13 Mar 2014

NIMEKUTANA na habari ya kushtua inayohusu jaribio la kumdhuru mkuu wa zamani wa Majeshi ya Rwanda, Jenerali Faustine Kayumba Nyamwasa anayeishi kama mkimbizi Afrika Kusini.
Habari hiyo ilieleza kuwa watu sita wametiwa nguvuni wakituhumiwa kuhusika na jaribio hilo, na watatu kati yao ni Watanzania. Nikabaki ninajiuliza, “baada ya Tanzania yetu kuchafuliwa na habari za       Watanzania wanaosafirisha madawa ya kulevya, sasa tumehamia kwenye ku-export (kusafirisha nje) wauaji (assassins)”
Baadaye nikajaribu kuamsha mjadala kuhusu suala hilo katika mtandao mmoja wa jamii (social media), na baadhi ya walioshiriki mjadala huo walionyesha wasiwasi wao iwapo watu hao watatu waliokamatwa ni Watanzania kweli au walikuwa wakitumia tu hati za kusafiria za Tanzania.
Pengine ni mapema mno kufahamu ukweli halisi wa suala hili hasa kwa vile uchunguzi bado unaendelea, lakini kimsingi habari hiyo ni mwendelezo wa ‘sifa zisizopendeza’ zinazoiandama nchi yetu.
Nimewahi kueleza katika makala zangu mbalimbali kuhusu tabia niliyojijengea ya kuanza siku yangu kwa kupitia mitandao mbalimbali ya huko nyumbani ili kufahamu kinachoendelea. Na mara baada ya kumaliza kusoma habari hiyo inayomhusu Jenerali Nyamwasa, rafiki wa zamani wa Rais wa Rwanda Paul Kagame aliyegeuka kuwa mmoja wa mahasimu wake wakubwa, nikakumbana na ‘filamu mbaya’ inayozidi kutawala vichwa vya habari, kuhusu maendeleo ya kikao cha Bunge la Katiba.
Ninaiita filamu mbaya kwa sababu japo vikao vya Bunge letu vimekuwa mahiri zaidi kwa vituko kuliko kuzungumzia masuala lukuki yanayomhusu Mtanzania, kinachoonekana ni kama Bunge la Katiba linajaribu kuchuana na ‘Bunge la kawaida’ kwa vituko.
Na pengine bila kuumauma maneno ni vema nikitanabahisha kuwa kama ilivyo katika vikao vya ‘Bunge la kawaida,’ chanzo kikubwa cha mambo yote ya kukera yanayojitokeza katika Bunge la Katiba ni kasumba ya chama tawala CCM kutanguliza maslahi ya kiitikadi mbele ya maslahi ya Taifa.
Baada ya kumalizika ‘kinyemela’ kwa mjadala mkali kuhusu posho ya wajumbe wa Bunge hilo la Katiba (madai yalikuwa kwamba kiwango cha posho cha shilingi 300,000 kwa siku hakitoshi), suala ‘jipya’ linalotishia hatma ya Bunge hilo ni kuhusu utaratibu wa kupiga kura- iwe siri au ya wazi.
Binafsi ninaunga mkono hoja ya kura ya siri kwa sababu moja ya msingi- katika mazingira ya siasa za vitisho na ubabe, namna pekee mpigakura anaweza kuwa huru kutumia haki yake ya kupiga kura ni kwa kupiga kura ya siri.
Na utaratibu wa kura ya siri umekuwa ukitumika katika ngazi mbalimbali, ndani na nje ya anga za kisiasa. Tunapochagua viranja-iwe shule ya msingi au sekondari, na tunapochagua viongozi vyuoni, kura hupigwa kwa siri. Kisiasa, chaguzi katika takriban ngazi zote-iwe ni udiwani au urais, kura hupigwa kwa siri. Sasa kwanini kwenye suala muhimu la Katiba mpya kura iwe ya wazi?
Nimeeleza kuwa chanzo cha tatizo ni CCM. Na sababu kubwa kwa chama hicho kuwa chanzo cha tatizo ni kasumba iliyozoeleka ndani ya chama hicho tawala kubinafsisha kila suala linalomhusu Mtanzania. Baada ya kuanzishwa mchakato wa kukusanya maoni kuhusu mabadiliko ya Katiba, CCM ikabinafsisha zoezi hilo na kutengeneza ‘rasimu mbadala’ ambayo kwa bahati nzuri ‘ilivuja’ na umma ukapata nafasi ya kutambua hila mbaya za chama hicho.
Kwa CCM, Katiba mpya inapaswa kupatikana kulingana na matakwa ya chama hicho. Na ili matakwa hayo yatimie, ni lazima nguvu, vitisho na hujuma vitumike kuhakikisha kuwa kila mjumbe kutoka chama hicho anatekeleza msimamo utakaolinda matakwa hayo, iwe ni kwa manufaa ya Mtanzania au la. Kuwa na msimamo wa pamoja si vibaya lakini ni muhimu msimamo huo uzingatie matakwa ya wengi.
Lakini kuilaumu CCM kana kwamba ni familia ya mtu mmoja ni kutoitendea haki. Hizo taarifa kwamba kuna baadhi ya wajumbe kutoka chama hicho wamedhamiria kupigania haki zao za kupiga kura kwa utashi wao na si kwa kushinikizwa na ‘msimamo wa pamoja,’ ni ishara tosha kuwa miongoni mwa wana-CCM kuna wanaotaka kuona demokrasia ikizingatiwa sambamba na haki ya kikatiba ya kufanya maamuzi pasipo kuingiliwa na mtu mwingine ilimradi kufanya hivyo hakuvunji sheria za nchi.
Kwa hiyo tunaweza kuilaumu CCM kwa umoja wake lakini ndani yake kuna wenye mtizamo wa kitaifa badala ya kiitikadi.
Lakini kama kuna mtu anayepeswa kubebeshwa lawama zote basi ni Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, ambaye kwa hakika ni kama anapelekeshwa tu  na wanaoitwa ‘wahafidhina’ ndani ya chama hicho.
Tangu mwanzo wa mchakato wa kupata Katiba mpya, Rais Kikwete ameonyesha kuyumba kimsimamo, ambapo mara kadhaa anapozungumzza kama Rais ameonyesha kutambua umuhimu wa zoezi hilo la upatikanaji wa Katiba mpya lilizingatie matakwa ya Watanzania wote pasi kujali tofauti zao za kiitikadi, lakini anapozungumza kama kiongozi mkuu wa CCM anaonekana kutaka kuwaridhisha wahafidhina wanaotamani kuona Katiba mpya ikizingatia matakwa yao binafsi.
Hili limezungumzwa mara nyingi (na kukanushwa mara nyingi pia) kwamba tatizo kubwa linaloathiri utendaji kazi wa serikali ya Rais Kikwete ni ombwe la uongozi. Yeye kama Mkuu wa nchi na Mwenyekiti wa chama tawala akiamua kuwa “ninataka tupate Katiba mpya itakayozingatia matakwa ya Watanzania wote” na itakuwa hivyo.
Lakini hilo haliwezekani kwa sababu upande mmoja, Kikwete anataka kuweka historia nzuri ya kuwaletea Watanzania Katiba mpya inayokidhi matakwa yao, lakini kwa upande mwingine anataka kuwafurahisha wana-CCM wenzie wanaotaka Katiba mpya itokane na matakwa ya chama hicho.
Kama nilivyomuusia katika makala yangu moja ya hivi karibuni, ni muhimu kwa Rais Kikwete kuangalia kalenda na kuhesabu siku zilizobaki kabla hajastaafu. Muda mfupi baada ya kustaafu atakuwa mwananchi wa kawaida tu, na asipokuwa makini, mara baada ya kustaafu anaweza kuandamwa kutokana na maamuzi mabaya yaliyofanyika wakati wa utawala wake.
Ndiyo, Mwalimu Nyerere, na marais wastaafu Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa walishiriki kufanya baadhi ya maamuzi ambayo pengine hayakuzingatia maslahi ya Watanzania wote kwa ujumla- kwa kutanguliza maslahi ya chama tawala pekee- lakini zama za Nyerere, Mwinyi na Mkapa ni tofauti na tulizo nazo sasa.
Japo Watanzania tunasifika kwa ‘upole’ ambao baadhi ya watu wanautafsiri kama ‘ugoigoi wa kuruhusu mambo yasiyofaa yatokee pasi wahusika kuchelea matokeo,’ kizazi hiki cha Facebook, Twitter na nguvu za mitandao ya kijamii, sambamba na jitihada za kuelimisha umma kuhusu haki zake ni tofauti sana na huko nyuma.
Kwa vile kwa hali ilivyo sasa kikwazo kikubwa ni mtizamo fyongo wa CCM kutaka kubinafsisha mchakato mzima wa kupata Katiba mpya, Rais Kikwete ana nafasi nzuri ya kuingilia kati na kuwaelimisha wana-CCM wenzie kuwa “tuache maji yafuate mkondo.”
Ni muhimu kutambua kuwa matakwa ya CCM kung’ang’ania muundo wa serikali mbili (na hili ndilo linalowaogopesha kuhusu kura ya siri) hayawezi kuua dhamira ya wanaotaka Muungano wa serikali Tatu.
Ni lazima Kikwete na CCM wafahamu kuwa moja ya vyanzo vya matatizo ya Muungano ni ‘usiri’ uliotawala katika upatikanaji wa Muungano huo. Usiri huo unathibitishwa na ukweli kwamba wajumbe wa Bunge la Katiba watajadili muundo wa Muungano huo bila kupatiwa ‘Articles of the Union’ (aidha kwa vile nyaraka hiyo haipo au kama ipo, basi ikiwekwa hadharani itazua sokomoko kubwa). Kwanini Turejee makosa hayohayo yanayoufanya Muungano wetu kuwa moja ya kero kubwa za siasa za Tanzania yetu?
Nimalizie makala hii kwa kuueleza bayana kuwa nimeanza kujiandaa kisaikolojia kuona Bunge la Katiba likitafuna mabilioni ya fedha za walalahoi wa Kitanzania na kuishia kuwa kumbukumbu mbaya tu ya vioja, vituko na kila jambo linalozifanya siasa zetu kuonekana za kibabaishaji.
Kama CCM haitoacha ‘uhuni’ wake, na kwa hakika kama Rais Kikwete hatoingilia kati kuhakikisha Katiba mpya yenye kujali maslahi ya Watanzania wote inapatikana, basi labda tutakachoishia kuambulia ni Katiba mpya kwa jina lakini fyongo na isiyo na manufaa kwa Mtanzania.
Mpira upo mezani kwa Rais Kikwete: akitaka asimamie maslahi ya Watanzania bila kujali tofauti ya itikadi zao za kisiasa, tutapata Katiba mpya ya kweli. Aking’ang’ania kutaka kuwaridhisha ‘wahafidhina’ ndani ya CCM, Katiba mpya itabaki kuwa kitendawili.

- See more at: http://www.raiamwema.co.tz/katiba-bora-au-bora-katiba-mpira-mezani-kwa-kikwete#sthash.1H7l4BPB.dpuf

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.