11 May 2009


AH,HAPA SIJUI NISEMEJE.HEBU SOMA KWANZA HABARI KAMILI HAPA CHINI KISHA TUJADILI.

Kompyuta za IGP, Mkemia Mkuu zaibwa
• Ni katika mazingira ya kutatanisha

na Deogratius Temba

WAKATI kesi ya watuhumiwa 11, walioiba kompyuta katika ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), ikiendelea imebainika Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP), Said Mwema, naye ameibiwa kompyuta ndogo (Laptop).

Wiki mbili baada ya tukio la wizi wa kompyuta za IGP Mwema, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, nayo iliibiwa kompyuta ya mezani ambayo inasadikika ilikuwa na kumbukumbu nyingi ambazo hazijabainishwa zinahusiana na mambo gani.

Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima Jumapili, kwa wiki kadhaa sasa umebaini kuwa kumekuwapo kwa wasiwasi mkubwa wa kuibwa kwa nyaraka na vifaa mbalimbali katika ofisi za viongozi wakubwa wa serikali akiwemo Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Mwanasheria Mkuu wa serikali (AG).

Chanzo kimoja kimelidokeza Tanzania Daima Jumapili, uchunguzi wa wizi wa kompyuta hizo mpaka sasa unaendelea ili kuwabaini wahalifu waliotenda tukio hilo na kujua walikuwa na lengo gani.

Chanzo hicho kimebainisha kuwa kikosi maalum kimeundwa kufuatilia wizi huo ambao umeonekana kuanza kushamiri katika ofisi nyeti za serikali hasa katika kipindi hiki ambacho kumekuwa na tuhuma nyingi za ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka yanayofanywa na viongozi.

Taarifa za ndani zinadai kuwa kompyuta ya IGP iliibwa mezani kwake majira ya mchana siku ya Ijumaa wakati mkuu huyo akiwa amekwenda msikitini kuswali. Katika meza hiyo kulikuwapo na simu za mkononi na kiasi cha fedha kinachodaiwa kuwa sh milioni saba, lakini ni kompyuta pekee ndiyo iliyoibwa.

Habari zaidi zinabainisha kuwa IGP aliporudi alishangaa kutoikuta kompyuta hiyo ilhali simu na fedha vilikuwapo kama alivyoviacha, baada ya kubaini wizi huo zilichukuliwa alama maalumu za vidole zikaonekana ni za mlinzi wake wa karibu (Board guard), ambaye inadaiwa huwa na kawaida ya kuingia mara kwa mara katika ofisi pasi na kutiliwa shaka.

Chanzo chetu cha habari kilieleza kuwa uchunguzi ulipofanyika ndani ya jeshi la polisi ilibainika kuwa kuna afisa wa jeshi hilo, mwenye cheo cha mkaguzi, ndiye aliyeichukua kompyuta hiyo, ambaye hadi sasa anahojiwa ili kulisaidia jeshi hilo liweze kupata chanzo cha uhalifu huo.

Aidha, taarifa zinasema kuwa aliyeichukua kompyuta hiyo, inadaiwa, amelipwa sh mil. 10 kama ujira wake kwa kazi hiyo. Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini (DCI), Robert Manumba, alipoulizwa juu ya hatua ambazo jeshi hilo linazichukua dhidi ya wizi huo ambao unaonekana wazi kulenga kuiba nyaraka muhimu za serikali, alisema huo ni wizi kama mwingine kwani wezi hao hawakulenga kuiba kompyuta hizo kwa lengo maalumu.

“ Siyo kwamba wizi haufanyiki, unafanyika sana; mara hii umetokea katika ofisi nyeti inayomhusisha mkuu wa jeshi la polisi, wizi huo umefanyika tu kama unavyoweza kufanyika nyumbani kwako, haukulenga ofisi hizi tu,” alisema DCI Manumba.

Pamoja na kusema hivyo, alilithibitishia Tanzania Daima Jumapili kuwa hatua za uchunguzi zinaendelea ili kuwabaini wahalifu hao ambao wamefikia hatua mbaya.

“Tanzania hatuna wizi wa kulenga ofisi maalumu za serikali, ndiyo maana unapotokea unawashangaza watu wengi lakini tumejipanga vilivyo katika uchunguzi kuhakikisha tunawakamata wale wote waliohusika,” alisema Manumba na kuongeza:

“Nakwambia ukweli, wewe umekuja kuniuliza kwa sababu wizi umetokea katika ofisi hii, lakini matukio kama haya yanatokea pia katika nyumba za watu binafsi, hata siwezi kukuhesabia idadi ya kesi hizo, tusiwashtue watu waamini kuwa ulilengwa kwa kazi hiyo.”

Manumba alizidi kusisitiza kuwa wizi upo dunia nzima na wanaweza kuiba mahali popote kama wataona kuna kitu, lakini hakuna wizi uliopangwa kulenga katika ofisi hizo za IGP, DPP , au kwa Mkemia Mkuu wa Serikali.

Taarifa zimeeleza kuwa kompyuta iliyoibwa katika Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali ilikuwa kubwa ya mezani (PC), ambayo ilichukuliwa kupitia dirishani katika mazingira ya kutatanisha wakati milango ikiwa imefungwa.

Chanzo chetu kutoka ndani ya ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, kimeeleza kuwa kompyuta hiyo ilikuwa ikitumika ndani ya ofisi ya Mkemia Mkuu, ambapo bado haijajulikana na nyaraka gani muhimu zilikuwa zimehifadhiwa humo.

“Ni kweli kompyuta iliibwa hapa, milango imefungwa tumefika tukaelezwa kuwa kompyuta ya msaidizi wa bosi wetu haionekani wakati milango ilikuwa imefungwa,” alisema mmoja wa watumishi wa ofisi hiyo ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini.

Aidha kuhusu tukio hilo lililotokea katika ofisi hizo zilizoko karibu na Taasisi ya Saratani, Ocean Road, imeelezwa kuwa bado uchunguzi unaendelea ili kubaini mtu aliyehusika kuiba kompyuta hiyo kama ni mmoja wa wafanyakazi au la.

Kutokea kwa wizi huo kunawafanya baadhi ya watu kuwa na wasiwasi kuwa kuna njama zimepangwa na baadhi ya watu kupoteza vielelezo au ushahidi wa tuhuma au kesi mbalimbali zinazowakabili.

Wasiwasi huo umechangiwa zaidi na matukio ya hivi karibuni ya kupandishwa mahakamani kwa baadhi ya vigogo wa serikali, wafanyabiashara na watu binafsi kwa wizi au matumizi mabaya ya madaraka.

Mpaka sasa watu 11 wameshapandishwa katika Mahakama ya Kisutu jijini Dar es salaam kujibu tuhuma za kuiba kompyuta katika ofisi ya Mkurugeni wa Mashtaka Nchini (DPP).

JANA NILIWEKA HABARI YA KIBAKA ALIYEFANIKIWA KUIBA UA IKULU.JUZIJUZI,USTAADH MMOJA ALIDIRIKI KUMZABA KIBAO RAIS MSTAAFU ALI HASSAN MWINYI.SIKU KADHAA ZILIZOPITA,TULISIKIA KUWA DPP AMEIBIWA LAPTOP YAKE.LEO TENA TUNASIKIA IGP NAE KALAMBWA KOMPYUTA.MATUKIO YOTE HAYA YANAASHIRIA KWAMBA TUNARUKARUKA KWENYE UTANDO WA BUIBUI ILHALI CHINI YA UTANDO HUO KUNA BWAWA LA TINDIKALI.

SWALI LA MSINGI KUJIULIZA KUHUSIANA NA WIZI HUO WA LAPTOP YA IGP NI KWANINI HABARI HIYO IMEVUJA KIRAHISI HIVYO?NI HABARI YA FEDHEHA AMBAYO KWA MAZOWEA TULIYONAYO YA "WAKUBWA HUWA HAWAKOSEI" INGEDHIBITIWA KWA NGUVU ZOTE.NIITE CONSPIRANCY THEORIST,LAKINI I STRONGLY SMELL SOMETHING FISHY.IT'S EITHER KUNA MTU (HUYO ANAYEDAIWA KULIPA MILIONI 10 BAADA YA KUFANIKIWA "WIZI" HUO) ANAYETAFUTWA ILI AWE IMPLICATED AU KUNA EVIDENCE INAPOTEZWA KWA EXCUSE YA "ILIKUWA NDANI YA LAPTOP ILIYOIBIWA."KATIKA ZAMA HIZI ZA UFISADI,LOLOTE KATI YA HIZO CONSPIRANCY THEORIES ZANGU INAWEZA KUWA SAHIHI.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.