Showing posts with label UFISADI. Show all posts
Showing posts with label UFISADI. Show all posts

14 Apr 2019

[Uchambuzi wa ACT Wazalendo Kuhusu Maeneo Kumi (10) Muhimu Kwenye Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Mwaka wa Fedha wa 2017/18].

- Ikulu Yatumika Kuficha Ukaguzi wa Manunuzi ya Ndege

- Bilioni 800 Hazikutolewa kwa Ukaguzi
- Trilioni 4.8 Zimetumika Bila Kupita Mfuko Mkuu wa Hazina
- Mikopo ya Ndani Yashindwa Kulipa Madeni Kikamilifu
- 40% ya Bajeti yategemea Mikopo na Misaada Kutoka Nje



Ndugu Wanahabari



A: Utangulizi 



Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Prof. Mussa Juma Assad ametoa taarifa yake ya Ukaguzi wa Mapato na Matumizi ya Fedha za Umma kwa mwaka wa fedha wa 2017/18. Licha ya changamoto mbalimbali zilizotokea kabla ya CAG kukamilisha wajibu wake huu wa kikatiba, taarifa hiyo sasa iko wazi kwa umma, baada ya kuwa imekabidhiwa rasmi bungeni. 



Sisi ACT Wazalendo, tumeisoma, kuipitia na kuichambua taarifa husika, kwa lengo la kuitumia ili itusaidie kutimiza wajibu wetu wa kuisimamia Serikali kama chama mbadala nchini na kama Chama cha Upinzani Bungeni. Tunafurahi kupata fursa ya kuwa nanyi hapa ili kuzungumza na umma, kupitia nyinyi, juu ya maeneo Kumi (10) muhimu kwenye ripoti ya CAG kwa mwaka wa fedha wa 2017/18.



B: Maeneo Kumi (10) Muhimu Katika Ripoti ya CAG



1. Bajeti ya Serikali Sio Halisia, Mapato Yasiyokusanywa ni Tarakimu Mbili



Kwenye bajeti ya mwaka wa fedha wa 2016/17, ambayo ni bajeti ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya Tano, mipango ya Serikali ilikuwa ni kukusanya shilingi 29.5 trilioni, kwa mujibu wa ripoti ya CAG ya 2016/17, kati ya fedha hizo, Serikali ilikusanya shilingi 25.3 trilioni. Na hivyo, kutokufikia lengo la makusanyo kwa 14.33%. Kwenye uchambuzi wetu wa mwaka jana tulieleza kuwa bajeti za Serikali si halisia.



Kwenye ripoti hii ya mwaka 2017/18, kwa mara nyengine, CAG amelithibitishia Taifa kuwa Serikali ya awamu ya tano inatunga Bajeti ambayo sio halisia. Katika Bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha wa 2017/18 jumla ya shilingi 31.7 trilioni zilitarajiwa kukusanywa na zilipitishwa kutumika na Bunge. Hata hivyo, kwa mujibu wa ripoti hii ya CAG, Serikali iliweza kukusanya kutoka vyanzo vyake vyote shilingi 27.7 trilioni tu, na kutumia shilingi 26.9 trilioni. Hivyo ikikosa makusanyo kwa 12.66% na ikikosa matumizi kwa 15.2%.



Kwa miaka mitatu ya mwisho ya Serikali ya awamu ya nne, wastani wa lengo lisilofikiwa na Serikali katika ukusanyaji wa mapato ya Bajeti ni tarakimu moja, 6.3% tu, ambapo kwa mwaka 2013/14 lengo halikufikiwa kwa 9%, kwa mwaka 2014/15 nako lengo halikufikiwa kwa 4%, na kwa mwaka wa fedha wa 2015/16 lengo halikufikiwa kwa 6% tu.



Hii inadhihirisha Kwa mara nyengine tena kuwa Serikali ya Awamu ya Tano hutangaza viwango vikubwa vya Bajeti ili kufurahisha umma ilhali uhalisia ni kuwa Bajeti ni ndogo zaidi. Kwa miaka 2 mfululizo CAG ametuonyesha kuwa Serikali inashindwa kufikia makadirio ya Bajeti Kwa zaidi ya shilingi Trilioni 4 kutoka Bajeti inayopitishwa na Bunge.



2. 40% ya Bajeti Inategemea Misaada na Mikopo



Ripoti ya CAG imetuonyesha kuwa ndani ya miaka miwili ya Serikali ya awamu ya tano uwezo wetu wa kujitegemea kibajeti umezidi kuzorota. Kwa mwaka wa fedha wa 2016/17 nchi yetu ilijitegemea Kibajeti kwa 65% kwa mapato ya ndani ya nchi, na 35% iliyobaki ndiyo iliyotokana na mikopo pamoja na misaada ya Wahisani. Hali Hiyo ni tofauti kwa mwaka wa Fedha wa 2017/18, tumedidimia zaidi.



CAG ameonyesha katika uchambuzi wake kuwa, nanukuu “Uchambuzi unaonyesha kwamba bila Mikopo na misaada kutoka kwa wahisani wa maendeleo, makusanyo ya ndani ya nchi yetu yangeweza kugharamia matumizi yote ya Serikali kwa asilimia 60 tu” (Chanzo: Ripoti ya Ukaguzi-Serikali Kuu-2017/18: Ukurasa wa 89).



Hii inaonyesha kuwa Bajeti yetu ya Tanzania ni tegemezi kwa 40% tofauti na tunavyoelezwa na Serikali kila wakati kuwa nchi yetu inaondoa utegemezi kwenye bajeti. Kwa mwaka 2016/17 utegemezi wetu uliongezeka kwa 27%, na kwa mwaka 2017/18 utegemezi wetu umeongozeka kwa 22%.



CAG ameonyesha kuwa Serikali ilikusanya shilingi 27.7 trilioni tu (makusanyo yote, ikiwemo misaada na mikopo kutoka ndani na nje) kwa mwaka wa fedha wa 2017/18. Makusanyo ya ndani yakiwa ni shilingi 16.7 trilioni, sawa na 60% ya makusanyo yote, na kwamba matumizi ya kawaida yaliyofanyika mwaka huo ni shilingi 15.3 trilioni, ambayo ni sawa na asilimia 55% ya makusanyo yote lakini ni 93% ya mapato ya ndani. Utegemezi huu utaathiri sana nchi yetu kwani gharama za kulipia mikopo (riba) zitakuwa kubwa kuliko hata uwezo wetu wa kuongeza mapato ya ndani.



3. Shilingi 800 Bilioni Hazikutolewa kwa Ukaguzi



Katika Uchambuzi wetu wa mwaka jana tulionyesha kuwa 6% ya fedha zilizokuwa zimekusanywa na Serikali hazijulikani zilipokwenda. Hizi zilikuwa ni shilingi 1.5 trilioni ambazo mjadala wake ulichukua mwaka mzima. Hoja yetu hiyo ilipelekea kufanyika kwa uhakiki maalumu na CAG, na ambapo bado Serikali ilishindwa kuonyesha zilipokwenda fedha hizo, zaidi ya kudai kuwa ilihamishia Ikulu matumizi ya shilingi 976 bilioni kati ya hizo 1.5 trilioni bila kumpa CAG uthibitisho wa uhamishaji huo wala kuonyesha fedha hizo zimefumikaje huko Ikulu.



Katika ukaguzi wa CAG wa Bajeti ya mwaka 2017/18, ambayo ni Bajeti ya Pili ya Serikali ya awamu ya 5, ameonyesha kuwa katika Bajeti ya shilingi 31.7 trilioni iliyoidhinishwa na Bunge, Serikali iliweza kukusanya shilingi 27.7 trilioni tu kutoka kwenye vyanzo vyote vya kodi, vyanzo visivyo vya kodi, mikopo ya ndani na nje, na misaada ya wahisani na washirika wa maendeleo. 



Serikali ilishindwa kukusanya kiasi cha shilingi 4 trilioni kama ilivyokuwa mwaka uliopita ingawa sasa ni sawa na 13% ya Bajeti yote ya mwaka 2016/17. Hata hivyo CAG anaonyesha kuwa shilingi 26.9 trilioni tu ndio zilitolewa kutoka Mfuko Mkuu wa Serikali na kwenda kutumika, hivyo shilingi 800 bilioni kati ya shilingi 27.7 trilioni zilizokusanywa kutokujulikana ziliko na hazikutolewa kwa ukaguzi.



4. Shilingi 4.8 Trilioni Zimetumika Bila Kupita Kwenye Mfuko Mkuu



Katika Ukurasa wa 91 wa ripoti yake yam waka wa fedha wa 2017/18, CAG anasema, nanukuu “Ikilinganishwa taarifa ya kutoa fedha (exchequer issue report) na taarifa ya Fedha zilizopokelewa na kuripotiwa katika taarifa za fedha za Mafungu husika pamoja na barua za kukiri mapokezi ya fedha kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, imebaini utofauti wa taarifa zilizoripotiwa…”. 



CAG ameeleza kuwa tofauti hiyo imesababishwa na kutokuwepo kwa mifumo thabiti ya usuluhishi kati ya fedha zilizotolewa na hazina na fedha zilizotolewa na wahisani wa maendeleo moja kwa moja kwenye miradi ya maendeleo katika Wizara. Ni muhimu sana kusisitiza hapa kuwa kwa mujibu wa CAG kuna fedha shilingi trilioni 4.8 ambazo makusanyo yake hayakuingizwa mfuko mkuu wa Serikali (tazama uk 91 wa Taarifa, tanbihi namba 15).



Suala la udhaifu wa Mifumo Katika Hazina pia limeelezwa kwa kina Katika Taarifa ya CAG ya Uhakiki wa Tofauti ya shilingi 1.5 Trilioni Katika mwaka wa Fedha 2016/17. Bado udhaifu huu unaendelea na madhara yake Katika usimamizi wa Fedha za Umma ni makubwa sana.



5. Bilioni 678 za Mamlaka Nyengine Ziliporwa na Mlipaji Mkuu wa Serikali



Kwenye ripoti ya CAG ya 2017/18 imeonyeshwa kuwa bado Serikali inatumia fedha ambazo sio zake (ring fenced) kama ilivyoonyeshwa kwenye ripoti ya mwaka 2016/17. Kwa mwaka 2017/18 CAG amebaini jumla ya shilingi 678 bilioni zilizokusanywa na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) kwa niaba ya taasisi nyengine hazikuhamishwa kwenda kwenye taasisi husika, na badala yake zilihamishiwa kwa Katibu Mkuu Hazina ambapo huko hazikuonekana kwenye ukaguzi kama sheria inavyotaka. 



Fedha zilizoporwa na Hazina ni pamoja na shilingi 169 bilioni za Shirika la Reli, shilingi 168 bilioni za Wadau wa Korosho nchini na shilingi bilioni 16 za Wakala wa Umeme Vijijini (REA). CAG kwa mara nyengine tena amependekeza sheria iheshimiwa kuhusu matumizi ya fedha hizi za Taasisi mbalimbali. Kwenye ripoti ya CAG ya mwaka 2016/17 kiasi cha shilingi 2.2 trilioni za mamlaka mbalimbali nchini hazikurejeshwa kwenye mamlaka husika mara baada ya fedha hizo kukusanywa na TRA. Tabia hii ya kupora Fedha za Mamlaka nyengine licha ya Kwamba Fedha hizo zimewekwa kisheria na kikatiba inaua misingi ya matumizi bora ya Fedha za Umma.



Kwa Upande wa TRA Bado kuna changamoto kubwa ambazo zinahitaji kutatuliwa. Makusanyo yetu ya kodi Bado ni kidogo sana (tax yield) tukiwa wa mwisho Katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, uwiano wa makusanyo ukiwa ni 12% tu ya Pato la Taifa. Hii inatokana tax base kuwa ndogo na mifumo sio rafiki kwa walipa kodi. Inawezekana TRA huchukua Fedha za Taasisi kupeleka Hazina ili kuonyesha makusanyo zaidi ilhali hali sio hiyo. Serikali inapaswa kukaa na sekta Binafsi kujadili kwa unyoofu (honestly) njia bora ya kupanua wigo wa Kodi ili nchi iweze kujitegemea. Katika uchambuzi wetu tumeacha mambo Mengi ikiwemo upotevu mkubwa wa mizigo ya transit ambao CAG ameuonyesha.



6. Kushuka kwa Thamani ya Shilingi Kunakuza Zaidi Deni la Taifa



Ripoti ya CAG ya 2017/18 imetuonyesha kuwa Deni la Taifa (Deni la Serikali) limefikia shilingi 50 trilioni mpaka Juni 30, 2018 likiwa na ongezeka la shiingi 4.85 trilioni, sawa na 10% kutoka shilingi 46 trilioni za Juni 30, 2017, deni hili likikua kwa shilingi 9.8 trilioni kwa muda wa miaka miwili tu kutoka Juni 30, 2016 mpaka Juni 30, 2018. CAG ameeleza kwamba kushuka kwa thamani ya shilingi ya Tanzania dhidi ya fedha za kigeni kumechangia kuongezeka kwa Deni kwa 20% kwa mwaka wa fedha wa 2017/18 (ongezeko kubwa zaidi ukilinganisha na 9% za mwaka wa fedha wa 2016/17). 



Hii inatokana na Deni letu la Nje kuwa kwenye Fedha za Kigeni na hivyo kuathirika sana kutokana na thamani ya shilingi kutetereka. Baada ya makosa ya kimaamuzi kwenye suala la Zao la Korosho, ni dhahiri kuwa Deni letu la Nje litaongezeka zaidi baada ya shilingi ya Tanzania kutetereka zaidi kwa kukosa Mapato ya Fedha za Kigeni. MAARIFA makubwa yanahitajika kuhami nchi kutokana na janga la Deni la Taifa.



7. Mikopo ya Ndani Yashindwa Kulipa Madeni Kikamilifu 



Lakini pia CAG ameeleza kuwa sababu Kuu zaidi ya kukua kwa deni la Taifa ni kwa kuwa tunaendelea kukopa zaidi. Kwa miaka mitatu iliyopita kukopa zaidi kulichangia ukuaji wa deni letu kwa 70%, ambapo kwa mwaka 2016/17 ilikuwa juu zaidi na kufikia 88%.



Zaidi CAG ameonyesha pia kuwa tulikopa mikopo ya ndani ya shilingi 5.7 trilioni kwa mwaka 2017/18 ambayo pamoja na kuwa na athari mbaya kwenye mikopo ya sekta binafsi nchini (maana inapunguza fursa ya wafanyabiashara wetu kukopeshwa na taasisi za ndani za fedha), lakini pia mikopo hiyo imeshindwa kulipa riba za mwaka za shilingi 6.1 trilioni. Na hivyo ilibidi Serikali kutafuta shilingi 448 bilioni kutoka kwenye vyanzo vingine ili kuweza kulipa riba hizo. 



Ripoti ya CAG imeeleza, nanukuu “Deni la Ndani halikuchangia kwenye miradi ya Maendeleo”. Hivyo tulikopa ndani ya nchi si kwaajili ya kufanya shughuli za maendeleo, bali kulipa deni la nyuma, na bado hata hiyo mikopo haikutosheleza ulipaji wa hayo madeni ya nyuma. Hali hii si afya kwa taifa letu.



Mfano kwa mwaka 2017/18 Kiwango cha kuhudumia Deni la nchi ni 108% ya fedha zilizopatikana kutoka kwenye mikopo ya ndani, na CAG ameonya kuwa jambo hilo lina athari kubwa. Ukurasa wa 141 wa Ripoti ya Ukaguzi wa Serikali Kuu CAG ameeleza, nanukuu “kuna uwezekano wa kuwa na madhara kwa uchumi (hali ya kuhudumia deni kwa 108%) isipotafutiwa ufumbuzi”. 



CAG pia ameonyesha kuwa kasi ya kukua kwa mikopo ya nje ni 38%, hali ambayo inaongeza gharama za kuhudumia madeni. Na jambo baya zaidi ni kuwa tunakopa zaidi mikopo ya kibiashara. CAG ameshauri watunga sera kuwa na busara wakati wa kuchagua miradi ya kupewa fedha za mikopo ya kibiashara, akishauri maamuzi yazingatie uzalishaji wa miradi husika. Vinginevyo Bajeti ya Taifa itakwenda kuhudumia deni tu.



Kwenye eneo hilo la Deni la Taifa pia ripoti ya CAG imeonyesha kuwa kuna upotoshwaji mkubwa wa mapokezi ya mikopo kutokana na mapungufu ya udhibiti wa ndani. Pia CAG ameonyesha kuwa mifumo wa kutunza madeni ni kianalojia (ya kizamani), jambo ambalo linaathiri kumbukumbu za madeni. 



8. Serikali Imeanza Kushindwa Kulipa Madeni (Defaulting)



Ripoti ya CAG imeonyesha kuwa Serikali imeshaanza kushindwa kulipa baadhi ya madeni yake (Defaulting). Tayari kuna fedha kiasi cha shilingi 212.7 bilioni Serikali imeshindwa kuzilipa kwa Benki Kuu nchini (BOT), zikiwa shilingi 199.79 bilioni ni riba ya nakisi ya Serikali, na shilingi 12.9 bilioni ni sehemu ya Serikali ya gharama za kudhibiti ukwasi kuanzia mwaka 2015/16 hadi 2017/18.



Serikali ilisaini Mkataba wa Makubaliano (MoU) na BOT, ambao unaitaka kulipa kila robo mwaka sehemu yake ya gharama ya kudhibiti ukwasi pindi hati ya madai inapotolewa. Ucheleweshwaji huu wa malipo utaongeza uwepo wa mali za BOT zisizo na tija, na ni dalili ya Serikali kushindwa majukumu yake kifedha.



9. Ikulu Yatumika Kuficha Ukaguzi wa Manunuzi ya Ndege



Hatujafanikiwa kuona Ukaguzi wa Manunuzi ya Ndege ikiwemo Ununuzi wa Ndege za Shirika la Ndege Nchini, ATCL ambao kwa sehemu umefanyika mwaka wa fedha 2016/17 na 2017/18.



Katika uchambuzi wetu wa ripoti ya CAG ya mwaka jana (ripoti ya mwaka wa fedha wa 2016/17) tuliwaeleza kuwa katika ripoti ile licha ya kuwa ni taarifa bora sana kwa maudhui na uchambuzi, kuna mambo muhimu kadhaa ambayo CAG aliyaacha. Na tukamtaka kwenye ripoti yake ya mwaka 2017/18 ayafanyie kazi, mojawapo ni ukaguzi wa Ununuzi wa Ndege Sita (6) zinazoendeshwa na Kampuni ya Ndege nchini, ATCL.



Mpaka sasa Serikali imeshatumia jumla ya Shilingi Trilioni1 kununua ndege sita (6) na katika makadirio ya Bajeti ya mwaka 2019/20 yanayoendelea sasa bungeni Serikali imeomba Bunge liidhinishe shilingi Bilioni 500 kwa ajili ya kulipia ndege mpya nyengine. Ufuatiliaji wetu umegundua kuwa Serikali imekuwa ikichukua Fedha za Umma kupitia Fungu 62 (Wizara ya Uchukuzi) na kufanya manunuzi ya ndege. Ndege hizo wanakabidhiwa Wakala wa Ndege za Serikali kama wamiliki na shirika la ATCL inakodishiwa ndege hizo kwa Mkataba maalumu (ambao haujawekwa wazi popote, hata kwa Bunge).



Tulitarajia kuwa ripoti hii ya CAG ya mwaka 2017/18 kwenye ukaguzi wa fungu Namba 62 tungeweza kuona ukaguzi wa manunuzi ya ndege hizi. Lakini Serikali kwa lengo la kuficha taarifa imeamua kuhamishia kwenye Ofisi ya Rais (fungu 20) Wakala wa Ndege za Serikali kupitia tangazo la Serikali namba 252 la Juni 2018.



Tumetafuta taarifa ya ukaguzi wa fedha hizo za umma zilizofanya manunuzi ya ndege bila mafanikio. Tunamwomba CAG;
- Afanye Ukaguzi Maalumu wa Fedha za Umma Shilingi Trilioni 1 zilizotumika kununua ndege.
- Afanye Ukaguzi wa usimamizi wa mkataba wa ukodishwaji wa ndege hizo kati ya Wakala wa ndege za Serikali na Shirika la Ndege la ATCL ili Watanzania wajue matumizi sahihi ya Fedha zao za Kodi.



Jambo hili ni muhimu sana, kwa sababu uzoefu unaonyesha kuwa kila jambo lenye harufu ya wizi au matumizi yenye mashaka basi Serikali huliamishia jambo hilo ikulu (Kwa kuwa inajua ukaguzi wake hautawekwa wazi). Hata kwenye fedha shilingi 1.5 trilioni ambazo tulizianisha kuwa hazijulikani ziliko kutokana na uchambuzi wetu wa ripoti ya CAG ya mwaka 2016/17, baada ya kuibana Serikali na kumtaka CAG afanye uchunguzi maalum, mwishowe Serikali ilihamishia Ikulu matumizi ya Shilingi 976 bilioni kati ya hizo shilingi 1.5 trilioni ili isihojiwe.



Mafungu mawili, Fungu 20 (Ofisi ya Rais Ikulu) na Fungu 30 (Sekretariati ya Baraza la Mawaziri) yanapaswa kumulikwa sana katika matumizi ya Fedha za Umma. Tumeona mwaka huu Serikali inaomba Bunge litenge shilingi Bilioni 302 kwa Fungu 30 kwa kile kinachoitwa ‘matumizi mbalimbali ya kitaifa’. Mwaka ujao, Mungu akituweka hai, tutafuatilia kwa kina kaguzi za mafungu Haya kwani inaonyesha ndimo inakuwa kichaka Cha kuficha Taarifa za namna Fedha za Umma zinatumika.



10. Hoja za Ukaguzi za Shilingi Bilioni 225 hazina majibu kabisa
Kwa ujumla, na kwa Serikali Kuu peke yake, Hoja zote za Ukaguzi zilizoibuliwa na CAG kwenye Hesabu za Mwaka 2017/18 ukiachana na hoja kubwa nilizoeleza hapo juu, zina thamani ya shilingi 225 bilioni kati ya Fedha zote zilizokusanywa kwenye mwaka wa Fedha husika. Hii inaonyesha kuwa bado Serikali haijaweza kufanyia kazi Hoja za CAG kwa wakati na kwamba mifumo ya Serikali bado inavujisha Fedha za Umma.



C: Mapendekezo ya ACT Wazalendo 



Baada ya kusoma taarifa hiyo ya CAG na kuyaanisha maeneo Kumi (10) muhimu, sisi ACT Wazalendo tuna mapendekezo yafuatayo:



1. ACT Wazalendo tunawasihi Wabunge wote bila kujali vyama vyao kutekeleza wajibu wao wa kuisimamia Serikali. Wabunge wasipotekeleza wajibu wao huo basi nchi yetu itaangushwa na matumizi mabovu na ya kinyume na Sheria kama tulivyoaina kwenye Uchambuzi wetu.



2. Serikali iwe inatunga Bajeti Halisia ambayo inatekelezeka, tofauti na inavyofanya kwa miaka minne mfululilo sasa, ambapo inataja namba kubwa ambayo Bajeti husika huwa haipatikani kwa ukamilifu wake na hivyo kuathiri sana miradi ya Maendeleo ambayo inakuwa imepangiwa mafungu ya Fedha. Ni bora kuwa na Bajeti ndogo ambayo inatekelezwa badala ya kuwa na Bajeti kubwa ambayo haitekelezwi ipasavyo.



3. Serikali itazame upya utekelezaji wa Sera zake za kiuchumi kwani dalili zinadhihirisha kuwa Uchumi wetu unaanguka. Ikibidi Kuwe na Mjadala wa Kitaifa juu ya hali ya uchumi wa nchi yetu, mjadala huo usaidie kupata uhalisia wa hali mbaya ya uchumi wetu, mbinu za kuunasua, na mawazo ya kuinasua nchi kutoka kwenye utegemezi wa misaaada pamoja na mikopo inayoongeza ukuaji wa deni la Taifa.



4. Serikali ionyeshe ilipo shilingi 800 bilioni isiyoonekana matumizi yake katika ripoti ya CAG yam waka wa fedha 2017/18.



5. Serikali ileze ni kwa nini Fedha Jumla ya shilingi Trilioni 4.8 hazikupita kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina ili utolewaji wake uweze kufuata masharti ya Katiba na Sheria za nchi. Fedha hizi za Wafadhili zinaonekana Katika Vitabu vya Bajeti Lakini CAG hazioni kuingia mfuko Mkuu na hivyo kutoka kwake kunaweza kuwa ni kinyume Cha Sheria. Menejimenti ya Wizara ya Fedha na Mipango ihakikishe inafanya usuluhishi sahihi wa taarifa za fedha zilizotolewa kwa Wizara mbalimbali na fedha zilizopokelewa moja kwa moja na wahisani wa maendeleo katika miradi. Hazina ifanyiwe usafi maalumu ili kuhakikisha ‘credibility’ ya Taarifa zake.



6. Serikali izingatie Sheria na Katiba Kuhusu Fedha za Taasisi ambazo zimetengwa kisheria Lakini Hazina inazitumia bila kujali Sheria. Hazina ihakikishe inazirejesha kwa wenyewe Ada, Tozo na mapato hayo ambayo TRA ilikusanya kwa niaba ya Idara, Wakala na Taasisi nyengine.



7. Wabunge, kama sehemu ya wenye wajibu wa kutunga sera tunayo nafasi ya kuisimamia Serikali kwenye suala la kushuka kwa thamani ya shilingi, kwanza kwa kuwawajibisha wote waliosababisha sintofahamu ya zao la korosho ambalo kama tungeuza basi kungepatikana unafuu kwenye deni la Taifa.



8. Ili kudhibiti kasi ya ukuaji wa Deni la Taifa, haswa Deni la Nje, kutokana na kushuka kwa thamani ya shilingi yetu, tunapendekeza kuwa Serikali ifanye hedging ya Deni la Nje ili kuwa na uhakika wa thamani ya fedha itakayotumika muda wote kuhudumia Deni hilo. Serikali ya Awamu ya Tano imeonyesha kutegemea sana mikopo ya kibiashara kutoka Mabenki ya Nje na hivyo kuweka nchi kwenye hatari kubwa ya Mtego wa Madeni (Debt Trap). Hedging inaweza kusaidia kudhibiti kasi ya ukuaji wa Deni la Nje.



9. Tunamsihi ndugu Rais atambue kuwa njia ya bora ya kupambana na rushwa na ufisadi ni kuwezesha mifumo kufanya kazi. Mtu mmoja hawezi kamwe kuwa dawa ya ufisadi ulioota mizizi nchini kwetu. Ripoti za CAG na madudu yaliyoibuliwa kila kona inaonyesha dhahiri kuwa silaha ya uhakika ni kujenga Taasisi imara za Uwajibikaji ili kudhibiti Fedha za Umma. Miaka 4 aliyepo madarakani imethibitisha kuwa nguvu ya Mtu mmoja haitoshi kukomesha ubadhirifu bali Mifumo Imara.



Ni matarijio yetu kuwa Watanzania wataendelea kuisoma na kuichambua Taarifa ya CAG na kuwaomba Wabunge watimize wajibu wao wa kuisimamia Serikali ili kujibu hoja zote za Ukaguzi. Bila Bunge kutimiza wajibu wake ipasavyo mzunguko wa uwajibikaji unakuwa haufungi. Tumeona Katika Taarifa ya CAG kuwa Hoja hazijibiwi na hivyo hazifungwi na madhara yake ni kuwa kila mwaka hoja zinaongezeka tu.


Ahsanteni Sana.

Kabwe Z. Ruyagwa Zitto
Mbunge, Kigoma Mjini
Kiongozi wa Chama, ACT W
azalendo
Aprili 14, 2019
Dodoma

29 Jan 2015

Enzi hizo: Rais Kikwete akiwa na James Rugemalira

RAIS Jakaya Kikwete anapaswa kuwajibika binafsi katika kashfa ya ukwapuaji wa mabilioni ya shilingi katika Akaunti ya Tegeta Escrow. Saed Kubenea anaandika…(endelea)

Mjumbe wa Kamati Kuu (CC) ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Mabere Marando amesema, Rais Kikwete, ndiye aliyeruhusu kiasi cha Sh. 321 bilioni kuchotwa katika mazingira yaliyosheheni udanganyifu.

“Fedha zile zimechukuliwa kwa maelekezo ya Rais Kikwete ili kumuwezesha chama chake kufanikishe kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka huu,” ameeleza Marando.

Hata hivyo, Marando anasema, “Tumeambiwa na watu waliokaribu na chama hicho, kuwa ni sehemu ndogo sana ya fedha iliyoibwa zilizofikishwa CCM. Nyingi ya fedha hizo zimechukuliwa na familia ya rais mwenyewe.”

Taarifa zinasema, familia ya Rais Kikwete imepata zaidi ya Sh. 9 bilioni, kutoka katika mgawo wa fedha zilizohifadhiwa katika akaunti ya Escrow.


“Kikwete anajua kila kitu. Yule singasinga – Harbinder Singh Sethi – alitokea Ikulu. Mpango wa uchotaji wa fedha za umma ulipangwa Ikulu na ulitekelezwa kwa maelekezo ya rais,” ameeleza.


Taarifa zinasema, anayejiita na kuitwa na serikali kuwa ni “mmiliki mpya wa IPTL/PAP,” Harbinder Singh Sethi, alichotewa fedha hizo baada ya kufikishwa Ikulu na baadaye akakutanishwa na gavana wa BoT, Prof. Benno Ndullu; na kutoka hapo alikwenda kukwapua mabilioni hayo ya shilingi hata bila kumfahamisha James Rugemalira – mbia mwenzake.

Sakata la ukwapuaji wa fedha katika akaunti ya Escrow ndilo lililomtupa nje ya ofisi, aliyekuwa waziri wa nishati, Prof. Sospeter Muhongo.

Taarifa zinasema, Prof. Muhongo, ni miongoni mwa wanaotajwa kunufaika na fedha za Escrow zilizopitia benki ya Stanbic. Mwingine ambaye jina lake lilitajwa bungeni na mmoja wa wabunge wa upinzani, ni Albert Marwa.

Marando anasema, “Pamoja na kujiuzulu kwa Prof. Muhongo, bado haitoshi bila kuhojiwa au kuwajibishwa kwa gavana Ndullu, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya, Katibu Mkuu wizara ya Fedha, Dk. Servacius Likwalile na maofisa wa ikulu na hata rais mwenyewe ambaye ndiye aliyeruhusu fedha hizo kutolewa.”

Akiongea kwa kujiamini, Marando anasema, “Wizi huu ulianzia Ikulu na umefanyika kwa baraka za Ikulu na mbele ya macho ya rais. Umewashirikisha baadhi ya maofisa wake na hata familia yake.”

Dk. Likwalile ndiye aliyewasilisha kwa gavana wa BoT kwa ajili ya utekelezaji, maagizo ya Rais Kikwete kuwa fedha katika akaunti ya Escrow zilipwe kwa PAP.

Alikuwa akirejea maagizo kutoka kwa Rais Kikwete kwa kunukuu barua ya tarehe 13 Novemba 2013, ambayo ilisainiwa na Katibu wa Rais, Bw. Prosper Mbena.


5 Dec 2014

Waingereza wana msemo ambao unatafsirika kwa Kiswahili kama "chuki ya pamoja ni mwanzo wa urafiki mkubwa." Kimahesabu kama A hapatani na B, na A anamchukia C kama ambavyo B anamchukia pia C, basi chuki ya A na B kwa C yaweza kuwa mwanzo wa wawili hao A na B kuwa marafiki wenye lengo la kumwangamiza C.

Binafsi, naomba kukiri kuwa kwa muda sasa nimekuwa siafikiani na mitizamo na mwenendo wa mwanasiasa mahiri wa upinzani, Zitto Kabwe. Siwezi kusema nina chuki dhidi yake bali mie sio miongoni mwa supporters wake.Pamoja na sababu nyingine, kubwa ni kile ninachokitafsiri kama mwanasiasa huyo kutanguliza mbele maslahi yake binafsi badala ya chama chake yaani Chadema. Kwa mtizamo wangu, mgogoro uliopelekea hatua ya Chadema kumvua madaraka Zitto ni matokeo ya 'imani potofu' kuwa kuna mwanasiasa anayeweza kuwa maarufu kuliko chama chake, Si kwamba haiwezekani kabisa kwa hilo kutokea lakini si kwa hatua waliyofikia Chadema hivi sasa.

Lakini lengo la makala hii si kumjadili Zitto wala ugomvi kati yake na Chadema. Ila nimegusia suala hilo kwa sababu nililazimika 'kurejesha urafiki' na mwanasiasa huyo, angalau kinadharia, wakati akifanya jitihada kubwa binafsi na kama mwenyekiti wa PAC kushughulikia ufisadi wa Tegeta Escrow. Kwa kutumia mfano huo hapo juu wa chuki za A kwa C na za B kwa C, na A ni Zitto, na B ni mie, huko C wakiwa mafisadi wa Escrow, basi 'urafiki' usingeepukika.

Hakuna Mtanzania atakayeshindwa kumpongeza Zitto na Kafulila pamoja na PAC kwa ujumla walivyofanya kazi kubwa na nzuri katika kushughulikia skandali hiyo. Nina imani hata wahusika wa ufisadi huo wa Escrow wanamkubali kwa jinsi alivyowakalia kooni...ALMOST.

Hata hivyo, mara baada ya kumalizika kwa 'timbwili' hilo la Escrow bungeni, nilitumiwa meseji na 'mjuzi mmoja wa mambo ya huko nyumbani' ambaye alidai kuwa pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na PAC, kuna 'mchezo mchafu' uliofanyika katika kufikia mwafaka miongoni mwa wajumbe, hususan wale wa kutoka CCM. Alidai kuwa kilichowezesha mwafaka huo kufikiwa ni pamoja na 'kumnusuru' Rais Jakaya Kikwete, ambaye kama Mbunge Tundu Lissu alivyobainisha bungeni, anatajwa kuhusika katika skandali hiyo. Kimsingi, hoja ya Lissu, ambaye pia aliilaumu Idara ya Usalama wa Taifa kwa kutowajibika ipasavyo katika mlolongo wa skandali mbalimbali zinazougubika utawala wa Rais Kikwet, iliuawa kimyakimya licha ya umuhimu wake mkubwa.

Hata hivyo, kwa uelewa wangu, jaribio lolote la kumhusisha Rais Kikwete na skandali hiyo hata kama ushahidi upo lingepelekea mparaganyiko mkubwa katika kamati hiyo ya Zitto. Na kama tulivyoshuhudia 'makada' wa CCM huko bungeni walivyopigana kufa na kupona hadi Waziri Mkuu Mizengo Pinda akanusuriwa, kwa hakika ishu ya Kikwete kuhusishwa na Escrow ingepelekea bunge hilo kuvunjika pasi kufikia hitimisho.

Lakini what if mkakati huo wa 'kumnusuru Rais Kikwete' unabeba mengi zaidi ya tunavyodhani? 


Kwa kifupi, tume-settle for less. Na Waingereza wana msemo unaotahadharisha kuhusu ku-settle for less, ambapo wanasema 'pindi ukikubali kupokea pungufu ya unachostahilki basi hatimaye utaishia kupokea pungufu zaidi ya kile ulichostahili awali.' Japo ni mapema kuhitimisha kwamba 'tumeingizwa mkenge,' lakini ukimya wa Rais Kikwete katika kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu Escrow umeanza kuzua wasiwasi.

Na 'kigugugmizi' kinachomkabili Rais Kikwete kina sababu kadhaa za wazi. Kwa mfano, kumtimua Mwanasheria Mkuu Jaji Werema kunaweza kupelekea kuzuka kwa skandali nyingine iwapo Jaji huyo ataamua 'mmemwaga mboga, na mie namwaga ugali' kwa maana anajua mengi yaliyojiri na yanayojiri katika utawala wa Rais Kikwete. Japo si kwamba haiwezekani kumtimua na kisha kumfunga mdomo, lakini historia ya wanasheria wakuu huko nyuma inapaswa kutukumbusha jinsi 'wanavyobebwa' kwa minajili ya 'kutotengeneza uadui na mtu anayejua siri nyingi.'

Kwa upande wmingine, ni muhimu kukumbuka kuwa kimsingi Rais Kikwete ndo aliyemleta Profesa Muhongo katika frontline politics. Hawa ni marafiki wa karibu. Na hadi sasa Muhongo ameendeleza jeuri yake ya kisomi na kusisitiza kuwa fedha za Escrow si za umma. Msimamo huo pia washikiliwa na Waziri Mkuu Pinda. Je kuna anayefahamu msimamo wa Rais Kikwete? Maelezo yanaonyesha kuwa yeye aliridhia malipo ya Escrow kufanyika. Je amebadili mawazo na kutambua kuwa hilo lilikuwa kosa?

Lakini wakati tayari tunafahamu majina mengi ya walionufaika na mgao wa Escrow kupitia Benki ya Mkombozi, inadaiwa kuwa mgao mkubwa zaidi uliopitia Benki ya Stanbic ulihusisha vigogo kadhaa lakini hadi muda huu hakuna jina hata moja lililowekwa hadharani. So far, gazeti la Raia Mwema limeripoti kuwa mke wa kigogo momja mwandamizi huko Ikulu alikatiwa shilingi bilioni 5. Sasa huhitaji kujua hesabati vizuri kubashiri kwamba kama mke wa kigogo alikatiwa mbilioni tano, mumewe alipewa kiasi gani? 

Hayo yote tisa, kumi ni kauli niliyokumbana nayo muda mfupi uliopita, na ambayo kwa hakika ndio iliyonisukuma kuandika makala hii. Kauli hiyo ni ya Jaji Mkuu Chande ambayo kimsingi inaharibu mwenendo wa kesi yoyote itakayofunguliwa dhidi ya wahusika wa ufisadi wa Escrow. Nimeinukuu kwa picha hapa chini.


Je Jaji Mkuu alikuwa anatoa tu tahadhari au alikuwa akifikisha ujumbe mahsusi kwamba hata tukiwapeleka mahakamani wahusika wa Escrow, utetezi wao upo bayana...kwamba walishahukumiwa bungeni. Na kama Jaji Mkuu 'hakutumwa' basi kwa hakika amewapatiwa washtakiwa-watarajiwa ushauri mzuri wa bure kisheria kuhusu jinsi ya kupambana na kesi yoyote watakayofunguliwa kuhusisna na suala hilo: wajitetee kuwa walishahukumiwa na bunge, na mawakili waoa waweza kutumia kauli hiyo ya Jaji Mkuu kama supporting evidence.

Anyway, pengine ni mapema mno kuhukumu lakini kama ambavyo Mzee Warioba alivyoonyesha mapungufu ya taarifa ya PAC na maazimio ya bunge kuhusu skandali ya Escrow, sintomshangaa mtu yeyote atakayeanza kupatwa na wasiwasi kuwa tumeingizwa mkenge...TENA.


Sijui msomaji mepndwa unaonaje. 





22 Oct 2014

Watanzania tuna sifa moja kuu isiyopendeza ya usahaulifu wa haraka. Kuna wanaodai si usahaulifu as such bali kutojali, lakini bottom line ni kwamba haichukui muda mrefu kwa jambo linalotokea Tanzania bila kujali ukubwa au athari zake kwa taifa hilo kusahaulika haraka. 

Ni kwa mantiki hiyo ndio ninajikuta nikijiuliza ni Watanzania wangapi wanakumbuka ujio wa Rais wa China huko nyumbani, ulioambatana na utiaji saini wa mikataba kumi na kitu ambayo hadi leo imebaki kuwa siri ya namna flani. Mengi yamesemwa kuhusu mikataba hiyo lakini kilicho wazi, kwa kwa kuzingatia uzoefu wetu huko nyuma, mnufaika mkubwa wa mikataba hiyo ni Wachina na pengine kikundi kidogo cha wenzetu waliovuna teni pasenti kwenye akaunti zao.

Ndio maana niliposikia kuwa Rais Jakaya Kikwete anaelekea China nikabaki najiuliza: HIVI KAMA RAIS WA CHINA ALIKUJA KWETU NA IKASAINIWA MIKATABA KADHAA NA TUKAFICHWA, JE MIKATABA ITAKAYOSAINIWA WAKATI WA ZIARA YA KIWEKTE HUKO CHINA TUTAFAHAMISHWA? Jibu la wazo ni BIG NO. Hatutojua kitu.

Wakati natafakari hayo, nikakutana na habari hii ambayo ni tamko la Katibu Mkuu wa Chadema Taifa Dkt Willibrod Slaa ikitoa tuhuma nzito kuhusiana na ziara hiyo ya Kikwete China. Soma taarifa hiyo hapo chini na angalia kwa makini maneno ya rangi nyekundu.


Kamati Kuu ilikuwa na jumla ya agenda kumi na moja, mengine tutayatoa kwa umma kadri muda unavyokwenda.
Kwa leo tutazungumzia masuala mawili ambayo yana sura ya utekelezaji, tena wa muhimu na haraka; Mchakato wa Katiba Mpya na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa;
Katiba;
 
Tunawataka Watanzania wanaopenda nchi yao sasa waache kulia lia, waache kunung’unika pekee, waache kulalamika. Tuingie kazini. Sasa ni wakati wa kuingia kazini.  
Wenzetu tangu siku ya kupokea rasimu ambapo Kikwete si kama rais wa nchi, bali kama Mwenyekiti wa CCM alianza kuipigia chapuo debe Katiba Inayopendekezwa. Sasa tuingie kazini…
Kikwete kama mwenyekiti wa CCM akitumia kofia ya rais wa nchi, baada ya kupokea rasimu ameendelea kuipigia chapuo, anawaambia wananchi wasome Katiba inayopendekezwa waelewe, sisi tunamwambia aache kuwadanganya Watanzania. Katiba si sawa na novel kwamba kila mtu anaweza kuisoma tu na kuelewa, ingelikuwa ni rahisi namna hiyo tusingekuwa na haja ya kuwasomesha akina Lissu (Tundu). 
Tunahitaji wananchi wetu wasaidiwe tafsiri hasa ya katiba yenyewe na maana yake, hadi yale mambo ya ndani kabisa. Ndiyo kazi ambayo CHADEMA tunaanza kuanzia kesho kuzunguka nchi nzima, ambapo timu ya kwanza itaongozwa na BAWACHA. Ujumbe utakuwa ni Katiba Mpya na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Tunataka kuwafafanulia Watanzania kwa kina. 
Wakati bado tunapigania Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka kesho, moja ya ujumbe wetu kuanzia sasa ni kuwataka Watanzania kujiandaa kufurika vituoni kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambalo litaanza kuandikishwa siku 21 kabla ya uchaguzi wenyewe. 
Watanzania wafurike kwa wingi. Wajiandikishe. Kuiondoa CCM kunahitaji vitendo. Tuingie kazini. 
Kwa mtindo huo huo wa kuingia kazini sasa kwa vitendo, tutatembea nchi nzima sasa kuwataka wananchi kujitokeza kwa wingi sana siku ya Desemba 14, kupiga kura kuwachagua viongozi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji… 
Tunawaagiza vile vile viongozi wetu katika ngazi zote za chama, kuanzia kanda, mikoa, wilaya, majimbo, kata, matawi na hadi misingi kuwaongoza Watanzania wote; 1. Kujiandikisha, 2. Kupiga kura na 3. Kusimamia taratibu za kikanuni… 
Tumeshabaini na kila Mtanzania sasa anajua kuwa kuwa Rais Kikwete si mtu wa kuaminika tena…ni mtu anayebadilika badilika na wala haoni haja ya kuomba samahani… 
Na sasa tumezidi kubaini kuwa Kikwete amefikia mahali pa kugeuka kuwa procurement officer na tumenasa nyaraka ambazo zinaonesha kuwa katika kujigeuza ofisa manunuzi huko yanafanyika maandalizi ya kufanya mapambano na wananchi badala ya kuandaa maridhiano.
Nyaraka…Rais amegeuka kuwa Ofisa Manunuzi, Ofisa Mawasiliano TCRA 
Tumepata taarifa za ziara yake ya kwenda China. Siwezi kusema atakwenda tarehe ngapi maana mimi si kazi yangu kutangaza tarehe za ziara za Kikwete ambazo sasa hata tumechoka kuhesabu maana zimeshakuwa nyingi mno zaidi ya 300+ ndani ya miaka kumi. 
Kilichotushtua si Kikwete kwenda ziara, maana siku hizi wala si habari tena, kilichotushtua ni hicho kinachompeleka huko China…ukimsikiliza Kikwete kwenye mazungumzo anapenda kuonekana mtu anayeoenda amani, mshikamano lakini si kweli.  
Amejigeuza Ofisa Manunuzi. Kwa miezi kadhaa sasa kumekuwa na jitihada za kupata helkopta tatu mpya…zingelikuwa ni kwa ajili ya Jeshi letu la Wananchi nisingekuwa na shida, shida inakuja namna zinavyotafutwa. Zinatafutwa kwa utaratibu ule ule wa kifisadi uliotumika kununua ndege ya rais wakati ule na hata rada. 
Tena anamtumia kampuni moja hivi ambayo tumekuwa tukiituhumu katika ufisadi. Sasa sisi tunahoji, hivi ni kwa nini Serikali ya CCM inashindwa kwenda kiwandani na kufanya order ya manunuzi kiwandani moja kwa moja hadi itumie taratibu za kifisadi au mafisadi kufanya kazi hizi… 
Kikwete anajua kuwa ninajua. Maana ameshalalamika kwa watu wake wa vyombo vya dola kwamba taarifa hizi zimefikaje kwa Dokta Slaa…
Wametumia fedha zetu za mikopo kutoka Ujerumani…ndege zinanunuliwa Ufaransa…anatuma fisadi kwenda kufanya manunuzi hayo badala ya Serikali… 
Kinachoonekana na taarifa na sisi hapa tunahoji je ni kweli ndege hizo zinataka kutumika kwa manufaa ya CCM? 
Rais pia ameomba kwenda Beijing kufuatilia mitambo ya Police Surveillance System…wanataka mitambo hiyo ifike hapa kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015…ujumbe huu umeandikwa na mtu anaitwa Mbelwa…Kairuki. Waandishi wa habari mtakuwa mnajua huko Wizara ya Mambo ya Nje. Anamwandikia Waziri wa Mambo ya Nje…ujumbe huu umeandikwa tarehe 7/10/2014… 
Sasa hizo ndege anayotaka kununua iko mji mwingine huko China si ule aliopangiwa katika ziara yake, sasa imeagizwa irushwe hadi pale atakapokuwa ili eti Rais mwenyewe aweze kuiona…nimeangalia kwenye budget component hiyo kitu hakuna. Kwa kawaida vitu vya kijeshi huwa havitajwi kwenye bajeti, lakini kwenye randamana ungeweza kuona mpango wa kununua kitu kama hicho. Hakuna. 
Sasa kinachoonekana ni kwamba kwa sababu wamejua mwaka 2015 wanaondoka madarakani, wanaanza kujiandaa kwa mapambano badala ya maridhiano. 
Nataka kumwambia Rais Kikwete kwamba nchi haiongozwi kwa misuli, haiongozwi kwa kutunishiana misuli. Wanataka kufanya kama walivyofanya majuzi kutunga Katiba Mpya kwa mitutu ya bunduki. 
Sasa tena uchaguzi unakaribia wanaanza maandalizi ya mitutu…tunamwambia Kikwete sisi tutakuwa wa mwisho kuona nchi hii inaingia katika vurugu. Ndiyo maana ili kuepusha mambo mabaya yasitokee kila taarifa kama hii tukiipata tutapiga kelele. Silaha kubwa ya mnyonge ni kupiga kelele. 
Katika mwendo huo huo wa Rais Kikwete kugeuka kuwa Ofisa Manunuzi, sasa amejigeuza kuwa Bwana TCRA, wanapanga kukutana na Kampuni ya HUAWEI ya China ili wanunue mtambo utakaowekwa ikulu kwa ajili ya kunasa simu za akina Dokta Slaa… 
Mitambo hiyo inapelekwa ikulu badala ya…ingepelekwa Usalama wa Taifa ningeelewa, ingepelekwa kwenye Jeshi letu ningeelewa, lakini ikulu? Tunasisitiza hatuna tatizo kama mambo haya ya ndege, helkopta au mitambo ya mawasiliano yangekuwa yanafanywa kwa ajili ya ulinzi na usalama wa nchi, lakini ni tatizo kubwa kama rais ndiye anakuwa Ofisa wa Manunuzi au Ofisa wa Mawasiliano, TCRA. 
Sasa wanatafuta na kuhangaika kutafuta kila njia ya kubaki madarakani. 
Tunamuonya Rais Kikwete kuwa hizo pesa anazotaka kuchezea kwa yeye kuwa Ofisa Manunuzi si za mfukoni mwake. Aache kuchezea fedha za Watanzania. Tulimuonya pia hivi hivi wakati alipochezea fedha za Stimulus Package. Kama anataka kutukamata atukamate lakini sisi tutasema. Haya ndiyo mambo ya madhara ya katiba inayopendekezwa, kama ambavyo tumeshasema vizuri mapema.


























































12 Jun 2014

Wakati taarifa zinatanabaisha kuwa nchi yetu ipo hoi kifedha,

Embedded image permalink

 huku deni la taifa likizidi kupaa, na serikali ikikuna kichwa kutengeneza bajeti ya kueleweka kwa mwaka ujao wa fedha, 

Embedded image permalink
haya ndio matumizi ya viongozi wajuu wa chama Tawala CCM



CHANZO: Jamii Forums

Nakuachia wewe msomaji na kila anayeipenda Tanzania kwa dhati kutoa hukumu hapo mwakani katika uchaguzi mkuu.

6 Mar 2014

Wakati haijafahamika nani aliyelipwa mabilioni ya shilingi yaliyokuwa kwenye akaunti ya Escrow katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kutokana na mvutano baina ya Tanesco na Kampuni ya IPTL, imebainika kuwa Bunge liliwahi kuagiza fedha hizo zisichukuliwe mpaka mitambo ya IPTL itakapokuwa chini ya Tanesco mwakani.
Hiyo imo katika taarifa ya iliyokuwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2007.
Hata hivyo, Gavana wa BoT, Profesa Benno Ndulu alithibitisha jana kuchotwa kwa Dola za Marekani 122 Milioni (Sh195.2 bilioni) katika akaunti hiyo, lakini akakataa kutaja nani hasa aliyelipwa.
Mkataba wa miaka 20 baina ya IPTL na Tanesco ulisainiwa mwaka 1995 na ulitakiwa kuisha 2015 na mitambo hiyo kuwa mali ya Tanesco.
Hata hivyo, ukiwa umebaki mwaka mmoja kumalizika, imebainika kuwa mitambo hiyo imeuzwa kwa Kampuni ya Pan African Power, ambayo inatarajiwa kuingia mkataba mwingine na Tanesco ili iwauzie umeme.
Ndulu alisema fedha zilizokuwa kwenye akaunti hiyo ni Dola za Marekani 22 milioni na Sh161 bilioni za Tanzania ambazo zote kwa pamoja ndizo zilizofikisha jumla ya Sh195.2 bilioni.
Vyanzo vingine vilitoa takwimu mbili tofauti, kimoja kikisema kiasi cha fedha hizo kilifikia Dola za Marekani 270 milioni na kingine Dola 250 milioni. Kuhusu nani mwenye mamlaka ya kutoa fedha hizo, Profesa Ndulu alisema kwa mujibu wa mkataba wa kufunguliwa kwa akaunti ya fedha hizo, ni Wizara ya Nishati na Madini pamoja na IPTL.
“Hakuna mtu mwingine anayeweza kuidhinisha kutolewa kwa fedha hizo zaidi ya hao, kwa hiyo hao ndiyo waliosaini kutolewa kwa hizo fedha na taratibu zote zilifuatwa,” alisema Profesa Ndulu.
Alipoulizwa ni nani aliyelipwa fedha hizo, Profesa Ndulu alisema IPTL ndiyo iliyokuwa na mamlaka ya kusema ni nani alipwe na ilifanya hivyo.
Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi alipoulizwa juu ya fedha hizo alisema: “Kwa kawaida huwa nina majibu mafupi sana, lakini kwa kuwa mmeamua kuandika uongo, endeleeni, siwezi kukujibu chochote wasiliana na hao IPTL wakujibu.”
Hata hivyo, haikuwa rahisi kumpata kiongozi wa IPTL kuzungumzia suala hilo kwa kuwa tayari kampuni hiyo ni mufilisi.
Msimamo wa Bunge
Ripoti ya POAC inasema Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) aliorodhesha matatizo ya mkataba kati ya Tanesco na IPTL na kuangalia mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mipango ya kununua mitambo hiyo na kuibadilisha iwe inatumia gesi badala ya mafuta mazito.
“Mgogoro uliopo hivi sasa kati ya Tanesco na IPTL unahusu kiwango cha malipo ya uwekezaji yaani capacity charges ambacho IPTL walikuwa wanalipwa na Tanesco. Kwa mujibu wa mkataba huo, capacity charge inapaswa kukokotolewa kwa kuzingatia mtaji wa asilimia 30 na mkopo wa asilimia 22.31.
Baada ya uamuzi wa Mahakama ya Kimataifa, ilikubalika kuwa mtaji uliowekezwa uwe ni Dola za Marekani 36 milioni.
Hata hivyo, baada ya uchunguzi wa Tanesco iligundulika kuwa IPTL haikuwekeza fedha hizo, bali Sh50,000,” inasema ripoti hiyo.
Ilisema kuwa, mpaka kufikia Mei 2008, Tanesco ilikuwa imeilipa IPTL Sh221 bilioni tangu ilipoanza uzalishaji umeme Januari 2002.
Kamati iliagiza: “Wanasheria wa Tanesco na Serikali watumie ushahidi wote uliopo kuhakikisha kuwa kiwango cha fedha kilichopo kwenye akaunti maalumu (Escrow) ndicho hichohicho kitumike kumaliza madeni yaliyopo na vilevile kufanyia marekebisho mitambo hiyo ili itumie gesi,” inasema taarifa hiyo.
Pendekezo hilo lilipitishwa na Bunge huku POAC ikitoa maelekezo kwa Gavana Ndulu kuwa fedha zilizopo Escrow zisitumike kwa namna yoyote ile bila mitambo ya IPTL kuwa ya umma na kubadilishwa na kutumia gesi asilia.
Aliyekuwa Mwenyekiti wa POAC, ambaye sasa ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe alisema ameshtushwa na taarifa za kutolewa kwa fedha hizo kinyemela.
“Tunaitaka Serikali kutoa taarifa kama kweli hizo fedha zimetolewa, kwa sasa siwezi kutoa msimamo wetu kwa kuwa hatujakaa kama kamati, tunatarajia kuitisha kikao cha dharura Dodoma kuzungumzia suala hili,” alisema Zitto.
 CHANZO: Mwananchi


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.