11 Dec 2015

‘HAPPY birthday Tanzania…happy birthday me.” Naam, leo ni sikukuu ya Uhuru na Jamhuri, siku ya kuzaliwa kwa Tanganyika (sasa Tanzania Bara), siku ambayo pia ni ya kuzaliwa kwangu.

Nilizaliwa Desemba 9, miaka kadhaa baada ya uhuru wa nchi yetu, na kila ninapoadhimisha siku ya kuzaliwa, ninaadhimisha pia siku ya kuzaliwa kwa nchi yetu.

Kwa kawaida, maadhimisho yangu ya siku ya kuzaliwa huwa sio sherehe bali hutumia siku hiyo kumshukuru Mungu, sambamba na kufanya tafakuri ya nilipotoka, nilipo na niendapo. Sherehe pekee ilikuwa kuimbiwa wimbo wa ‘Happy Birthday’ na marehemu baba, ambaye kwa bahati mbaya hayupo nasi sasa. Kwa hiyo hii itakuwa birthday yangu ya kwanza kukosa ‘sherehe’ hiyo iliyoambatana na sala za kumshukuru Mungu na kuniombea mafanikio.

Lakini wakati wa kusherehekea siku ya kuzaliwa pamoja na ‘birthday-mate’ (mtu mliyezaliwa naye siku moja) Tanzania imekuwa kama tukio la kihistoria na la kujivunia, kwa upande mwingine kila ninapofanya tafakuri kuhusu ‘mwenzangu’ huyo alipotoka, alipo na aendako huishia kupatwa na maumivu.

Si kwamba nimefanikiwa sana kuliko ‘mwenzangu’ huyo bali angalau kwa upande wangu kila nikiangalia nilipotoka, nilipo na niendako, nimekuwa naona mwanga zaidi. Kwa ‘mwenzangu’ Tanzania, wakati huko alikotoka kulileta matumaini, alipo na aendako (kwa miaka ya hivi karibuni) kulinipa shaka.

-Lengo la kupata uhuru halikuwa kumwondoa tu mkoloni bali pia kujenga jamii yenye amani na usawa, pamoja na mambo mengine. Japo katika miaka 54 ya uhuru wetu, Tanzania imeendelea kuwa nchi ya amani kwa maana ya kutokuwepo vita, lakini katika miaka ya hivi karibuni amani kwa maana ya kuwa na uhakika wa mlo wa kesho, au wanafunzi kuwa na hakika ya ajira wanapomaliza masomo au wakulima kuwa na uhakika wa mauzo ya mazao yao, au wagonjwa kuwa na uhakika wa huduma wanayostahili katika vituo vya afya na uhakika katika maeneo mengine, vimekuwa ni mgogoro.

Kadhalika, amani yetu imeonekana kuwanufaisha zaidi ‘mchwa’ wachache walioigeuza Tanzania yetu kuwa shamba la bibi, wenzetu ambao miaka michache iliyopita tuliwaita kupe, wanaovuna wasichopanda, wanaoneemeka kwa jasho la wengine.

Mara kadhaa, maadhimisho ya sikukuu ya uhuru wetu yameambatana na swali gumu, je kweli tupo huru? hasa ikizingatiwa kuwa kwa kiasi kikubwa nchi yetu imeendelea kuwa tegemezi kwa wafadhili, miongoni mwao wakiwa watu walewale tuliowafukuza mwaka 1961.

Kuna wenzetu wengi tu wanaodhani kuwa uhuru wetu ulifanikiwa kumtimua mtu mweupe lakini miaka kadhaa baadaye huku tukiwa huru tumeshuhudia ukoloni mpya unaofanywa na mtu mweusi. Na japo wakoloni hawawezi kuwa na kisingizio cha kututawala, lakini walipoinyonya nchi yetu walikuwa na malengo ya kunufaisha nchi zao na sio watu binafsi. Kadhalika, hawakuwa na uchungu na nchi yetu kwa vile sio yao.

Kinyume chake, wakoloni weusi sio tu ni wenzetu bali wengi wao aidha walisomeshwa bure au kwa fedha za Watanzania wenzao, lakini badala ya kurejesha fadhila kwa kulitumikia taifa kwa uadilifu, wameishia kuwa wanyonyaji wasio na huruma. Tofauti na wakoloni weupe, wenzetu hawa hawana kisingizio japo kimoja kwani wanainyonya nchi yao wenyewe.

Moja ya vikwazo vya kutuwezesha kufaidi matunda ya uhuru ni ukosefu wa uzalendo. Licha ya jitihada kubwa za Mwalimu Nyerere kuhamasisha mapenzi na uchungu kwa nchi yetu – uzalendo- tawala zilizofuatia baada ya yeye kung’atuka zikawekeza katika kuboresha maslahi binafsi badala ya maslahi ya taifa. Japo mabadiliko yaliyoikumba dunia wakati Mwalimu anataka madaraka yalisababisha haja ya mageuzi katika itikadi ya ujamaa, lakini kilichofanyika si mageuzi tu bali kuua kabisa mfumo wa ujamaa.

Kuna wanaodai kuwa isingewezekana kufanya mageuzi ya kisiasa na uchumi huku tukikumbatia mfumo wa ujamaa. Hilo sio sahihi, kwani tunashuhudia taifa kubwa kama China ambalo limefikia hatua ya juu kabisa ya ujamaa yaani ukomunisti, likimudu kuendelea kuwa taifa la kijamaa huku likijihusisha pia na sera za uchumi wa kibepari kama vile uwekezaji.

Nikirejea kwenye siku ya kuzaliwa Tanzania Bara, na yangu, Ninaomba kukiri kuwa baada ya muda mrefu, mwaka huu sikukuu yetu ya kuzaliwa mie na ‘mwenzangu’ inaleta furaha na matumaini.

Na yote hayo ni matokeo ya ninachokitafsiri kama kusikilizwa kwa dua/sala zetu kwa Mwenyezi Mungu kuturejeshea Nyerere na (Waziri Mkuu wa zamani marehemu Edward) Sokoine wengine. Tumejaaliwa kumpata Rais mpya, Dk. John Magufuli, ambaye mwezi mmoja tu tangu aingie madarakani ameweza kwa kiasi kikubwa kurejesha matumaini yaliyopotea.

Na pengine kuashiria kuwa Nyerere amerudi kupitia Dkt Magufuli, mwaka huu tunaadhimisha siku ya uhuru na Jamhuri kwa shughuli za usafi wa mazingira, na hii inakumbusha dhana ya Mwalimu ya Uhuru na Kazi. Na kwa hakika hatuwezi kuwa huru kwa kuwafanyia kazi wenzetu wanaotuibia kila kukicha.

Majuzi akiwahutubia wafanyabiashara wakubwa huko nyumbani (Tanzania), Rais Dk. Magufuli alieleza bayana jinsi tunavyoweza kutoka kundi la nchi masikini na ombaomba na kuwa miongoni mwa nchi wafadhili iwapo tutatumia raslimali zetu vizuri, sambamba na kupambana na ufisadi. Uhuru wa bendera pekee, wa kumwondoa mkoloni mweupe huku tukisumbuliwa na mkoloni mweusi ni tatizo kwani suala si rangi ya mkoloni bali ukoloni wenyewe. Tukimudu kuboresha uchumi wetu na kuweza kujitegemea, tutakuwa na uhuru kamili.

Kadhalika, kama Mwalimu alivyotufundisha, uhuru bila nidhamu ni uwendawazimu. Hatuwezi kuwa na uhuru kamili kama hatuna nidhamu ya matumizi na tuliowapa dhamana ya kutuongoza hawana nidhamu kwa maadili ya taifa.

Ni matumaini yetu wengi kuwa maadhimisho haya ya siku ya uhuru na Jamhuri kwa njia ya uhuru na kazi, sambamba na kasi kubwa ya Dk. Magufuli kutumbua majipu ni ishara njema kuwa Tanzania tuliyoitarajia Desemba 9, 1961 na kufaidika nayo zama za Mwalimu, ipo mbioni kurejea.

Nimalizie makala hii kwa kusema tena ‘Happy birthday Tanzania, happy birthday to me.’

Mungu Ibariki Tanzania.
Mungu mbariki Rais wetu Dk. John Magufuli.

Mungu tubariki Watanzania. 

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.