tunafahamu kuwa wanataka kuendelea kuwepo kwa ajili ya chaguzi zijazo.Lakini wasiwasi wangu ni pale watakapokosana na wenzao walio madarakani.Uwezekano huo upo japo sio mkubwa kwa sasa.Upo kwa vile baadhi ya wanamtandao hawako ndani ya chama na serikali,sasa ipo siku yatatolewa maamuzi ambayo yatalenga zaidi maslahi ya chama au Taifa kwa ujumla kuliko maslahi ya wanamtandao walio nje ya uongozi.Niite “conspirancy theorist” (mwanafalsafa mwenye kuhisi “hapa kuna namna”) lakini historia imeonyesha kuwa ni rahisi sana kwa vikundi visivyo rasmi na vinavyoendeshwa kwa usiri kuingia kwenye migogoro hasa kwa vile nidhamu ya uongozi katika vikundi vya namna hii huwa ni haba,wengi wa “wanachama” huwa na matarajio makubwa pengine zaidi ya uwezo wa wanaowategemea kutimiza matarajio hayo na wakati mwingine kuna tabia ya kuoneana “donge” (wivu) kwamba “mbona mie nilifanya kazi kubwa sana kumfikisha flani hapa alipo lakini sithaminiwi kama flani ambaye mchango wake ni mdogo kuliko wangu.”Angalia mfano huu: CCM ikishindwa kuafikiana kuhusu uteuzi mgombea wake ajae watawekana chini na demokrasia ya namna flani itatumika kufikia muafaka kwa maslahi ya chama.Kwenye mtandao je?Hivi mnaoongea na wanamtandao wanawaeleza maslahi yao halisi ni kwenye nini?Chama,mgombea au matumbo yao binafsi?

Neno la mwisho,nimesoma kwenye magazeti kuwa hatimaye kampuni ya Richmond wameanza kuleta mitambo.Lakini badala ya kuomba radhi kwa kuchelewa kutimiza ahadi zao ndani ya muda waliojiwekea wenyewe eti wanalalamika kuwa walikuwa wanapigwa majungu.Enewei,kuna msemo kwamba ahadi haina maana hadi inapotekelezwa.Tunasubiri hizo jenereta zianze kufanya kazi tukitarajia kuwa hii sio miujiza kama ya Mv Alina.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.