13 Nov 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Kwanza nitoe salamu zangu za rambirambi kwa familia ya dereva wa daladala aliyeuawa kwa kupigwa risasi na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Braza Dito.Ni matarajio yetu wengi kuwa sheria itachukua mkondo wake na haki itatendeka,na kwa wakati huu inatupasa tuiachie mahakama ifanye kazi yake bila kuingiliwa.

Wakati naandaa makala hii wananchi wa Marekani wanapiga kura katika uchaguzi wa kati ya muhula (mid-term) ambao unaotazamiwa kutoa hukumu kwa Rais George W Bush kuhusu sera zake za Irak.Pamoja na kwamba kuna mambo mengine ambayo wapiga kura wanayaangalia kwa makini lakini sio siri kwamba vita ya Irak ndio imekuwa ajenda kubwa zaidi.Uchaguzi huu unanikumbusha jambo moja lililowahi kujitokeza katika Uchaguzi Mkuu uliopita wa mwaka 2004 ambapo Rais Bush alirejea tena madarakani.Wakati wa kampeni za uchaguzi huo ilijitokeza ishu ya binti ya Makamu wa Rais Dick Cheney aitwaye Mary ambaye (ashakum si matusi) ni msagaji (lesbian).Ilikuwa inafahamika bayana kuwa Cheney kama mhafidhina haafiki mapenzi au ndoa ya watu wa jinsia moja,lakini mwanae ndio hivyo tena.Pengine ni kwa vile tu chama cha makamu huyo wa Rais (Republicans) ni wajanja wa kuzima ishu zenye utata ndio maana suala hilo liliweza kudhibitiwa “kiaina” ili lisiathiri kampeni za Bush na Cheney na chama chao.Nimetoa mfano huo kuonyesha jinsi gani familia ya kiongozi ilivyo muhimu katika suala zima la uongozi na taswira anayotoa kwa anaowaongoza.

Mwaka 2002 nilibahatika kukutana na mtoto mmoja wa marehemu Baba wa Taifa.Huyu bwana anaitwa Makongoro Nyerere.Ndiye aliyenipokea mie na wenzangu tulipofika hapa kwa mara ya kwanza.Kwa vile kabla ya hapo nilikuwa sijawahi kukutana na mtoto wa Rais aliyestaafu au aliye madarakani basi nilikuwa na hisia kwamba huyu jamaa atakuwa kile watoto wa mjini wanaita “pozi” (pengine kwa Kiswahili kizuri tuite dharau,kujiskia au maringo).Lakini Makongoro alikuwa mtu tofauti kabisa.Yaani kwa “lugha ya mama” (Kiingereza) tungeweza kumwita “a down-to-earth person”,hakuwa na maringo,kujiskia au dharau bali alinichukulia mimi na jamaa zangu kama watu tunaotoka katika familia moja.Sintamsahau huyu bwana.Lakini nikapata bahati nyingine ya kuishi na mtu aliyetokea kuwa rafiki yangu wa karibu hadi kesho anaitwa Eustace,mtoto wa jaji flani mwandamizi huko nyumbani,na ambaye kabla hatujakutana hapa Uingereza alishawahi kukaa sana huku ughaibuni.Sasa kwa mazowea yetu,mara nyingi watu wa aina hiyo huwa ni wa kujiskia na wasioelewa namna ya kuishi na sie tuliokulia katika maisha ya kawaida.Lakini huyu rafiki yangu (mwenyewe atakuwa anacheka akisoma haya nayoandika,maana ni “muumini” wa safu hii na gazeti hili) alinithibitishia tena kuwa kutoka katika familia ya kigogo hakumzuii mtu kuwa wa kawaida.Niseme hivi,huyu jamaa kama sio ule mwonekano wake kuwa anatoka familia yenye neema huwezi kabisa kumdhania kuwa ni mtoto wa kigogo kwa vile ni “mtu wa kujichanganya” sana na hajitofautishi na mtu yoyote yule ukilinganisha na wengine ambao pengine hawako hata “levo” moja na familia anayotoka yeye.

Wikiendi iliyopita nilialikwa kwenye “bethdei pati” ya rafiki yangu mmoja anayeishi huko Salford,Greater Manchester.Kabla ya kuamua niende au la,nilidadisi kuhusu waalikwa wengine kwenye pati hiyo.Nikaambiwa miongoni mwao ni mtoto wa Jakaya aitwaye Ridhwani.Nikajikuta nimerudi kulekule kwenye mawazo nilokuwa nayo kabla sijamfahamu Makongoro au rafiki yangu mtoto wa Jaji mwandamizi.Unajua tena,sherehe ikiwa na baadhi ya wahudhuriaji ambao ni watu wenye majina au wale wenye kujiskia au wenye maringo basi inakuwa kama karaha vile kwa sie tuliozowea “maisha ya chinichini” au kwa kimombo “low profile”.Niite mwoga lakini naamini wengi wetu tuliotoka familia za kawaida huwa hatujiamini sana tukiskia kuwa kuna mjumuiko na watu kama viongozi wa juu serikalini au watoto wao.

Nikapiga moyo konde na kuamua liwalo na liwe,naenda kwenye pati.Mimi niliwasili sehemu ya sherehe kabla ya Ridhwani kwa hiyo nilikuwa na fursa nzuri ya kumwelewa ni mtu wa namna gani pindi atakapowasili.Kwani kama isingekuwa kufanana kwake na JK ningeweza kumdhania kuwa huyu ndio mtoto wa Rais wetu?Alipoingia hapo kwenye sherehe alitusalimia wote kwa namna ileile ambavyo marafiki mtaani wanasalimiana,kwa heshima,taadhima na furaha tele bila hata chembe ya kuonyesha yeye ni mtoto wa mtawala na sie ni watu wa kawaida tu.Baadae nilipata fursa ya kuongea nae kwa kirefu kiasi na sikumficha jinsi “nilivyozimia” anavyoweza kutojionyesha kuwa yeye ni mtoto wa Rais (kwa taarifa yako,watoto wengi wa vigogo wanasumbua sana huku na hawapendi “kujichanganya” na watu wa kawaida,na hiyo sio kwa watoto wa vigogo wa Tanzania pekee bali hata wa sehemu nyingine duniani ikiwa ni pamoja na wale wa Ughaibuni).Yeye akaniambia kuwa amelelewa katika maisha ya kawaida,ya Kitanzania na ya Kiafrika halisi kwamba kutoka katika familia iliyo juu kabisa hakumfanyi ajione kuwa yuko tofauti na watu wengine.Na nisiseme kuwa labda ni mie pekee niliyepewa upendeleo huo wa kuwa karibu na “JK Junior” bali kila mtu aliyekuwepo pale.Na pia sio mimi pekee niliyependezwa na tabia ya mtoto wa Rais wetu bali kila niliyeongea nae alionekana kukunwa na hilo.Jamaa mmoja ambaye yuko chuo kimoja na Ridhwani alinambia kuwa inawezekana kabisa huyu bwana akawa (kwa kimombo) “the most down-to-earth son of a president in the entire world.” (yaani mtoto wa Rais aliye “wa kawaida” zaidi kulinganisha na watoto wa marais wengine duniani)..

Wengi wetu tunafahamu jinsi watu wanavyopenda wawe “wenye majina” ndio maana niliwahi kuambiwa kuwa kwenye baadhi ya kumbi za starehe huko nyumbani kuna baadhi ya watu wanatoa fedha kwa DJ au “rapa” wa bendi atangaze kwamba “flani tuko naye hapa” (lugha wanayotumia wenyewe ni kama “papaa nanihii yuko ndani ya nyumba”…kwa lafudhi ya Kikongo).Na pia niliwahi kudokezwa kwamba baadhi ya wanamuziki huzawadiwa ili wataje majina ya watu flani kwenye tungo zao.Na imewasaidia,kwa vile baadhi ya watu “wenye majina” tumewafahamu kupitia kwenye rapu za kina Ally Choki,Muumini au Banza Stone.Sasa ukikutana na mtu ambaye hahitaji hata kutajwa kwenye nyimbo ili jina lake lijulikane kwa vile tayari jina lake liko juu,halafu yeye anajiweka kuwa mtu wa kawaida kabisa,nadhani itakuwa ni dhambi kutomsifia.Na ndio maana makala yangu ya leo imemlenga Bwana Ridhwani Kikwete.Si tu kwamba tabia yake inamfanya apendeke bali pia inatusaidia wengine kuijua familia ya JK.Na kama nilivyosema hapo awali,familia ya kiongozi ni sehemu muhimu ya uongozi wake na inatoa taswira flani kwa wananchi wake.

Alamsiki

Tembelea http://chahali.blogspot.com na http://chahali.livejournal.com kwa makala za zilizopita.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.