21 May 2017


Baada ya safari ya muda mrefu iliyodumu takriban miaka 20 sasa, ya uandishi wa makala magazetini, hatimaye nimeamua kutundika daluga (kustaafu)

Nilianza rasmi uandishi mwaka 1998, nilipokuwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Mlimani. Aliyenishawishi kuingia kwenye fani hiyo ni aliyekuwa mwandishi mkongwe, Albert Memba, ambaye alidai kuwa nina kipaji cha asili cha kuandika.

Nilianza uandishi katika gazeti la kwanza kabisa la udaku, lililokuwa linajulikana kwa jina la "Sanifu." Gazeti hili lilikuwa maarufu sana, na mpaka leo sijui kwanini halikudumu muda mrefu. 

Wakati nikiwa 'Sanifu' sikuwa nikiandika makala as such bali nilikuwa na safu yangu iliyohusu unajimu, well sio kama ule wa Marehemu Sheikh Yahya lakini karibu kidogo. Ulikuwa utani wa aina flani ambao baadhi ya watu waliuchukulia serious. Na kama 'kachumbari,' ninajipa jina la 'Ustaadh Bonge.' Na hadi leo baadhi ya marafiki zangu wa enzi za Mlimani (UDSM) wananiita jina hilo.

Baadaye nikapata kolamu katika gazeti jipya la 'Kasheshe.' Hili lilikuwa gazeti la pili nchini Tanzania lililohusu udaku. Na huko nako nilikuwa na safu inayohusu unajimu, nikiendelea na jina la 'Ustaadh Bonge.' Nilikuwa nikifarijika kila nilipomsikia marehemu Julius Nyaisanga akieleza wasomaji watarajie nini kwenye toleo la wiki husika la gazeti la Kasheshe huku akiwakumbusha "bila kusahau safu ya unajimu ya Ustaadh Bonge." Sema enzi hizo hata neno "kiki" lilikuwa halijazaliwa.

Na kuna watu ambao baada ya mie kujitambulisha walipatwa na mshangao na kusema, "ah mie nilijua Ustaadh Bonge ni mzee flani wa pwani..." na mie nikiishia kucheka tu. 

Baadaye tena nikapata safu kwenye gazeti-dada la 'Kasheshe' lililoitwa 'Komesha,' ambako pia niliendelea na 'unajimu' wangu nikitumia jina lilelile la Ustaadh Bonge.

Hatimaye likaanzishwa gazeti jipya la habari na makala lililojulikana kwa jina la 'Kulikoni.' Na hili ndilo hasa lililopelekea kuzaliwa kwa jina la blogu hii yaani 'Kulikoni Ughaibuni.' Blogu hii ilianzishwa kwa lengo la kuwa sehemua mabyo Watanzania walio nje ya nchi wangeweza kusoma makala zangu zilizochapaishwa katika gazeti la 'Kulikoni' lakini hazikuwepo mtandaoni kwa vile gazeti hilo halikuwa na tovuti. 

Kumbuka wakati huko kulikuwa hakuna Facebook, wala Twitter, wala Instagram, wala selfie...hizo zilikuwa zama za Hi5, Myspace, na kwa Tanzania kulikuwa na blogu chache tu na mtandao maarufu wa DarHotWire. 

Anyway, kwa vile nilikuwa nakabiliwa na majukumu mbalimbali, ilibidi niachane na uandishi katika magazeti ya udaku na kukazania uandishi wa makala. Safu yangu katika gazeti la 'Kulikoni'  ilikuwa ikijulikana kama 'Kulikoni Ughaibuni.'

Baadaye kidogo nikapata safu kwenye gazeti la Mtanzania, nikaipa jina 'Mtanzania Ughaibuni,' kabla ya kuanzishwa kwa gazeti la Raia Mwema ambako nilikuwa miongoni mwa wana-makala wa awali kabisa, na safu yangu ikijulikana kama 'Raia Mwema Ughaibuni.'

Moja ya matukio ambayo sintoyasahu katika uandishi wa makala ni uamuzi wangu wa kuvalia njuga sakata la Richmond. Licha ya kujivunia kama mwana-makala pekee niliyevalia njuga suala hilo vya kutosha, athari zake zilikuwa kubwa mno. Kilichotokea wakati huo ndio kilichonisukuma kumuunga mkono mgombea wa CCM kwenye nafasi ya urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, John Magufuli. 

Uandishi wa makala ulinikuta nikikumbana na 'msala' mwingine mwaka 2013, ambapo mwanzoni mwa mwezi Februari (mwaka huo) nilijulishwa na vyombo vya dola hapa Uingereza kuwa kulikuwa maisha yangu yalikuwa hatarini.

Kwahiyo hadi kufikia uamuzi wa kustaafu uandishi wa makala magazetini ni takriban miaka 20 sasa (actually ni miaka 19, yaani 2017 kutoa 1998).

Nikipima 'faida' na 'hasara' za uandishi wa makala hizo, jibu ni rahisi kabisa: faida zilizidi hasara. Ndio, uandishi wa makala hizo umenigharimu mno kimaisha, lakini ndani kabisa ya nafsi yangu ninaamini kuwa uamuzi wangu kuwasemea wasio na sauti (to be the voice of the voiceless) ulikuwa uamuzi sahihi.

Ninaamini ilikuwa sahihi kusimama kidete kuhusu skandali ya Richmond, tangu mwanzo hadi mwisho, licha ya gharama kubwa kimaisha kwa upande wangu.

Ninaamini nilikuwa sahihi kwa safu zangu kuwa sauti adimu iliyopigania haja ya mageuzi katika Idara ya Usalama wa Taifa, kwa minajili ya kuondoa siasa katika utendaji kazi wa taasisi hiyo muhimu, kuhamasisha uzalendo na kwa ujumla kubaki kuwa chombo muhimu kwa ustawi wa Tanzania yetu.

Uandishi wa makala umenitengenezea marafiki wengi mno, japo pia umenitengenezea maadui wachache wenye nguvu kisiasa au kijamii. Na jana nilipotoa taarifa rasmi huko Facebook nilipata fursa adimu ya kufahamu kuwa kumbe kuna idadi kubwa tu ya watu waliovutiwa na makala zangu.

Uamuzi wangu kustaafu uandishi wa makala magazetini hauhusiani na 'yaliyonikumba wiki hii inayoisha leo.' Kwa upande mmoja nilipewa taarifa na ushahidi kuwa Rais Magufuli hakupendezwa na makala yangu ya mwisho katika gazeti la Raia Mwema, ambayo ndani yake nilimkosoa kuwa "yeye kama Amiri Jeshi mkuu ni mfariji mkuu pia na anapaswa kuhudhuria misiba ya kitaifa.

Japo kumkosoa kwangu hakukuwa tofauti na kauli ya Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa ambapo kiongozi huyo wa Chadema alieleza bayana kushangazwa kwake na hatua ya Rais kutohudhuria msiba wa wanafunzi 32 wa shule ya Lucky Vncent ya Arusha, akisisitiza kwamba ni msiba mzito kitaifa ambao ilipaswa Rais kuhudhuria.

Wakati kauli ya Lowassa ilijibiwa na Ikulu, mie makala yangu imepelekea msala ambao nitauelezea siku nyingine.

Kwa upande mwingine, kuna watu waliohojiwa kuhusiana na tweet ya utani niliyoandika kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Ni kwamba, katika 'mila na desturi' za Twitter, kuna kitu kinaitwa 'future tweet,' ambacho huandikwa kama alama ya reli #FutureTweet. Kitu hicho hutumika kama utani unaoashirika kuwa 'sikuzijazo kutakuwa na tweet ya aina hii baada ya kitu hiki kutokea.' 

Ni UTANI usiopaswa kuipotezea muda serikali sio tu kuandika taarifa rasmi za kuukanusha na kuahidi kuchukua hatua bali pia kuhoji watu kadhaa kuhusu mie mwandishi wa #FutureTweet hiyo. Huu ni UTOTO. Serikali ilioingia madarakani kwa mbwembwe za #HapaNiKaziTu inaonekana kioja kwa sio tu kushindwa kuelewa #FutureTweet ni kitu gani bali pia kituko kwa kufikia hatua ya kukanusha #FutureTweet na hatimaye kuhoji watu kuhusu mie mwandishi wa #FutureTweet hiyo. 

Niwe mkweli, sikupendezwa na gazeti la Raia Mwema kutonijulisha kuwa walihojiwa kuhusu mie na kisha kutonambia kuhusu suala hilo. Kama walifanya hivyo kwa sababu ya uoga wao au waliamriwa kunificha, binafsi nimetafsiri kama 'wameninyima ushirikiano,' na sioni umuhimu wa kuendelea kuwa mwana-makala katika gazeti hilo. 

Lakini kubwa zaidi, sitaki kuwasababishia usumbufu wasiostahili. Ungetegemea gazeti kubwa kama hilo lingepata ujasiri kuzungumzia kadhi hiyo ya kubughudhiwa na serikali kwa ajili yangu lakini ni wazi kuwa vyombo vyetu vya habari vimetishwa na tishio la Rais Magufuli kuwa "visidhani vina uhuru kiasi hicho." 

Nihitimishe makala hii kwa kuwashukuru nyote mliosoma makala zangu mbalimbali katika miaka hii takriban 20 ya utumishi wangu kwenu. Naomba ifahamike kuwa kustaafu kuandika makala magazetini hakumaanishi kuwa nimestaafu pia katika kublogu. Hapana. Na pia haimaanishi nimestaafu kuwa muumini wa #SharingIsCaring. Nitaendelea kutumia mitandao ya kijamii kuelimisha, kuhabarisha, kukosoa...na pengine kuburudisha.

Nimeitumikia Tanzania yangu vya kutosha. Licha ya takriban miaka 20 ya uandishi wa makala, niliitumia Tanzania yangu kwa uadilifu mkubwa kama mtumishi wa serikali, na pia kupitia #SharingAndCaring na kublogu na uandishi wa vitabu.Lakini kubwa zaidi ni kwa kuwa raia mwema, ambaye licha ya kuwa mbali na nchi yangu, nimejitahidi kuwatumikia Watanzania wenzangu angalau kwa kushiriki mijadala muhimu kuhusu mustakabali wa taifa letu.

Licha ya kuwa nitaendelea kublogu, kuandika vitabu na kudumisha #SharingAndCaring kwenye mitandao ya kijamii, kustaafu uandishi wa makala magazetini kunanipa fursa ya kuanza safari mpya ya maisha yangu: kuzalisha 'waleta mabadiliko wa kesho' (future change makers) kupitia ujasiriamali jamii (social entreprenuership). 




3 comments:

  1. Ya kuandika ni mengi sana kaka kuhusu wewe. Mi nakuombea sana kwa Mwenyezimungu nguvu yake na nuru yake vyote vizidi kuwa karibu yako. Nashukuru sana kwa ushauri na ukaribu wako kwangu. Nakupenda sana kaka.

    ReplyDelete
  2. Mhuu mbona hivyo wakati bado

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.