Showing posts with label FEGI.LONDON. Show all posts
Showing posts with label FEGI.LONDON. Show all posts

3 Sept 2007

Asalam aleykum,

Nianze na nyepesi nyepesi.Majuzi,kibibi kimoja kilisherehekea “bethdei” yake ya 100 (karne hiyo!!) kwa kuvuta sigara yake ya 170,000 (naomba kusisitiza,laki moja na alfu sabini).Kikongwe hicho,Anne Langley,mkazi wa Croydon,kusini mwa jiji la London,alianza kuvuta sigara siku chache baada ya kuibuka kwa vita kuu ya kwanza ya dunia mwezi Juni mwaka 1914,wakati huo akiwa na miaka mitano tu.Na aliadhimisha kutimiza karne moja tangu azaliwe kwa kuwasha “mche” wake (sigara) kwenye mshumaa ulopandikizwa kwenye keki yake ya kumtakia “hepi bethdei.”Anne,aliyepachikwa jina la utani la “mstaafu mwenye mapafu ya chuma (iron-lunged pensioner)” anasema alianza “kubobea” kwenye vutaji sigara siku tano tu tangu aanze kuvuta na tangu wakati huo hajafikiria kuacha fegi licha ya kampeni kali kabisa zinazoendeshwa kumshawishi wavutaji watundike madaluga (majuzi serikali ya hapa imetangaza kwamba kuanzia mwakani pakti zote za sigara zitakuwa na picha “za kutisha” kuonyesha madhara ya sigara kwenye mwili wa mvutaji).Alipoulizwa siri yake ya kuvuta sigara kwa muda mrefu namna hiyo pasipo kudhurika,kibibi huyo alidai kwamba siri yake pekee ni kuwa katika muda wote ambo amekuwa mvuta sigara hajawahi kumeza moshi.Mie nadhani pengine siri yake kuu ni hayo “mapafu ya chuma”,na chuma chenyewe ni kile kisichishika masizi au kutu,au chuma cha pua.

Tukiendelea kucheza kwenye mada hiyo hiyo “ya hovyo hovyo” ya fegi,mwanamama mmoja huko Sweden amepigwa stop kuvuta sigara uwani kwake kwa vile jirani wanayepakana ana “allergy” na moshi wa sigara.Mahakama ya mazingira katika mji wa Arkapin uliopo kusini mwa Sweden,ilimwamuru Ingela Olofsson ku-stop mara moja kuvuta sigara awapo uwani kwani jirani yake,mwanasheria Richard Berggren,alidai kuwa huwa analazimika kuvaa “oxygen mask” kila asubuhi wakati anapokwenda kwenye gari lake analilipaki uwani karibu na jirani yake huyo,na kila anaporejea jioni kutoka kazini,.Vita kati ya majirani hao imedumu kwa kitambo sasa kabla ya kufikishwa mahakamani ambapo mwanzoni suluhu ilitafutwa kwa njia za kidiplomasia pasipo na mafanikio.Ingela ameishutumu mahakama hiyo kwa uamuzi huo aliouita kuwa ni “wa kichaa.” Wanasheria wa Michael waliowahi kumwandikia barua Ingela wakidai kwamba mteja wao amelazimika kutofungua baadhi ya madirisha ya nyumba yake kwa zaidi ya miaka miwili sasa kwani anapofungua tu moshi mkuuubwa wa sigara mithili ya ule wa treni za kale unaingia kutoka kwa jirani yake, na kumsababishia matatizo ya kupumua.Ni ujirani wa gubu,kunyimana uhuru au vituko vya ughaibuni?Hilo nakuachia wewe msomaji wangu mpendwa uamue.

Hebu sasa tuongelee mambo “siriaz.” Wiki chache zilizopita zimekuwa sio nzuri kwa Rais Joji Bush.Ilianza kwa tangazo la kujiuzulu kwa mshirika wake wa karibu na mpanga mikakati (strategist) wake wa muda mrefu,Karl Rove,ikafuatia tangazo jingine la kujiuzulu kwa mwanasheria mkuu na swahiba wa Bushi,Albert Gonzalez,na majuzi tena likaja “soo” la nguvu:seneta mkongwe wa jimbo la Idaho,Larry Craig alilazimika kujiuzulu baada ya kukumbwa na kashfa ya kuzengea “shoga” kwenye choo cha wanaume katika uwanja wa ndege wa Minneapolis.Skandali la seneta huyo ambaye amekuwa madarakani mihula matatu mfululizo lilitokea mwezi Juni mwaka huu ambapo askari kanzu mmoja aliyekuwa akiwinda watu wanaozengea mashoga kwenye vyoo alipominywa mguu na seneta huyo katika namna ambayo mashoga wanaitumia kuonyesha dhamira ya kutaka mapenzi.Inaelezwa kuwa vyoo vya umma ni sehemu maarufu za mawindo ya wanaotafuta mapenzi ya jinsia moja,na mara kwa mara askari kanzu “hujichanganya” katika maeneo hayo ili kuwanasa wenye malengo ya “kumendeana.” Baada ya kukamatwa na askari huyo,seneta Larry alikiri kufanya kosa wakati wa mahojiano katika kituo cha polisi (ambapo baadae alijitetea kwamba aliamua kukiri kosa hilo ili suala hilo lipotee kimyakimya).Na inaelekea kama mbinu hiyo ilikuwa linaelekea kufanikiwa hadi majuzi zilipoibuka habari kwamba alikamatwa takriban miezi miwili iliyopita.Awali alishikilia msimamo wake kwamba yeye siyo shoga,na alighafilika tu kukiri kosa mbele ya polisi,na ana mpango wa kuwasiliana na mwanasheria wake ili kurekebisha mambo.Kwa seneta kukiri mbele ya mamlaka ya sheria kwamba amefanya kosa,kisha kudai kuwa hakufanya kosa hilo,ilimaanisha kuwa alidanganya,ambalo ni kosa kubwa zaidi pengine zaidi ya hilo la kufumaniwa chooni.

Haikuwa habari mbaya kwa Bushi pekee bali kwa chama kizima cha Republican ambacho kwa upande mmoja kinakabiliwa na shinikizo la mwenendo mbaya wa vita huko Iraki,na upande mwingine kinahangaika kutengeneza mazingira mazuri ya ushindi katika uchaguzi mkuu wa Marekani hapo mwakani.Dalili kwamba seneta huyo “angebana lakini mwishowe angeachia” (angebadili msimamo wake wa kudai hana hatia) ilianza kujitokeza pale baadhi ya maseneta wenzie akiwemo anayewania kupitishwa na chama hicho kugombea urais mwakani,seneta John McCain wa jimbo la Arizona,walipotamka bayana kwamba ni muhimu kwa Craig “kuachia ngazi” (kujiuzulu).Ni skendo ambayo kwa namna flani imegusa kwenye “moyo” wa mtizamo wa kisiasa wa chama cha Republican,ambacho kinasisitiza maadili mema katika familia na kina upinzani mkali dhidi ya mahusiano ya kimapenzi ya jinsia moja.Pia seneta Craig alikuwa mpinzani mkali wa suala la ndoa za mashoga (same-sex marriage) na anafahamika kama mtetezi mzuri wa maadili ya kifamilia.Baadhi ya wajuzi wa siasa za ndani za Marekani wanatabiri kuwa huo ndio mwisho wa maisha ya kisiasa ya seneta huyo.

Tukirejea huko nyumbani,nimevutiwa sana na mjadala kuhusu Miss Tanzania “mpya.” Kwanza nimpatie pongezi zake na kumsisitiza kwamba safari yake ya kulitangaza jina la Tanzania ndio imeanza.Mijadala inayoendelea kwenye mtandao (na pengine huko nyumbani,japo sina uhakika na hilo) ni kuhusu “uasia” wa binti huyo.Naomba nitofautiane na wanaoleta hoja ya ubaguzi.Mwalimu Nyerere alitusisitiza tuepuke kuhukumiana kwa misingi ya rangi au asili zetu.Sijui kwanini binafsi nilihisi huyo binti angeibuka mshindi,na nikashiriki kwenye “shindano” la bloga Shamim Mwasha la kutabiri nani angeibuka Miss Tanzania mwaka huu,ambapo kura yangu nilimpa mshindi huyo.Ubaguzi wa rangi sio suala zuri na binti huyo asihukumiwe kwa asili yake bali ushiriki wake kwenye mashindano yajayo ya Miss World.Tukubali kwamba kwa vile nchi yetu ina “pasenteji” flani ya Watanzania wenye asili ya Asia na mabara mengine basi kuna uwezekano wa kuwa na Miss Tanzania ambaye ni Mtanzania mwenye asili ya Asia,kama vile tulivyo na wabunge wenye asili ya Kiasia.Kwa Miss Tanzania mpya,namna ya kuwanyamzisha wapinzani wako ni kufanya kile Waingereza wanachoita “proving them wrong.” Ni kama ukiwa mwanafunzi halafu wazushi wanadai wewe ni “kilaza” (shule haiendi vyema),cha kufanya hapo sio kubishana nao bali “kufaulu kwa rangi zinazopepea” (passing with flying colours).

Mwisho,nashawishika kuhoji kuhusu wimbi la wasomi wanaokimbilia kwenye siasa.Nimesoma kwenye gazeti flani ambapo maprofesa flani wamebwagwa kwenye mchakato wa kugombea uongozi wa CCM katika mkoa flani.Na sio kwamba walibwagwa na maprofesa wenzao.Pengine hoja itakuwa ni kuutumikia umma ndani ya chama cha siasa,lakini nadhani hoja hiyo inapingana na ukweli kwamba kwa kufanya kazi “ya wito” ya kufundisha,msomi anautumikia umma mkubwa zaidi ya ule anaotaka kuutumikia ndani ya chama.Natambua bayana kwamba kila raia ana uhuru wa kujihusisha na siasa alimradi kwa kufanya hivyo hakinzani na sheria za nchi,za uchaguzi au za chama husika,lakini kwa vile sote tunatambua umuhimu wa wasomi wetu kubaki kwenye taaluma zao (kutokana na uhaba wa wasomi tulionao sambamba na mahitaji halisi ya taifa letu “changa”) ingekuwa vizuri kwa wataaluma kuendelea kulitumikia taifa huko mashuleni na vyuoni badala ya hili wimbi la kukimbilia kwenye siasa.Na iwapo taasisi za elimu hazitoi mazingira mwafaka ya kuutumikia umma kwa namna msomi angependa basi pengine si vibaya kwa wasomi kuja na mawazo kama kuanzisha “think-tanks” ambazo zikiendeshwa kiufanisi zinaweza kuwa za umuhimu kama au hata zaidi ya vyama vya siasa.

Alamsiki


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.