28 Mar 2007

Asalam aleykum,

Wiki hii kumefanyika maadhimisho ya miaka 200 ya kutokomezwa kwa biashara ya utumwa.Hafla maalumu zilifanyika sehemu mbalimbami hapa Uingereza pamoja na huko Jamaika na nchini Ghana.Kwa hakika,maadhimisho hayo yalikuwa yamegusa hisia za watu wengi hususan wale ambao wanajihesabu kuwa ni vizazi vya watumwa.Pia maadhimisho hayo yamezua mjadala ambao umedumu kwa muda mrefu kuhusu nini kifanywe na waliohusika katika biashara hiyo kwa namna moja au nyingine.Baadhi ya watu wamekuwa wakisisitiza kuwa licha ya nchi husika kuomba radhi kutokana na kuhusiaka kwao kwenye biashara hiyo isiyo ya kibinadamu,kunahitajika malipo kwa wahanga wa utumwa.Lakini swali ambalo limekuwa likiulizwa kila siku ni kuwa je malipo hayo yafanywe kwa nani na kama yakifanyika je kiasi gani kitakuwa sahihi kufidia uharamia huo.

Wapo wanaopinga suala la malipo kwa kigezo kwamba fedha haziwezi kutosha kufuta athari za biashara ya utumwa ambazo hadi leo bado zinaendelea hasa katika nchi za Magharibi.Miongoni mwa athari hizo ni suala la ubaguzi wa rangi ambao kwa hakika ni tatizo sugu sana katika nchi ambazo zilikuwa vinara wa biashara ya utumwa.Kwa mfano,kwa kiasi kikubwa jamii ya watu weusi hapa Uingereza na huko Marekani ni vizazi vya watumwa walioletwa kutoka Afrika kuja kujenga uchumi wa nchi hizo.Jamii hizi za weusi zimeendelea kuwa majeruhi wakubwa wa masuala ya ubaguzi wa rangi.

Pia suala lililoonekana kuzua mjadala wakati wa maadhimisho hayo ni namna umuhimu ulivyoelekezwa kwa wanasiasa wazungu waliohamasisha kukomeshwa kwa biashara hiyo huku jitihada za wasio wazungu (ambazo pengine ndio zilikuwa muhimu zaidi) zikisahaulika kwa makusudi.Kuna bwana mmoja Muingereza aliyekuwa akiitwa William Wilberforce.Huyo alijitahidi kulichachafya bunge la nchi yake kuhakikisha linapitisha sheria za kukomesha biashara ya utumwa.Katika maadhimisho hayo,Wilberforce ndiye aliyekuwa shujaa na kinara wa mapambano dhidi ya utumwa,suala ambalo limeonekana kama la kibaguzi miongoni mwa jamii za watu weusi hasa kwa vile mchango wa mashujaa kadhaa weusi (waliosimama kidete aidha wao pekee au kwa kushirkiana na wazungu wasiopenda utumwa kuhakikisha kuwa biashara hiyo inamalizwa ) unaonekana kupuuzwa kabisa.
Na kama vile kutia chumvi kwenye kidonda kibichi,baadhi ya wazungu wamekuwa wanadai kuwa si sahihi kuendelea kuwalaumu wao kwa makosa yaliyofanywa na mababu zao,na kwa mantiki hiyo hawaoni haja ya kuomba msamaha .Sambamba na “kiburi” hicho ni hoja kwamba biashara hiyo ya utumwa ilifanyika kwa ushirikiano kati ya wazungu na watawala wa Kiafrika.Hapa inakuwa kama hadithi ya nani kaanza kati ya kuku na yai.Je biashara hiyo ingekuwa kubwa namna hiyo kama wazungu wasingekuja kufuata watumwa Afrika?Au,je biashara hiyo ingekuwepo iwapo baadhi ya watawala wa Kiafrika kwa kushirkiana na wafanyabiashara wa Kiarabu wasingejihusiha na kuuza watumwa kwa wazungu?Yaani kimsingi ni kama biashara ya uchangudoa ilivyo:kama akina dadapoa hawatakuwepo maeneo kama Ohio na “vijiwe” vinginevyo wazinzi wataenda kufanya nini huko,na iwapo wazinzi hawatakwenda huko akina dadapoa watakwendaje kuumwa na mbu ilhali hakuna wateja.

Lakini maadhimisho hayo yamesaidia kwa namna flani kukumbusha kuwa licha ya ukweli kuwa biashara hiyo kukomeshwa bado utumwa unaendelea katika sehemu mbalimbali duniani japo pengine sio kwa kiwango kikubwa kama ilivyokuwa katika zama za “biashara ya pembe tatu” (Triangular Trade).Kumekuwa na taarifa mbalimbali zinazoonyesha kuwa aina flani ya utumwa inaendelea nchini Sudan japokuwa serikali ya nchi hiyo imekuwa ikikanusha kama inavyokanusha kuwepo kwa mauaji ya halaiki huko Darfur.

Pia kuna utumwa unaoendelea katika nchi mbalimbali za Magharibi ambapo akinadada wenye ndoto za maisha bora hujikuta wakirubuniwa kuondoka kwenye nchi zao kukimbia umasikini na hatimaye kujikuta wakiishia mikononi wa magenge yanayomiliki biashara ya ukahaba wa kimataifa.Wahanga wakubwa wa biashara hii ni akinadada kutoka nchi za Ulaya ya Mashariki ambao mara nyingi huahidiwa kupatiwa kazi bora pindi watapoletwa Ulaya Magharibi lakini wafikapo wanapokwenda hunyang’anywa pasi zao za kusafiria na kulazimishwa kulala na wanaume kadhaa kwa siku na wakati huohuo kutakiwa kulipia huduma za malazi,chakula na nyinginezo wanazopatiwa na hao wanaowatumikisha.Wanapoonyesha nia ya kukataa, “wamiliki” wao hitishia kuwaripoti kwenye mamlaka za uhamiaji kwa vile kwa wakati huo akinadada hao huwa wanaishi kama wahamiaji haramu kwa kuwa hati zao za kusafiria ziko mikononi mwa wamiliki hao.

Pengine baadhi yenu wasomaji wapendwa ambao hamkereki mnaposikia muziki wa kufokafoka (rap) mtakuwa mmeshasikia kibao cha mwanamuziki wa Kimarekani,50 Cent kinachoitwa P.I.M.P (ambacho amemshirkisha “mfokaji” mwingine Snoop Dogg). “Pimp” ni mtu anayekuwadia wanawake kupata mabwana,na japo kwa namna flani mahusianao kati ya “Pimp” na wanawake husika huwa kama ya ridhaa,bado yana dalili za utumwa wa namna flani.Ma-Pimp ni maarufu zaidi huko Marekani hususan miongoni mwa jamii ya watu weusi na inasemekana akinadada wanaojihusisha na ma-Pimp huwa kama wametekwa akili kwa namna wanavyowategemea “makuwadi” hao kwa kila kitu,hali ambayo inawafanya waendelee kutumikishwa huku ma-Pimp wakipendelea kutengeneza faida.

Ripota wa televisheni ya Sky News Emma Herd alipokuwa akiripoti kutoka mjini Accra,Ghana kuhusu maadhimisho ya kutokomezwa biashara ya utumwa alionyesha kushangazwa na namna ambavyo maadhimisho hayo yaliwavutia zaidi watalii kutoka nchi za Magharibi (hasa Wamarekani Weusi) ilhali Waghana wenyewe “wakiwa hawana mpango” na shughuli hiyo.Lakini baadaye alikiri kuwa wenyeweji hapo wana mambo lukuki ya “kudili” nayo kila kukicha badala ya kupoteza muda wao kuadhimisha siku moja ambayo kwao haileti tofauti yoyote katika maisha yao.Na hilo lina ukweli kwa sababu wengi wetu tunafahamu kuwa katika jamii zetu za Kiafrika bado tunakabiliwa na aina flani za utumwa ambazo kwa kiwango kikubwa tunaziona kama sehemu ya maisha yetu ya kila siku.Mfano mwepesi ni namna baadhi ya watumishi wa ndani (housegirls) wanavyotumikishwa kama watumwa kwenye makazi mbalimbali huko mitaani.Licha ya ahadi luluki wanazopewa wakati wanatolewa vijijini, baadhi ya mahauzigeli hao huishia kuwa “watumwa wa kisasa” ambao hupatiwa malazi duni,ujira mdogo,hunyimwa mawasiliano na ndugu zao na wengine hawaruhusiwi hata kwenda nje bila ruhusa ya “wamiliki wao.”

Kundi jingine linalofanyishwa kazi karibu kabisa na namna ya utumwa ulivyokuwa ni “mabaamedi.”Pasipo kuwadhalilisha,yayumkinika kusema wengi wa dada zetu hawa wanatumikishwa kwa namna mmiliki wa baa anavyotaka ilhali mshahara wanaopewa ni mdogo sana kiasi kwamba “wasopochangamkia wateja” wanaweza kujikuta wanapoteza muda wao kufanya kazi hapo baa.Hili ni kundi ambalo limesahaulika kabisa kwenye sheria za kazi.Tafiti zangu zisizo rasmi wakati nikiwa huko nyumbani zilionyesha kuwa tofauti na hisia kwamba akinadada hao hupenda “kuondoka na wateja wao” kwa hiari baada ya kumaliza kazi,ukweli ni kwamba wengi wao hulazimika kufanya hivyo ili angalau kupata nauli ya kurudi nyumbani na kujia kazini siku inyofuata au kujiongezea kipato kwenye mishahara kiduchu wanayolipwa na wenye baa,mishahara ambayo haitoshi kulipia kodi za nyumba wanazoishi,haitoshi kwenye nauli ya kwenda na kurudi kazini,na haitoshi kwa vile mara nyingi huwa inakatwa kutokana na “demeji” ya chupa au glasi.

Wakati Waingereza na wapenda ubinadamu wengine wanaadhimisha miaka 200 ya kutokomezwa biashara ya utumwa,ni jukumu la jamii yetu yote inayothamini ubinadamu kufanya kila siku iwe ya mapambano dhidi ya uonevu,unyanyasaji,utumikishwaji na utumwa.Hebu tuungane kuwafanya mahauzigeli,mabaamedi,“mateka wa ma-Pimp” na wale walio katika “ndoa za kijeshi” wawe huru kama ambavyo mie na wewe tunavyopenda kuwa huru.

Alamsiki

1 comment:

  1. Evarist!
    Nashukuru kuifahamu nyumba yako. Nitakutemblea mara kwa mara. Vp lkn UK!

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.