7 Jun 2011


Ama kwa hakika Rais Jakaya Kikwete anaweza kabisa kushinda tuzo ya kuiongozi mbabaishaji aliyepindukia.Hivi inahitaji rocket science kwa mkuu wa nchi kufahamu majina ya viongozi wa dini wanaojihusisha na uuzaji wa madawa ya kulevya,kisha akayakalia majina hayo hadi kwenye halfa ya kidini na kulalamika BADALA YA kuchukua hatua stahili?Hata askari mgambo angeweza kuchukua hatua katika tuhuma kama hii kwa kuliripoti kwa vyombo vya dola.

Kikwete ni mbabaishaji,period.Nasema hivyo kwani hii si mara yake ya kwanza kukurupuka na kauli zake tunazoweza kabisa kuziita za kizushi akidai anawafahamu wahalifu.Mwaka 2006,mara tu baada ya kuukwaa urais kwa nguvu za wanamtandao (ambao baadhi yao leo wanaitwa magamba),Kikwete alifanya kituko kwa kudai sio tu anawafahamu wala rushwa bali anawafahamu kwa majina.Badala ya kuchukua hatua stahili,yeye akatoa deadline kuwa wajirekebishe la sivyo watamwona mbaya.

Ni dhahiri wala rushwa waliamua kumpuuza,na yeye mwenyewe ameamua kupuuza deadline hiyo kwani hadi leo hajaigusia tena.Ukidhani kuwa labda amejifunza lolote kuhusu tabia hiyo ya uropokaji,baadaye alifanya ziara Bandarini Dar na kudai tena kuwa anawafahamu watu wanaosaidia kukwepa ushuru bandarini hapo,na kwamba atawasilisha majina kwa wahusika ili wachukuliwe hatua.Kwa vile ubabaishaji uko damuni kwake,hakuweza kuwasilisha majina hayo wala kuchukua hatua stahili.

Sasa sijui ni kucnganganyikiwa au mwendelezo wa ubabaishaji,safari hii kakurupuka tena na uzushi mwingine akidai kuwa baadhi ya viongozi wa dini wanashiriki kwenye biashara haramu ya madawa ya kulevya.Hivi jamani,Rais mzima anasubiri hadi aalikwe kwenye sherehe ya kidini ndio atangaze kuwa anafahamu viongozi wa dini wanaojihusisha na uhalifu?Ina maana Kikwete hajui majukumu yake kama Rais wa Tanzania ni pamoja na kulinda sheria sambamba na kuchukua hatua dhidi ya wanaovunja sheria (including wazungu wa unga)?

Lakini safari hii,ubabaishaji wake unaweza kumtokea puani baada ya viongozi wa dini kumpa masaa 48 (hadi muda huu yatakuwa yamebaki kama 24 hivi) kuwataja hadharani viongozi hao wa dini anaodai wanashiriki katika biashara ya madawa ya kulevya.Na wamemtega vizuri kwelikweli kwa kumwambia aidha ataje majina hayo ndani ya masaa 48 au jamii imhukumu kuwa ni mnafiki na mzushi.

Soma habari husika hapa chini

JK awapasha viongozi wa dini
• Asema wapo wanaouza dawa za kulevya
na Stephano Mango, Songea

RAIS Jakaya Kikwete, amewaonya viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini nchini kuacha tabia ya kushiriki biashara ya kuuza dawa za kulevya na badala yake washirikiane na viongozi wa serikali kuidhibiti biashara hiyo haramu.

Alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akihutubia waumini wa Kanisa Katoliki Jimbo la Mbinga wakati wa ibada maalumu ya kupewa daraja la uaskofu na kusimikwa kwa askofu wa jimbo hilo, Mhashamu John Ndimbo, katika kanisa la kiaskofu la Mtakatifu Killian iliyohudhuriwa pia na Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamini Mkapa.

Alisema baadhi ya viongozi hao wamekuwa wakishiriki kufanya biashara hiyo ya dawa za kulevya kwa kuwatumia vijana ambao huwafanyia mipango ya kuwatafutia hati za kusafiria (Passport) kwenda nchi za nje.

Badala yake Rais Kikwete amewataka viongozi hao nchini kuikemea biashara hiyo na kujenga uhusiano mzuri na vyombo vya dola katika kuhakikisha biashara hiyo inakomeshwa kwa kuwafichua wahusika wanaoifanya ili wachukuliwe hatua za kisheria.

“Inasikitisha sana na kutisha, biashara hii haramu sasa inawavutia hata watumishi wa Mungu, taifa letu litaharibika tusipokuwa makini katika hili kwani baadhi yenu tumewakamata.

“Kwa kauli zenu kemeeni jambo hili kwa kuelimisha jamii hususan vijana waweze kuepuka na matumizi ya dawa hizi,” alisema Rais Kikwete

Chanzo: Tanzania Daima

Maaskofu CCT wampa Rais Kikwete saa 48 kuwataja Viongozi wa Dini "wauza unga"
06/06/2011

L-R: Kadinali Pengo, Rais Kikwete, Askofu John Ndimbo (picha: C.Sikapundwa)Katika taarifa ya habari iliyosomwa leo saa mbili usiku kupitia kituo cha runinga cha ITV, imetamkwa kuwa Maaskofu wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania, CCT, wamempa Rais Kikwete saa 48 za kuwataja kwa majina viongozi wote wa Dini anaowatuhumu kuhusuka na biashara haramu ya madawa ya kulenya "unga".

Maaskofu hao wamesema endapo Rais atashindwa kufanya hivyo, basi itachukuliwa kwamba siyo mkweli.

Agizo la CCT lilitolewa na Mwenyekiti wake taifa, Askofu Peter Kitula jijini Dar es Salaam katika mkutano na waandishi wa habari linasema, “Tunampa saa 48 rais awataje kwa majina viongozi hao ambao yeye anadai wanajihusisha na kuuza dawa na kama atashindwa kufanya hivyo tunamtafsiri ni mwongo na mzushi... Tunasikitishwa na kushangazwa kwa kauli hiyo na tunamheshimu kama kiongozi wa nchi, hivyo tunampa masaa hayo awataje kwa majina” alisema Kaimu Mwenyekiti wa CCT, Askofu Mokiwa akichangia hoja.

Kauli ya Rais kuhusu viongozi wa dini kuhusika na biashara ya madawa ya kulevya inanukuliwa kuwa ilitamkwa siku ya Jumapili, Juni 5, 2011 wakati akiwa aalipowahutubia waumini wa Kanisa Katoliki la Jimbo la Mbinga wakati wa ibada maalumu ya kuwekwa wakfu na kupewa daraja la uaskofu na hatimaye kusimikwa kuwa Askofu wa jimbo la Mbinga, Mhashamu John Ndimbo.

Misa hiyo ilifanyika katika Kanisa la Kiaskofu la Mtakatifu Killian na kuhudhuriwa na Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa pamoja na mkewe, Anna Mkapa.

Rais Kikwete amenukuliwa na vyombo vya habari (1), (2), (3), (4), (5), (6) ... kuwa alisema ,“Inasikitisha sana na kutisha biashara hii haramu sasa inawavutia hata watumishi wa Mungu, Taifa letu litaharibika tusipokuwa makini katika hili, baadhi yenu tumewakamata,”... “Kauli zenu kemeeni jambo hili kwa kuelimisha jamii hususani vijana waweze kuepuka na matumizi ya madawa ya kulevya.”

Kwamba, baadhi ya viongozi hao wamekuwa wakishiriki kufanya biashara ya madawa ya kulevya kwa kuwatumia vijana ambapo huwafanyia mipango ya kuwatafutia hati na pasi za kusafiria kwenda nchi za nje kufanya biashara hiyo. Rais akawataka viongozi wa dini nchini kuikemea biashara hiyo na kujenga uhusiano mzuri na vyombo vya dola katika kuhakikisha biashara hiyo inakomeshwa kwa kuwafichua wahusika wanaoifanya ili wachukuliwe hatua za kisheria.

Wakahoji, ikiwa Rais anawafahamu viongozi wa dini wanaohusika na biashara ya kuuza "unga" iweje ashinde kuwachukulia hatua za kisheria ikiwemo kuwakamata na kufunguliwa mashitaka?

Walisema viongozi wa dini wanalo jukumu la kutetea na haki mbalimbali za wananchi, na kuionya Serikali pale inapokosea.

CHANZO: Wavuti

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.