29 Apr 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-58

Asalam aleykum,

Kuna habari moja niliyoiona kwenye runinga hivi karibuni kuhusu falsafa ya ushindani huko nchini China imenivutia sana kiasi najiskia “kushea” nawe msomaji mpendwa.Stori hiyo ilikuwa inazungumzia kuhusu binti mmoja wa miaka minane ambaye huamshwa na baba yake kila siku saa 9 alfajiri kwa ajili ya mazoezi ya mbio za marathon.Mazoezi hayo hudumu kwa zaidi ya masaa mawili na sio suala la hiari bali ni sehemu ya maisha ya binti huyo na familia yake.Anapoulizwa kuwa haoni kwamba “kwa kumpelekesha puta” binti yake namna hiyo ni kama anamwadhibu,baba yake anamnukuu Adolf Hitler kwenye usemi wake kwamba “askari asiyepania kuwa jenerali hastaili kuwa jeshini” akimaanisha kwamba ni muhimu kwa mwanadamu kupania mafanikio ya juu kabisa kama anataka kufanikiwa katika maisha.Mzazi huyo anaamini kuwa baadaye bintiye atavuna anachopanda hivi sasa hasa kwa vile “kufukuza upepo” (riadha) ni mchezo wenye maslahi makubwa sana.Na inahitaji maandalizi ya mapema kweli ili uweze kuibuka kijogoo kwenye fani yoyote ile katika nchi kama China ambayo ina watu zaidi ya bilioni moja.

Wazazi mnaosoma makala hii,mnaonaje na nyie mkaanzisha utaratibu wa kuwachukua vijana wenu kwenda sehemu ambazo zitawaandalia “future” bora maishani mwao.Kwa wewe mzazi Mwislam unayeamka alfajiri kwa ajili ya swalat alfajir,unaonaje kama utaambatana na mwanao ili kumjengea msingi bora wa kiroho?Nimetolea mfano wa swala ya alfajiri ili kuendana na stori hiyo hapo juu lakini si lazima iwe muda huo tu,bali hata alasir,adhuhur,magharib au isha.Haihitaji kuwa na PhD ya dini ili kufahamu kuwa mara nyingi familia inayothamini ibada huwa familia bora,imara ,yenye mwelekeo na isiyoyumbishwa na vitu visvyo na msingi hasa vile vya kishetani.Unadhani familia yenye kuendekeza ibada inaweza kuzaa mla rushwa?No way.Wala rushwa ni watu waliopotoka kimaadili,ni wezi wanaovunja amri za Mungu,na ibada siku zote inasisitiza kumheshimu Mungu na kutekeleza yale anayotaka,ambayo siku zote ni mambo mema.

Wazazi Wakristo ndio hawapaswi kuwa na kisingizio hata kidogo kwa vile idadi ya sala kwa siku huko kanisani (ukitoa Jumapili) ni chache kulinganisha na wenzao Waislam.Kwa Wakatoliki,sala ya asubuhi katika siku za juma ni moja tu,na laiti mzazi mwenye dhamira ukiamua,basi inawezekana kabisa kwamba kila asubuhi wakati unaelekea kibaruani na mwanao anaelekea mkaambatana kwenda “kupata neno” kanisani kabla hamjaendelea na ratiba zenu.Amin nakuambia,siku inayoanza kwa sala inakuwa siku ya amani,na mwanao atakwenda shule akiwa na wazo moja tu la “kitabu” na sio sketi za wanafunzi wa kike,na wewe mzazi utawajibika kibaruani kwa namna ya kumpendeza Mungu wako,na utapomaliza job jioni njia ya kwenda nyumbani itakuwa pana zaidi ya ile nyembamba inayoelekea baa au nyumba ndogo.


Baada ya hayo,sasa naelekeza macho yangu kwenye muziki.Lakini kabla sijaingia kwa undani kwenye mjadala wangu,ngoja nikudokezee utata huu unaendelea huko Marekani na baadhi ya nchi nyingine za magharibi.Ni hivi,ni kosa linaloweza kumpeleka jela mtu mweupe pindi akimwita mtu Mweusi “nigger.” Ni neno ambalo ni zaidi ya mwiko na pindi likitumiwa kwenye vyomba vya habari basi hutajwa kama “neno lenye N” (the N-word).Kichekesho ni kwamba neno hilo ni la kawaida sana miongoni mwa watu weusi.Kulirembesha na kuwa “nigga” badala ya “nigger” hakubadilishi lolote zaidi ya kuongeza utata.

Sio siri kuwa muziki wa kufokafoka (rap) umekuwa na mwonekano (image) mbaya sana zaidi miongoni mwa jamii ya watu weupe na hata kwa watu weusi.Marapa weusi wamekuwa wakishutumiwa sana kwa kile kinachoonekana kama kuchochea matumizi ya silaha,utumiaji wa mihadarati na kibaya zaidi ni dharau yao kwa jinsia ya kike,ambapo kwa wengi wao kila mwanamke kwao ni “biach”, “hoo”,n.k (malaya) utadhani wao walizaliwa kwenye testi tyubu.Wanaelimishaji miongoni mwa jamii ya watu weusi wamekuwa wakitoa kilio chao dhidi ya udhalilishaji wa namna hiyo,na kukemea matumizi ya neno “nigga” lakini marapa hao hawana muda wa kusikia.Baadhi ya watu weupe wanalalamika kwamba iweje wako wakimwita mtu Mweusi “nigger” inakuwa kosa la ubaguzi wa rangi lakini wenyewe kwa wenyewe wanaitana hivyo.Hoja yao ni kwamba kama neno hilo ni sawa na tusi basi iwe hivyo kwa watu wote pasipo kuangalia rangi ya mtu.

Kwa muziki wetu wa nyumbani,mie bado nataabika na mwonekano “image” wa baadhi ya wasanii wetu.Najua hapa nitatofautiana kimawazo na baadhi ya watu,lakini tutafika.Hivi unapata picha gani unapokuta kundi zima la kikundi cha bongofleva likiwa na watu waliosokota minywele yao katika kile wenyewe wanakiita rasta huku wamevaa miflana yenye picha za majani ya bangi!Na hapa ntakuwa muwazi zaidi.Mvumo wa bongofleva ulijiri wakati mie nimeshaondoka huko nyumbani.Nilipoona mtandaoni kuwa muziki wa kizazi kipya umefunika mipasho na “bakulutu” nilidhani ni stori tu.Lakini nilipokuja huko home mwaka jana nikajionea mwenyewe namna gani bongofleva ilivyofanikiwa kuteka hisia za wapenda muziki.Kundi moja ambalo nililikubali mara moja ni TMK Wanaume (kabla halijameguka).Lakini tatizo la msingi nililokuwa nalo dhidi yao ni hiyo taswira waliyokuwa wanajitahidi kuitengeneza na kuindekeza:taswira ya “jah people”,taswira ya “marastafari”,kwa lugha ya wazi taswira ya wavuta bangi.

Jana nimeona kwenye blogu ya Michuzi picha ya basi la ziara ya Juma Nature na kundi lake huko Mwanza,na ndani ya basi hilo kuna kijipicha chenye jani la bangi.Hivi hawa watu wanataka kutuambia nini kuhusu taswira hiyo ya “widi” wanayoonekana kuitukuza sana?Hivi huwezi kuwa supastaa mpaka uwe na mwonekano wa ajabuajabu?Mbona Mista Two amedumu miaka nenda miaka rudi huku “pesonaliti yake ni ya kishua” (yaani anaonekana zaidi kama meneja flani kuliko rapa).Solo Thang,Prof Jay,Banana,Mike Tee,Mr Paul na wengineo,ni mwiongoni watu ambao wamekuwepo “kwenye gemu” kwa kitambo sasa lakini hawajajichafulia mwonekano wao katika namna ya kuabudia “majani.”

Mie sio mpinzani wa mtindo wa rasta,wala sina chuki na imani ya urastafari.Lakini mtu yeyote mwenye busara atafikiria mara mbilimbili kabla ya kujitundika mtindo ambao kwa namna moja au nyingine unaweza kumfanya aonekane “mvuta bangi flani.”Nafahamu kuwa cha muhimu zaidi sio mtindo wa nywele bali “fleva na meseji” lakini nani asiyejua kuwa meseji inayotolewa na mlevi inaweza kupoteza fleva yake kwa vile tu mtoaji ni mlevi!Hiyo mibangi mnayoendekeza na kuiwekea lebo kila mahali itawapeleka pabaya.

Mibangi hiyo ndio inayofanya matamasha yenu yawe ya kuvutia kwa vile changamoto hapo huwa ni “stimu za widi” lakini likija suala la kutengeneza video za kueleweka,unamkuta msanii anaionea aibu kamera,kisa hajashtua hisia zake.Sio siri kuwa kwa namna flani hatma ya baadhi ya mastaa wa bongofleva iko mikononi mwa hayo majani wanayoyaendekeza.Nasema hivyo kwa sababu bangi sio kitu chema,na ukichanganya na mikanganyiko ya kawaida katika maisha ya kila siku,basi si ajabu baadhi ya mastaa hao wakajikuta “wanatema vesi” wakiwa Mirembe.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.