21 Oct 2015



Sababu Tisa kwanini CCM itashinda katika Uchaguzi Mkuu Jumapili hii, Oktoba 25

Na January Makamba

Tarehe 25 mwezi huu Oktoba, Watanzania watapiga kura kumchagua rais wao wa tano, wabunge na madiwani. Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu umekuwa na msisimko mkubwa zaidi tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1995. Mengi yamendikwa kuhusu uchaguzi huu, hususan kutokana na hisia kwamba safari hii Upinzani una nafasi ya kukiondoa madarakani moja ya vyama vikubwa na vyenye muundo bora barani Afrika, chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM). Matukio mbalimbali kuelekea uchaguzi huo yameleta shauku inayoweza kutengeneza hadithi ya kusisimua.

Nikiwa sehemu ya Timu ya Kampeni ya CCM,na kwa manufaa ya wote ambao wangependa kuwa na mtizamo tofauti, ninatoa sababu 9 kwanini tunaamini kuwa CCM itaibuka mshindi na kwanini Dkt John Pombe Magufuli atakuwa Rais ajaye wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

1.    Ugombea ‘fyongo’ (flawed) wa Edward Lowassa

Ilishabainika kuwa uchaguzi huu ungekuwa mgumu kwa CCM bila kujali nani angekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Upinzani. Lakini matokeo ya uchaguzi huu yalielemea upande wa CCM pale Upinzani ulipomchagua Lowassa kuwa mgombea wao. Ni rahisi kwa CCM kuchuana na Lowassa kuliko laiti mgombea wa Upinzani angekuwa Dkt Wilbrod Slaa, ambaye ndiye aliandaliwa kuwa mgombea kabla ya ‘ukusukumwa kando’ na nafasi hiyo kupewa Lowassa. Slaa alikuwa na uadilifu katika maeneo mengi, na aliaminika. Kwa Lowassa, ni vigumu na inanyima raha kuchuana na mfumo aliyoshiriki kujenga na ambao ulikuwa sehemu ya maisha yake hadi Agosti mwaka huu alipohamia Upinzani. CCM ilikuwa na nafasi ya kumpitisha Lowassa kuwa mgombea wake wa nafasi ya urais. Hatukufanya hivyo kwa sababu rahisi tu kwamba ingekuwa vigumu mno kumkabidhi kwa wananchi mgombea wa matarajio ya baadaye ambaye ni kiashirio cha yale yasiyowaridhisha wananchi kuhusu CCM. Kuna wanaoamini kuwa uchaguzi huu ni mgumu kwa vile Lowassa ndiye mgombea wa Upinzani. Sisi twaamini kwamba uchaguzi huu ungekuwa mgumu mara kumi zaidi laiti Lowassa angekuwa ndiye mgombea wetu.

2.    Upinzani umesalimisha ajenda yake ya kupinga ufisadi

Kipindi cha miaka 10 iliyopita kimetawaliwa na matukio mbalimbali ya kuwabainisha mafisadi na kuwachukulia hatua. Vyombo vya habari, taasisi za kiraia na Bunge vimefanya kazi nzuri kushughulikia suala hilo. Rais Jakaya Kikwete ameweka historia kwa kuamuru ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kupatikana kwa wananchi na kujadiliwa kwa uwazi Bungeni. Waziri Mkuu aliyekuwa madarakani, si mwingine bali Lowassa, alijiuzulu kwa sababu ya kashfa ya rushwa. Mawaziri kadhaa walitimuliwa kazi na manaibu waziri wawili wanatumikia vifungo jela. Huu ni uwajibikaji wa hali ya juu japokuwa kuna wanaoweza kudhani ni hatua ndogo. Umma umeamka.

Upinzani ulijenga hadhi yake kwa kuongelewa sana kuhusu ufisadi. Kilele cha Upinzani kilijiri mwaka 2007 katika mikutano mkubwa wa hadhara ambapo walitangaza majina 10 ya watu waliowaita mafisadi wakubwa zaidi, katika kilichokuja kufahamika kama Orodha ya Aibu (List of Shame). Lowassa alikuwa kinara kwenye orodha hiyo.

Ilitarajiwa kuwa Uchaguzi Mkuu huu uwe ‘hukumu’ kwa CCM kuhusu ufisadi. Upinzani ulitarajiwa kuitumia ajenda ya ufisadi ambayo inawagusa watu wengi. Lakini ghafla, kwa kumteua mwanasiasa, ambaye kwa jitihada zao wenyewe Wapinzani,  amefahamika zaidi kwa ufisadi, iliwalazimu kuzika ajenda hiyo. Kilichofuata baada ya hapo ni kituko na kichekesho. Wale mashujaa wa mapambano dhidin ya ufisadi walijikuta wakilazimika ‘kulamba matapishi yao.’ Wengi wao waliokuwa mahiri katika mitandao ya kijamii walilazimika kufuta historia ya baadhi ya waliyoyaandika mtandaoni walipokuwa wakikemea ufisadi, lakini si kabla ya maandiko yao kunaswa kwa ‘screenshots.’ Ulikuwa ni ukweli wa kushangaza. Ni Dkt Slaa na Professa Ibrahmi Lipumba, viongozi muhimu wa Upinzani tangu miaka ya Tisini, walioamua kujiuzulu nyadhifa zao kwa kukerwa na uamuzi wa Upinzani kumpokea Lowassa.Matokeo yake, Upinzani walijikuta wakichana kadi yao turufu- ajenda dhidi ya ufisadi. Ni nadra kwao kuongelewa suala hilo, na wanapojaribu kufanya hivyo, ni kwa kujitetea tu.

Jioni moja mwezi Agosti, nilimwona Mbunge wa Upinzani, Peter Msigwa, katika mdahalo kwenye runinga. Aliongelea kitu ambacho kilijumuisha mtizamo wa Upinzani kwa muda huo, na kiliniacha hoi. Alisema, kabla hawajampokea Lowassa, walifanya utafiti wao, na “ufisadi sio ajenda muhimu kwa taifa letu.” Alidai kwamba wenye ushahidi kuhusu ufisadi wa Lowassa wajitokeze hadharani.Alionekana kusahau kuwa walipomtaja Lowassa katika List of Shame, walitangaza hadharani kuwa wana ushahidi. Muda si mrefu uliopita, CCM ilikuwa ikiwaomba Wapinzani kuleta ushahidi kila yalipojitokeza madai ya ufisadi dhidi ya viongozi wa chama na serikali allegations were leveled against the party and its leaders. Haikupendeza kuingiza hoja za kisheria katika masuala ya kimaadili. Upinzani sasa umeamua kwa hiari yao kuchukua ‘chembemoyo’ wakati ambapo viongozi wa CCM wanaongelea ufisadi kwa ujasiri na msisitizo.

Uchaguzi huu Mkuu ni muhimu sana kwa Upinzani. Kimsingi, unaweza kuwa na madhara makubwa. Endapo watashindwa hapo Jumapili, ‘watapotea’ kwa muongo mzima ujao. Ndio maana inashangaza kuona wamechukua uamuzi wa kukimbia ajenda yao kuu ya kupambana na ufisadi  ambayo iliwatambulisha na kuwaimarisha. Na kuwapa nguvu kukubalika kwa wapigakura. Kuona wanatarajia kushinda ni miujiza mkubwa.

3.    Mabadiliko ambayo kamwe huwezi kuyaamini

Ukizinguka jijini Dar es Salaam utakutana na mabango ya Upinzani yanayodaia “Ni Muda wa Mabadiliko.” Lakini ukisikiliza mikutano yao ya kampeni, ni porojo na hasira tu. Wasemaji wakuu katika mikutano hiyo ni Waziri Mkuu wa zamani na kada wa muda mrefu wa CCM, Frederick Sumaye na Lowassa mwenyewe. Kwa pamoja, wamekuwa wana-CCM na katika nyadhifa  za juu serikalini kwa zaidi ya miaka 50. Kwa hiyo inasikitisha kusikiliza kauli zao – zinazokosa imani na kupalizwa na aibu – wakipambana na mfumo walioshiriki kujenga, uliojenga tabia zao za kisiasa, na ambao walikuwa wakiusifu miezi mwili tu iliyopita.
Kutokuwa wakweli na kuweka mbele maslahi binafsi kwawatuma kudai kuwa CCM haijafanya chochote katika miaka miaka 50 iliyopita. Inapotokea viongozi wawili waandamizi wa chama na serikali  kwa zaidi ya miaka 30, wote wakiwa walioshika Uwaziri Mkuu, kudai kuwa hakuna chochote kilichofanyika katika miaka 50 iliyopita, wajihukumu wenyewe. Si kwa muundo, mwonekano au ukweli, wanasiasa hao wanasimamia mabadiliko. Yayumkinika kuhitimisha kuwa mabadiliko wanayoongelea ni kuhusu kubadili chombo kilichowaingiza madarakani, mabadiliko ya sare tu za chama. Hawana habari na mabadiliko ya maisha ya wananchi wa kawaida. Wapigakura wameanza kushtukia ukweli huo.

4.    Migogoro na mkanganyiko ndani ya UKAWA

Huko nyuma, kila ulipojiri uchaguzi, Upinzani ulijaribu kuunganisha nguvu ili kuing’oa CCM madarakani.Na kila mara jitihada za ushirikiano zilishindikana. Mwaka 2014, mjadala kuhusu Katiba Mpya kuataka serikali tatu uliwapatia ajenda ya kuwaunganisha pamoja. Kisha wakaamua kutafsiri ushirikiano huo kuwa wa kisiasa, wakaafikiana kusimamisha mgombea mmoja katika nafasi ya urais na kugawana majimbo.

Baada ya hapo kukajitokeza unafiki wa wazi. Kuonyesha kuwa matamanio yaliwekwa mbele ya kanuni zilizopatikana kwa jitihada ngumu, chama ambacho jina lake linajumuisha maneno ‘demokrasia’ na ‘maendeleo’ kilitemea mate mchakato wake chenyewe wa kidemokrasia na mshikamano kupata mgombea wake wa urais, na kukurupuka kumpitisha kada wa muda mrefu wa CCM ambaye jitihada zake kuwania urais kwa tiketi ya chama hicho tawala ziligonhga mwamba.

Waliamini kwamba uamuzi wa Lowassa kuhama CCM ungekiathiri chama hicho tawala, wakitarajia vigogo kadhaa wangemfuata huo Upinzani. Badala yake, ujio wake huko ukapelekea kuondoka kwa wanasiasa wawili waliokuwa nguzo muhimu kwa Upinzani, Dkt Slaa na Prof Lipumba.Kadhalika, wanachama wengine muhimu waliohama na kujiunga na chama cha ACT- Wazalendo, ambacho hakikujiunga na UKAWA.
Kana kwamba hiyo haitoshi, makubaliano ya UKAWA kusimamisha mgombea mmoja  kila jimbo yalikumbwa na mushkeli katika majimbo kadhaa na kupelekea malalamiko yaliyosababisha ugumu katika kampeni za Lowassa.

Huko Masasi, mgombea mwenza wa Lowassa, Juma Duni, alilazimika kuokolewa jukwaani baada ya waliohudhuria mikutano wake wa kampeni kupiga kelele kuwa wataipigia kura CCM. Katika jimbo la Nzega, Lowassa alilazimika kuendesha ‘kura ya sauti’ kuwauliza waliohudhuria mikutano wake wa kampeni wanamhitaji mgombea gani kati ya wawili wa UKAWA waliokuwa wanachuana. Mpango mzima wa ushirikiano miongoni mwa vyama vinavyounda UKAWA umekwenda mrama.CCM sasa ipo katika nafasi nzuri ya kujinyakulia majimbo ambayo vinginevyo yangekwenda kwa wagombea wa Upinzani.

Lakini kilele cha unafiki wa UKAWA ni hiki. Umoja huo uliundwa ili kutetea Katiba Pendekezwa iliyoshauri muundo wa Muungano wa serikali tatu. Kanuni hiyo ya msingi iliwekwa kando pale UKAWA walipomchagua mgombea wao wa tiketi ya urais, Lowassa, ambaye alikuwa mtetezi mkubwa wa muundo wa Muungano wa serikali mbili. Kwa wengi wasioendeshwa na propaganda, uamuzi wa kutelekeza suala la msingi lililopelekea umoja wa vyama hivyo, kwa ajili tu ya imani ya kufikirika ya kushinda urais, yaashiria uchu wa madaraka na sio mabadiliko yanayohubiriwa kwa wananchi.


5.    Lowassa kushindwa kufanya kampeni nchi nzima

Lowassa anaonekana kutokuwa na uwezo wa kusafiri kwa urefu na upana wa Tanzania kufanya kampeni. Mara nyingi amekuwa akitumia usafiri wa anga kwenda mikoani ambako hufanya mikutano mikubwa kwenye makao makuu ya mikoa, kutembelea majimbo mawili au matatu ya jirani kwa helikopta, na kurejea jijini Dar es Salaam. Huko Tanga, kwa mfano, alifanya kampeni katika majimbo matatu tu kati ya tisa mkoani humo. Mkoani Ruvuma, alifanya kampeni katika majimbo matatu kati ya tisa, Kigoma majimbo mawili kati ya manane, na Kagera majimbo matatu tu.

Kinyume chake, mgombea wa CCM, Magufuli amekuwa barabarani tangu Agosti 23, huku akipumzika kwa siku tatu. Anatumia usafiri wa gari, akitembelea kijiji baada ya kijiji, na kufanya mikutano kati ya minane hadi 12 kwa siku. Aina hii ya kufanya kampeni ‘kwa rejareja’ inabaki kuwa nguzo pekee ya kujihakikishia ushindi kwenye uchaguzi mkuu nchini Tanzania, hususan katika maeneo ya vijijini ambayo usikivu na kuonekana kwa vyombo vya habari ni mdogo. Wakati Lowassa anavutia wahudhuriaji wengi katika mikutano yake katika miji mikubwa, Magufuli anajipatia wahudhuriaji wengi katika kila kona ya Tanzania. Kama idadi ya wahudhuriaji katika mikutano hiyo ya kampeni inamaanisha wingi wa kura, basi kwa hakika CCM itashinda. Lakini tofauti na Upinzani, CCM haidanganyiki na wingi huo wa wahudhuriaji katika mikutano ya kampeni. Rekodi ya mahudhurio makubwa ilikuwa ikishikiliwa na Agustino Lyatonga Mrema, mgombea maarufu wa kiti cha urais kwa tiketi ya Upinzani mwaka 1995 (ambaye pia alijiunga na Upinzani akitokea CCM). Hata hivyo alishindwa kwenye uchaguzi huo. Sie twategemea kitu kingine.

6.    Mfumo imara wa CCM katika uhamasishaji kuanzia ngazi ya chini kabisa.

Katika Tanzania, vyama vichache mno vinavyoweza kuchuana na uwezo wa CCM kuhamasisha wananchi. Wakati Wapinzani huhadaiwa na ‘mahaba’ wakati wa kampeni za uchaguzi, mahudhurio makubwa kwenye mikutano yao ya kampeni na vichwa vya habari magazetini, CCM hutumika nguvu yake ya kimuundo na kuwasha ‘mashine zake za kisiasa,’ kuanzia ngazi ya mtaa (ujumbe wa nyumba kumi) kwa nchi nzima. Kimuundo, jumiya ya wanawake wa CCM (UWT) pekee ni kubwa kuliko Chadema, chama kikuu cha upinzani. CCM Haihitaji kusafiri ili kufanya kampeni. CCM ipo kila mahala, ikifanya kampeni katika makundi madogo, vijijini na mitaani, kila siku na mbali ya upeo wa vyombo vya habari. Kwa wanaofahamu muundo wa chama hicho, ushindi kwake si jambo la kushangaza.

Kwenye miaka ya 1950s, wakati wa harakati za kusaka uhuru kutoka kwa mkoloni, uwezo wa TANU kuhamasisha ulikuwa nguzo muhimu kwa Tanganyika kupata uhuru wake.CCM imerithi vinasaba vya TANU. Mwalimu Nyerere aliijenga CCM kuwa imara kwa nyakati kama hizi. Mwaka jana, huku umaarufu wake ukiwa umepungua, CCM ilimudu kushinda uchaguzi wa serikali za mitaa kwa asilimia 80 dhidi ya umoja Huohuo wa Upinzani inaokabilina nao katika uchaguzi huu Mkuu.Tofauti haipo kwenye nini kinachoonekana kwenye vyombo vya habari au mitandao ya kijamii bali jinsi gani makada wa chama hicho tawala walivyofanya uhamasishaji katika kila mtaa na kijiji. Uchaguzi huo wa serikali za mitaa, ambao hufanyika mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu, hutoa dalili nzuri kuhusu matokeo ya uchaguzi mkuu.

7.    Umahiri wa Dkt Magufuli

Mwaka jana, baadhi ya waandishi wa habari walikiri kwamba ni vigumu mno kumshambulia na kumshinda Dkt Magufuli. Ana rekodi imara ya usafi, uchapakazi na anayetaka kuona matokeo sahihi. Hajawahi kuvutiwa na harakati za kisiasa, na ilikuwa mshangao alipotangaza kuwania urais. Na alipotangaza, hakufanya mbwembwe wala kijitangaza kwenye vyombo vya habari. Alizingatia kanuni za chama kwa ukamilifu. Dkt Magufuli analeta kumbukumbu za mgombea mwingine aliyekuwa hajulikani mwaka 1995 -  Benjamin Mkapa. Wakati umaarufu wa CCM ukiwa chini, huku ikikabiliwa na upinzani kutoka kwa Naibu Waziri Mkuu aliyehama kutoka chama hicho tawala, CCM ilimchagua turufu yake ambayo ilikuwa ngumu kuikabili.Miaka 20 baadaye, ikikabiliwa na upinzani wa Waziri Mkuu maarufu wa zamani aliyehama chama hicho na kujiunga na Upinzani, CCM imefanya tena ‘vitu vyake.’ Siku zote, CCM hujua ‘kufanya pigo la haja.’

8.    Ufanisi wa CCM katika maeneo ya vijijini

Mimi ni Mbunge wa jimbo lisilo mjini, lenye idadi ya wastani ya wapigakura. Mwaka 2010, katika uchaguzi ulionekana kuwa mgumu, CCM ilishinda jimbo langu kwa asilimia 80., na kitaifa kwa asilimia 61. Hivi sasa, tunatarajia ushindi wa CCM kuwa wa asilimia 90 hivi. Tanzania ina  majimbo kadhaa yaliyo kama jimbo langu. Upinzani hupenda kuwapuuza wananchi katika majimbo yasiyo ya mijini, kama jimbo langu, kwa kudai kuwa wanaichagua CCM kutokana na ujinga wao. Wasingeweza kukosea zaidi ya hivyo.

Popote walipo, watu hupiga kura kulingana na mahitaji yao. Mwaka 2000, vijiji vinne tu katika jimbo langu ndivyo vilikuwa na umeme. Leo, vijiji 44 vina umeme. Japo hatujaweza kutoa huduma zote kwa kiwango cha kumfurahisha kila mtu, lakini hali halisi yaonyesha wingi wa wanafunzi mashuleni, walimu zaidi, madaktari na manesi zaidi, zahanati nyingi zaidi zimejengwa, huduma za mawasiliano ya simu zinapatikana kwa wingi, barabara nyingi za lami, nk. Porojo kuwa hakuna kilichofanyika Kwahiyo wapigakura wasiichague CCM haieleweki katika maoneo hayo ambay kimsingi ndiyo yenye wapigakura wengi. Na wagombea wa CCM wanaposema watafanya zaidi ya waliyokwishafanya, kwa kuzingatia mafanikio yaliyokwishapatikana, wananchi wanawaamini. Hotuba za kampeni ni mwonekano na mantiki.

Chaguzi sio kuhusu ahadi tu bali jinsi gani ahadi hizo zitaandaliwa na kutekelezwa. Jukwaa ambalo kila chama kitanadi ajenda zake za uchaguzi hujengwa wakati wa uzinduzi wa kampeni za chama husika. Yahitaji mtu kuangalia tu uzinduzi wa kampeni za za Lowassa na Magufuli. Lowassa aliongea kwa dakika 9 tu  - akiahidi, pamoja na mambo mengine, kuwaachia huru wabakaji (sio kama ninazusha hili) wanaotumikia vifungo vyao na watuhumiwa ugaidi wanaosubiri kesi zao. Bila kujali alikuwa na malengo gani wakati anatoa ahadi hizo, makosa hayo hayastahili msamaha wa rais.  Kwa upande wake, Magufuli aliongea kwa dakika 58, akielezea kwa undani ajenda za maendeleo katika nyanja za elimu, ajira, afya, ufisadi, huduma za maji, na miundombinu. Kuanzia hapo, kwa muda wote wa kampeni, mwenendo umekuwa hivyo, kwa uzito wa ujumbe kwenye hotuba zake na muda wa kuhutubia

Wanaohudhuria mikutano ya Dkt Magufuli huondoka katika mikutano hiyo wakiwa na matumaini na wenye nguvu. Kwa upande mwingine, wahudhuriaji katika mikutano ya Lowassa huondoka wakiwa wamekanganywa. Siku ya kupiga kura, wapigakura wanamkumbuka jinsi mgombea alivyoonekana na alivyoongea, na jinsi walivyojisikia walipomwona jukwaani. Kwa kigezo hiki, ni bora ningekuwa upande wa Magufuli.  

9.    Uongo, uongo na takwimu

Tanzania haina utamaduni wa kura za maoni kupima nafasi za wagombea katika uchaguzi. Tuna utaratibu wa muda mrefu wa kupata maoni ya wananchi katika maamuzi makubwa ya kisera – kuingia mfumo wa vyama vingi vya siasa, marekebisho ya Katiba, na kadhalika. Mwaka 2005, kulifanyika kura ya maoni, iliyobashiri ushindi mkubwa kwa CCM. Na kwa hakika, CCM ilishinda kwa asilimia 80. Mwaka 2010, kura ya maoni iliyoendeshwa na kampuni ya Ipsos-Synovate iliashiria kuwa idadi ya kura za CCM ingepungua hadi kufikia asilimia 61. CCM ilipinga matokeo ya kura hiyo ya maoni ikidani kuwa yalikuwa kiasi kidogo sana. Matokeo ya uchaguzi huo yalikuwa kama yalivyotabiriwa katika kura hiyo ya maoni. CCM ilipata asilimia 61 ya kura zote.

Hivi karibuni, kura mbili za maoni zilichapishwa. Zote zilifanywa na taasisi huru zinazoheshimika. – Twaweza and Synovate-Ipsos tena- zote zikijihusisha na utafiti wa kusaka maoni. Taasisi mbili tofauti, zilizotumia mbinu tofauti za kufanya utafiti, katika nyakati tofauti, matokeo yaleyale. CCM itashinda kwa asilimia 62 ya kura zote.

Inaruhusiwa, na kwa yumkini ni jambo zuri, kupingana na sababu hizi tisa za kwanini CCM itashinda. Lakini namba zina tabia ya ukandamizaji. Ndio mwelekeo wa kura huwezi kubadilika. Lakini kwa kuzingatia yote yaliyokwishaongelewa kuhusu kinachodaiwa kuwa ufuasi mkubwa kwa Upinzani, basi muda huu ingetarajiwa tuwa tunajadiliana kuhusu ufuasi wa wengi kutoka Upinzani kuelekea CCM– na sio kutarajiwa ufuasi wa wengi kutoka CCM kuelekea Upinzani. Na ndiyo, kura za maoni zaweza kukosea, na tusiwekee mkazo sana.Lakini hoja hii sasa ndiyo hupendelewa zaidi na upande unaelekea kushindwa kwenye uchaguzi.


January Makamba ni Mbunge wa Bumbuli (CCM), Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, na msomaji wa Kampeni za CCM 

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.