24 Jun 2011

Waziri Mkuu Pinda akimwaga machozi Bungeni mwaka 2009
Kwa kifupi tu,Jaji mtajwa katika habari ifuatayo hastahili kuendelea na wadhifa wake.Hili ndio tatizo la kuteua majaji weeeengi mpaka wababaishaji kama hawa wanapata fursa.Pia habari hii imenikumbusha lile tukio la Waziri Mkuu Mizengo Pinda kulia Bungeni alipobanwa kuhusu kauli yake kuhusu wauaji wa maalbino (aliropoka kuwa wauaji hao nawe wauawe)

Jaji aangua kilio akijitetea
Thursday, 23 June 2011 21:49

Hadija Jumanne
JAJI Atuganile Flora Ngwale wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam kitengo cha Ardhi, jana alishindwa kujitetea kuhusu kushindwa kwake kujaza fomu zinazohusu mali na madeni yake, kwa mujibu wa sheria ya maadili ya viongozi wa umma.

Jaji huyo alishindwa kufanya hivyo mbele ya Baraza la Maadili ambako aliangua kilio na hivyo kusababisha wanasheria kushindwa kumhoji.

Hali hiyo ililazimisha baraza kusitisha usikilizaji wa shauri hilo.Wakati akiangua kilio, jaji huyo alilieleza baraza kwamba alishindwa kujaza fomu hizo na kuomba msamaha.Wakati akiangua kilio, jaji huo alisema "sina mali yoyote, kazi ndio maisha yangu, watoto wangu wanategemea kazi hii siwezi kudharau mtu, naomba mnisamehe, nimejifunza Mungu wangu,"alisema jaji huyo.

Jaji Ngwale alisimama katika baraza hilo ili kuanza kujitetea, lakini ghafla aliangua kilio kwa sauti ya juu huku akiomba baraza hilo limuonee huruma kwa kutojaza fomu."Ni kweli sijajaza fomu na kama kuna mtu aliniona nimejaza fomu hizi ajitokeze ndani ya baraza hili la maadili," alisema.

"Kazi hii ndio maisha yangu, kazi hii ndio faraja ya watoto wangu hivyo naitegemea sana sina mali zozote za kunitesa na kuniita katika Baraza la Maadili,"alisema Ngwale huku akimwaga machozi.

Baada ya Barazakuona Jaji Ngwale ameshindwa kujitetea kwa njia ya mdomo, lilimtaka atoe utetezi wake kwa njia ya maandishi na kulazimika kusitisha kuendelea na shauri hilo.Mbali na baraza hilo kusitisha kuendelea kusikiliza shauri hilo, pia wanasheria wa sekretarieti ya maadili na hawakupata nafasi ya kumhoji Jaji Ngwale kutoka na hali hiyo.

Baada ya baraza hilo kusitisha kuendelea kusikiliza shauri hilo walimuomba jaji huyo aondoke mbele ya baraza hilo, lakini jaji huyo alikaidi agizo la wanasheria hao na badala yake aliendelea kulia mpaka baraza hilo lilipomuomba mmoja wa wanasheria ambembeleze na baada ya kubembelezwa alikubali kwenda kutoa maelezo yake kwa njia ya maandishi na baadaye aliruhusiwa kuondoka.

Baraza hilo litaendelea leo kwa ajili ya kuhoji watu wanne ambao hawakujaza fomu hizo za maadili ya umma mwaka jana, miongoni mwa watu hao watakaohojiwa ni pamoja na Diwani wa Kata ya Kanazi Mathias Bisoma Mgatta, Mkurugenzi wa Shirika la Hifadhi ya Jamii la Taifa (NSSF), Crecencius Magori.

Wengine ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Tafiki Mwanza, Francis Bayona Katunzi na Diwani wa Mpanda mjini Ally Juma Nsokolo.

CHANZO: Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.