9 Sept 2011


Sijui imetokea kwa bahati mbaya tu au makusudi,lakini kuongoza shirika la ndege lisilo na ndege kunaweza kabisa kumtia mtu UCHIZI.Hatimaye Serikali imemteua Bwana Paul CHIZI kuwa Kaimu Mkurugenzi wa ATCL,moja ya mashirika ya ndege vichekesho kabisa duniani.

Tatizo kubwa linaloikabili ATCL ni sawa kabisa na yale yanayoyakabili mashirika mengi mengine yaliyoendelea kuwa chini ya milki ya serikali.Kama ambavyo Tanesco imegeuzwa mradi wa mafisadi,manyang'au wanaendelea kuyanyonya mashirika hayo mithili ya ng'ombe dhaifu ambaye baada ya kuishiwa maziwa sasa anatoa damu.

Huyu CHIZI aliyekubali uteuzi huu atakuwa anaenda kujichukulia mshahara wa bure tu.Yaani Tanzania yetu imekuwa hadhithi nyiiingi lakini utendaji sifuri.Inakera kuona kuna burudani kadhaa zinazoendelea sehemu mbalimbali kusherehekea MIAKA HAMSINI TANGU TUPATE UHURU.Tuwe wakweli,TUNASHEREHEKEA NINI?Miaka 50 ya kuwa na shirika la ndege lisilo na ndege huku wenzetu Wakenya wakitikisha dunia na Kenyan Airways yao?Yani tumepigwa bao hata na nchi iliyo mahututi kiuchumi ya Zimbabwe?

Unajua nini?Laiti huyu Rais wetu mzururaji Jakaya Kikwete angekuwa analazimika kuzurura kwa kutumia ndege za ATCL basi lazima angalau kungekuwa japo na ndege moja ya kumwezesha kutekeleza jukumu lake la kuzunguka dunia.Sawa,tungeendelea kupigia kelele safari hizo lakini angalau pale anapochoka kusafiri ndege husika ingeweza kutumika kwa shughuli za kibiashara.

Lakini mtu huyu ambaye hana idea as to kwanini aligombea kuongoza nchi ni sehemu ya tatizo linaloua mashirika yetu ya umma.Hivi mtu mwenye uchungu na nchi anaweza kumteua swahiba wake mwenye rekodi chafu kufufua shirika kama ATCL?Tusiume maneno,miongoni mwa watu walioisindikiza kaburini ATCL ni pamoja na David Mattaka,ambaye wakati anang'atuka alijigamba kwa MAFANIKIO YA NEMBO MPYA YA ATCL.Hovyooo!

Kama ambavyo wizara mbalimbali za serikali zinavyoendeshwa kwa mtindo wa bora liende ndivyo ambavyo taasisi nyingine za umma zinavyojikuta katika hali hiyohiyo.Rais anateua wazembe kwa vigezo anavyojua mwenyewe.Lakini tutegemee nini kutoka kwa mtu aliyehongwa suti na Waarabu naye akawapa fadhila ya pande la ardhi kwenye mbuga ya wa wanyama?Hata Chifu Mangungo hakuwa mzembe wa kufikiri kiasi hicho.Suti tano kwa ardhi wapi na wapi?

Nimalizie kwa kusema kuwa I can't wait kuona mwaka 2015 unafika na Kikwete anafungasha virago vyake.Lakini ni muhimu kwake kutambua kuwa dunia inabadilika, Tanzania nayo inaweza kubadilika.Japo Kikwete na CCM wanaamini watatawala milele,inawezekana kabisa mwaka 2015 tukashuhudia hadithi tofauti.Sasa aendelee kuomba CCM ibaki madarakani maana itaendelea kumlinda kama yeye anavyomlinda fisadi mwenzie Benjamin Mkapa aliyegeuza Ikulu kuwa sehemu ya biashara huku akiwahadaa wananchi na kauli za "Uwazi na Ukweli." Labda alikuwa anamaanisha uwazi wa afya yake iliyokuwa inashamiri kila kukicha, ukweli kuwa hakuna nchi nyepesi kuongoza (hata kama ni fisadi) kama Tanzania.Lakini hayo yana mwisho,na ikibidi tutaingia kwenye siasa kuhakikisha mwisho huo hauji 2050 bali miaka michache tu ijayo.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.