3 Nov 2008


Kizitto Noya, Kilwa Masoko
WAKATI baadhi ya watu wakiamini kuwa serikali ilitumia busara kuhakikisha fedha zilizochotwa kwenye Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), zinarejeshwa kabla ya wezi kufikishwa mahakamani, katibu mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad haamini kama fedha hizo zimerejeshwa.

Na badala yake waziri huyo kiongozi wa zamani wa Zanzibar anasema madai ya kurejeshwa kwa Sh69 bilioni kati ya Sh133 ni mwendelezo wa usanii wa chama na serikali yake.

Maalim Seif alisema hayo mwishoni wa wiki alipokuwa akihutubia maelfu ya wakazi wa Mkoa wa Lindi kwenye Uwanja wa Kilwa Masoko, baada ya kupokea maandamano ya CUF ya kupinga ufisadi na kushinikiza wezi hao wa fedha za EPA wafikishwe mahakamani.

Alisema hawezi kuamini kwamba mafisadi hao wamerudisha fedha mpaka aone kwamba wamefikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili za kuiba Sh133bilioni.

"Mimi naamini kwamba, hakuna hata mtuhumiwa mmoja wa ufisadi wa EPA aliyerudisha fedha na kauli ya Rais (Jakaya) Kikwete ni mwendelezo wa usanii wa serikali ya CCM kuwalaghai Watanzania ili waamini kuwa kazi imefanyika," alisema.

Alisema yeye kama Watanzania wengine wenye akili timamu, hataamini kwamba kuna fedha iliyorudishwa na mafisadi wa EPA na kwamba atafanya hivyo ikiwa ataona mafisadi hao wanafunguliwa kesi mahakamani.

Kauli ya Maalim Seif ilifuatia maswali ya waandamanaji hao kumtaka aeleze msimamo wa CUF kuhusu ufisadi wa EPA na mazungumzo ya mwafaka baina ya chama chake na CCM.

Alisema CUF hairidhishwi na namna serikali inavyoshughulikia suala la EPA na ndio maana viongozi wake wakuu wanazunguka nchi nzima kufanya maandamano ya amani kupinga ufisadi huo na kuishinikiza serikali iwafikishe mahakamani.

Rais Kikwete alitaka wezi hao warejeshe fedha kabla ya Oktoba 31 na kwamba wale ambao watashindwa kuzirejesha, wafikishwe mahakamani ifikapo Novemba mosi.

Katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi aliyoitoa Oktoba 31, Rais Kikwete alisema jumla ya Sh69 bilioni zimesharejeshwa na kwamba, ametoa ruhusa kwa watuhumiwa kufikishwa mahakamani.

Hata hivyo, hadi jana Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), alikuwa bado hajawasimamisha watuhumiwa hao mahakamani.

Kuhusu mwafaka, Maalim Seif alisema CCM ilianza kutumia nguvu ya ulaghai katika suala hilo kwa kujifanya inataka kumaliza mgogoro wa mpasuko wa Zanzibar wakati ikijua kuwa haina nia hiyo.

Alisema: "CUF tumegundua ulaghai huo na sasa tumewaambia kwamba haturudi tena kwenye mikutano ya mwafaka. Tunataka kama wana nia njema na mwafaka, wasaini makubaliano yaliyofikiwa," alisema.

Alisema CUF pia imefunga mjadala na vikao vya mwafaka baina yake na CCM baada ya kuona kuwa wenzao wa CCM wanawarubuni na kuwahadaa.

Kuhusu nguvu ya utajiri wa kifisadi, Maalim Seif alisema CCM inatumia fedha nyingi kuwarubuni wananchi kwa zawadi ili waendelee kuiamini na kuwachagua, fedha ambazo baadaye wanazirudisha kwa wizi wa mali za umma na ufisadi.

"Pia CCM wanatumia ya nguvu dola kuwatisha wananchi na kuwapiga wananchi ili wasiwe huru kuwachagua vingozi wanaowapenda," alisema.

CHANZO: Mwananchi

PENGINE HOFU YA AINA HII INATOKANA NA UKWELI KWAMBA HAO WANAODAIWA KUREJESHA MABILIONI HAYO WAMEENDELEA KUWA ANONYMOUS.IWAPO MAJORITY YA WATOA SADAKA MAKANISANI NA ZAKA MISIKITINI (SUALA AMBALO NI LA HIARI NA SI LA KISHERIA HUJIWEKA WAZI) HOW COME THEN WADAIWA (SUALA LA KISHERIA) WAHIFADHIWE?NI SIMPLE LOGIC:KAMA MDAIWA NI ANONYMOUS,ITAPOELEZWA KUWA AMELIPA DENI NA KUENDELEA KUBAKIA ANYNYMOUS BASI LAZIMA KUTAKUWA NA STRONG SUSPICION KAMA DENI HILO LIMELIPWA KWELI.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.