11 Dec 2015

Julai 8 mwaka huu itabaki moja ya siku zenye kumbukumbu chungu maishani mwangu. Ni siku ambayo baba yangu mzazi, Mzee Philemon Chahali alifariki dunia baada ya kuugua kama kwa wiki hivi.  Japo miaka 7 kabla ya hapo nilikumbwa na msiba mwingine ambapo mama yangu mepndwa, Adelina Mapango, alifariki baada ya kupoteza fahamu kwa zaidi ya miezi mitano, na japo hakuna msiba wenye nafuu, lakini angalau marehemu mama alifariki nikiwa huo Tanzania nilikoenda kumuuguza.  Lakini katika kifo cha baba, kilitokea nikiwa mbali na nyumbani. Na kwa hakika, nyakati za misiba, tunahitaji mno sapoti ya wenzetu kutuliwaza na kukabiliana na uchungu wa kufiwa.

Kwanini ninarejea habari hiyo ya kuskitisha? Kwa sababu tukio hilo ndilo lilinipa nafasi ya kumfahamu vema zaidi mmoja wa wanasiasa maarufu nchini Tanzania, January Makamba, Mbunge wa CCM Bumbuli na mmoja wa makada zaidi ya 40 waliojitokeza kuwania Urais kupitia CCM, na alifanikiwa kuingia katika 'Tano Bora.'

Mara baada ya kutangaza kuwa nimefiwa, January alinipigia simu kunipa pole, na kuulizia jinsi ya kuwasilisha rambirambi yake, ambayo baadaye aliiwasilisha. Pengine kwa watu wengine wanaweza kuliona hili kama ni jambo dogo tu na la kawaida. Lakini kimsingi, sote twafahamu viongozi wetu walivyo busy na majukumu yao, ambayo kwa kiasi kikubwa huwafanya waonekane kama binadamu wasiofikika (inaccessible). Kwa Afrika, ni vigumu sana kukuta kiongozi awe wa kisiasa au kwenye sekta nyingine akiwa karibu na raia wa kawaida, au kufuatilia yanayowasibu. Na kwa wanaomfahamu, amekuwa akiwasaidia watu wengi waliofiwa na wenye matatizo mbalimbali, at least ninaowafamu mie mtandaoni. Ni wazi mtu akiwa mwema kwa watu mtandaoni lazima pia ni mwema katika maisha yake nje ya mtandao.

Nimeanza makala hii na suala hilo binafsi kwa sababu ndilo lililonipa fursa ya kumfahamu kwa karibu zaidi. Awali nilimfahamu kama mwanasiasa kijana aliye karibu na watu wengi, hususan mitandaoni, lakini sikujua 'human side' (utu) yake. 

Tukiweka hilo kando, katika siasa za hivi karibuni za Tanzania, January alikuwa mwanasiasa wa kwanza kabisa kutangaza azma yake ya kuwania urais mwaka huu. Alitoa nia yake takriban mwaka mzima kabla ya kuanza rasmi kwa mchakato huo. Wengi walipokea tamko lake hilo, hasa kwa matarajio kuwa lingewashawishi wanasiasa wengine waliokuwa wanawania nafasi hiyo kujitokeza, na hiyo ingesaidia kuwafahamu vizuri. Kwa hiyo, kwa kifupi, January ndiye aliyepuliza rasmi kipenga cha kuwania urais wa awamu ya tano/

Wakati ukaribu wa mwanasiasa huyo kijana na wananchi, hususan katika mitandao ya kijamii ilikuwa ni turufu yake muhimu, moja ya downsides za kufahamiana na watu wengi ni uwezekano wa baadhi ya 'wakorofi' kujipa uhuru wa kusema chochote kile hata isipostahili. Na katika hili, January alikumbana na mengi: wapo waliomdhihaki wakiona dhamira yake ya urais kama ndoto tu, kashfa zisizostahili, nk. Hata hivyo, mara zote alimudu kuwajibu 'wapinzani' wake kwa lugha ya kistaarabu.

Baadaye alichapisha kitabu chake kilichokuwa na visheni yake ya urais. Again, kitabu hicho kilipokelewa kwa mtizamo chanya na Watanzania wengi japo kulikuwa na kundi dogo 'waliokiponda.' Kimsingi, kitabu hicho kilikuwa na masuala mengi ya msingi kuhusu matatizo ya Tanzania yetu na mikakati ya kuyakabili. Kwahiyo, kinaweza kabisa kuwasaidia watu mbalimbali wanaotaka kuifahamu vema nchi yetu.

Mchakato wa CCM kumpata mgombea wake ulipoanza rasmi, January aliibuka kuwa mwanasiasa pekee tishio kwa Edward Lowassa, kada amabye alitajwa kuutaka urais kwa miaka kadhaa. Tofauti na Lowassa ambaye umaarufu wake ulichangiwa zaidi na uwezo wake wa kifedha, mafanikio ya January katika kampeni yake yalichangiwa zaidi na ukaribu wake kwa watu, hususan vijana.

Na japo hakufanikiwa kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, kuingia kwake kwenye 'Tano Bora' ni mafaniko makubwa kabisa, hasa ikizingatiwa kuwa bado ni kijana anayeweza kuyatumia mafanikio yake ya mwaka huu katika chaguzi zijazo. Yayumkinika kuhitimisha kuwa mwanasiasa pekee ambaye mpaka muda huu anatajwa kuwa rais ajaye wa Tanzania baada ya Magufuli ni January.

Baada ya Magufuli kushinda urais, zikaanza tetesi kuwa 'January anataka Uwaziri Mkuu.' Ni muhimu kukumbuka kuwa katika muda mwingi wa harakati zake za kisiasa, mwanasiasa huyo amekuwa akiandamwa na 'wasemaji wasio rasmi' wanaojifanya kumjua zaidi ya anavyojijua mwenyewe. Hakuna wakati au mahali popote ambapo January alisema ana matarajio ya kuwa Waziri Mkuu. Ni hisia tu za watu - waliomtakia mema kutokana na mchango wake mkubwa katika kampeni za CCM katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, na 'wabaya' wake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakimzushia vitu mbalimbali.

Rais Magufuli alipomtangaza Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu, yakazuka maneno kuwa 'January kakosa Uwaziri Mkuu,' kana kwamba alitangaza kuwa anawania au anatarajia nafasi hiyo. 

Baada ya kitendawili cha uwaziri mkuu kuteguliwa, likabaki fumbo la baraza la mawaziri. Hapo napo yakazuka maneno chungu mbovu. January akapangiwa Wizara kadhaa na 'wanaomjua zaidi ya anavyojijua mwenyewe.' Lakini kuna waliodiriki kuweka 'chuki' zao hadharani na kuombea asiwemo kabisa katika baraza jipya la mawaziri. Ukiwauliza 'kwa lipi alilowakosea,' nina hakika hawana jibu.

Jana baraza likatangazwa. Na January akapanda kutoka Unaibu Waziri katika Awamu iliyopita na kuwa Waziri Kamili. Haya ni mafanikio makubwa kwa mwanasiasa kijana kama yeye. Kama kazini, hiyo ni promosheni, kutoka unaibu waziri hadi uwaziri kamili. Lakini kwa vile 'wabaya' wake walishampangia wizara, January kupewa Uwaziri katika ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira imetafsiriwa nao kama 'amepewa kitu pungufu.' Jamani, mtendeeni haki mwanasiasa huyu. Pungufu kivipi ilhali kiukweli amepandishwa cheo kutoka unaibu waziri hadi kuwa waziri kamili?

Jana nilitwiti matarajio yangu kwa January katika nafasi hiyo mpya, na ninashukuru mapokeo yalikuwa mzuri. Maeneo mawili ya majukumu yake ya kiuwaziri ni muhimu sana, na nina hakika atawashangaza wengi. Kwa upande wa Muungano, sote twaelewa hali ya kisiasa ilivyo huko Zanzibar. Kwahiyo, kwa nafasi yake, January anatarajiwa ku-play role muhimu katika jitihada za kutafuta suluhisho la mgogoro wa kisiasa visiwani humo. Lakini licha ya mgogoro huo, moja ya vitu vinavyotishia ustawi wa Muungano wake ni kero zake za muda mrefu. Kwa vile Janaury ni msomi katika tasnia ya usuluhishi wa migogoro (confilict resolution), na kutokana na profile yake kubwa kimataifa, ninatarajia kuwa ataweza kuyashughulikia masuala yote mawili kwa ufanisi mkubwa.

Na katika suala la mgogoro wa kisiasa huko Zanzibar, hali ya 'ubinadamu' kwa maana ya utu au 'humani side' ya January itakuwa na umuhimu wa kipekee. Migogoro ya aina hiyo inahitaji mtu mwelewa, mtulivu, na mwenye busara, sifa ambazo January anazo. Kuweza kuwashawishi Wazanzibari waweke maslahi ya taifa mbele ya maslahi ya vyama vyao kunahitaji mtu ambaye anapoongea anaonekana kama ndugu au rafiki na si mwanasiasa au kiongozi flani. Kwa kifupi, human side ya mpatanishi ni muhimu mno katika tasnia ya utatuzi wa migogoro.

Lakini kama kuna eneo ambalo ninatarajia makubwa zaidi kutoka kwa mwanasiasa huyo ni MAZINGIRA. Moja ya masuala muhimu kabisa dunain kwa sasa ni masuala ya mazingira. Japo kwa Afrika, masuala hayo hayazungumziwi sana japo bara hilo ndilo lililo hatarini zaidi kimazingira, hususan kutokana na matatizo ya kiuchumi na umasikini, Mijadala mbalimbali muhimu inayoendelea duniani kwa sasa nipamoja na kuhusu masuala ya mazingira. Kubwa zaidi ni suala la global warming ambalo wanasayansi wanatahadharisha kuwa lisiposhughulikiwa kikamilifu linaweza kupelekea kuangamia kwa sayari yetu.

Kwa nchi masikini kama Tanzania, masuala ya mazingira yana umuhimu wa kipekee (japo hayazungumziwi inavyostahili) kwa sababu kama tunakwama katika kukabiliana na matatizo yaliyo katika uwezo wa kibinadamu, hali inakuwaje tunapokabiliwa na matatizo ya kiasili (natural) yaliyo nje ya uwezo wa kibinadamu?

Kwa upeo mkubwa alionao na uhodari wake wa kuwasilisha hoja, sintoshangaa kuona huko mbeleni January akitokea kuwa mmoja wa watu muhimu duniani katika masuala ya mazingira. Na uzuri ni kwamba ameingia katika wizara inayishughulikia masuala hayo wakati ambapo jina la Tanzania limeanza kuvuma kwa uzuri kutokana na sifa za uchapakazi wa Rais Magufuli.

Ninasema pasi hofu kuwa sintoshangaa miaka michache ijayo tukashuhudia kwa mara ya kwanza Tanzania ikitoa mshindi wa Tuzo ya Nobel aidha katika usuluhishi wa mgogoro wa Zanzibar au masuala ya mazingira, au hata yeye kuchaguliwa kuwa Mtu wa Mwaka wa jarida la kimataifa la TIME la Marekani (TIME's Person of the Year). 

Nimalizie kwa kueleza kuwa lengo la makala hii ni kuweka sawa kumbukumbu kuhusu watu muhimu katika tanzania yetu, kama January, kwa mahitaji ya sasa na huko mbeleni. Kma taifa, tunakabiliwa na mapungufu makubwa ya uhifadhi wa kumbukumbu. Na japo mie si mbashiri, natumaini kuna siku makala hii itatumika kama reference baada ya 'January kuishangaza dunia' katika eneo fulani. 

Mwisho, ninawatakia kila la heri mawaziri wote walioteuliwa na Rais Magufuli katika kabineti yake mpya, nikiwa na matumaini makubwa kuwa wataendana na kasi yake ya uchapakazi na hivyo kutupatia Tanzania tunayostahili. 

Nawatakia siku njema.



1 comment:

  1. namuelewaga kitambo,anaelewa na hana majivuno.. yuko real

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.