22 Mar 2009


Na Khamis Mkotya

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA), imesema orodha ya majina ya watumishi wasio waaminifu kwenye kitengo cha kudhibiti mapato bandarini (TISCAN), bado haijawasilishwa Makao Makuu kama ilivyoahidiwa na Rais Jakaya Kikwete. Akizungumza Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Elimu kwa Walipa Kodi, Protus Mmanda, alisema Menejimenti ya TRA chini ya Kamishna Mkuu, Hary Kitillya, inayasubiri majini hayo kuweza kuchukua hatua stahili.

Mmanda alisema, watumishi wote wa TRA watakaotajwa kwenye orodha hiyo watashughulikiwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zote za nidhamu, ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi kama Rais alivyoagiza. Machi 2, mwaka huu, Rais Kikwete alifanya ziara ya ghafla bandarini kukagua utekelezaji wa maagizo yake kuhusu ufanisi katika utendaji kazi wa bandari ya Dar es Salaam, hasa kuhusu mrundikano wa makontena. Katika ziara hiyo, Rais alionyesha kukerwa na baadhi ya watumishi wa TISCAN ambao wamekuwa wakishirikiana na wafanyabiashara wakubwa kuwaonyesha mbinu za kukwepa kodi, vitendo vinavyolisababishia taifa hasara. Rais Kikwete alisema, orodha ya watumishi wanaoendekeza mchezo huo mchafu anayo na kumtaka Kamishna Mkuu wa TRA, kuwafukuza kazi watumishi hao atakapokabidhiwa majina.

Orodha ya majina hayo bado haijafika kwetu, tunaendelea kusubiri sijui yatakuja lini, maana mimi kwa wadhifa wangu siwezi kwenda Ikulu kuuliza majina hayo yataletwa lini. “Labda kwa kuwa nyinyi waandishi wa habari mnakutana na Salva Rweyemamu, (Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu) muulizeni hayo majini yatakuja lini, lakini sisi huku hatuwezi kuuliza, hadi hapo yatakapoletwa,” alisema. Mmanda alisema kuwa, wakati majina hayo yanasubiriwa, TRA imechukua hatua kadhaa zinazolenga kuweka mfumo mzuri wa utendaji, ikiwa ni pamoja na kufanya mabadiliko kwa baadhi ya maofisa wake.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo, TRA imeshafanya mabadiliko kwa kuwahamisha idara baadhi ya maofisa wake, wanaoonekana kuwa na chembe za ukosefu wa maadili kama hatua za awali za kutekeleza maagizo ya Rais. “Hatuwezi kukaa tu bila kufanya tathimini yoyote juu ya utendaji kazi wetu, kwa sababu tunasubiri majina kutoka kwa Rais. Baadhi ya hatua tulizochukua ni pamoja na kufanya mabadiliko katika baadhi ya idara zetu. “Tumefanya marekebisho pale palipostahili, mahala palipokuwa na watumishi wazembe wasiokuwa waadilifu tumewaondoa na kuweka watumishi wengine,” alisema Mmanda, ingawa hakutaja idara na maofisa wake walioguswa na zoezi hilo.

Mkurugenzi huyo alisema, hatua nyingine zilizochukuliwa ni pamoja na kurahisisha taratibu za usajili wa magari, kuondoa kero ya muda mrefu ambayo imekuwa ikilalamikiwa kuhusu uchelewashaji wa usajili wa magari. Kwa mujibu wa Mmanda, taratibu zote za usajili wa magari yanayoingizwa nchini hivi sasa zitafanywa na ofisi moja, ili kuondoa usumbufu kwa watu, tofauti na zamani ambako taratibu hizo zilikuwa zikishughulikiwa na ofisi zaidi ya moja. Alisema kuwa, utaratibu huo mpya pia utasaidia kuondokana na watu wa ‘kijiweni’ maarufu kwa jina la ‘vishoka’, ambao wamekuwa wakiwatapeli watu kwa kisingizio cha kuwasaidia katika taratibu za usajili wa magari.

CHANZO: Mtanzania

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.