Showing posts with label COVID-19. Show all posts
Showing posts with label COVID-19. Show all posts

22 Mar 2020


#Thread: Awali nilipangilia kuwa thread hii iwe maalum kwa ajili ya kueleza jinsi hali ilivyo hapa Uingereza kuhusiana na janga la #Coronavirus kwa matarajio kwamba nanyi huko nyumbani au kwingineko duniani mnaweza kuwa na moja au mawili ya kujifunza. 

Hata hivyo, katika pitapita zangu kabla ya kuandika thread hii nilikutana na makala moja ndefu kuhusu jinsi janga la jorona lilivyoibuka nchini Italia na kwanini nchi hiyo imeathirika vibaya mno, na pia endapo kinachojiri nchini humo ni "template" ya yatayojiri kwingineko. 

Kwahiyo nadhani ni vema nikianza kuongelea kwa kifupi kuhusu makala hiyo, maana ina funzo kwa sie tulioko huku na kwa nyie mliopo huko. 

Kwa kifupi kabisa, moja ya sababu iliyopelekea maambukizi kuwa makubwa na ya kasi nchini Italia ni kusuasua kwa mamlaka kuchukua hatua stahili. 

Kwa mujibu wa makala hiyo, Italia ilikuwa na fursa nzuri ya kujikinga na janga hilo endapo tu kusingekuwepo dhana kwamba "korona ni sawa na mafua tu," (nikamkumbuka MwanaFA na madai yake ya "malaria ni hatari zaidi kuliko korona") na hisia kuwa "korona ni tatizo la China pekee. "

Kilichopaswa kufanywa na mamlaka za taifa hilo ni
(a) "kuyatenga" maeneo yenye maambukizi
(b) kuzuwia movements za watu kitaifa na kuhakikisha sheria kali zinatumika kuhakikisha utekelezaji
(c) mfumo wa mawasiliano usiokanganya kutoka kwa mamlaka husika kwenda kwa wananchi. 

Inaelezwa kuwa katika siku za mwanzo za mlipuko wa janga hilo, Waziri Mkuu wa Italia Conte na viongozi wengine wa ngazi zajuu walijaribu kujenga picha kuwa ugonjwa huo sio tishio kwa nchi hiyo. Walijenga imani feki kuwa mambo ni shwari #tupovizuri

Na hata maambukizi yalipozidi kukua, maelezo yaliyotolewa ni kwamba ongezeko hilo ni matokeo ya "aggressive testing" yaani jitihada kubwa za kupima watu mbalimbali bila hata kujali kama wana dalili za maambukizi. Na kulijitokeza lawama dhidi ya approach hiyo. 

Kama ambavyo sura ngumu Polepole alivyodai majuzi kuwa Tanzania ikifunga mipaka itaathiri sekta ya utalii, awali baadhi ya viongozi wa Italia ikiwa ni pamoja na Waziri Mkuu Conte walikuwa namtazamo kuwa hatua kali dhidi ya korona zingeathiri uchumi wa nchi hiyo. 

Lakini pengine kikubwa zaidi ni kwamba Italia iliangalia kilichokuwa kinatokea China kama "filamu ya sayansi ya kutunga (science fiction movie) ambayo haiwahusi Wataliano."

Kichekesho ni kwamba hali ilipoanza kuwa mbaya nchini Italia, nchi nyingi hasa barani Ulaya na Marekani ziliangalia kinachotokea huko kama "tatizo la Italia tu" kama ambavyo awali Italia ilivyoiangalia korona kuwa ni "tatizo la China tu."

Mtu anayedhaniwa kuwa ndio "msambazaji wa kwanza wa korona" (Patient One) ni mwanaume wa miaka 38 ambaye Februari 18 alikwenda hospitali akiwa na mafua makali lakini hakuna aliyebaini kuwa ni mwathirika wa korona. Na kibaya zaidi, mgonjwa huyo alikataa kulazwa/

Hata hivyo, siku hiyohiyo jamaa huyo alirudi tena hospitalini hapo na kulazwa kwenye wodi ya kawaida (yaani isiyo maalum kwa ajili ya wagonjwa flani). Siku mbili baadaye alizidiwa mno, akapelekwa ICU ambako vipimo vilionyesha ana maambukizi ya korona

Kabla ya kukutwa na korona, mtu huyo alizunguka sehemu mbalimbali ambapo miongoni mwa matukio muhimu ni kuhudhuria pati tatu, alikwenda kucheza futiboli na pia alishirki kwenye jogging na timu ya soka. Yote hayo yalijiri wakati mtu huyo tayari ana maambukizi ya korona

Lakini la kupigia mstari ni kwamba hakuwahi kukutana na mtu yeyote kutoka China wala kutembelea China. 

Maana yake ni kwamba mtu huyo aliambukizwa humohumo Italia, which means kabla yake tayari kulikuwa na mtu/watu wenye maambukizi ya ugonjwa huo. 

Kwa kumalizia kuhusu kilichojiri Italia, moja ya vitu vilivyochangia sana mkanganyiko katika siku za awali ni kitu wanaita "infodemic" yaani kama "pandemic ila inayohusu information."

Kwa hapa Uingereza, hali ni mbaya. Na inatarajiwa kuwa mbaya zaidi. 

Tatizo la hapa ni kama ilivyokuwa Italia, ambapo kulikuwa na kusuasasua kuchukua hatua stahili. Kwa mfano, badala ya "kufunga kila kitu" mapendekezo ya mwanzo yalikuwa kitu kinaitwa "herd immunity."

Herd immunity ni kuacha maambukizi yasambae kisha wingi wa walioambukizwa upelekee kinga ya baadaye dhidi ya wasioambukizwa. 

Matarajio ni kwamba mtu akishaambukizwa virusi vya ugonjwa husika na kupona, anakuwa na kinga ya kuzuwia kuambukizwa tena. 

Lakini wazo hilo la herd immunity lilipingwa vikali hasa baada ya kubainika kuwa lingeweza kupelekea vifo laki mbili unusu au zaidi. 

Kwahiyo serikali ya Waziri Mkuu Boris Johnson ikaja na mkakati wa "watu kujitenga" (social distancing). 

Social distancing inamaanisha hatua kama wafanyakazi kutokwenda makazini na kufanyia kazi kutoka majumbani, sambamba na watu kukwepa kukutana kusiko kwa lazima. 

Kadhalika, mkazo umewekwa kwenye kuongeza kasi ya kupima watu wenye dalili za maambukizi ya korona. 

Sambamba na hilo ni hatua kali dhidi ya mikusanyiko, na kufungashule, sehemu za starehe mabaa, na kupunguza safari za vyombo vya usafiri. Kadhalika, serikali imewekeza vya kutosha kwenye tafiti mbalimbali za kusaka kinga na tiba ya korona. 

Vilevile serikali imechukua jukumu la kulipa asilimia 80 ya mishahara ya waajiriwa ili kuwezesha waajiri kuruhusu wafanyakazi wao wasiende kazini au wafanye kazi kutokea nyumbani. Ikumbukwe pia kuwa hapa watu wasio na kazi hulipwa posho ya kujikimu na ya makazi. 

Inatarajiwa kuwa wiki 12 zijazo zitakuwa ngumu sana kwa nchi hii kwa sababu ndio kipindi ambapo jitihada kubwa zinafanyika kuzuwia maambukizi mapya sambamba na kuzuwia kusambaa kwa maambukizi yaliyopo huku ikitarajiwa kuwa mamilioni ya watu wataweza kujipima wenyewe majumbani. 

Tayari makampuni mbalimbali yamesitisha uzalishaji wa bidhaa zao na kuelekeza nguvu kwenye uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zinazohitajika katika kipindi hiki cha janga la korona hapa Uingereza. Lakini ni ngumu kubaishiri kuwa hatua hizo zinazochukuliwa muda huu zitafanikiwa kukabili janga hilo.

Kwa upande mmoja, ugonjwa huo ni mpya na upya huo unapelekea ugumu wa kuuelewa vizuri. Kwa mfano hakuna uhakika wa kutosha kuwa mtu akipona hatoambukizwa tena. 

Kuhusu huko nyumbani, kwa kweli mie binafsi nina wasiwasi mkubwa. Kwa upande mmoja, licha ya majigambo ya watawala wetu, sie ni masikini wa kutupa. Hatuna uwezo wa lolote bila kutegemea wafadhili. Kibaya ni kwamba wafadhili wetu nao wapo vitani dhidi ya korona. 

Lakini pengine adui mbaya zaidi kwetu ni kasumbailiyoota mizizi ya kufanya kila jambo kuwa ni la kisiasa. Majuzi mmemsikia sura ngumu Polepole akiufananisha ugonjwa wa korona na wapinzani. Na akajigamba kuwa kama wanavyomudu kupambana na wapinzani basi wataimudu korona pia. 

Wakati ambapo taifa linapaswa kuwa kitu kimoja, hawa wahuni wanaleta mzaha wa siasa. Lakini korona hii si ya kuchezewa maana haibagui kati ya huyu wa chama tawala na huyu mpinzani wala kiongozi na raia wa kawaida. 

Pia tuna tatizo la "infodemic."Pandemic ya information. Kwa upande mmoja ni jitihada za akina Bashite kutumia watu kuhadaa kuwa hali ni shwari, kosa ambalo kama umefuatilia vema thread hii linaigharimu Italia na hata Uingereza na Marekani. 

Lakini pengine baya zaidi ni taarifa ninazopokea kila siku kuwa sehemu kadhaa wananchi wamepigwa marufuku "kuongelea korona," ikiwa ni pamoja na watumishi wa sekta ya afya kutishwa kwamba wakiripoti matukio ya korona kwenye hospitali zao wataadhibiwa. 

Mwisho, tuna Bwana @MagufuliJP ambaye hadi leo sijui siku ya ngapi hajaona umuhimu wa kujitokeza hadharani kuongea na Watanzania. Hizi sio dharau tu bali ni kukosa utu. Lakini hali hiyo imeshazoeleka sasa. Kila linapotokea janga anaingia mitini. 

Hata hivyo, tunashukuru tumefanikiwa kupata uongozi mbadala wa Mheshimiwa @zittokabwe ambaye juzi alihutubia taifa kuhusu janga la korona, hotuba bora kabisa yenye taarifa za kutosha na iliyojaa upendo kwa Watanzania. Icheki hapa (youtu.be/Jc7ZD3PDrXc)

Nimalizie kwa kuwasihi nyote mchukue tahadhari dhidi ya janga hili. Pia ni muhimu kukazania sala/dua. Pia tufahamishane taarifa mbalimbali hususan zinazofichwa kwa minajili ya kisiasa au zozote zile zitakazoisaidia jamii kukabiliana na korona.

Be safe. Jumapili njema

UPDATE: Hatimaye Rais Magufuli amehutubia Taifa japo baadhi ya kauli zake zinaweza kuwa kukwaza jitihada za mapambano dhidi ya #coronavirus. Pichani ni baadhi ya kauli hizo





9 Mar 2020


#Thread: Naamini kwamba takriban kila mmoja wetu - hata wale wenye uadui na news - wanafahamu kuhusu balaa jipya la virusi vya #Corona.

Na ni balaa kubwa kweli kweli, maana licha ya wataalam wa afya kutofahamu kwa undani hukusu virusi hivyo, kuna mambo kadhaa yanayoweza kulifanya janga hilo kuwa kubwa zaidi. Hadi wakati naandaa #thread hii, idadi ya maambukizi imevuka watu 100,000 na zaidi ya nchi 90 duniani zimeripoti kufikwa na janga hilo. Japo takriban nusu ya waliokumbwa na virusi hivyo wamepona, idadi ya maambukizi mapya inazua tafaruki kubwa. 

Lakini hofu kubwa zaidi ni pindi janga hilo litakaposambaa barani Afrika, bara ambalo linakabiliwa na changamoto lukuki. Tayari takriban nchi 8 za Afrika zimeripoti maambukizi ya virusi hivyo. Nchi hizo ni Misri, Aljeria, Naijeria, Senegal, Kameruni, Togo, Moroko, na karibu nasi (Afrika Mashariki) ni Afrika Kusini ambakoidadi ya maambukizi hadi jana ni watu wawili. 

Siku chache zilizopita nilihudhuria mkutano flani hapa Uskochi, na japo haukuhusu masuala ya afya, suala la virusi vya #corona liliibuka kwenye maongezi. Kilichonisikitisha ni kwamba watu wengi walionekana kudhani kuwa (a) hofu kuhusu virusi hivyo inakuzwa kuliko hali halisi (b) virusi hivyo ni sawa tu na vya mafua (flu)

Tunaishi katika zama ngumu kwa kweli. Ofkoz, tuna janga jingine (japo si hatari kama virusi vya #corona) na #fakenews. Na kwa hakika watu wana sababu za msingi kutoamini baadhi ya vyombo vya habari hasa kutokana na kasumba ya "kuongeza chumvi" au kuongopa waziwazi. 

Hata hivyo, licha ya kasoro hizo, tegemeo kubwa zaidila kupata jabari ni kwa kupitia vyombo vya habari hivyo hivyo ambavyo baadhi ya watu hawana imani navyo. Na yayumkinika kuamini kuwa endapo vyombo vya habari vikipuuzia kuhusu virusi vya #corona vitaishia kulaumiwa. 

Kuna "janga" jingine huko Marekani. Janga hili ni Donald Trump na wapambe wake. Kwa upande mmoja Trump na wapambe wake wanaamini kuwa "janga hilo la virusi vya #corona linakuzwa makusudi ili yeye aonekane hafai, na hivyo asichaguliwe tena kwenye uchaguzi mkuu ujao hapo Novemba."


Kwa upande mwingine, Trump na chama chake ni "maadui wa kudumu dhidi ya sayansi." Kwahiyo si jamba la kushangaza kusikia wengi wao wakidai "virusi vya #corona havina tofauti na vile vya mafua (flu)," na kwamba taarifa za wanasayansi na vyombo vya habari ni #fake news. 

Virusi vya #corona ni janga pia kwa sababu kutokana na "upya" wake, inawawia vigumu wataalam wa afya kufahamu vya kutosha kuhusu janga hilo, na hivyo kuwa ngumu kwao kupambana nalo. Ni vigumu kukabiliana na adui usiyemjua vizuri. 

Lakini kama "upya" huo wa virusi hivyo hautoshi kuwa janga kubwa, kuna tatizo jingine la jinsi maambukizi yanavyosambaa kwa kasi. Kwahiyo kwa upande mmoja kuna "race against time" kutafuta chanjo na/au tiba, na kwa upande mwingine ni kukabiliana na maambukizi mapya. 

Ni kwamba, hata mtu akiona dalili zakuwa na virusi vya #corona, anapokwenda hospitali anaweza asipatiwe tiba "ya maana" zaidi ya "tiba ya mafua" kwa sababu hadi muda huu hakuna tiba dhidi ya virusi hivyo. Nimetanabaisha awali kuwa janga hili likisambaa barani Afrika itakuwa balaa kubwa hasa kwa sababu bara hilo linakabiliwa na chngamoto nyingi.

Changamoto hizo ni pamoja na umasikini. Licha ya umasikini ambao umedumu miaka nenda miaka rudi huku baadhi ya wanasiasa wakishindana kutumia #fakenews kuwaaminisha wananchi kuwa umasikini unapungua, kuna umasikini unaochangiwa na vipaumbele fyongo vya serikali zilizo madarakani. 

Pengine ni vema kutumia mifano hai. Kwa mfano wa Tanzania yetu, wakati ununuzi wa bombadia ni muhimu, uwekezaji kwenye sekta ya afya ni muhimu zaidi. Na hauhitaji kuwa mwelewa sana wa Tanzania yetu kubaini kuwa mabilioni yaliyotumika kununua bombadia yalihitajika zaidi mahospitalini.

Kwahiyo moja ya sababu zinazochangia umasikini wa nchi nyingi za Afrika ni vipaumbele fyongo vya watawala. Na japo twaombea Mola aepushe janga hilo lisifike huko nyumbani, vipaumbele vya watawala wetu ni moja ya vikwazo hata wakati huu. 

Kama ambavyo Trump yupo bize kuonyesha kila kitu kipo vizuri huku maambukizi yakisambaa, watawala wetu nao wapo bize kujigamba kuwa "tupo vizuri" ilhali twaelewa vema kuwa wababaishaji hawa hawana A wala B wajualo katika kujiandaa kukabiliana na janga hilo. 

Na majuzi tu tumeshuhudia lundo wa watalii kutoka China wakiwasili huko KIA. Yaani wakati nchi zilizopiga hatua kubwa kimaendeleo zikidhiditi wasafiri kutoka China, sie hohehae twafanya ubishi katika suala hatari kama hili. Niliandika kirefu kuhusu hilo katika makala hii "Hatuna Uhaba Wa Vingozi Wapumbavu Lakini Hili La Kupuuza #Coronavirus Ni Zaidi Ya Upumbavu (bit.ly/2wHI8oA)

Wakati tunapaswa kuendelea kumuomba Mola ili janga hilo lisitie mguu huko nyumbani, ni muhimu pia kujiandaa kisaikolojia endapo (God forbid) hatimaye litafika huko.atuna Uhaba wa Viongozi Wapumbavu Lakini Hili La Kupuuza #Coronavirus Ni Zaidi Ya Upumbavu

Kuna watakaolaumu kuwa "unatisha watu bure) lakini naamini kuwa ni vema kuchukua tahadhari kabla ya hatari. Majuzi, Rais Cecil Ramaphosa wa Afrika Kusini alipotangaza kuwa tayari nchi hiyo ina mgonjwa mmoja (wapo wawili hadi wakati naandika makala hii), alitanabaisha kuwa haoni haja ya kuficha ukweli kuwa nchi hiyo nayo imekumbwa na janga hilo. 

Nimegusia hilo kwa sababu utawala wa wa Rais @Magufuli umekuwa maarufu mno kwenye "kanusha,kanusha, na kanusha zaidi." Ni utawala unaotaka kuongelea "habari njema" tu. Je kwa bahati mbaya, virusi hivyo vikiingia Tanzania (Mola aepushie mbali hili), hawatokanusha pia? 

Enewei, lengo la #thread hii sio kuzungumzia vitu vya kufikirika - kwa mfano hali itakuwaje pindi virusi vya #corona vikiingia Tanzania - japo ni muhimu kuchukua tahadhari kabla ya hatari. Badala yake, lengo ni kutoa elimu kuhusu virusi hivyo, kwa lugha rahisi kueleweka. Na kwa vile mie sio tabibu, nitaeleza kwa lugha isiyo ya kitalaamu/kitaaluma, kwa kimombo wanasema "in layman's language."

Kwanza, wakati janga hilo linafahamika zaidi kwa jina la virusi husika, yaani #coronavirus, maradhi yanayotokana na maambukizi ya virusi hivyo yanafahamika kama COVID-19, kifupi cha "Corona Virus Disease 2019."

Japo kama nilivyoeleza awali kuwa mengi hayafahamiki kuhusu virusi na maradhi husika, watu walio kwenye hatari zaidi ya maambukizi ni ambao tayari wana magonjwa mengine na watu ambao kinga za mwili ni pungufu. Kundi hili linajumuisha watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi. 

Lakini kana kwamba habari hiyo sio mbaya, kwa Afrika kuna tatizo la ziada kuhusu "uhusiano kati ya virusi vya #corona na watu ambao tayari wana maradhi mengine." Kutokana na sababu mbalimbali, kuna idadi kubwa ya watu barani Afrika ambao wana "maradhi mengine" lakini hawafahamu. Aidha hawafahamu kwa vile hawajafanya jitihada ya kufahamu kuhusu afya zao au hawajafahamu kwa sababu wana vipaumbele vingine muhimu zaidi ya kufahamu kuhusu afya zao.

 Kuna watu wanakwepa kupima ukimwi kwa vile "wana mambo mengi mno kichwani, na wasingependa kuongeza mengine (kama kubaini wana ukimwi baada ya kupima).Na huwezi kumlaumu mtu "anayekwepa habari mbaya kwa vile hata akijua hatojua cha kufanya kuhusu habari hiyo mbaya.

Kingine cha kuogofya kuhusu virusi hivyo ni ukweli kwamba ni vigumu mno kukwepa "mikusanyiko" katika maisha yetu ya kila siku barani Afrika. Hebu pata picha ya sehemu kama "Shimoni Kariakoo" au kwenye jinsi daladala zinavyopenda "nyomi" (hivi msamiati huu bado hai?)

Kama nilivyotanabaisha awali, kuna wanaodai "COVID-19 ni sawa na mafua tu." Japo mie si mwanasayansi, lakini kwa mujibu wa takwimu zilizopo, wakati "kiwango cha vifo" (mortality rate) kwa mafua ni 0.1%, kwa upande wa COVID-19 tayari ni 2.5% na huenda kiwango hicho kikaongezeka. 

Hata hivyo, kiwango hicho ni kidogo kulinganisha na "majanga" mengine kama Ebola, ambayo "mortality rate" yake ni kati ya 25% na 90%. Again, hali inaweza kuwa mbaya zaidi kwa upande wa COVID-19 kutokana na kusambaa kwake kwa kasi. 

Wengi wa wanaopatwa na maambukizi ya virusi vya #corona huwa na dalili kama za homa kidogo, kikohozi na kupumua kwa shida kidogo. Takriban 20% ya wagonjwa afya zao huwa mbaya na kupatwa na "numonia" (pneumonia) na matatizo makubwa ya kupumua yanayoweza kupelekea mtu apumue kwa mashine.

Lakini si kila anayeambukizwa virusi vya #corona huugua sana au kwa wastani. Makundi yaliyo kwenye hatari zaidi ni watu ambao tayari wana maradhi mengine kabla ya kuambukizwa virusi hivyo: 5.6% kwa wenye kansa; 6% kwa wenye "BP," 6.3%; 7.3% kwa wenye kisukari na 10.5% kwa wenye ugonjwa wa moyo. 

Kundi lililo kwenye hatari kubwa zaidi ni wazee wenye miaka 80 na kuendelea, wakiwa na takriban 15 ya maambukizi ya virusi hivyo hatari. Hata hivyo, habari njema ni kwamba watoto hasa wenye chini ya umri wa miaka 9 wanaonekana kutoathiriwa na janga hilo. 

Kadhalika, takwimu zilizopo zinaashiria kuwa wanaume wapo hatarini zaidi kuliko wanawake, lakini takwimu hizo zinaweza kuathiriwa na ukweli kwamba kwa mahali zilipokusanywa, yaani China, wanaume wengi huvuta sigara kuliko wanawake. Hadi muda huu wataalamu hawajui inachukua muda gani kwa virusi hivyo. 

Hata hivyo kwa wanaopatwa na maambukizi ya virusi vya #corona na hatimaye kuugua ugonjwa wa COVID-19, dalili huwa homa, kikohozi na "kuishiwa pumzi," lakini ni za muda mfupi tu. Kadhalika, mtu akifikia hatua ya kuugua COVID-19, seli za njia ya hewa kwenye mapafu huathirika, lakini kuathirika huko "hushtua" kinga ya mwili ambayo hatimaye hukabiliana na virusi vilivyosababisha maradhi hayo, yaani vya #corona. Ndio maana watu wenye mapungufu kwenye kinga ya mwili wanakuwa kwenye hatari pindi wakiambukizwa virusi hivyo.

Njia zinazoshauriwa "kupunguza uwezekano wa maambukizi ya virusi vya virusi hivyo" ni pamoja na kutowajongelea watu wenye maambukizi; kuepuka kufikicha macho na kuepuka kugusa mdomo na pua; kutotoka nyumbani pindi endapo unaumwa; kuziba mdomo kwa tishu pindi unapopiga chafya au kukohoa, na kutupa tishu baada ya kuitumia;


Ushauri wa muhimu zaidi ni kunawa mikono mara kwa mara, na kwa wastani wa sekunde 20, hususan baada ya kwenda msalani, kabla ya kula, baada ya kupiga chafya au kukohoa. Sijui kama unafahamu hili, ila "kanuni isiyo rasmi" ya kunawa mikono ni "kunawa mikono huku unaimba wimbo wa hepi besidei mpaka uishe." Kwa wastani, wimbo huo una sekunde 20

Nimalizie #thread hii kwa kurudia kukumbusha kuwa mie si mwanasayansi wala mtaalam wa afya. Nimeandika #thread hii kwa msaada wa machapisho mbalimbali kuhusiana na virusi vya #corona na ugonjwa wa COVID-19. Nakaribisha kukosolewa na wataalam.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.