27 Jul 2014

Spy central: The MI5 headquarters near Vauxhall Cross on the River Thames
Jengo la makao makuu ya Idara ya ushushushu ya Uingereza,jijini London
Kuna ukweli mmoja usiofichika wala kupingika kwamba watu wengi sana wanapenda kazi ya ushushushu, yaani Uafisa Usalama wa Taifa.Hiyo sio kwa Tanzania pekee bali sehemu nyingi duniani. Ukiingia mtandaoni utakutana na watu wengi wanaozungumzia taaluma ya intelijensia au/na wahusika katika hali ya kutamani kuifahamu taaluma hiyo nyeti  au kuwa mhusika.

Leo nitaanza mlolongo (series) wa makala kuhusu taaluma hiyo adimu. Hata hivyo ni vema nikatahadharisha mapema kwamba nitakachoandika ni kile tu kinachoruhusiwa kuandikwa hadharani. Kimsingi,taaluma ya ushushushu inatawaliwa na usiri,na mengi ya yanayohusiana na taaluma hayo yanabaki kuwa siri. Hata hivyo,kuna maelezo ambayo yapo wazi japo inahitaji uelewa wa aina flani kuchora mstari kati ya kipi ni siri na kipi ni ruksa kuwa hadharani.

Kwa tafsiri rahisi, ushushushu ni taaluma inayohusu ukusanyaji wa taarifa za kiusalama kwa njia za siri (clandestine methods). Japo kwa kiswahili ushushushu ni intelijensia, kiundani kuna tofauti kati ya ushushushu unaofanyika ndani ya nchi na unaofanyika nje ya nchi.Kwa hapa Uingereza, Idara ya ushushushu inayoshughulika na masuala ya ndani inajulikana kama MI5 na inayohusiska na ushushus nje ya nchi ni MI6.Kwa huko nyumbani, tofauti hizo zipo ndani ya muundo wa taasisi husika, kwa maana kwamba kuna taasisi moja tu lakini ndani yake kuna mgawanyo wa kimajukumu ya ndani na ya nje.

Kadhalika, japo mashushushu wamekuwa wakifahamika pia kama spies, ukweli ni kwamba spy ni shushushu anayefanya kazi nje ya nchi yake,kitu kinachojulikana kiusalama kama ujasusi au espionage kwa Kiingireza.

Japo mataifa mbalimbali yana miundo tofauti ya Idara zao za Usalama wa Taifa,lengo na kazi kuu ni ukusanyaji wa taarifa hizo.Kwa minajili ya makala hizi, nitazungumzia zaidi mazingira ya huko nyumbani Tanzania. Kwa mujibu wa Sheria ya Usalama wa Taifa ya mwaka 1996, Idara yetu ya Usalama wa Taifa ni idara ya serikali iliyo chini  ya Ofisi ya Rais,ambayo ina jukumu la kukusanya na kuchambua taarifa za usalama na kuziwasilisha 'mahala kunakohusika' katika namna ambayo Mkurugenzi Mkuu wa Idara hiyo ataona inafaa.

Kimsingi, mkuu'halisi' wa Idara hiyo ni Rais mwenyewe,ambaye kwa lugha ya kiusalama anafahamika kama 'sponsor.' Wakuu wa Idara za usalama popote pale duniani hufahamika kama spymaster.

Maeneo makuu ya kazi za Idara ya Usalama wa Taifa ni kukusanya na kuchambua habari za kiusalama zinazohusiana na ujasusi (espionage),uzandiki (subversion),uhujumu (sabotage) na ugaidi (terrorism). Lakini jukumu la Idara hiyo si kukusanya taarifa hizo na kuzichambua tu bali pia kuzuwia matukio hayo yanayofahamika kama matishio ya usalama wa taifa.

Ni kwa vile utendaji wa kazi wa Idara yoyote ile ya Usalama wa Taifa unaegemea katika usiri mkubwa ndio maana kwa 'mtaani' kuna hisia tofauti kuhusu umuhimu wa taasisi hiyo. Ukweli ni kwamba laiti umma ungefahamu nini kinafanywa (au kinapaswa kufanywa) na Idara hiyo basi kwa hakika ingethaminiwa zaidi ya kuogopwa tu. Ni muhimu hapa nisisitize kuwa ninazungumzia 'hali mwafaka' yaani kwa Kiingereza ideal situation. Hivi karibuni kumekuwa na malalamiko mengi miongoni mwa wananchi wakiishutumu Idara yetu ya Usalama wa Taifa kuwa imeleemea mno kwenye siasa hasa kuibeba CCM,imezembea mno kiasi cha kuruhusu ufisadi kushamiri, na imekuwa ikilaumiwa pia kutokana na matukio mbalimbali yanayotishia usalama wa Taifa kama vile ugaidi.

Wanaotoa lawama hizo wapo sahihi kwa kiasi flani,kwani  kushamiri kwa maovu katika jamii sambamba na mwendelezo wa matukio yanayotishia usalama wa taifa ni viashiria kuwa Idara ya Usalama ya nchi husika ina mapungufu kiutendaji.

Hata hivyo,ni muhimu kutambua kanuni moja muhimu ya ufanisi au kushindwa kimajukumu kwa Idara ya Usalama wa Taifa popote pale.Ni kwamba wakati Idara husika inapaswa kuwa macho katika kila sekunde kuzuwia matendo ya kidhalimu, wanaopanga kufanya matendo hayo wanahitaji mara moja tu kufanikisha azma yao.Mfano halisi ni kwenye matukio ya ugaidi. Wakati gaidi anahitaji fursa moja tu kufanikisha tukio la kigaidi, Idara ya Usalama inahitaji kila fursa- kila sekunde,dakika,saa,siku,wiki,mwezi,mwaka-kuhakikisha gaidi hafanikiwi.

Kadhalika, wakati inaweza kuwa rahisi kuilaumu Idara ya Usalama wa Taifa inaposhindwa kuzuwia tukio flani, kwa mfano shambulio la kigaidi nchini Kenya, kiuhalisi suala zima la ukusanyaji wa taarifa za kiusalama ni gumu mno. Hebu pata picha: unaletewa tetesi kuwa kuna mtu anataka kulipua bomu kanisa au msikiti. Mara nyingi tetesi hizo huwa hazibainishi jinsia ya mtu huyo,wajihi wake,ni mwenyeji au mgeni na vitu vingine muhimu vya kuweza kumtambua japo kwa ugumu. 

Kutokana na ugumu wa zoezi la kukusanya taarifa za kiusalama,ndio maana wahusika-mashushushu/maafisa wa Idara ya Usalama wa Taifa-wanapaswa kuwa watu wenye akili isiyo ya kawaida, au angalau wenye uwezo mkubwa wa kutumia akili.Neno lenyewe intelijensia linahusiana na matumizi ya akili.Lakini si akili tu, bali pia maafisa usalama wa taifa hupaswa kujifunza na kuendeleza hisia ya sita (6th sense). Mwanadamu wa kawaida ana hisia 5: HARUFU  kwa kutumia pua; LADHA kwa kutumiamdomo/ulimi, KUGUSWA (touch) kwa kutumia ngozi, KUONA kwa kutumia macho, KUSIKIA kwa kutumia masikio. Lakini kwa mashushushu wanapaswa kuwa na hisia ya ziada ya kutambua kitu zaidi ya kutumia hisia hizo 5 kuu. Si kazi rahisi hata kidogo.

Basi kwa leo niishie hapa.Nitaendelea na mfululizo wa makala hizi angalau kila wiki. Usikose kutembea blogu hii kupata habari na makala zaidi kuhusu taaluma hii nyeti ya ushushushu kwa kubonyeza hapo juu ya blogu kwenye seksheni ya INTELIJENSIA 



0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.