17 Jun 2010

Desemba 9 mwakani,Tanzania yetu itatimiza miaka 50 tangu ipate uhuru.Pengine tarakimu 50 inapunguza uzito,kwahiyo ni vema kubainisha kuwa umri huo ni sawa na NUSU KARNE (herufi kubwa kuonyesha msisitizo).Wakati umri huo wa mtu mzima ungepaswa kuwa habari njema,hali ni tofauti kwetu.Tulowakabidhi dhamana ya kutuongoza wanakurupuka na mambo ya ajabu ajabu kana kwamba wako ndotoni au wako kwenye mchezo wa kuigiza usio na ujumbe wowote.

Ngoja niende moja kwa moja kwenye pointi.Hivi Mtanzania mwenzangu inakuingia akilini kweli kusikia kauli kwamba jengo la Bunge letu tukufu "litafanyiwa ukarabati wa kufa mtu" unaotarajiwa kugharimu shilingi bilioni 30.9 "ili kuwawezesha waheshimiwa sana waendane na teknolojia ya kisasa wanapokuwa Bungeni"!!!?Kwa mujibu wa Spika Samuel Sitta mchakato wa ukarabati huo umeshakamilika na unatarajiwa kuanza mara moja,ambapo utapokamilika kila kiti cha mbunge kitakuwa na runinga pamoja na mawasilino ya kisasa ya kompyuta.

Ofkozi,ni muhimu kwenda na wakati katika suala zima la teknolojia lakini pamoja na umuhimu huo shilingi bilioni 30 na ushee ni nyingi mno na tunazihitaji kwenye maeneo mengine yaliyo hio bin taaban kama vile miundombinu,huduma za afya,maji,nk.Hivi kweli runinga kwenye kiti cha mbunge ni muhimu kuliko madawati au nyumba za walimu?Je hizo bilioni 30 zingeweza kujenga zahanati ngapi au visima vingapi vya kuwapatia walalahoi huduma ya maji ya uhakika?

Lakini kabla sijatuliza hasira zangu kutokana na kauli hiyo ya Spika Sitta,JK nae amekuja na mpya akidai kwamba katika miaka mitano ijayo kila mwalimu atakuwa na laptop.Namheshimu sana Rais wangu lakini baadhi ya kauli zake zinanitatiza sana.Hivi kipaumbele katika elimu yetu ya kusuasua ni laptop kwa walimu au makazi bora kwa walimu hao sambamba na kuboreshewa maslahi yao na mazingira yao ya kazi?Mwalimu mwenye laptop anafundishaje wanafunzi waliokaa chini ya mti?Na wakati JK anatoa mpya hiyo hajatuambia umeme wa kuziwezesha laptop hizo utakuwa wa nguvu za jua au zitatumia mafuta ya taa kwani sote tunafahamu uhuni wa TANESCO.


Sijui ni uzembe wa watawala wetu kuelewa matatizo yetu na vipaumbele vyetu kama taifa au ni makusudi tu lakini kwa mwenendo huu itatuwia vigumu kutembea vifua mbele hapo mwakani tutaposherehekea nusu karne tangu tupate uhuru. 

Enewei,hebu soma mazingaombwe hayo HAPA na HAPA.

2 comments:

  1. Kazi tunayo! Kufa hatutakufa ila cha moto tutakiona :-(

    ReplyDelete
  2. Kuishi ama kuendesha shughuli zozote pasipo kuwa na kufanya tathmini wapi tulipo, wapi tunakwenda, nani anatufikisha kwenye malengo yetu, njia zipi zinatumika, na kwanini tunashindwa kufikia malengo....Hilo ndiyo tatizo letu la kudumu kwenye kila asasi zote(kiuchumi, kisiasa na Jamii, watu binafsi. Hivi kweli kama tunataka maendeleo basi CCM kama chama na viongozi wake wamepitwa na wakati kabisa katika karne hii...ushahidi hupo wazi na kila mtu anatambua hilo kitaifa na kimataifa...Hatima ya maendeleo ya Tanzania yapo mikononi mwa watanzania wenyewe kama wanataka maendeleo ama kama walivyoamua sasa kuendelea kuwa maskini wakutupwa....

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.