18 Nov 2013

Kapuya aibua mapya

KASHFA ya kumbaka na kutishia kumuua msichana wa miaka 16, inayomkabili Mbunge wa Urambo Magharibi, Profesa Juma Kapuya (CCM), imeibua mambo mapya.
Wakati serikali inakusudia kufungua mashtaka mawili ya kubaka na kutishia kuua dhidi ya Profesa Kapuya, waziri huyo wa zamani bila woga ameendelea kutuma ujumbe mfupi kupitia simu yake ya mkononi kwa binti huyo na kusisitiza kuwa lazima amuue.
Mbali na kutishia kumuua binti huyo na ndugu yake na mtu mwingine yeyote atakayejitokeza kumsaidia, gazeti hili limenasa baadhi ya mawasilino ya simu za ujumbe mfupi wa kuhamisha fedha kutoka kwa Profesa Kapuya kwenda binti huyo ambaye juzi kupitia baadhi ya vyombo vya habari Kapuya alikana kumfahamu na kwamba hajawahi kukutana naye.
Uchunguzi wetu umebaini kuwa mara baada ya taarifa ya gazeti hili jana kuandika mwendelezo wa kashfa hiyo, huku likimkariri Waziri wa Ushirikiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Samuel Sitta, akihoji ukimya wa serikali katika kashfa hiyo, Profesa Kapuya alituma ujumbe mwingine wa kutishia kumuua binti huyo.
Ujumbe huo kutoka simu namba 0784993930 inayomilikiwa na Kapuya kwenda kwa namba inayomilikiwa na binti huyo, unasomeka hivi:
“Ni lazima nitakuua wewe na ndugu yako na atakaetaka kuwasaidia, huyo Sita asijiingize kwenu, yaani nitakuua tena sijui  leo mtalala wapi! We unadhani nani atakayenifunga? Ndo nishakupa ukimwi, sasa nakutaka uache mara moja kuongea na mtu, nitakuwinda popote tuone!” inasomeka sehemu ya ujumbe huo unaodaiwa kutoka kwa Kapuya.
Ujumbe huo wa vitisho vya kuuawa, unafanana na ule uliokaririwa na gazeti hili ambao pia unadaiwa kutoka kwa Profesa Kapuya kwenda kwa binti huyo anayedai kubakwa na Kapuya.
Sehemu ya ujumbe uliopita unasomeka: “Mkiuawa itakuwa vizuri….itawapunguzia gharama za kuishi; usitake kugombana na serikali mtoto mdogo kama wewe.
“Sisi ndiyo wenye nchi yetu, mwenye hilo gazeti ni Mbowe sasa mwambieni nyumba ya kuishi si mmemuingizia hela leo? Mnatumika tu bure watu wanaingiza hela nyingi, ila mmenitibua lazima niwaue wiki hii haitaisha; nitapiga kambi kote. Jana si walikuficha? Tuone kama utalindwa milele; maana washatengeneza hela lazima mvae sanda  tu hilo sio ombi ni wajibu wenu. Mnajitia na nyie Mafia watoto siyo!!?
“Watoto wetu wanauza unga nani anawakamata? Nani atapingana  nasi!?”
Katika kuthibitisha kwamba Kapuya amekuwa na mawasiliano na binti huyo na kwamba anamjua tofauti na anavyodai kuwa hamjui, gazeti hili limenasa mawasiliano ya kutumiana fedha kutoka kwa Kapuya kwenda kwa binti huyo.
Baadhi ya mawasiliano hayo ni pamoja na yale yaliyofanyika Agosti 31 mwaka huu kupitia simu ya Kapuya ambapo alituma sh 300,000 kwenda kwa binti huyo kama sehemu ya makubaliano ya kutuma pesa kila mwezi kwa ajili ya matunzo.
Mawasiliano hayo ni kama ifuatavyo:
R93NY448 ImethibitishwaUmepokea Tsh505,000kutoka kwa JUMA KAPUYA
Tarehe 21/6/13 saa 11:07 AM
Salio lako la M-PESA ni Tsh 505,000
U26UG365. Imethibitishwa Umepokea Tsh 300,000
kutoka kwa JUMA KAPUYA
Tarehe 31/8/13 saa 3:28 PM
Salio lako la M-PESA ni Tsh 300,000
V04EU470 Imethibitishwa Umepokea Tsh 400,000
kutoka kwa JUMA KAPUYA
Tarehe 24/9/13 saa 2:38 PM
Salio lako la M-PESA ni Tsh 400,040
Tayari serikali kupitia jeshi lake la polisi, limesema linakusudia  kufungua mashtaka mawili dhidi ya mbunge huyo.
Mashtaka yanayotajwa kumkabili mbunge huyo ambaye amepata kuwa waziri katika awamu tofauti za uongozi kuwa ni pamoja na ya ubakaji na kutishia kuua.
Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, aliliambia gazeti hili juzi kuwa jeshi hilo halitakuwa na sababu ya kumuacha mbunge huyo kuendelea kutamba mitaani huku akituma ujumbe wa vitisho kwa binti wa miaka 16  anayedaiwa kumbaka.
Wakati Kamanda Kova akisema hawatakuwa na ajizi na tuhuma za kubaka na kutishia kuua zinazomkabili Profesa Kapuya, Ikulu ya Rais Jakaya Kikwete imekerwa na kauli ya mbunge huyo wa Urambo Magharibi kuwa serikali haiwezi kumfanya jambo lolote.
Pia CCM ambayo baadhi ya maafisa wake walijitahidi kutoa Kapuya kwenye kashfa hiyo, kimeamua kumtosa mbunge huyo aliyewahi kuongoza Wizara ya Elimu na Ulinzi kwa nyakati tofauti baada ya kumtaka aache kukihusisha chama na kashfa yake ya kubaka.
Mbunge  huyo anadaiwa kumbaka binti huyo kwenye hoteli moja ya kitalii iliyoko jijini Dar es Salaam mwaka 2011, na kurudia tena kitendo ndani ya ofisi yake katika Jengo la Biashara Complex lililoko Mwananyamala Juni 3, 2012 alipoitwa kwenda kuchukua ada kwa mara ya pili.
Kutokana na mfululizo wa habari hiyo ambayo imekuwa ikichapishwa na gazeti hili, Profesa Kapuya kupitia kwa wakili wake Yasin Memba, ametishia kuliburuza gazeti hili mahakamani endapo halitamwomba msamaha ndani ya siku saba.
Mbali na kutishia kulipeleka gazeti hili na baadhi ya mitandao ya kijamii mahakamani pia Profesa Kapuya alikana kumfahamu binti anayedai alibakwa huku akikanusha  kumiliki simu namba 0784993930 ambayo imekuwa ikitumiwa kuwasiliana naye ikiwemo kumtumia ujumbe mfupi wa maneno (sms) wa vitisho.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.