Showing posts with label LOWASSA. Show all posts
Showing posts with label LOWASSA. Show all posts

10 Jan 2018

Image result for magufuli lowassa
Jana Januari 9, 2018, wiki moja na siku mbili baada ya kuanza kwa mwaka huu mpya, duru za siasa za Tanzania zilitikiswa na habari kuhusu kiongozi maarufu wa Chadema, Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kukutana na Rais John Magufuli kwa “mazungumzo”, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Baada ya “mazungumzo” hayo Lowassa alimmwagia pongezi Magufuli kwa kile alichokiita “kazi nzuri anayoifanya” na kutaja mafanikio katika sera ya elimu bila malipo, ujenzi wa mradi wa uzalishaji wa umeme katika maporomoko ya mto Rufiji (Stiegler’s Gorge), na ujenzi wa viwanda na ujenzi wa reli ya “standard gauge”.

Nimepata faraja sana kuja hapa Ikulu kuonana na Mheshimiwa Rais, tumezungumza nae na nimempongeza kwa kazi nzuri anayoifanya, lazima tukiri anafanya kazi nzuri na anahitaji kutiwa moyo,” alinukuliwa Lowassa aliyejiunga na Chadema miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 baada ya ndoto zake kuwania urais kwa tiketi ya CCM “kuota mbawa.”


Image result for magufuli lowassa

Mwanasiasa huyo ambaye baada ya kujiunga na Chadema alipitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya muungano wa vyama vinne vya upinzani – Chadema, CUF, NCCR Mageuzi na NLD – uliofahamika kama UKAWA, aliendelea kusema kuwa “Moja kubwa ambalo ni la msingi sana ni la kujenga ajira, katika kuanza ujenzi wa reli ya kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro hapo anajenga ajira, na kwenye nchi yoyote inayoendelea suala muhimu ni kujenga ajira, Stiegler’s Gorge ni kujenga ajira na mingine ya aina hiyo, lazima kuwepo na kipaumbele cha kusema kwamba tunajenga ajira. Jingine ni la elimu, ni muhimu sana, hauwezi kuacha elimu katika mambo yako unayofanya, hili nalo lazima lisemwe vya kutosha, kwa kweli nakushukuru Mheshimiwa Rais, you made my day.

Rais Magufuli kwa upande wake alimpongeza Lowassa kwa kile alichokiita “kutambua kazi kubwa inayofanywa na Serikali” na kumtaja Lowassa kama mmoja wa viongozi ambaye kwa wakati wake alitoa mchango wake katika nchi.

Magufuli alimmwagia sifa Lowassa akidai kuwa “ni mwanasiasa mzuri kwani hata wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita ambao naye aligombea kiti cha Urais, hakuwahi kumtukana.”

Mheshimiwa Lowassa ameniomba mara nyingi nikutane nae, na leo nimekutana nae, tumezungumza mambo mengi, ameniambia ya kwake na mimi nimemwambia ya kwangu. Kwa ujumla Mheshimiwa Lowassa ni mwanasiasa mzuri na tuendelee kuwaenzi wazee hawa ambao kwa nyakati fulani walifanya mambo mazuri, na mimi napenda kumpongeza Mhe. Lowassa ambaye kama alivyosema hapa kuwa tumefanya mambo mazuri mengi,” alisema Rais Magufuli

Ametaja miradi mbalimbali tunayotekeleza, ametaja mradi wa Stiegler’s Gorge utakaogharimu zaidi ya Shilingi Trilioni 7, amezungumzia juu ya elimu bure, amezungumzia juu ya maji ambayo kwa bahati nzuri yeye alikuwa Waziri wa Maji na anafahamu sasa tumefikia wapi, amezungumza juu ya umeme tulivyosambaza katika vijiji mbalimbali, elimu bure, huduma za hospitali na mengine” aliongeza Rais Magufuli.

Kwanza, ni muhimu kutambua kuwa kama Mtanzania yeyote yule, Lowassa alikuwa na kila haki ya kukutana na Rais wake. Kadhalika, kama mmoja wa viongozi wakuu wa upinzani, isingepaswa kuwa jambo la kushangaza kwa viongozi hao wawili kukutana.

Hata hivyo, Lowassa sio tu amekutana na Magufuli, bali pia ammemwamgia sifa. Je ni dhambi kwa kiongozi wa chama cha upinzani kumwagia sifa Rais aliyepo madarakani? Jibu lingepaswa kuwa “si dhambi,” laiti uhusiano kati ya Rais Magufuli, serikali yake na taasisi zake (kama vile jeshi la polisi, Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa), watendaji wa serikali (hasa mawaziri na manaibu wao, na wakuu wa mikoa na wilaya), pamoja na chama cha Magufuli yaani CCM, na chama anachotoka Lowassa, yaani Chadema, na Upinzani kwa ujumla, ungekuwa mzuri.

Lakini ukweli ni kwamba japo tangu kuruhusiwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, uhusiano kati ya CCM, serikali zake na taasisi zake, na vyama vya upinzani umekuwa “wa kusuasua,” hali katika miaka miwili tu ya utawala wa Magufuli imekuwa mbaya zaidi hususan kutokana na ukweli kwamba hakuna jitihada za kuficha chuki iliyopo dhidi ya Upinzani.

Kama kiongozi wa ngazi za juu kabisa wa Chadema, na pengine mwanasiasa anayeheshimiwa zaidi ya kiongozi mwingine yoyote ndani ya chama hicho, ni wazi Lowassa anafahamu vema msimamo na mtazamo wa chama chake kuhusu Magufuli na utendaji kazi wake, na serikali yake, na chama chake.

Pengine kwa kuweka picha sawia, inaelezwa kwamba hadi wakati huu, zaidi ya wana-Chadema 400 ikiwa ni pamoja na viongozi na wanachama, aidha wapo jela au wana kesi zinazoendelea mahakamani ambazo takriban zote ni matokeo ya chuki za kisiasa zinazofanywa na Magufuli, serikali yake na chama chake.

Kadhalika, katika utawala wa Magufuli, vyama vya upinzani ikiwemo Chadema ambayo Lowassa ni kiongozi wake wa kitaifa vimepigwa marufuku kufanya shughuli zao za kisiasa ikiwa ni pamoja na mikutano na maandamano. Hayo yanatokea wakati CCM ikiwa huru kufanya mikutano na maandamano itakavyo, mara nyingi ikitumia raslimali za umma.

Sambamba na jitihada za Magufuli kubana fursa ya siasa (political space), utawala wa kiongozi huyo umekuwa mstari wa mbele kuvibana vyombo vya habari na kudhibiti uhuru na haki ya wananchi kutoa mawazo yao kama Katiba inavyowaruhusu.

Lakini jingine ambalo Chadema ni mhanga mkubwa, kada maarufu wa chama hicho Ben Saanane “alipotea” Novemba mwaka jana na hadi leo hajapatikana.

Na ni wakati ninaandika makala hii nimebaini kuwa Lowassa hajawahi kuongelea suala la kada huyo (naomba nikosolewe kama nimekosea).
Kubwa zaidi linaloweza kuhalalisha hasira za Chadema kwa utawala wa Magufuli ni tukio la hivi karibuni ambapo Mbunge wake maarufu, ambaye pia alikuwa mpinzani maarufu dhidi ya Magufuli, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, kunusurika kuuawa baada ya shambulio la risasi kadhaa huko Dodoma. Kwa sasa Lissu yupo nchini Ubelgiji kwa matibabu, lakini japo Lowassa alimtembelea alipokuwa hospitalini Nairobi, Magufuli hakuwahi kutia mguu kumjulia hali mwanasiasa huyo ambaye pia ni mnadhimu mkuu wa upinzani bungeni na Rais wa Tanganyika Law Society (TLS).

Kwahiyo japo pongezi za Lowassa kwa Magufuli zinaweza kuwa na uzito, mapungufu ya utawala wa rais huyo wa awamu ya tano, hususan kuhusiana na chuki na uonevu dhidi ya vyama vya upinzani, hususan Chadema, yalipaswa “kumzuwia” kada huyo wa zamani wa CCM kumwaga pongezi hizo.

Kibaya zaidi, imebainika kuwa Lowassa alishawahi kumwomba Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amsaidie kukutana na Magufuli. Hata hivyo, Gambo alipotamka hilo hadharani, Lowassa “aliruka kimanga.”


Hata hivyo, jana Magufuli alitamka bayana kuwa Lowassa aliomba mara kadhaa kukutana naye. Kwahiyo, alichosema Gambo kilikuwa kweli, na Lowassa hakuwa mkweli alipokana kuwa hajaomba kukutana na Magufuli.

Tukio hilo la Lowassa kukutana na Magufuli na kumwagia pongezi limepokelewa kwa hisia tofauti. Wakati kuna kundi dogo la wana-Chadema waliopongeza hatua hiyo, kwa mfano “kada” mmoja wa chama hicho Yericko Nyerere, wengi ikiwa ni pamoja na baadhi ya viongozi wamepingana waziwazi na Lowassa.

Wakati Yericko aliandika haya


Mbunge maarufu wa Chadema, Godbless Lema alikuwa wa kwanza kueleza bayana kutoafikiana na pongezi za Lowassa kwa Magufuli.


Baadaye, Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe, naye alieleza kuwa kauli za Lowassa ni zake binafsi na sio msimamo wa chama hicho.

Kadhalika, Mbowe alionekana kumkumbusha Lowassa kuhusu matukio mbalimbali yasiyopendeza katika utawala wa Magufuli

Lakini pengine aliyeeleza kwa kirefu kuhusu suala hilo ni Lissu, ambaye akiwa hospitalini huko Ubelgiji, alitoa waraka huu hapa chini.



Waheshimiwa habari za Tanzania na poleni kwa yote.
Naomba na mimi niseme kwa uchache kuhusu suala hili. Samahani kama 'uchache' wangu utakuwa mrefu kidogo.
Baada ya Mwenyekiti kuzungumzia jambo hili, inaelekea kuwa wazi kwamba Mheshimiwa Lowassa hakumshirikisha Mwenyekiti kabla ya kukubali au kuamua kwenda Ikulu kukutana na Rais Magufuli.
Na juzi tu wakubwa wetu hawa wawili walikuwa pamoja hospitalini kumsalimia Mzee Ngombale Mwiru.
Je, inawezekana Mheshimiwa Lowassa hakuwa anajua tayari kwamba ana appointment Ikulu?
Kama alikuwa anajua, kutokumshirikisha Mwenyekiti wake kuna tafsiri gani hasa?
Katika mazingira ya sasa ya Tanzania ya Magufuli, uamuzi wowote wa kufanya nae mazungumzo, hata kwa nia njema yoyote ile, bila kushauriana au kuwashirikisha viongozi wa juu wa chama, ni uamuzi usio sahihi na mgumu kukubalika.
Vile vile, kauli za aina ambayo tumeisikia leo kutoka kwa Mheshimiwa Lowassa, zina athari kubwa kisiasa.
Sio tu zinachanganya wanachama na wafuasi wetu, lakini pia zinawapa mtaji wa kisiasa maadui zetu.
Kuanzia sasa tutegemee sana kuwasikia maCCM yakishangilia 'busara' za Mheshimiwa Lowassa.
Masuala ya ukiukwaji haki za binadamu, uvunjwaji wa Katiba na mengine mengi sasa yatajibiwa kwa namna moja: Lowassa amemkubali Magufuli nyie wengine mnapiga kelele za nini.
Huu ni mtaji wa bure kwa Magufuli. Ukweli, ambao umesemwa sana humu, ni kwamba amefeli karibu katika kila jambo.
Hata hiyo reli anayosifiwa nayo na Lowassa bado ni ndoto tu: nani ajuaye itajengwa kwa hela za nani???
Za Wachina kama tulivyoambiwa mwanzoni; au za Waturuki kama tulivyoambiwa baadae; au za Afrika Kusini kama alivyosema mwenyewe anaenda kumwomba Zuma???
Kama chama hatujawahi kukataa mazungumzo na Rais au kiongozi mwingine yeyote wa serikali.
Na hatukatai kuzungumza na Magufuli kuhusu matatizo mengi na makubwa yanayoikabili nchi yetu.
Lakini ni muhimu na lazima viongozi wakuu wa chama washirikishane na washauriane kabla ya mazungumzo hayo.
Na baada ya mazungumzo, ni lazima viongozi wakubaliane juu ya kauli za kutoa hadharani kwa umma ili wote tuwe kwenye ukurasa mmoja.
Katika mazingira ya sasa, ambako viongozi na wanachama wetu wanashambuliwa hadharani kwa mapanga na hata kwa risasi, kumsifia Rais ni kumuunga mkono yeye na matendo yake.
Katika mazingira ya kesi nyingi za kutunga dhidi yetu, 'kazi nzuri' inayofanywa na Magufuli ina maana gani hasa, kama sio kuhalalisha ukandamizaji tunaofanyiwa.
Katika mazingira ambapo hata jumuiya ya kimataifa imeanza kuhoji mwenendo wa Rais Magufuli, kutoa kauli kwamba 'anafanya kazi nzuri' ni 'kumtupia taulo' la propaganda litakalomfichia madhambi mengi aliyowafanyia Watanzania katika miaka hii miwili.
Kwa vyovyote vile, kitendo cha Mheshimiwa Lowassa sio cha kunyamaziwa au kuhalalishwa kwa hoja nyepesi nyepesi.
TUNDU LISSU(MB).
Top of Form

Kadhalika, kada maarufu wa kike wa chama hicho, Hilda Newton nae alieleza masikitiko yake kutokana na kauli za Lowassa.



Kama alivyotahadharisha Lissu, ni wazi kwamba CCM watakuwa wamepewa “silaha” mpya katika “kumpamba” Magufuli na “kuwapenda” wapinzani, kwamba “hata Lowassa wenu anamkubali Magufuli.” Na ni rahisi kwa CCM kuonekana wana mantiki katika hoja hiyo, kwa kudai “kama mtu muhimu kabisa kwenye chama chenu (yaani Lowassa) ambaye ndiye aliyekuwa mpinzani mkuu wa Magufuli kwenye uchaguzi mkuu uliopita, anamkubali mkuu huyo wa nchi, ninyi ni akina nani kumpinga?”

Wakati ni wazi kwamba uamuzi wa Lowassa kukutana na Magufuli, na kumwagia pongezi, umezua “sintofahamu” huko Chadema, kuna masuala kadhaa ya muhimu yanayopaswa kuangaliwa kwa makini kwa ajili ya mustakabali wa chama hicho.

Kwanza, ni muhimu kwa viongozi na wanachama wa Chadema kutambua nafasi ya Lowassa katika chama hicho. Wakati baadhi ya wachambuzi wa siasa – mie nikiwa mmoja wao – wanaamini kuwa ujio wa Lowassa katika chama hicho ulikuwa na hasara zaidi kuliko faida, jitihada zilizofanywa na chama hicho kumpigania mwanasiasa huyo zimemjengea hadhi ambayo haipo kwa mwanasiasa mwingine yoyote ndani na nje ya chama hicho.

Ikumbukwe kuwa hadi wakati jina lake lilipokatwa na vikao vya CCM katika mchakato wa kusaka mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho tawala, Lowassa alikuwa ndiye mwanasiasa maarufu kuliko wote Tanzania. Yayumkinika kusema alikuwa mtu wa pili kwa umaarufu baada ya marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere. Licha ya kulazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008 kutokana na kashfa ya Richmond, Lowassa aliendelea kuwa mwanasiasa maarufu na mwenye nguvu kuliko yeyote yule ndani ya CCM, hata zaidi ya Rais na mwenyekiti wa taifa wa chama hicho wakati huo, Jakaya Kikwete.

Na japo kukatwa kwa jina la Lowassa huko CCM kulimpunguzia kidogo umaarufu wake kwa siasa za Tanzania – ilikuwa kama miujiza kuona CCM ilikuwa na ujasiri wa kukata jina la mwanasiasa huyo- alihamia Chadema akiwa na sapoti ya kutosha kiasi japo si kubwa kama ilivyotarajiwa.

Japo kuna “tuliopishana nae mlangoni” – kwa maana yeye alipoingia, sie tukatoka – ujio wake ulipelekea kuwa mwanasiasa maarufu zaidi ya wote wa Upinzani. Na ndio maana haikuwa vigumu kwake kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya UKAWA.

Nimeeleza kuwa baadhi yetu “tulipishana nae mlangoni” kwa sababu mie binafsi nilikuwa naiunga mkono Chadema, si kama mwanachama bali ukweli kwamba kwa muda mrefu nimekuwa nikijihusisha na harakati za mapambano dhidi ya ufisadi, na chama hicho kilijitokeza kuwa championi wa mapambano hayo. Kwahiyo, “naturally” nilijikuita nikikiunga mkono.

Hata hivyo, ujio wa Lowassa katika chama hicho ulinikimbiza. Sababu kuu ni binafsi zaidi, na nisingependa kuongelea hapa, lakini sababu nyingine ni kile nilichotafsiri kama usaliti wa Chadema. Ikumbukwe kuwa tangu mwaka 2006, chama hicho “kilimkalia kooni” Lowassa kumtuhumu kuwa ni fisadi, na ndicho kilichofanya jitihada kubwa zilizopelekea mwanasiasa huyo kujiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008.

Sasa bila hata kutumia jitihada kidogo tu za busara, chama kilichomwandama Lowassa kuwa ni fisadi, kwa miaka 9 mfululizo, yaani 2006 hadi 2015, kilionekana kituko kwa baadhi yetu tuliokuwa tukikiamini, kwa sababu, pamoja na mengine, isingewezekana kutumia miezi mitatu (Julai 2015 Lowassa alipojiunga na chama hicho hadi Oktoba wakati wa uchaguzi mkuu) kumsafisha vya kutosha.

Na gharama ya ujio wa Lowassa ilikuwa kubwa. Moja kubwa zaidi ilikuwa lazima kwa Chadema “kuitosa” turufu yake muhimu, ajenda ya vita dhidi ya ufisadi. Ililazimika kufanya hivyo kwa sababu kuzungumzia ufisadi ilhali chama hicho kimemkumbatia mwanasiasa kiliyemwita “baba wa ufisadi” kwa miaka 9 mfululizo ingeonekana kioja.

Kadhalika, kwa kumpokea Lowassa, Chadema ilikuwa haina jinsi ya kukwepa tuhuma kutoka CCM kuwa chama hicho upinzani ni cha kifisadi kwa sababu ya kumkumbatia mwanasiasa ambaye kilikuwa kikimuita fisadi. Jitihada za Chadema kujibu mashambulizi kuwa “kama Lowassa ni fisadi mbona hajachukuliwa hatua,” zilikuwa hazina mashiko.

Lakini jingine lililoipa jeuri CCM ni ukweli kwamba kwa chama hicho, Lowassa alikuwa ni “makapi” sambamba na wanasiasa wengine waliomfuata huko Chadema. Hiyo ilikipa chama hicho tawala “jeuri” ya namna flani. Na waliitumia vema kwenye kampeni, kwamba “hawa jamaa si lolote si chochote. Yani wameshindwa hata kutafuta mgombea wao wenyewe mpaka wakasubiri makapi kutoka kwetu ndo wakapata mgombea urais.” Na pamoja na maneno hayo kuwa machungu, ndo ukweli ulivyokuwa.

Chadema na UKAWA kwa ujumla walikuwa na takriban mwaka mzima wa kujipanga; kuafikiana kuhusu mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo, na kumnadi, huku wakitumia “advantage” ya “vita vya wenyewe kwa wenyewe” kati ya zaidi ya makada 40 waliokuwa wakichuana kuteuliwa na CCM.

Badala yake, kumbe tayari kulikuwa na makubaliano ya siri kati ya uongozi wa baadhi ya viongozi wa juu wa Chadema kwamba wasubiri kutangaza mgombea wao hadi baada ya mchakato wa CCM kupata mgombea wake, ka maana ya “kumhifadhia nafasi Lowassa endapo jina lake litakatwa huko CCM.”

Kabla ya kwenda mbali na makala hii ningependa nishauri Chadema irejee suala hilo la Lowassa kuandaliwa nafasi ya kuwania urais japo wakati huo alikuwa CCM. Hatua stahili zinapaswa kuchuliwa dhidi ya wote waliohusika na mpango huo.

Na ujio wa Lowassa ulipelekea Chadema kumpelekea mmoja wa magwiji wa siasa za upinzani, Dokta Willbrord Slaa. Umahiri wa Dokta Slaa haukuwa tu katika kuchukia ufisadi kwa dhati bali umahiri wake mkubwa katika kujenga hoja kisomi. Kadhalika, alikuwa akiaminiwa na watu mbalimbali muhimu ndani ya serikali, kiasi kwamba baadhi yao walihatarisha ajira zao kwa kumpatia mwanasiasa huyo nyaraka muhimu zilizoiwezesha Chadema kuwa na ushahidi mbalimbali katika vita yake dhidi ya ufisadi.

Na kuonyesha kuwa alikuwa na msimamo imara, Dokta Slaa aliamua kujiweka kando katika uongozi kupinga Lowassa kupewa ugombea urais wa UKAWA. Lakini jambo la kusikitisha mno, kiongozi huyo aliyekifanyia mengi chama hicho alidhalilishwa na kutukanwa kupita kiasi.
Na “akina sie” tulishindwa kustahimili ujio wa Lowassa, na kwa vile kwa baadhi yetu ilikuwa muhimu kumzuwia asiingie Ikulu, na hivyo kulazimika kumpigia kampeni mpinzani wake yaani Magufuli, tulitukanwa kila aina ya matusi. Sijui watu hawa waliojitoa ufahamu wataweka wapi sura zao pindi Lowassa “akirejea nyumbani” CCM.

Wakati anajiweka kando na uongozi wa Chadema, Dokta Slaa alikitahadharisha chama hicho kuwa ili kuleta mabadiliko ya kweli (badala ya hayo “ya kisanii” aliyokuwa akiyanadi Lowassa) chama hicho kinahitaji mkakati makini utakaoongozwa na watu makini. Na kwa hakika, tangu wakati huo, Chadema imekuwa kama kundi la wanaharakati wa kudandia hoja kuliko chama cha siasa chenye ajenda ya kueleweka. Uamuzi wa kuitelekeza ajenda ya vita dhidi ya ufisadi ulipelekea chama hicho kutokuwa na ajenda moja ya maana, huku CCM “wakipora” kiurahisi ajenda ya vita dhidi ya ufisadi.

Je mustakabali wa Chadema ukoje? Japo sio rahisi sana kubashiri kwa uhakika kuhusu hatma ya chama hicho, binafsi – kwa kutumia uzoefu wangu na uelewa wa kutosha wa siasa za Tanzania, sambamba na kuwa na fursa ya kufahamu “yanayojiri nyuma ya pazia” la siasa za nchi yetu – ninadhani kuwa kuna uwezekano mkubwa tu kwa Lowassa kurudi CCM kama sio kuachana kabisa na siasa.

Kwanini Lowassa anaweza kurudi CCM? Kuna sababu kuu mbili. Moja ni dalili za wazi kuwa ndoto zake za urais kupitia chama hicho ni kama zimeyeyuka. Umaarufu wake umegubikwa na kuibuka na kuimarika kwa umaarufu wa Lissu. Ni dhahiri kwamba ikipigwa kura ya maoni kuwa nani kati ya Lowassa na Lissu awe mgombea urais kwa tiketi ya Chadema mwaka 2020, Lissu ataibuka mshindi. Na Lowassa anafahamu kuwa hakuna njia ya mkato kwa yeye “kulazimisha” awe mgombea katika uchaguzi mkuu huo ujao, licha ya ukweli kwamba alishatangaza kuwa atagombea.

Sababu nyingine ni binafsi zaidi. Lowassa ni mmoja wa matajiri wakubwa nchini Tanzania. Kama utajiri huo ulipatikana kihalali au kifisadi, si lengo la makala hii kujiingiza katika mjadala huo. Lililo wazi ni ukweli kwamba licha ya kuwa mwanasiasa, yeye pia ni mfanyabiashara. Na kwa mujibu wa vyanzo vya kuaminika, serikali ya Magufuli imefanikiwa kutumia nyenzo yake muhimu dhidi ya wapinzani ambao pia ni wafanyabiashara, KODI.

Inaelezwa pia kwamba mali mbalimbali za mwanasiasa huyo zipo hatarini kutokana na uwepo wake huko Upinzani. Inadaiwa kuwa hata jengo la Tanesco Ubungo ambalo serikali imetangaza kulivunja, linamilikiwa na Lowassa, na tishio la kulivunja lilikuwa kama kufikisha ujumbe kwake.

Katika hili, Lowassa hatoonekana mtu wa ajabu akiamua kurudi CCM ili asibughudhiwe kuhusu biashara na mali zake. Ni nani kati yetu anayeweza kujitoa mhanga kwa ajili tu ya imani yake ya siasa? Si kama hawapo ila ni adimu mnooo! Na kibaya zaidi, hata akiamua kung’ang’ania huko Chadema, hatma yake na ya chama hicho haieleweki kwa sababu hadi muda huu – na hii ni licha ya zuwio la Magufuli dhidi ya vyama vya upinzani kufanya shughuli zao za siasa – chama hicho kikuu cha upinzani “kipo kipo” tu. Hakina ajenda moja ya kueleweka zaidi ya kudandia kila tukio linalojiri.

Iwapo Lowassa ataamua kubaki Chadema, hiyo itakuwa fursa mwafaka kwa chama hicho kumpumzisha. Naamini kuwa wana-Chadema wakiweka kando ushabiki wa kisiasa, wanafahamu fika kuwa mwanasiasa huyo hana nguvu, uwezo wala mvuto wa kukabiliana na siasa hatari zinazoendelea muda huu huko nyumbani.

Kwa upande mwingine, tukio la Lowassa kukutana na Magufuli Ikulu linaweza pia kuhusishwa na tamko la hivi karibuni la Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad, ambaye kama Lowassa, alimmwagia sifa Magufuli.

Nimefanya uchambuzi kuhusu kauli za wanasiasa hao wawili hapa, lakini ninachoweza kugusia hapa ni haja ya kutambua kuwa wanasiasa hao bado wanatunzwa na serikali kutokana na nyadhifa walizowahi kushika huko nyuma. Haihitaji uelewa mkubwa kuhusu "siasa za kibabe" kuhisi kwamba huenda "malezi" wanayopewa na serikali yametumika kama "chambo" cha kuwavuta karibu na Magufuli.

Kuhusu matatizo yanayoikabili Chadema muda huu,ukweli ni kwamba ni zaidi ya uwepo wa Lowassa ndani ya chama hicho. Japo huu ni ukweli mchungu usioruhusiwa kabisa kusikika ndani ya chama hicho, licha ya kazi nzuri ya kuifikisha Chadema ilipo leo, mwenyekiti wa taifa Mbowe anapaswa kutoa fursa kwa wana-Chadema wengine kusukuma gurudumu la chama hicho. Na hatua hiyo wala haihusiani na mchango wake mkubwa wa kumleta Lowassa ndani ya chama hicho na “kumpa” ugombea urais wa UKAWA.

Kirefu cha Chadema ni Chama cha DEMOKRASIA na Maendeleo. Sasa ni demokrasia gani hiyo ambayo inaruhusu mwenyekiti mmoja kuwa madarakani milele? What if “uenyekiti wa milele” ni miongoni mwa vikwazo kwa maendeleo ya chama hicho?

Lakini hata kama “muda wa Mbowe kutoka madarakani haujafika,” busara tu inapaswa kumfahamisha kiongozi huyo kuwa ni vema kuzingatia busara za akina Nyerere waliojing’atua wakiwa bado wanahitajika. Sipendi kubashiri hili, lakini laiti Mbowe asipohamasisha mageuzi kwenye medani ya uongozi wa chama hicho, haitokuwa jambo la ajabu akiishia kung’olewa kwa nguvu.

Na kwa bahati mbaya kwake, hili “songombingo” alilolianzisha Lowassa jana linaweza kuwa kama mnyororo mrefu ambao mahala flani yupo Mbowe. Ndiye aliyemkaribisha Lowassa.

Moja ya mapungufu makubwa mno yanayoitafuna Chadema muda huu ni pamoja na kulipuuza kundi muhimu linalokisaidia mno chama hicho, lundo la vijana wanaoshinda na kukesha katika mitandao ya kijamii wakijaribu kukinadi chama hicho angalau kwa kuikemea serikali ya Magufuli au CCM kwa ujumla.

Laiti chama hicho kingekuwa na ajenda ya kueleweka, basi jeshi hili la vijana lingekuwa nyenzo muhimu mno. Ni rahisi kuwalaumu vijana hawa kuwa “kazi yao kubwa ni kudandia hoja tu,” lakini ukweli ni kwamba chama chao hakiwapatii ajenda ya/za kueleweka. Kibaya zaidi, hata pale wanapojaribu kutengeneza ajenda wao wenyewe – kwa mfano jitihada za kumsaka Ben Saanane – hawapati sapoti ya kutosha kutoka uongozi wa juu wa chama hicho.

Ni hivi, wengi wa hawa vijana wanahatarisha maisha yao kwa kuwa tu “upande usiotakiwa” na serikali ya Magufuli. Hawategemei malipo yoyote zaidi ya kuamini kuwa siku moja wanaweza kukiingiza chama chao madarakani. Hakuna jitihada za makusudi za uongozi wa juu wa chama hicho kuwa karibu na kundi hili muhimu.

Ukiwa UVCCM una uhakika wa angalau “kuhongwa na Bashite” au kualikwa kwenye “mnuso” sehemu flani. Lakini ukiwa kijana wa upinzani, “zawadi” kubwa yaweza kuwa kusumbuliwa na vyombo vya dola na kuishi maisha ya wasiwasi. Kwahiyo vijana wa upinzani wana kila sababu ya kuichukia siasa, kwa sababu inahatarisha maisha yao, lakini mapenzi yao katika imani ya chama inawalazimisha kung’ang’ania hivyo hivyo.

Niionye Chadema kuwa katika zama hizi za “ununuzi wa binadamu kama zama za utumwa,” chama hicho kisishangae pindi wengi wa vijana hawa watakapoamua kubwaga manyanga na kukubali “kununuliwa.” Kwanini waendelee kuhatarisha maisha yao ilhali uongozi wa juu wa chama hicho hauna muda nao?

Akina Hilda Newton, Ben Malisa, Bob Wangwe, Ndehani Mwenda, Noel Shao, Gift Nanyaro ni miongoni mwa vijana wanaofanya kazi kubwa kwa ajili ya Chadema, bila ya matarajio ya malipo au fadhila flani, zaidi ya kuhatarisha maisha yao. Kama ilivyo kawaida ya mwanadamu yeyote yule, inaweza kufika mahala mtu akarudi nyuma na kujiuliza, “is it worth it?” Na japo sitarajii kuona makada hao vijana wakiamua kuipa kisogo Chadema, lakini sintoshangaa baadhi yao wakiamua kuipa kisogo siasa, hasa kama tasnia hiyo itaendelea kuwa “yenye manufaa kwa genge flani tu.”

Nihitimishe makala hii kwa kukuhamasisha msomaji kujipatia nakala yako ya kitabu changu kipya cha kielektroniki kinachochambua kwa kina miaka miwili ya utawala wa Magufuli. 




Baadhi ya niliyaoyazungumzia kwenye makala hii yamezungumwa kwa kirefu katika kitabu hicho ambacho hakielemei upande wowote. Kitabu hicho kwa sasa kinasubiri uzinduzi rasmi utakaokiwezesha kununulika kwa “mobile money” kama m-pesa, tigopesa,nk. Nitawataarifu. Ila kwa wasiohitaji kusubiri, waweza kukinunua HAPA

21 Oct 2015




OKTOBA 25 mwaka huu, Tanzania itafanya Uchaguzi Mkuu wa Rais, wabunge na madiwani. Mchuano mkali zaidi unatarajiwa kuwa katika nafasi ya urais, ambapo licha ya vyama vinane kusimamisha wagombea wao katika nafasi hiyo, ushindani mkali ni kati ya mgombea wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli, na yule wa umoja wa vyama vinne vya upinzani (Ukawa), Edward Lowassa.
Ushindani huo unatokana na unachangiwa zaidi na ukweli kwamba mgombea urais kwa tiketi ya Ukawa, Lowassa, awali alijaribu kuwania nafasi hiyo akiwa mwanachama wa CCM, lakini jina lake halikupitishwa, na hatimaye alijiunga na moja ya vyama vinavyounda Ukawa, Chadema, na kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo unaojumuisha pia chama cha National League for Democracy (NLD), NCCR- Mageuzi na Chama cha Wananchi (CUF).
Yayumkinika kuhitimisha kuwa Rais wa Tano wa Tanzania, atakayemrithi Rais wa sasa, Jakaya Kikwete, atakuwa kati ya Dk. Magufuli au Lowassa, huku mgombea urais kwa tiketi ya chama kipya cha Alliance for Change and Transparency (ACT- Wazalendo), Anna Mghwira akitarajiwa kushika nafasi ya tatu.
Dalili kuwa uchaguzi huo ungekuwa na ushindani mkubwa zilianza kujitokeza katika mchakato wa CCM kumpata mgombea wake, ambapo licha ya baadhi ya wanasiasa wa chama hicho waliokuwa na nia ya kuwania urais kujitokeza kutangaza nia takriban mwaka mzima kabla ya kuanza rasmi kwa mchakato huo, jumla ya makada 43 walichukua fomu za kuwania kuteuliwa kuwa wagombea urais, huku 38 kati yao wakifanikiwa kurejesha fomu.
Kwa upande wa Lowassa, jina lake lilianza kusikika katika duru za siasa za Tanzania kuhusu mrithi wa Rais Kikwete, mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010. Ikumbukwe pia kuwa Lowassa alikuwa na mchango mkubwa katika kampeni za urais mwaka 2005, ambapo hatimaye Rais Kikwete alishinda. Kadri Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu ulivyozidi kujongea, ndivyo jina la Lowassa lilivyozidi kuvuma. Kimsingi, mchakato wa CCM kupata mgombea wake uligubikwa zaidi na shauku ya Watanzania iwapo Lowassa angepitishwa au la.
Hata hivyo, hatimaye jina la Lowassa halikupitishwa, na badala yake akapitishwa Magufuli, hatua ambayo pia ilihitimisha tetesi za muda mrefu kuwa urafiki kati ya Lowassa na Rais Kikwete ulikuwa umefikia kikomo, hasa ikizingatiwa kuwa hoja iliyokuwa na nguvu katika harakati za Lowassa kuwania urais kupitia CCM ni hisia kuwa huenda Kikwete angemsaidia Lowassa kuwa mrithi wake.

Kwa upande wa Ukawa, umoja wa vyama vinne vya upinzani ulioundwa katika Bunge Maalumu la Katiba mwaka jana kwa lengo la kushinikiza matakwa ya wananchi yaheshimiwe katika mchakato wa kupata Katiba mpya, mchakato wa kumpata mgombea wao wa urais ulitawaliwa na ukimya kwa muda mrefu, kabla ya Lowassa kujiunga na Chadema na hatimaye kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo. Ujio wa Lowassa uliamsha hamasa kubwa miongoni mwa wafuasi wa vyama vinavyounda umoja huo, sambamba na kuleta ushindani mkubwa dhidi ya CCM.
Hata hivyo, uamuzi wa Chadema kumpokea Lowassa, mwanasiasa ambaye chama hicho kilimwandama na tuhuma za ufisadi kwa muda mrefu, ulipokelewa kwa hisia tofauti na Watanzania wengi, huku baadhi wakiuona umaarufu wake kama mtaji muhimu kuwezesha kuishinda CCM, huku wengine wakidhani kitendo hicho ni cha usaliti, hususan kwa Chadema ambayo ajenda yake kuu ilikuwa kupambana na ufisadi.
Licha ya uamuzi wa Lowassa kujiunga na umoja huo wa wapinzani, ukweli kwamba kwa mara ya kwanza, vyama vya upinzani nchini humo vimeweza kushirikiana kwa kusimamisha wagombea mbalimbali katika nafasi ya urais, ubunge na udiwani, imeufanya uchaguzi huo kuwa wa kwanza katika historia ya Tanzania ambapo nafasi ya ushindi kati ya chama tawala na upinzani zinakaribiana.
Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa idadi kubwa ya Watanzania sio wanachama wa chama chochote cha siasa. Na kundi hili licha ya kutarajiwa kuwa muhimu katika kuwezesha ushindi katika uchaguzi huo, pia linajumuisha wapiga kura wanaokabiliwa na uamuzi mgumu kujiunga mkono CCM na mgombea wake licha ya chama hicho kutuhumiwa kuwa kumechangia matatizo mengi yanayoikabili nchi hiyo, au kujiunga mkono Ukawa ambayo mgombea wake wa urais, Lowassa, licha ya kuhubiri kuhusu mabadiliko, anaonekana kama hana tofauti na chama hicho tawala, hasa ikizingatiwa alikuwa huko kwa muda mrefu.
Kwa tathmini hadi wiki hii ya mwisho kabla ya uchaguzi huo, chama tawala CCM 

kinatarajiwa kufanya vizuri zaidi ya vyama vya upinzani katika nafasi zote, yaani urais, ubunge na udiwani. Kwa upande wa urais, nguvu za CCM zimekuwa katika maeneo kadhaa ikiwa ni pamoja na kujenga picha kuwa mpinzani wao mkuu, Lowassa, hafai ndio maana jina lake lilikatwa katika mchakato wa chama hicho kupata mgombea wake.
Kujenga picha kuwa Lowassa, pamoja na viongozi wachache wa CCM walimfuata huko upinzani ni wenye uchu wa madaraka, wanaotumia malalamiko ya wananchi dhidi ya CCM kwa manufaa yao kisiasa.
Tuhuma za ufisadi dhidi ya Lowassa ambazo kimsingi zilitangazwa zaidi na vyama vya upinzani hususan Chadema. Katika hoja hiyo, CCM pia imejaribu kuionyesha Chadema na Ukawa kwa ujumla kama wanasiasa wasio na msimamo na walioikimbia ajenda yao ya kupinga ufisadi ili ‘kumsitiri’ Lowassa.
Kutofanikiwa kwa Lowassa na Ukawa kuelezea kwa undani kuhusu ajenda yao ya mabadiliko. CCM na mgombea wake Magufuli wamekuwa wakitumia muda mwingi kubainisha sera zao na jinsi watakavyotekeleza.
Takriban asilimia 85 ya Watanzania wanaishi maeneo ya vijijini ambayo kiasili ni ngome kubwa ya CCM kwenye chaguzi. Kwa upande mwingine, Ukawa hawajafanikiwa kujipenyeza vya kutosha katika maeneo hayo, ambapo pia kuna uelewa mdogo kuhusu muundo wa umoja huo.
Kwa mujibu wa takwimu za Tume ya Taifa ya Uchaguzi, idadi ya wanawake –kundi ambalo kiasili ni ngome muhimu ya CCM – ni kubwa zaidi ya wanaume, na hii inatarajiwa kukinufaisha chama hicho tawala na mgombea wake Magufuli.
Magufuli, amekuwa waziri kwenye awamu mbili za urais Tanzania, Awamu ya Tatu ya Rais Benjamin Mkapa, na hii ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete, na anasifika kwa uchapakazi. Kwa upande mwingine, ugombea wa Lowassa umeendelea kugubikwa na kashfa ya Richmond iliyosababisha ajiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008.
Kadhalika, licha ya kuwa na mtandao mkubwa nchi nzima, kuanzia ngazi ya mtaa hadi taifa, CCM inanufaika na hoja inayojiri kwenye kila uchaguzi mkuu, kuwa kuwapa ushindi Wapinzani ni sawa na kuwapa fursa ya kufanya majaribio ya uongozi ilhali CCM ina uzoefu wa kutosha.
Mapema wiki hii ziliibuka tena taarifa kuwa mmoja wa viongozi wakuu wa Chadema alihamisha mabilioni ya shilingi kwenda nje ya nchi, fedha zinazodaiwa zilipatikana baada ya kiongozi huyo ‘kukiuza chama hicho’ kwa Lowassa.
Hata hivyo, changamoto kubwa kwa CCM ni kinachotafsiriwa kama hasira za Watanzania wengi kutokana na matatizo mbalimbali yanayoikabili nchi hiyo, ambayo CCM inabebeshwa lawama, kubwa zaidi likiwa ufisadi unaotajwa kama chanzo kikuu cha umasikini.
Wachambuzi mbalimbali wa siasa za Tanzania wanatafsiri kuwa ufuasi mkubwa kwa Lowassa na Ukawa unachangiwa zaidi na manung’uniko ya wananchi wengi dhidi ya CCM, kiasi cha kuwa radhi kumwamini mwanasiasa ambaye kwa muda mrefu ameandamwa na tuhuma za ufisadi. Kauli kama ‘bora kulipigia kura jiwe kuliko CCM’ sio tu imekuwa ikisikika mra kwa mara miongoni mwa wafuasi wa upinzani bali pia inaashiria manung’uniko hayo.
Kadhalika, kwa vyama vinne vya upinzani kuweza kushirikiana na kumsimamisha mgombea mmoja wa urais, na kuongezewa nguvu na ujio wa Lowassa pamoja na makada kadhaa waliohama CCM, kwa mara ya kwanza Wapinzani wanaona kuna uwezekano wa kukishinda chama hicho tawala. Mikutano yao ya kampeni imeshuhudia umati mkubwa japokuwa lawama kwa Lowassa imekuwa ni kuhutubia kwa muda mfupi mno.
Wakati Magufuli na CCM wanaonekana kujiamini na kuwa na uhakika wa ushindi, kwa upande wa Lowassa na Ukawa, licha ya kuwa na matumaini makubwa ya kushinda, wanaonekana kuwa na hofu ya kuhujumiwa na chama hicho tawala.
Kwenye nafasi za ubunge na udiwani, CCM inatarajiwa kusinda viti vingi zaidi kwa sababu licha ya kuwa na mtandao mzuri majimboni, Ukawa inaonekana kuwekeza nguvu zaidi katika kumnadi Lowassa kuliko katika kampeni zake majimboni. Kadhalika, takwimu zinaonyesha kuwa mgombea wa CCM, Magufuli, ametembelea maeneo mengi zaidi ya mgombea wa Ukawa, Lowassa.
Kwa upande wa vyama vingine vinavyoshiriki uchaguzi huo, inatarajiwa kuwa ACT-Wazalendo kitashika nafasi ya tatu nyuma ya CCM na Ukawa, na kinatarajiwa kuimarika zaidi baada ya uchaguzi huo hasa kwa vile inahisiwa kwamba iwapo Ukawa itashindwa, wafuasi wake wengi wanaweza kuiona ACT-Wazalendo kama mpinzani wa kweli dhidi ya CCM.
Kwa hitimisho, changamoto kubwa kwa chaguzi nyingi barani Afrika huwa kwa chama cha kikuu cha upinzani kukubali matokeo pindi kikishindwa. Kwa mara ya kwanza, Tanzania inafanya uchaguzi wake mkuu huku kambi ya upinzani ikiwa na imani kubwa kuwa itaibuka na ushindi.
Kadhalika, kadri uchaguzi unavyozidi kukaribia ndivyo Wapinzani (hasa Ukawa) wanavyozidi kuonyesha kutokuwa na imani na mfumo mzima wa uchaguzi. Bila kujali upande gani utakaoibuka na ushindi, mustakabali wa Tanzania unategemea busara za viongozi na wafuasi wa kila chama kuhamasisha amani badala ya vurugu. Ushindi mkubwa katika uchaguzi huo ni kwa Watanzania kuendelea kubaki na umoja na amani.
Pia, mshindi katika uchaguzi huo atakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazoikabili Tanzania, kubwa zaidi ikiwa kuleta uwiano kati ya utajiri wa raslimali lukuki katika nchi hiyo na hali ya maisha ya wananchi, kupunguza pengo kati ya matajiri na masikini, na kuwaunganisha Watanzania kuwa kitu kimoja baada ya uchaguzi huu ambao kwa kiasi kikubwa umejenga mpasuko kijamii na kisiasa.
Mwisho, kwa vile hii ni makala yangu ya mwisho kabla ya uchaguzi huo hapo Jumapili, na kwa vile safu hii imekuwa ikifuatilia maendeleo ya uchaguzi huo tangu mwanzo, basi si vibaya kufanya ubashiri wa matokeo katika nafasi ya urais. Na ubashiri kuwa Magufuli atashinda urais, na CCM itashinda viti vya jumla katika nafasi za ubunge na udiwani, huku Ukawa, hususan Chadema, ikipata viti pungufu zaidi ya ilivyokuwa katika uchaguzi mkuu uliopita.
Hata hivyo, mshindi halisi katika uchaguzi huo ni Tanzania na Watanzania wenyewe. Kuna maisha baada ya uchaguzi, kwa hiyo ni muhimu kwa upande utakaoshindwa kutanguliza mbele maslahi ya taifa, badala kufanya vurugu.
MUNGU UBARIKI UCHAGUZI MKUU. MUNGU IBARIKI TANZANIA.



Sababu Tisa kwanini CCM itashinda katika Uchaguzi Mkuu Jumapili hii, Oktoba 25

Na January Makamba

Tarehe 25 mwezi huu Oktoba, Watanzania watapiga kura kumchagua rais wao wa tano, wabunge na madiwani. Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu umekuwa na msisimko mkubwa zaidi tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1995. Mengi yamendikwa kuhusu uchaguzi huu, hususan kutokana na hisia kwamba safari hii Upinzani una nafasi ya kukiondoa madarakani moja ya vyama vikubwa na vyenye muundo bora barani Afrika, chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM). Matukio mbalimbali kuelekea uchaguzi huo yameleta shauku inayoweza kutengeneza hadithi ya kusisimua.

Nikiwa sehemu ya Timu ya Kampeni ya CCM,na kwa manufaa ya wote ambao wangependa kuwa na mtizamo tofauti, ninatoa sababu 9 kwanini tunaamini kuwa CCM itaibuka mshindi na kwanini Dkt John Pombe Magufuli atakuwa Rais ajaye wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

1.    Ugombea ‘fyongo’ (flawed) wa Edward Lowassa

Ilishabainika kuwa uchaguzi huu ungekuwa mgumu kwa CCM bila kujali nani angekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Upinzani. Lakini matokeo ya uchaguzi huu yalielemea upande wa CCM pale Upinzani ulipomchagua Lowassa kuwa mgombea wao. Ni rahisi kwa CCM kuchuana na Lowassa kuliko laiti mgombea wa Upinzani angekuwa Dkt Wilbrod Slaa, ambaye ndiye aliandaliwa kuwa mgombea kabla ya ‘ukusukumwa kando’ na nafasi hiyo kupewa Lowassa. Slaa alikuwa na uadilifu katika maeneo mengi, na aliaminika. Kwa Lowassa, ni vigumu na inanyima raha kuchuana na mfumo aliyoshiriki kujenga na ambao ulikuwa sehemu ya maisha yake hadi Agosti mwaka huu alipohamia Upinzani. CCM ilikuwa na nafasi ya kumpitisha Lowassa kuwa mgombea wake wa nafasi ya urais. Hatukufanya hivyo kwa sababu rahisi tu kwamba ingekuwa vigumu mno kumkabidhi kwa wananchi mgombea wa matarajio ya baadaye ambaye ni kiashirio cha yale yasiyowaridhisha wananchi kuhusu CCM. Kuna wanaoamini kuwa uchaguzi huu ni mgumu kwa vile Lowassa ndiye mgombea wa Upinzani. Sisi twaamini kwamba uchaguzi huu ungekuwa mgumu mara kumi zaidi laiti Lowassa angekuwa ndiye mgombea wetu.

2.    Upinzani umesalimisha ajenda yake ya kupinga ufisadi

Kipindi cha miaka 10 iliyopita kimetawaliwa na matukio mbalimbali ya kuwabainisha mafisadi na kuwachukulia hatua. Vyombo vya habari, taasisi za kiraia na Bunge vimefanya kazi nzuri kushughulikia suala hilo. Rais Jakaya Kikwete ameweka historia kwa kuamuru ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kupatikana kwa wananchi na kujadiliwa kwa uwazi Bungeni. Waziri Mkuu aliyekuwa madarakani, si mwingine bali Lowassa, alijiuzulu kwa sababu ya kashfa ya rushwa. Mawaziri kadhaa walitimuliwa kazi na manaibu waziri wawili wanatumikia vifungo jela. Huu ni uwajibikaji wa hali ya juu japokuwa kuna wanaoweza kudhani ni hatua ndogo. Umma umeamka.

Upinzani ulijenga hadhi yake kwa kuongelewa sana kuhusu ufisadi. Kilele cha Upinzani kilijiri mwaka 2007 katika mikutano mkubwa wa hadhara ambapo walitangaza majina 10 ya watu waliowaita mafisadi wakubwa zaidi, katika kilichokuja kufahamika kama Orodha ya Aibu (List of Shame). Lowassa alikuwa kinara kwenye orodha hiyo.

Ilitarajiwa kuwa Uchaguzi Mkuu huu uwe ‘hukumu’ kwa CCM kuhusu ufisadi. Upinzani ulitarajiwa kuitumia ajenda ya ufisadi ambayo inawagusa watu wengi. Lakini ghafla, kwa kumteua mwanasiasa, ambaye kwa jitihada zao wenyewe Wapinzani,  amefahamika zaidi kwa ufisadi, iliwalazimu kuzika ajenda hiyo. Kilichofuata baada ya hapo ni kituko na kichekesho. Wale mashujaa wa mapambano dhidin ya ufisadi walijikuta wakilazimika ‘kulamba matapishi yao.’ Wengi wao waliokuwa mahiri katika mitandao ya kijamii walilazimika kufuta historia ya baadhi ya waliyoyaandika mtandaoni walipokuwa wakikemea ufisadi, lakini si kabla ya maandiko yao kunaswa kwa ‘screenshots.’ Ulikuwa ni ukweli wa kushangaza. Ni Dkt Slaa na Professa Ibrahmi Lipumba, viongozi muhimu wa Upinzani tangu miaka ya Tisini, walioamua kujiuzulu nyadhifa zao kwa kukerwa na uamuzi wa Upinzani kumpokea Lowassa.Matokeo yake, Upinzani walijikuta wakichana kadi yao turufu- ajenda dhidi ya ufisadi. Ni nadra kwao kuongelewa suala hilo, na wanapojaribu kufanya hivyo, ni kwa kujitetea tu.

Jioni moja mwezi Agosti, nilimwona Mbunge wa Upinzani, Peter Msigwa, katika mdahalo kwenye runinga. Aliongelea kitu ambacho kilijumuisha mtizamo wa Upinzani kwa muda huo, na kiliniacha hoi. Alisema, kabla hawajampokea Lowassa, walifanya utafiti wao, na “ufisadi sio ajenda muhimu kwa taifa letu.” Alidai kwamba wenye ushahidi kuhusu ufisadi wa Lowassa wajitokeze hadharani.Alionekana kusahau kuwa walipomtaja Lowassa katika List of Shame, walitangaza hadharani kuwa wana ushahidi. Muda si mrefu uliopita, CCM ilikuwa ikiwaomba Wapinzani kuleta ushahidi kila yalipojitokeza madai ya ufisadi dhidi ya viongozi wa chama na serikali allegations were leveled against the party and its leaders. Haikupendeza kuingiza hoja za kisheria katika masuala ya kimaadili. Upinzani sasa umeamua kwa hiari yao kuchukua ‘chembemoyo’ wakati ambapo viongozi wa CCM wanaongelea ufisadi kwa ujasiri na msisitizo.

Uchaguzi huu Mkuu ni muhimu sana kwa Upinzani. Kimsingi, unaweza kuwa na madhara makubwa. Endapo watashindwa hapo Jumapili, ‘watapotea’ kwa muongo mzima ujao. Ndio maana inashangaza kuona wamechukua uamuzi wa kukimbia ajenda yao kuu ya kupambana na ufisadi  ambayo iliwatambulisha na kuwaimarisha. Na kuwapa nguvu kukubalika kwa wapigakura. Kuona wanatarajia kushinda ni miujiza mkubwa.

3.    Mabadiliko ambayo kamwe huwezi kuyaamini

Ukizinguka jijini Dar es Salaam utakutana na mabango ya Upinzani yanayodaia “Ni Muda wa Mabadiliko.” Lakini ukisikiliza mikutano yao ya kampeni, ni porojo na hasira tu. Wasemaji wakuu katika mikutano hiyo ni Waziri Mkuu wa zamani na kada wa muda mrefu wa CCM, Frederick Sumaye na Lowassa mwenyewe. Kwa pamoja, wamekuwa wana-CCM na katika nyadhifa  za juu serikalini kwa zaidi ya miaka 50. Kwa hiyo inasikitisha kusikiliza kauli zao – zinazokosa imani na kupalizwa na aibu – wakipambana na mfumo walioshiriki kujenga, uliojenga tabia zao za kisiasa, na ambao walikuwa wakiusifu miezi mwili tu iliyopita.
Kutokuwa wakweli na kuweka mbele maslahi binafsi kwawatuma kudai kuwa CCM haijafanya chochote katika miaka miaka 50 iliyopita. Inapotokea viongozi wawili waandamizi wa chama na serikali  kwa zaidi ya miaka 30, wote wakiwa walioshika Uwaziri Mkuu, kudai kuwa hakuna chochote kilichofanyika katika miaka 50 iliyopita, wajihukumu wenyewe. Si kwa muundo, mwonekano au ukweli, wanasiasa hao wanasimamia mabadiliko. Yayumkinika kuhitimisha kuwa mabadiliko wanayoongelea ni kuhusu kubadili chombo kilichowaingiza madarakani, mabadiliko ya sare tu za chama. Hawana habari na mabadiliko ya maisha ya wananchi wa kawaida. Wapigakura wameanza kushtukia ukweli huo.

4.    Migogoro na mkanganyiko ndani ya UKAWA

Huko nyuma, kila ulipojiri uchaguzi, Upinzani ulijaribu kuunganisha nguvu ili kuing’oa CCM madarakani.Na kila mara jitihada za ushirikiano zilishindikana. Mwaka 2014, mjadala kuhusu Katiba Mpya kuataka serikali tatu uliwapatia ajenda ya kuwaunganisha pamoja. Kisha wakaamua kutafsiri ushirikiano huo kuwa wa kisiasa, wakaafikiana kusimamisha mgombea mmoja katika nafasi ya urais na kugawana majimbo.

Baada ya hapo kukajitokeza unafiki wa wazi. Kuonyesha kuwa matamanio yaliwekwa mbele ya kanuni zilizopatikana kwa jitihada ngumu, chama ambacho jina lake linajumuisha maneno ‘demokrasia’ na ‘maendeleo’ kilitemea mate mchakato wake chenyewe wa kidemokrasia na mshikamano kupata mgombea wake wa urais, na kukurupuka kumpitisha kada wa muda mrefu wa CCM ambaye jitihada zake kuwania urais kwa tiketi ya chama hicho tawala ziligonhga mwamba.

Waliamini kwamba uamuzi wa Lowassa kuhama CCM ungekiathiri chama hicho tawala, wakitarajia vigogo kadhaa wangemfuata huo Upinzani. Badala yake, ujio wake huko ukapelekea kuondoka kwa wanasiasa wawili waliokuwa nguzo muhimu kwa Upinzani, Dkt Slaa na Prof Lipumba.Kadhalika, wanachama wengine muhimu waliohama na kujiunga na chama cha ACT- Wazalendo, ambacho hakikujiunga na UKAWA.
Kana kwamba hiyo haitoshi, makubaliano ya UKAWA kusimamisha mgombea mmoja  kila jimbo yalikumbwa na mushkeli katika majimbo kadhaa na kupelekea malalamiko yaliyosababisha ugumu katika kampeni za Lowassa.

Huko Masasi, mgombea mwenza wa Lowassa, Juma Duni, alilazimika kuokolewa jukwaani baada ya waliohudhuria mikutano wake wa kampeni kupiga kelele kuwa wataipigia kura CCM. Katika jimbo la Nzega, Lowassa alilazimika kuendesha ‘kura ya sauti’ kuwauliza waliohudhuria mikutano wake wa kampeni wanamhitaji mgombea gani kati ya wawili wa UKAWA waliokuwa wanachuana. Mpango mzima wa ushirikiano miongoni mwa vyama vinavyounda UKAWA umekwenda mrama.CCM sasa ipo katika nafasi nzuri ya kujinyakulia majimbo ambayo vinginevyo yangekwenda kwa wagombea wa Upinzani.

Lakini kilele cha unafiki wa UKAWA ni hiki. Umoja huo uliundwa ili kutetea Katiba Pendekezwa iliyoshauri muundo wa Muungano wa serikali tatu. Kanuni hiyo ya msingi iliwekwa kando pale UKAWA walipomchagua mgombea wao wa tiketi ya urais, Lowassa, ambaye alikuwa mtetezi mkubwa wa muundo wa Muungano wa serikali mbili. Kwa wengi wasioendeshwa na propaganda, uamuzi wa kutelekeza suala la msingi lililopelekea umoja wa vyama hivyo, kwa ajili tu ya imani ya kufikirika ya kushinda urais, yaashiria uchu wa madaraka na sio mabadiliko yanayohubiriwa kwa wananchi.


5.    Lowassa kushindwa kufanya kampeni nchi nzima

Lowassa anaonekana kutokuwa na uwezo wa kusafiri kwa urefu na upana wa Tanzania kufanya kampeni. Mara nyingi amekuwa akitumia usafiri wa anga kwenda mikoani ambako hufanya mikutano mikubwa kwenye makao makuu ya mikoa, kutembelea majimbo mawili au matatu ya jirani kwa helikopta, na kurejea jijini Dar es Salaam. Huko Tanga, kwa mfano, alifanya kampeni katika majimbo matatu tu kati ya tisa mkoani humo. Mkoani Ruvuma, alifanya kampeni katika majimbo matatu kati ya tisa, Kigoma majimbo mawili kati ya manane, na Kagera majimbo matatu tu.

Kinyume chake, mgombea wa CCM, Magufuli amekuwa barabarani tangu Agosti 23, huku akipumzika kwa siku tatu. Anatumia usafiri wa gari, akitembelea kijiji baada ya kijiji, na kufanya mikutano kati ya minane hadi 12 kwa siku. Aina hii ya kufanya kampeni ‘kwa rejareja’ inabaki kuwa nguzo pekee ya kujihakikishia ushindi kwenye uchaguzi mkuu nchini Tanzania, hususan katika maeneo ya vijijini ambayo usikivu na kuonekana kwa vyombo vya habari ni mdogo. Wakati Lowassa anavutia wahudhuriaji wengi katika mikutano yake katika miji mikubwa, Magufuli anajipatia wahudhuriaji wengi katika kila kona ya Tanzania. Kama idadi ya wahudhuriaji katika mikutano hiyo ya kampeni inamaanisha wingi wa kura, basi kwa hakika CCM itashinda. Lakini tofauti na Upinzani, CCM haidanganyiki na wingi huo wa wahudhuriaji katika mikutano ya kampeni. Rekodi ya mahudhurio makubwa ilikuwa ikishikiliwa na Agustino Lyatonga Mrema, mgombea maarufu wa kiti cha urais kwa tiketi ya Upinzani mwaka 1995 (ambaye pia alijiunga na Upinzani akitokea CCM). Hata hivyo alishindwa kwenye uchaguzi huo. Sie twategemea kitu kingine.

6.    Mfumo imara wa CCM katika uhamasishaji kuanzia ngazi ya chini kabisa.

Katika Tanzania, vyama vichache mno vinavyoweza kuchuana na uwezo wa CCM kuhamasisha wananchi. Wakati Wapinzani huhadaiwa na ‘mahaba’ wakati wa kampeni za uchaguzi, mahudhurio makubwa kwenye mikutano yao ya kampeni na vichwa vya habari magazetini, CCM hutumika nguvu yake ya kimuundo na kuwasha ‘mashine zake za kisiasa,’ kuanzia ngazi ya mtaa (ujumbe wa nyumba kumi) kwa nchi nzima. Kimuundo, jumiya ya wanawake wa CCM (UWT) pekee ni kubwa kuliko Chadema, chama kikuu cha upinzani. CCM Haihitaji kusafiri ili kufanya kampeni. CCM ipo kila mahala, ikifanya kampeni katika makundi madogo, vijijini na mitaani, kila siku na mbali ya upeo wa vyombo vya habari. Kwa wanaofahamu muundo wa chama hicho, ushindi kwake si jambo la kushangaza.

Kwenye miaka ya 1950s, wakati wa harakati za kusaka uhuru kutoka kwa mkoloni, uwezo wa TANU kuhamasisha ulikuwa nguzo muhimu kwa Tanganyika kupata uhuru wake.CCM imerithi vinasaba vya TANU. Mwalimu Nyerere aliijenga CCM kuwa imara kwa nyakati kama hizi. Mwaka jana, huku umaarufu wake ukiwa umepungua, CCM ilimudu kushinda uchaguzi wa serikali za mitaa kwa asilimia 80 dhidi ya umoja Huohuo wa Upinzani inaokabilina nao katika uchaguzi huu Mkuu.Tofauti haipo kwenye nini kinachoonekana kwenye vyombo vya habari au mitandao ya kijamii bali jinsi gani makada wa chama hicho tawala walivyofanya uhamasishaji katika kila mtaa na kijiji. Uchaguzi huo wa serikali za mitaa, ambao hufanyika mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu, hutoa dalili nzuri kuhusu matokeo ya uchaguzi mkuu.

7.    Umahiri wa Dkt Magufuli

Mwaka jana, baadhi ya waandishi wa habari walikiri kwamba ni vigumu mno kumshambulia na kumshinda Dkt Magufuli. Ana rekodi imara ya usafi, uchapakazi na anayetaka kuona matokeo sahihi. Hajawahi kuvutiwa na harakati za kisiasa, na ilikuwa mshangao alipotangaza kuwania urais. Na alipotangaza, hakufanya mbwembwe wala kijitangaza kwenye vyombo vya habari. Alizingatia kanuni za chama kwa ukamilifu. Dkt Magufuli analeta kumbukumbu za mgombea mwingine aliyekuwa hajulikani mwaka 1995 -  Benjamin Mkapa. Wakati umaarufu wa CCM ukiwa chini, huku ikikabiliwa na upinzani kutoka kwa Naibu Waziri Mkuu aliyehama kutoka chama hicho tawala, CCM ilimchagua turufu yake ambayo ilikuwa ngumu kuikabili.Miaka 20 baadaye, ikikabiliwa na upinzani wa Waziri Mkuu maarufu wa zamani aliyehama chama hicho na kujiunga na Upinzani, CCM imefanya tena ‘vitu vyake.’ Siku zote, CCM hujua ‘kufanya pigo la haja.’

8.    Ufanisi wa CCM katika maeneo ya vijijini

Mimi ni Mbunge wa jimbo lisilo mjini, lenye idadi ya wastani ya wapigakura. Mwaka 2010, katika uchaguzi ulionekana kuwa mgumu, CCM ilishinda jimbo langu kwa asilimia 80., na kitaifa kwa asilimia 61. Hivi sasa, tunatarajia ushindi wa CCM kuwa wa asilimia 90 hivi. Tanzania ina  majimbo kadhaa yaliyo kama jimbo langu. Upinzani hupenda kuwapuuza wananchi katika majimbo yasiyo ya mijini, kama jimbo langu, kwa kudai kuwa wanaichagua CCM kutokana na ujinga wao. Wasingeweza kukosea zaidi ya hivyo.

Popote walipo, watu hupiga kura kulingana na mahitaji yao. Mwaka 2000, vijiji vinne tu katika jimbo langu ndivyo vilikuwa na umeme. Leo, vijiji 44 vina umeme. Japo hatujaweza kutoa huduma zote kwa kiwango cha kumfurahisha kila mtu, lakini hali halisi yaonyesha wingi wa wanafunzi mashuleni, walimu zaidi, madaktari na manesi zaidi, zahanati nyingi zaidi zimejengwa, huduma za mawasiliano ya simu zinapatikana kwa wingi, barabara nyingi za lami, nk. Porojo kuwa hakuna kilichofanyika Kwahiyo wapigakura wasiichague CCM haieleweki katika maoneo hayo ambay kimsingi ndiyo yenye wapigakura wengi. Na wagombea wa CCM wanaposema watafanya zaidi ya waliyokwishafanya, kwa kuzingatia mafanikio yaliyokwishapatikana, wananchi wanawaamini. Hotuba za kampeni ni mwonekano na mantiki.

Chaguzi sio kuhusu ahadi tu bali jinsi gani ahadi hizo zitaandaliwa na kutekelezwa. Jukwaa ambalo kila chama kitanadi ajenda zake za uchaguzi hujengwa wakati wa uzinduzi wa kampeni za chama husika. Yahitaji mtu kuangalia tu uzinduzi wa kampeni za za Lowassa na Magufuli. Lowassa aliongea kwa dakika 9 tu  - akiahidi, pamoja na mambo mengine, kuwaachia huru wabakaji (sio kama ninazusha hili) wanaotumikia vifungo vyao na watuhumiwa ugaidi wanaosubiri kesi zao. Bila kujali alikuwa na malengo gani wakati anatoa ahadi hizo, makosa hayo hayastahili msamaha wa rais.  Kwa upande wake, Magufuli aliongea kwa dakika 58, akielezea kwa undani ajenda za maendeleo katika nyanja za elimu, ajira, afya, ufisadi, huduma za maji, na miundombinu. Kuanzia hapo, kwa muda wote wa kampeni, mwenendo umekuwa hivyo, kwa uzito wa ujumbe kwenye hotuba zake na muda wa kuhutubia

Wanaohudhuria mikutano ya Dkt Magufuli huondoka katika mikutano hiyo wakiwa na matumaini na wenye nguvu. Kwa upande mwingine, wahudhuriaji katika mikutano ya Lowassa huondoka wakiwa wamekanganywa. Siku ya kupiga kura, wapigakura wanamkumbuka jinsi mgombea alivyoonekana na alivyoongea, na jinsi walivyojisikia walipomwona jukwaani. Kwa kigezo hiki, ni bora ningekuwa upande wa Magufuli.  

9.    Uongo, uongo na takwimu

Tanzania haina utamaduni wa kura za maoni kupima nafasi za wagombea katika uchaguzi. Tuna utaratibu wa muda mrefu wa kupata maoni ya wananchi katika maamuzi makubwa ya kisera – kuingia mfumo wa vyama vingi vya siasa, marekebisho ya Katiba, na kadhalika. Mwaka 2005, kulifanyika kura ya maoni, iliyobashiri ushindi mkubwa kwa CCM. Na kwa hakika, CCM ilishinda kwa asilimia 80. Mwaka 2010, kura ya maoni iliyoendeshwa na kampuni ya Ipsos-Synovate iliashiria kuwa idadi ya kura za CCM ingepungua hadi kufikia asilimia 61. CCM ilipinga matokeo ya kura hiyo ya maoni ikidani kuwa yalikuwa kiasi kidogo sana. Matokeo ya uchaguzi huo yalikuwa kama yalivyotabiriwa katika kura hiyo ya maoni. CCM ilipata asilimia 61 ya kura zote.

Hivi karibuni, kura mbili za maoni zilichapishwa. Zote zilifanywa na taasisi huru zinazoheshimika. – Twaweza and Synovate-Ipsos tena- zote zikijihusisha na utafiti wa kusaka maoni. Taasisi mbili tofauti, zilizotumia mbinu tofauti za kufanya utafiti, katika nyakati tofauti, matokeo yaleyale. CCM itashinda kwa asilimia 62 ya kura zote.

Inaruhusiwa, na kwa yumkini ni jambo zuri, kupingana na sababu hizi tisa za kwanini CCM itashinda. Lakini namba zina tabia ya ukandamizaji. Ndio mwelekeo wa kura huwezi kubadilika. Lakini kwa kuzingatia yote yaliyokwishaongelewa kuhusu kinachodaiwa kuwa ufuasi mkubwa kwa Upinzani, basi muda huu ingetarajiwa tuwa tunajadiliana kuhusu ufuasi wa wengi kutoka Upinzani kuelekea CCM– na sio kutarajiwa ufuasi wa wengi kutoka CCM kuelekea Upinzani. Na ndiyo, kura za maoni zaweza kukosea, na tusiwekee mkazo sana.Lakini hoja hii sasa ndiyo hupendelewa zaidi na upande unaelekea kushindwa kwenye uchaguzi.


January Makamba ni Mbunge wa Bumbuli (CCM), Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, na msomaji wa Kampeni za CCM 

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.