23 Jul 2016

Munich-locator-600px
Ujerumani imekumbwa na janga jingine baada ya lile la siku nne ambapo kijana mmoja, mhamiaji kutoka Afghanistan, aliwashambulia abiria kwenye treni kwa kutumia shoka na kujeruhi watu wanne. 

Kijana huyo, Riaz Khan Ahmadzai (au Muhammad Riyad, kwa jina jingine), aliyekuwa na umri wa miaka 17, na aliyewasili Ujerumani mwaka jana kama mtoto anayesaka ukimbizi, aliuawa kwa kupigwa risasi na polisi.
Katika tukio lililotokea jana, watu 10 wameuawa hadi wakati ninaandika makala hii na wengine kadhaa kujeruhiwa baada ya shambulio la risasi katika mgawaha wa McDonald kwenye kitongoji cha biashara katika jiji la Munich.
Awali, ilikuwa haifahamiki idadi kamili ya waliofanya shambulio hilo japo taarifa za awali zilitaja wahusika kuwa watatu. Licha ya shambulio hilo kwenye mgahawa huo ulio kwenye duka kubwa (mall), ilidaiwa kuwa milio ya risasi ilisikika pia maeneo mengine ya Munich.
Kulikuwa kuna theories tatu - mbili zenye uzito na moja yenye uzito mdogo kiasi - kuhusu nani hasa alihusika na tukio hilo. Theories hizo ni kama ifuatavyo.

Theory ya kwanza: shambulio hilo ni kazi ya magaidi, sanasana ISIS

Imekuwa ni kawaida sasa kwa nchi za Magharibi kwamba kunapotokea tukio lolote la kigaidi, hisia za kwanza ni usual suspects, yaani kama sio ISIS basi ni Al-Qaeda. Haya ndio makundi mawili ya kigaidi yanayoziandama mno nchi za Magharibi. Na kwa sasa, ISIS ndio inaongoza kwa mfululizo wa mashambulizi ilhali Al-Qaeda 'imekuwa kimya' kitambo sasa.

Hisia kwamba wahusika katika shambulio hilo walikuwa ISIS (au Al-Qaeda) ni, kwanza, tukio la majuzi la huyo kijana aliyefanya shambuli kwa kutumia shoka ambalo nimelieleza mwanzoni mwa makala hii. 

Pili, ni ukweli kwamba ISIS imekuwa ikifanya jitihada kubwa kuishambulia Ujerumani na nchi nyingine za Magharibi. Kama ilivyo kwa Uingereza, wataalamu wa usalama wa kimataifa wanaeleza kuwa shambulio la ISIS kwa Ujerumani sio suala la "iwapo litatokea" bali "lini litatokea." 

Tatu, ISIS walishangilia tukio hilo la Munich, katika akaunti yao ya Telegram, kama inavyoonyesha pichani chini
ISIS rejoice in Munich attack

Hata hivyo, theory hii kuwa wahusika ni ISIS ilikabiliwa na 'pungufu' hili: ilielezwa kuwa moja ya maiti hizo 9 ni ya mmoja wa wahusika wa tukio hilo. Hiyo ilikuwa na maana gani? Ni kwamba, magaidi wa ISIS na wenzao wenye mrengo kama wao, hupania kuuawa na sio kujiuwa. Wanaamini kuwa kwa kuuawa - badala ya kujiuwa - wanakuwa wamejitoa mhanga kwa ajili ya imani yao. Kama sio kuuawa kwa kupigwa risasi basi kifo kitokane na kujilipua kwa bomu la kujitoa mhanga.

Lakini kifo cha mtu huyo anayedhaniwa kuwa mmoja wa wahusika wa shambulio hilo hakikutokana na kupigwa risasi na polisi au yeye kujilipua. Sababu pekee ya kifo inaweza kuwa alijipiga risasi mwenyewe, mbinu ambayo sio chaguo la magaidi wa ISIS na wenzao.

Theory ya pili: Wahusika walikuwa kikundi cha wabaguzi wa rangi wenye msimamo mkali dhidi ya Waislam, wakimbizi na raia wa kigeni

Jana ilikuwa ni kumbukumbu ya miaka mitano ya shambulio kubwa la kigaidi lililofanyika huko Utoya, nchini Norway, Julai 22 mwaka 2011 ambapo mbaguzi wa rangi mwenye msimamo mkali, Anders Behring Breivik, aliwapiga risasi na kuwauwa watu 77.
Wachunguzi wa masuala ya usalama walieleza kuwa kulikuwa na uwezekano kwamba shambulio hilo la Munich lilifanywa na kikundi cha kibaguzi chenye mrengo mkali kama maadhimisho ya tukio hilo la Norway, na pengine kama kumwenzi Breivik ambaye ni 'shujaa' kwa vikundi vya wabaguzi wa rangi.
Kingine kilichoipa uzito theory hii ni ukweli kwamba mmoja wa wahusika wa shambulio hilo alisikika akisema kuwa yeye ni Mjerumani asilia, na akawatukana wahamiaji nchini humo. Wataalamu wa lafidhi walieleza kuwa sio rahisi kwa mtu asiye mzaliwa wa Ujerumani kuwa na lafidhi iliyotumiwa na mtu huyo.

Theory ya tatu, wahusika sio watatu bali mtu mmoja tu aliyekuwa anayesumbuliwa na matatizo ya akili

Katika kile kinachotafsiriwa kama unafiki, 'mzungu' akiuwa watu kadhaa, maelezo yatakuwa "mtu mwenye matatizo ya akili." Uthibitisho wa hivi karibuni ni maelezo kuhusu mtu aliyemuuwa mbunge Jo Cox wa hapa Uingereza hivi karibuni. Ilielezwa kuwa muuaji huyo "alikuwa na historia ya matatizo ya akili."
Laiti angekuwa Muislam au Mwarabu basi maelezo hapo yangeelemea zaidi kuhusu Uislam wake, na wabaguzi wasingekawia kudakia hoja kuwa dini hiyo ni tishio kwa ustawi wa mataifa ya Magharibi.

Ilielezwa kuwa mtu huyo niliyemwelezea katika theory ya pili, licha ya kudai yeye ni Mjerumani na kuwatukana wahamiaji, pia alieleza kuwa ni mgonjwa wa akili na yupo kwenye matibabu.

Taarifa rasmi ya polisi kuhusu mhusika

Baadaye, polisi wa Munich waliitisha mkutano na waandishi wa habari na kueleza kuwa uchunguzi wao umethibitisha kwamba aliyefanya shambulio hilo ni kijana mwenye umri wa miaka 18, Mjerumani mwenye asili ya Aljeria, na alihamia nchini humo miaka miwili iliyopita.

Kama taarifa hiyo ya polisi haina mapungufu, ukweli kwamba siku 4 zilizopita mhamiaji kutoka Afghanistan alifanya shambulio la kigaidi kwa kutumia shoka na kujeruhi watu wanne kabla ya kuuawa, na jana mhamiaji mwingine kutoka Iran, mwenye umri wa mwaka mmoja tu zaidi ya huyo wa majuzi, naye amefanyanya shambulizi na kuuwa watu 10 (hadi wakati naandika makala hii), chuki dhidi ya wageni inaweza kuongezeka maradufu.

Ikumbukwe kuwa Ujerumani imekuwa ikipokea idadi kubwa ya wakambizi miongoni mwa nchi za Magharibi. Licha ya upinzani mkali, hususan kutoka kwa makundi ya kibaguzi yenye mrengo mkali, Kansela Angela Markel amekuwa mstari wa mbele sio tu kuhamasisha nchi za Magharibi zipokee wakimbizi, bali pia ameruhusu idadi kubwa kabisa ya wakimbizi kuingia na kuishi katika nchi hiyo.

Kama kuna 'nafuu' kidogo, basi ni hiyo asili yake ya Iran, nchi ambayo ni nadra kuzalisha magaidi. Pia ukweli kuwa alijiuawa mwenyewe inaweza kuendana na hiyo theory ya pili hapo juu kuwa magaidi wa ISIS na wenzao huwa hawajiuwi kwa kujipiga risasi, huuawa kwa kupigwa risasi au kujilipua wenyewe, na kwa kufanya hivyo huwa wamejitoa mhanga kwa ajili ya imani yao.

Hata hivyo, huo u-Iran wake unaweza kuwapa nguvu wabaguzi wa rangi kuendeleza upinzani wao dhidi ya serikali ya Kansela Markel kuruhusu ujio wa wakimbizi nchini humo, ambao wanatizamwa kama 'magaidi watarajiwa.'

Endelea kutembelea blogu hii kwa uchambuzi wa kina wa mada mbalimbali kama hii inayohusu masuala ya intelijensia, na nyinginezo.







1 comment:

  1. Makala hizi zimenisaidia kupanua uelewa wangu kuhusu ushushushu wakati naandika kitabu changu. Kitabu inachoandika haikizungumzi tasinia hii ya ushushushu lakini ina kipengele kinachohusisha upeplezi wa ishu fulani. Pia hongera unanadika kwa Kiswalihi kizuri, kinachoeleweka! J.M

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.