21 Feb 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-51

Asalam aleykum wasomaji wapendwa wa safu hii.

Kwanza,kwa wale wanaofuatilia kwa karibu makala hii watagundua kuwa mambo mawili niliyaoyazungumzia katika makala zilizopita yametokea kama nilivyobashiri.Simaanishi kujisifia kuwa sasa nimekuwa mtabiri halisi bali nachofanya hapa ni kukumbushana tu.Nilielezea kuhusu uwezekano wa kuzuka mzozo ndani ya wana-Msimbazi na majuzi nimesoma kwenye gazeti moja taarifa kwamba baadhi ya wanachama wa klabu hiyo wamerejea mahakamani kuupinga uongozi wa klabu hiyo.Hizo si habari njema kwa wana-Simba kwa vile iwapo mahakama itaridhia kesi hiyo itamaanisha kurejea enzi za “mwaka 47” ambapo kundi moja linalishtaki kundi jingine ambalo nalo linalishtaki kundi jingine,alimradi vurugu mtindo mmoja.Kwa vile wanaofanya hivi ni watu wazima wenye akili zao,sanasana tunachoweza kuwaomba ni kutambua kuwa klabu hiyo sio mali yao.Kuwa kiongozi au mwanachama haimaanishi kumiliki klabu kama mali binafsi.

Kama hiyo haitoshi,nimesoma pia kuwa baadhi ya wachezaji wa klabu hiyo wamesusa kusajili kwa msimu ujao wa ligi kwa vile hawajapatiwa fedha za usajili.La kushangaza kwenye taarifa hiyo ni habari kwamba mmoja wa wafadhili wa timu hiyo alishatoa mamilioni ya shilingi kwa ajili ya kukamilisha zoezi hilo.Hapa naweza kumlumu mfadhili huyo japo natambua kuwa dhamira yake ilikuwa nzuri tu.Hivi mfadhili huyo haoni kuwa lingekuwa jambo la busara kukabidhi fedha hizo kwa wahusika (wachezaji) na sio kupitia kwa uongozi?Wakati mwingine kumwaga mamilioni kwenye hivi vilabu vyetu ni sawa kabisa na kumwaga petroli kwenye sehemu inayofuka moshi;ni dhahiri utalipuka moto mkubwa tu.Enewei,natumaini walofungua kesi na viongozi “watasomeshana” na hatimaye kuinusuru klabu hiyo isitumbukie kwenye balaa jingine la migogoro.

Jingine nililogusia huko nyuma ni taarifa kuwa vikundi vya wanaharakati wa ushoga wanataka kuchochea ushawishi wa kijamii kuhakikisha kuwa uanaharamu huo unapata nguvu huko nyumbani.Nimeona kwenye gazeti flani kuwa tayari wanaharakati hao wameshapata wawakilishi wa Kitanzania watakaosimamia miradi mbalimbali itakayoanzishwa na mashoga hao wa kimataifa.Hili linaweza kuonekana kuwa ni jambo dogo lakini kwa namna navyofahamu umakini wa wanaharakati hawa wa mambo ya ushoga sintoshangaa iwapo azma yako ikafanikiwa zaidi ya matarajio yao.Tatizo ni kwamba wameamua kutumia “uchawi wa mtu mweupe”,yaani fedha.Hebu angalia mfano huu:iwapo tuna Watanzania wenzetu ambao tunaishi nao huko mitaani,wengine ni ndugu na marafiki zetu,au pengine tunakutana nao makanisani na misikitini lakini linapokuja suala la fedha wanatusahau kabisa na kuendekeza matumbo yao.Kwa maana nyingine,watu hawa (wala rushwa na wabadhirifu) wanatelekeza ubinadamu kwa ajili ya fedha.Lakini wengi tunatambua pia kuwa hata kwenye Maandiko Matakatifu fedha ilisababisha Yuda amsaliti Yesu.Kwa mantiki hiyo,tusipokuwa makini tunaweza kukuta baadhi ya wenzetu wanaweka kando uanadamu wao na kuchangamkia mihela haramu ya mashoga hao na hatimaye kutumbukia kabisa kwenye u-Sodoma na Gomora.Kwa wale wenye tamaa ya bingo za harakaharaka wanapaswa kutambua kuwa fedha za mashoga hao sio sawa na utajiri wa kuokota bali zitakuja kumtokea mtu pauni.

Kuna habari moja ambayo imevuta hisia za vyombo vya habari mbalimbali vya kimataifa,nayo inamhusu Rais wa Gambia Yahya Jammeh ambaye anadai kuwa ana uwezo wa kutibu ukimwi.Tiba hiyo ambayo inaonekana kuwa kama mradi wa kitaifa inahusisha aya kadhaa za kidini na maji flani ambayo nadhani kwa lugha mwafaka yanaweza kuitwa “kombe”.Kinachowatia hofu wanaharakati wa ukimwi ni taarifa kwamba ili mwathirka apatiwe tiba hiyo sharti aache kutumia vidonge vya kupunguza makali ya virusi vya ugonjwa huo (ARVs).Na kama hiyo hazitoshi,mwezi uliopita Rais huyo aliwashangaza wanadiplomasia waliko nchini humo alipodai kuwa licha ya kuwa na uwezo wa kuponyesha ukimwi,pia anaweza kuponyesha ugonjwa pumu (asthma).Jambo jingine linaloleta mashaka kwenye madai ya Rais Jammeh ni usiri mkubwa unaotawala zoezi zima la utoaji wa tiba hiyo ambayo hata hivyo inatolewa bure,na miongoni mwa zahanati kuu za matibabu ni katika Ikulu ya nchi hiyo.

Kumekuwa na taarifa nyingi za tiba zisizo za kisayansi za ugonjwa huo unaoteketeza watu kwa kasi kubwa.Nyingi ya taarifa hizo zimekuwa zikitokea Afrika.Kwa bahati mbaya,nchi za Magaharibi zina ka-ugonjwa flani ka kutoamini habari njema kutoka Afrika.Walichozowea kusikia kutoka Afrika ni vita,njaa,ukame na mabalaa mengine kama vile Ebola na ukimwi.Kwa namna flani hali hii ya kutoamini kila chema kinachotokea Afrika imezifanya habari za tiba inayodaiwa kutolewa na Rais Jammeh zionekane kama kichekesho flani.Lakini wapo wanaojiuliza mtu mwenye mamlaka kubwa kama Rais wa nchi atakuwa anataka nini hadi afikie hatua ya “kuzusha” muujiza huo.Angekuwa mganga wa kienyeji wa kawaida tu basi watu wangesema huyo anataka kuwalia watu fedha zao kwa utapeli.Lakini kama nilivyoeleza hapo mwanzo,matibabu hayo yanatolewa bure na waliopatiwa matibabu hayo wanadai kuwa wamepona japo hakuna uthibithisho unaojitegemea.Vyovyote itakavyokuwa,ni mapema mno kutoa hitimisho lolote kuhusu madai ya Rais Jammeh.Ukweli kwamba tamko lolote la Rais huyo ni kama sheria inamaanisha kuwa hata kama taarifa hizo ni za uzushi basi hakuna namna ya kufahamu hilo mapema,japo kama hayati Bob Marley alivyowahi kusema “unaweza kuwadanganya watu wachache kwa muda flani,au kuwadanganya watu wengi kwa muda flani,lakini kamwe huwezi kuwadanganya watu wote milele.”Ni dhahiri kuwa ukweli utafahamika,na ukweli huo unaweza kumfanya Rais Jammeh kuwa mithili ya Nabii au unaweza kumfanya kuwa kichekesho cha karne.Tusubiri.

Kuna habari nyingine ambayo naona imekuwa ikiendelea kwa muda sasa huko nyumbani kuhusu suala la popobawa.Kiumbe huyu anadaiwa kuwa na mchezo mchafu wa kuwaingilia watu kimwili nyakati za usiku.Habari za popobawa zimekuwa zikisikika zaidi kutokea huko Tanzania Visiwani lakini safari hii inaelekea zimehamia Bara.Ugumu wa kuthibitisha habari hizi unatokana na ukweli kwamba suala la kuingiliwa kimwili pasipo ridhaa ni la aibu,sasa kwa mantiki hiyo ni vigumu kwa mtu kujitokeza hadharani kutoa ushahidi wa dhati kuwa kiumbe amemwingilia.Lakini hata kama itathibitika kuwa habari hizo ni za kweli,ugumu mwingine unakuja kwenye kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo.Naona suala hili limechukua sura mpya baada ya madiwani wawili huko wilayani Mkuranga kutoa maelezo yanayoashiria kuwa wao wanaamini habari hizo za popobawa ni za kweli.Inasemekana kuwa hivi majuzi mtoto mmoja wa kiume alikufa huko Yombo Dovya baada ya kuingiliwa na popobawa.

Nadhani namna pekee ya kuthibitisha madai ya namna hiyo ni kwa wanaodai kufanyiziwa na popobawa kufanyiwa vipimo ambavyo vinaweza kuthibitisha madai hayo.Hakuna haja ya kuona aibu kuongelea mambo kama haya kwa vile wengi wetu tunafahamu kuwa kabla ya ujio wa “dini za kisasa” mababu na mabibi zetu walikuwa waumini wa Dini ya Asili ya Afrika (African Traditional Religion) ambayo kimsingi hadi sasa bado ina waumini kadhaa miongoni mwetu (ingawaje kwa tafsiri ya haraka uumini kwenye dini hiyo unaweza kuhusishwa na ushirikina).Kwahiyo,kwa kuwa utamaduni wetu kwa namna flani unaruhusu matumizi ya “mafundi” (wataalamu wa mambo ya asili) katika kuondoa majanga yasiyoelezeka kisayansi basi halitokuwa wazo baya kuwashirikisha “mafundi” hao kwenye utatuzi wa tatizo hili iwapo litabainika kuwa sio uzushi kama ule wa “mtu aliyegeuka nyoka pale Buguruni.”
Alamsiki

2 comments:

  1. Mzee!Hii mara yangu ya kwanza kutinga hapa.Kijiweni kwako nimepapenda

    ReplyDelete
  2. Umepita muda hujatupa aya. Vipi?

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.