21 Feb 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-50


Asalam aleykum,

Katika makala yangu iliyopita nilizungumzia ubabaishaji kwenye soka,na nilivinyooshea kidole vilabu vya Simba na Yanga.Nilishawahi kutamka huko nyuma kwamba mie nina mapenzi na wana-Msimbazi (naamini hilo halitonikosanisha na wapenzi wa safu hii ambao ni wana-Jangwani).Zamani hizo,Simba ikifungwa basi ilikuwa ni mithili ya msiba kwenye familia yetu.Kaka zangu walionitangulia wote ni Simba damu,kama ilivyo kwa wadogo zangu.Dada zangu hawana mpango na mambo ya futiboli.Baba sio mpenzi wa soka lakini aliamua kuisapoti Yanga ili kuleta usawa kwenye familia.Hoja yake ilikuwa kwamba haiwezekani familia nzima ielemee upande mmoja tu.Mama yangu alikuwa mpenzi wa Pan Afrika kwa vile mtoto wa kaka yake (binamu yangu) alikuwa nyota wa timu hiyo.Nadhani wafuatiliaji wa soka wanamkumbuka Gordian Mapango “Ticha”…huyo ndio alomfanya shangazi yake (mama yangu) aipende Pan Afrika.

Sikushtuka wala kuumia niliposikia Simba wametolewa na Wamsumbiji.Kimsingi,walikuwa wamejitengenezea maandalizi ya kutolewa mashindanoni hata kabla ya mechi hiyo.Tungetegemea nini wakati kwa wiki kadhaa tumekuwa tukisoma kwenye magazeti kuhusu mgogoro wa chinichini kati ya Mwenyekiti na Katibu Mkuu wa klabu hiyo.Sidhani kama Simba wametolewa kwa vile hawakuwa na uwezo wa kuwatoa Wamsumbiji hao bali mazingira yaliyotengenezwa na viongozi wao ndio chachu ya kichapo walichopewa.Pengine viongozi walileweshwa na ile sare ya ugenini na nakumbuka nilisoma sehemu flani ambapo kingozi mmoja wa timu hiyo alikuwa akijigamba kwamba ushindi ni lazima.Nilitamani kuamini maneno ya kiongozi huyo lakini nikakumbuka kuwa ni mtu huyohuyo ambaye hapo awali aliskika akidai kuwa kocha Mbrazil wa timu hiyo lazima angerejea japo kocha huyo alishatamka bayana kuwa hiyo ni ndoto ya mchana.Tatizo la soka la Bongo ni kwamba kiongozi anaweza kukurupuka usingizini na kutoa matamshi ya ajabuajabu bila hata kutafakari.Siiombei mabaya timu ambayo bado naipenda lakini sintashangaa nitakaposkia kwamba gogoro la nguvu linajichomoza hivi karibuni.

Nilibaki nacheka niliposoma kwamba kiongozi mmoja wa timu hiyo anaahidi kuwa nao wataleta kocha wa kigeni kama ilivyotokea kwa watani wao wa jadi.Kuleta kocha wa kigeni ni jambo zuri na si la kuchekesha,ila kilichoniacha kinywa wazi ni hoja zake kwamba eti “Yanga watatucheka na kututambia wakiwa na kocha mzungu wakati sie hatuna…”Kwa maana nyingine,haitakuwa maajabu iwapo watamkamata mtalii ambaye hajui hata kupiga mpira na kumfanya kocha alimradi ni mzungu!Hivi tuambiane ukweli,hayo mazingira yaliyopo Msimbazi yatamfaa kocha gani wa kigeni anayetaka kuona timu anayofundisha inafanya vizuri?Huyo “Micho” wa Yanga nae ni uvumilivu na kupenda kazi yake tu ndio vimemfanya hadi muda huu tunaoongea awe bado na wana-Jangwani.Kwanini nasema hivyo?Jibu ni kichekesho kingine nilichokisoma hivi majuzi kuwa kocha huyo alikuwa bado hana kibali cha kazi (sijui ameshakipata au la).Viongozi makini wataletaje kocha kabla ya kumtafutia kibali cha kazi.Ni kwa vile tu jamaa wa Idara ya Uhamiaji wametumia uungwana la sivyo “Micho” angekuwa ameshatimuliwa nchini kwa vile waajiri wake walimtangaza kuwa kocha wa timu hiyo kabla hawamtafutia kibali cha kazi.Huo ndio ubabaishaji wa viongozi wa soka wa Simba na Yanga.Ni wepesi wa kuitangaza habari zitakazowafanya waonekane wanawajibika lakini wanapuuzia kutengeneza mazingira mazuri ya kuzifanya habari hizo ziwe na maana ya kweli kwa wapenzi wa klabu hizo.Narudia kutoa ombi kuwa kuna haja ya msingi ya kuwabana watu wababaishaji kwenye uongozi wa vilabu vya soka na michezo mingineyo huko nyumbani.

Tukiachana na mjadala huo wa soka ngoja niangalie ishu nyingine ambayo naamini imevuta hisia za wengi.Hiyo si nyingine bali suala la mashoga ndani ya Kanisa la Anglikana wakati wa mkutano wa maaskofu wakuu wa kanisa hilo ambao unafanyika hapo Dar.Kwa kweli suala hili limeleta mgawanyiko mkubwa sana ndani ya kanisa hilo hususan huku Ulaya na huko Marekani.Kimsingi,suala la ushoga limekuwa ni mada moto sio kwenye masuala ya dini tu bali hata kwenye maeneo mengine.Kwa mfano,siku chache zilizopita kulizuka songombingo la nguvu hapa Uingereza kuhusu sheria inayolazimisha mashoga kupewa haki kadhaa kama wanazopata watu walio kwenye ndoa za asili,yaani kati ya mwanaume na mwanamke.Suala hilo lilifanikiwa kwa namna flani kuwaunganisha viongozi wa dini zote kuu,yaani Wakristo,Waislam na Wayahudi,ambao waliilaumu serikali ya Bwana Blair kwa kung’ang’ania kupitisha sheria hiyo ambayo wao waliiona kama kufuru flani na tishio kubwa kwa ustawi wa familia asilia.Hata hivyo,kwa vile wenyewe hapa wanadai kutetea haki za makundi yote ya jamii ikiwa ni pamoja na mashoga,sheria hiyo ilipitishwa na makali yake yanatarajiwa kuwaathiri zaidi watoa huduma mbalimbali ambao imani zao za kidini “haziivi” kabisa na mambo ya ushoga.

Yaani kwa mfano watu kama Michuzi na Fotopoint yake wakialikwa kwenda kupiga picha kwenye harusi ya mashoga kisha wakakataa kwa vile wanaona ushoga ni haram,basi kwa sheria za sasa za hapa watajikuta wakifunguliwa mashtaka ya ubaguzi.Na iwapo mwenye hoteli atakataa kuwapatia malazi “bibi na bwana” ambao ni mashoga basi nae atajikuta anatizamana na mkono mrefu wa sheria.

Kama ni kuitwa mbaguzi basi na bora iwe hivyo,lakini katika mila zetu za Kiafrika haya mambo ya u-Sodoma na Gomora hayana nafasi hata chembe.Nimesoma mahala flani kwenye mtandao kwamba kuna wanaharakati wa mambo ya mashoga wameweka kambi hapo Dar wakidai wanataka kulishinikiza Kanisa la Anglikana kukubali mabadiliko.Lakini katika habari hiyo,inadaiwa kuwa wanaharakati hao wana ajenda zaidi ya hiyo ya kidini.Inadaiwa kuwa wanataka kuanza kuhamasisha ushawishi wa kijamii na kisiasa ili mashoga wapatiwe haki zao sawa na watu wengine.Yaani kwa lugha nyepesi ni kwamba wanataka ushoga uhalalishwe katika sehemu mbalimbali za bara letu la Afrika ikiwa ni pamoja na hapo nyumbani.Kumbukumbu yangu zinaonyesha kuwa miongoni mwa mambo yalomfanya Mungu aiadhibu miji ya Sodoma na Gomora ni pamoja na hilo la tendo la ndoa kwa watu wenye jinsia moja.Hivi hawa mashoga hawawezi hata kujifunza kwa viumbe walionyimwa utashi wa kibinadamu kwa mfano kuku,mbwa,paka na wengineo ambao huwezi kukuta dume akifanya tendo la ndoa na dume mwingine.Yaani wanataka kutuaminisha kuwa wanyama na wadudu wana busara zaidi kuliko sie binadamu!Haki zao za binadamu waziache hukuhuku kwao lakini wasije kutuletea mabalaa huko nyumbani.Pindi itapobainika kwamba ni kweli kuwa wanaharakati hao wa mambo ya ushoga wanataka kuleta hamasa kwa vijana wetu basi dawa yao ni moja tu:kuwatandika bakora hadi waingie mitni bila kuaga.Sichochei watu kuchukua sheria mkononi lakini katika hilo acha tu waonjeshwe joto la jiwe la mila zetu za Kiafrika ili wabaini kuwa Afrika hakuna nafasi ya uanaharamu.

Mwisho, wiki hii watu wamesherehekea siku ya wapendanao.Najua wapo waliopeleka maua kwa wapenzi wao na wakatolewa baruti kwa hoja kwamba “badala ya kuleta maua ambayo hatuwezi kula kwanini usingenunua fungu la mchicha” na wapo wale ambao walikuwa na wakati mgumu wa kuchagua wapi pa kula Valentine:kwa mama watoto au kwa nyumba ndogo.Bila shaka katika mazingira hayo kulikuwa na safari nyingi za dharura za kwenda kwenye semina nje ya mji ili kuepusha kimbembe.Laiti ningekumbuka mapema kutoa salamu za Valentine basi walengwa wangu wangekuwa wale walio kwenye ndoa na mapenzi ya dhati bila kuwasahau wala rushwa ambao ningewaomba watumie siku hiyo kukumbuka kuwa tunahitaji upendo wao wa dhati.

Alamsiki


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.