Showing posts with label SIASA. Show all posts
Showing posts with label SIASA. Show all posts

28 Jul 2015

Ninaipenda siasa...kama stadi  (study, yaani kuisoma), lakini kwa hakika ninapata shida sana na jinsi mengi ya ninayosoma katika stadi za siasa (political studies) yanavyogeuka inapokuja kwenye matendo au shughuli za kisiasa an zinazohusiana na siasa. 

Stori kidogo. Fani niliyotamani sana kuisoma na pengine kubobea ni utabibu. Nilitamani mno kuwa daktari. Lakini ndoto yangu ya udaktari ilipata kikwazo baada ya kupata matokeo ya mtihani wa kumaliza kidato cha nne. Japo nilipata A kwenye Kemia na C kwenye Baiolojia, niliambulia D kwenye Hisabati na kufeli kabisa Fizikia ambapo nilipata F. Na japo nilipata Division One, uwezekano wa kuchukua 'combination ya udaktari' yaani PCB (Fizikia, Kemia na Baiolojia) kidato cha tano uliathiriwa na hiyo F ya Fizikia. Uwezekano pekee ulibaki kwenye kujaribu combination ya CBG (Fizikia, Kemia na Jiografia) ambayo ingeniwezesha kuikwepa Fizikia.

Nilipojiunga na kidato cha tano katika sekondari ya wavulana ya Tabora (Tabora Boys') nikakumbana na vikwazo vingine. Kwanza, Kemia ya kidato cha kwanza mpaka cha nne ni tofauti kwa kiasi kikubwa na ile ya kidato cha tano na cha sita. Kuna kitu inaitwa Physical Chemistry ambayo kimsingi ni kama mchanganyiko wa Kemia, Hisabati na Fizikia. Sasa kama nilivyotanabaisha hapo awali, udhaifu wangu katika Fizikia na Hisabati ulimaanisha kuwa nisingeweza kuimudu Kemia ya High School.

Pili, shule yetu ilikuwa haina mwalimu ya Jiografia, na ilibidi tuwe tunakwenda shule ya jirani ya Tabora Girls' kuhudhuria vipindi vya somo hilo. Angalau Baiolojia haikuwa tatizo japo kiukweli ilihitaji uwezo mkubwa wa kukariri na kuelewa majina ya sampuli za viumbe ambayo mengi yana asili ya Kilatini au Kigiriki. Kwahiyo kwa kifupi, dhamira yangu ya kusoma combination ya CBG ilikufa kifo cha asili.

Hivyo nikaamua kusoma combination yenye masomo ya Historia, Jiografia na Kiingereza. Hii ilikuwa mteremko kwa kiasi kikubwa, lakini ndoto yangu ya kuwa daktari ndio ikayeyuka. Lakini wanasema kile unachotaka sio lazima ndio unachopata (what you wish for is not always what you get).

Sukuma miaka kadhaa baadaye, nikajiunga na chuo kikuu cha Dar es Salaam na hapo nikajikuta nina uchaguzi wa ama kuzamia kwenye sayansi za siasa na utawala wa umma (pilitical science and public administration au sosholijia, elimu inayohusu masuala yya jamii. Mwaka wa pili, nikafanya uamuzi wa kuchukua hiyo choice ya pili, yaani Sosholojia. Kwa hakika niliipenda sana sosholojia. Yaani ilinisaidia mno kuielewa jamii. Miongoni mwa masomo ya kupendeza sana yalikuwa lile lilifundisha kuhusu uhusiano wa jamii, utamaduni na afya; somo la jinsia na uhusiano wa kijinsia, na zaidi ya yote ni sosholojia ya dini ambapo pamoja na mambo mengine tulifundishwa kuhusu Ukristo, Uislamu na Imani za Asili. 

Sukuma miaka kadhaa zaidi mbele, nikapata skolashipu ya kuja hapa Uingereza kusoma Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (Politics and International Relations), mkazo ukiwa kwenye masuala ya usalama. Kwa vile skolashipu ni kama zawadi, mwanafunzi anakuwa hana uchaguzi. Nilitamani sana kuendelea na Sosholojia lakini sikupewa fursa ya kuchagua. Na hivyo ndivyo nilivyojikuta nikiingia kwenye stadi za siasa. Tuishie hapo/

Kwanini nimeelezea stori hiyo? Ni kwa sababu kama nilivyosema awali, ninaipenda siasa kama stadi. Yaani baada ya kutokuwa na choice ya kusoma sosholojia, na 'kulazimishwa' kusoma Siasa, ikabidi niipende tu. Niliipenda pia kwa sababu siasa za kimataifa zina 'raha' yake kuzielewa, ukichanganya na maeneo kama diplomasia, amani na 'ugomvi' (peace and conflicts) na masuala ya usalama wa kimataifa (international security).

Lakini tatizo la siasa kama stadi ni ukweli mchungu kwamba kile unachosoma darasani mara nyingi hakiakisi hali halisi mtaani. Siasa kama fani au stadi sio mbaya, ina mafunzo mengi, inafundisha miongozo mingi na kanuni nyingit muhimu kwa maisha ya mwandamu, lakini mtaani hali ni tofauti.  Sihitaji kuelezea kwa undani kwanini watu wengi wanaichukia siasa. Lakini mfano mwepesi ni kwenye kampeni za uchaguzi ambapo utasikia chama kikitanabaisha sera nzuri kabisa lakini baada ya kuingia madarakani kikaishia kufanya kinyume kabisa na kilichoyaahidi. Na kwa Tanzania yetu tuna mfano hai wa jinsi sera tamu za CCM zinavyoishia kuwanufaisha matajiri na mafisadi huku zikiwadidimiza walalahoi.

Na mfano mchungu zaidi, uliopelekea niandike makala hii, ni jinsi Chadema katika mwavuli wa UKAWA inavyoelekea kuwasaliti mamilioni ya Watanzania kwa uwezekano wa kumpokea fisadi Edward Lowassa kuwa mgombea wa urais.

Jana niliumia mno nilipoona picha kadhaa zinazomwonyesha Lowassa akiwa na viongozi wa UKAWA. Baadaye, mwenyekiti wa NCCR, moja ya vyama vinavyounda UKAWA pamoja na Chadema, CUF na NLD, alitamka bayana kuwa wanamkaribisha Lowassa kujiunga nao.

Lakini baadaye kidogo nikapata ahueni baada ya kupatikana taarifa zilizothibitishwa na akaunti ya Twitter ya Chadema Media kuwa picha zilizokuwa zinamwonyesha Lowassa na viongozi wa UKAWA ni feki, yaani zilikuwa photoshopped. Hata hivyo furaha hiyo haikudumu muda mrefu baada ya Mbatia na wenzake kutangaza bayana kuwa wanamkaribisha Lowassa . Na kuna uwezekano leo Jumanne, aidha UKAWA wakamtangaza Lowassa kuwa mgombea wao wa Urais au Lowassa mwenyewe akatangaza kujiunga nao.
Huu ni usaliti mkubwa mno hasa upande wa Chadema, chama kilichojidhihirisha kuwa kinauchukia ufisadi kwa dhati. Sote twakumbuka jinsi Chadema ilivyojipatia umaarufu kwa kupambana na ufisadi, hasa baada ya kutangaza hadharani 'orodha ya aibu' (list of shame) pale Mwembeyanga jijini Dar ambapo walitaja orodha ya mafisadi akiwemo Lowassa. Kadhalika Chadema ilifanya jitihada kubwa kuibua ufisadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na skandali ya Richmond iliyopelekea Lowassa kujiuzulu Uwaziri Mkuu. Vilevile chama hicho kilitufumbua macho kuhusu ufisadi wa EPA, Meremeta, Dowans, Buzwagi, TanGold, Kiwira, nk. Kwa kifupi, ilikuwa haiwezekani kuzungumzia mapambano ya  ufisadi Tanzania bila kuitaja Chadema.

Na katika harakati zake za kupambana na ufisadi, kuna Watanzania wenzetu waliopoteza maisha yao na wengine kujeruhiwa vibaya na kuachiwa ulemavu kwa kukiunga mkono chama hicho. 


Na kwa kuonyesha kuwa Chadema ilikuwa mwarobaini kwa CCM na mafisadi kwa ujumla, chama hicho kilifanyiwa kila aina ya hujuma. Mara kiliitwa chama cha kidini, baadaye kikaitwa cha kikabila, na hadi hivi majuzi kiliitwa chama cha kigaidi. Lakini taratibu Watanzania walifumbuka macho na kubaini kuwa sababu kubwa ya CCM na serikali yake kuiandama Chadema ni kwa vile chama hicho cha upinzani kilichofanya vizuri tu katika uchaguzi mkuu uliopita kinasimamia maslahi ya wanyonge ilhali CCM inatetea mafisadi na ufisadi.
Japo mie binafsi sikuwa mwanachama wa Chadema, nilikiunga mkono kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi kulingana na msimamo wangu kwenye suala hilo. Nilikuwa nina imani kuwa laiti Chadema ikifanikiwa kuingia Ikulu basi kwa hakika safari ya kuipeleka Tanzania yetu mahali inapostahili kuwa inawezekana. 
Sasa hili la kumpokea Lowassa ni pigo kubwa mno na ni usaliti wa hali ya juu kabisa. Ndio, Lowassa anaweza kuwasaidia Chadema na UKAWA kuingia Ikulu. Lakini kwa kuangalia tu maswahiba wa Lowassa utaweza kujua tutakuwa na serikali ya aina gani. Sipati shida kubashiri kuwa tutaishia kuikumbuka CCM. 

Embedded image permalink

Na huo ndio ubaya wa siasa katika vitendo, tofauti na ilivyo nzuri na mwafaka katika stadi. Kwamba kistadi za siasa, Chadema ilijijenga na kupata umaarufu kwa kuzingatia kanuni ilizojiwekea na ikajitambulisha kama chama kilichopo kwa maslahi ya wanyonge, tofauti na CCM iliyokimbia kanuni zake na kuwakumbatia matajiri na mafisadi. Lakini ghafla bin vup, Chadema inaelekea kwenda kulekule ilipo CCM. 

Nimalizie makala hii kwa kuahidi kufanya uchambuzi wa kina kuhusu suala hili katika makala yangu ya wiki ijayo katika gazeti la Raia Mwema. Spoiler alert, wiki hii katika toleo litakalokuwa mtaani kesho ninamjadili Magufuli. 

Asanteni kwa kuchukua muda wenu kunisoma.

11 Aug 2014

                   
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba nusura wapigane baada ya kupishana kauli wakati wa mjadala wa ndani ya Kamati Namba Sita inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira.
Habari kutoka ndani ya kamati hiyo inayofanyia vikao vyake katika moja ya kumbi za Dodoma Hoteli zinasema, mvutano huo ulitokea Alhamisi iliyopita na kusababisha Wassira kusitisha kwa muda kikao hicho, kisha kwenda kuwasuluhisha.
Jana, Wassira licha ya kukiri kutokea kwa mvutano huo, alikanusha taarifa kwamba aliahirisha kikao hicho kwa ajili ya kuwasuluhisha.
“Kupishana katika masuala haya makubwa ni jambo la kawaida, hivyo mimi sidhani kama ni jambo linalopaswa kwenda mpaka kwenye magazeti maana kila wakati hutokea tofauti hizi na ndiyo maana sisi wenyeviti tupo ili kusimamia mijadala,” alisema Wassira na kuongeza:
“Lakini kwamba eti hilo jambo lilisababisha kikao kuahirishwa au kusitishwa hapana, kikao kiliendelea na kazi yake baada ya hilo lililoleta na ubishani kumalizwa”.
Habari zilizolifikia gazeti hili zinasema mvutano huo ulitokea wakati kamati hiyo ilipokuwa ikijadili Sura ya Nne na Tano, hususan suala la uraia wa nchi mbili. Sura ya tano ndiyo inayozungumzia masuala ya uraia.
“Sophia Simba yeye anataka uraia wa nchi mbili wakati Werema alikuwa akisema hilo jambo haliwezekani kutokea kwa sasa,” kilisema chanzo chetu.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, mvutano huo uliendelea baina ya viongozi hao na ndipo Jaji Werema aliposimama katika mchango wake na kuhoji elimu ya Simba, hivyo kuamsha hasira za waziri huyo ambaye pia alijibu mapigo.
“AG alipopewa nafasi ya kuzungumzia baada ya mabishano ya muda alihoji shule (elimu) ya Simba kwamba amesoma shule gani akimaanisha kwamba ni mgumu kuelewa, kwa hiyo waziri alikasirika na yeye alianza kujibu mapigo,” kiliongeza chanzo hicho.
Baada ya kutokea mvutano huo, baadhi ya wajumbe waliingilia kati kusitisha mzozo huo, ndipo Mwenyekiti Wassira alipositisha kikao hicho kwa muda kisha kuwasuluhisha wahusika.
Walipotafutwa jana kwa nyakati tofauti kuzungumzia mzozo wao, Werema na Simba hawakuwa tayari kubainisha kilichotokea.


Werema alitaka aachwe apumzike na kwamba mambo ya kamati yaachwe kwenye kamati.
“Jamani hamtuachi hata tupumzike Jumapili yote hii? Tafadhali bwana niache nipumzike, hayo mambo kama ni ya kamati, yaachwe kwenye kamati,” alisema Werema na kukata simu.
Simba baada ya kuulizwa alisema: “Heeeee hayo makubwa… I have no comment (sina cha kusema”), kisha alikata simu.
Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Khamis Hamad alisema ofisi yake haikuwa imepata taarifa kuhusu mzozo huo na kwamba angefuatilia ili aweze kufahamu kuhusu kilichojiri.
“Nina maofisa wa kutosha katika kila kamati, sasa nashangaa kwamba jambo kubwa kama hilo litokee halafu nisipate taarifa, lakini ngoja nifuatilie lakini kwa sasa sina taarifa yoyote,” alisema Hamad.
Werema
Juni mwaka huu, Jaji Werema alitaka kumtia adabu Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila bungeni Dodoma baada ya Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Azzan Zungu kuahirisha kikao cha Bunge, ikiwa ni muda mfupi baada ya Werema na Kafulila kurushiana maneno bungeni.
Jaji Werema alichukia baada ya Kafulila kumwita mwizi, akijibu mapigo baada ya mbunge huyo kuitwa tumbili na mwanasheria huyo.
Hali hiyo ilijitokeza baada ya kutofautiana kauli kuhusu mgogoro wa fedha za akaunti ya Escrow kulipwa Kampuni ya Kufua Umeme ya IPTL.
CHANZO: Mwananchi 
ANGALIZO: Picha ni kielelezo tu 

1 Jun 2012




FRIDAY, JUNE 1, 2012


#ZANZIBAR REVEALED

 kuna dhana ya kuwa karume aliuawa kulinda muungano, mazingira yote ya kuuawa kwa karume haiihusishi tanganyika kwa namna moja ama nyengine katika mauaji hayo na kwamba ni wananchi walichoshwa na serikali yao. kinachotokea leo zanzibar, ni msingi mbovu wa utawala wa tokea awali na kamwe tanganyika isihusishwe. 

jarida moja la kila mwezi 'Africa Events' la Agosti 1992 (uk. 27) ,linadai sababu za kuuawa kwa Karume zilikuwa za kibinafsi kwa njia ya kulipa kisasi. Inaelezwa kwamba Muhammed Hamud, mtoto wa Hamud Muhammed Hamud, aliyetiwa kizuizini miezi michache baa­da ya mapinduzi ya 1964 akituhumiwa kutaka kuipindua Serikali ya Karume.
Miaka, rnichache baadaye, Luteni Hamud Muhammed Hamud akiwa katika mafunzo ya kijeshi huko Tashkent (Urusi ya zamani), aliambiwa na mwanafun­zi mwenzake kwamba mzee Hamud alinyongwa na Karume akiwa kizuizini hila kufunguliwa mashtaka. Kwa taarifa hiyo, Luteni Hamud alisikika akiapa ange­muua Karume akirejea Zanzibar.
Taarifa ya kusudio la Hamud la kuua ilifikishwa kwa vyombo vya usalama Visiwani na wenzake, lakini hakukamatwa wala kuwekwa wa chini ya uchunguzi mkali ali­porejea Zanzibar; badala yake ali­pandishwa cheo kuwa luteni na Karume mwenyewe.
Jarida hili halisemi lolote juu ya raja Ali Khatibu Chwaya na ko­plo mwingine juu ya kushiriki kwao katika mauaji haya. Hata hivyo,. Kushiriki kwao kunaelekea kutetea dhana ya pili kwamba kwa sababu Serikali Karume ilishindwa kukidhi matarajio ya Wazanzibari wengi, hapakuwa na njia mbadala ila kumwondoa Karume ili kuleta mabadiliko.


Hapa panazuka swali; kama lengo la Hamud la kumuua Karume lilikuwa kulipa kisasi, kwa nini tukio hili lilihusisha watu zaidi ya mmoja? Si hivyo tu; kwa nini watu zaidi ya 1,000 walikamatwa kutokana na mauaji hayo kama haukuwa mpango mpana?
Dhana ya kulipiza kisasi inapungua nguvu kwa kushindwa kusimama kwa miguu miwili. inatuacha njia panda wakati huo ikijaribu kumezwa na dhana mpango wa mapinduzi, kama ilivyodai Serikali.
Inadaiwa kuwa mpango kuipindua, Serikali ya Karume ulibuniwa mwaka 1968 na wanharakati wa mapinduzi ya 1964 wakiwemo raia  na Wanajeshi wachache.
Inasemekana kikao cha mwisho cha mpango huo kilifanyika Aprili 2, 1972 nyumbani kwa Luteni Hamud, ambapo ilikubaliwa kwamba mauaji hayo yafanyike Aprili 7, 1972.
Mpango wa utekelezaji ulikuwa kwamba Hamud na Ahmada wachukue jukumu zito sana la kuiba silaha kutoka Kambi ya Jeshi yaBavuai.


Katika kutekeleza mapinduzi hayo, ambayo mipango na operesheni yake ilifanana kabisa na ya mapinduzi ya 1964, mtu mmoja, Suleiman Sisi, alipewa jukumu la kuongoza mashambulizi kwenye Kambi ya Jeshi la Mtoni na Ahmada alipewa jukumu la Kambi ya Bavuai, Makao Makuu ya Jeshi la Chuo cha Jeshi la Ma­funzo ya Redio ambazo zote ziko eneo la Migombani.


Kambi ya Ubago haikupangi­wa mtekaji kwa kuamini kwamba kama kikosi cha Ahmada kingeweza kuziteka sehemu kili­chopangiwa, Ubago ingesalimu amri sawia.


Kituo cha Polisi Malindi kingetekwa na kikosi ambacho kingeongozwa na Hamud, am­bapo magari yenye redio za mawasiliano yangepatikana kwa watekaji. Ilipangwa kuwa wakati mashambulizi haya yakiendelea, kituo cha Polisi Ziwani kingevamiwa na askari polisi walitarajiwa kuajiriwa na kuongozwa na askari Yusuf Ramadhan.


Mtu mwingine, Amour Dughesh, alipangwa kuteka Ikulu na alipewa jukumu lakumkamata­Karume na kumpeleka Kituo cha Redio kutangaza kupinduliwa kwa Serikali rake.


Inaelezwa pia kwamba baada ya redio kutekwa, ingewekwa chi­ni ya udhibiti wa Badawi Qual­letein, Miraji Mpatani na Ali Mtendeni. Uwanja wa Ndege ungedhibitiwa na Ali Sultan Issa, ambapo Makao Makuu ya Umoja wa Vi­jana wa AS P (ASPYL) yangetekwa na Baramia.


Makao Makuu ya ASPYL ya­likuwa Kituo Kikuu cha Mkuu wa Usalama wa Ndani ya Serikali ya Karume, Kanali Seif Bakari. Kanali Bakari aliongoza kikun­di cha ukatili kilichojiita kamati ya watu 14, kilichotesa na kuua waliodhaniwa wapinzani na Karume. Abdulrahman Mo­hammed Babu, akiandikia jarida la kila mwezi 'CHANGE' (Vol 4 No. 7,) la 1996, ukurasa 11, anakiri:- "Kutaja pekee jina la Kamati ya Watu 14 kulitosha kumtia mtu woga na kutishika”.


 Kamati hii ili­husika na mauaji ya mamia ya Wazanzibari wasio na hatia, waki­wemo, viongozi, wana’mapinduzi wa kimaendeleo kama Abdallah Kassim Hanga, Abdulaziz Twala, Saleh Saadala, Othman shariff na wengine wale waliuawa kwa jina la Karume."


Abdallah Ameir alipewa jukumu la kuzuia mashambulizi kutoka nje siku hiyo yamapinduzi.
Inadaiwa kuwa katika kikao hicho, Aprili 2, 1972 mtu mmoja, Amar Salim Kuku, alidokeza kuwa Ali Salim Hafidh ambaye nafasi yake haikutajwa katika mpango wa mapinduzi wa Aprili 7, angefi­ka Zanzibar na Abdulrahman Babu na wafuasi wake wa Dar es salaam, usiku wa Aprili 6 kwa mtumbwi kuungana na wanamapinduzi wengine.


Ukiwaondoa Luteni Hamud na Kepteni Ahmada katika mpango huu, na kama ni kweli kwam­ba mpango wote ilikuwa jaribio la mapinduzi (coup d'etat) kama ilivyodai Serikali ya Zanzibar, 'basi staili ya mpango huo haiwezi kut­ofuatishwa na ile ya mapinduzi ya umwagaji damu ya Aprili 12, 1964 ,ambao haukuhusisha jeshi.
Mapinduzi ya 1964 ya kushtukizwa dhidi ya utawala wa Sultan Jamshid na majeshi yake, yali­fanikiwa kwa sababu ya utawala huu kujitenga mbali na wananchi, hivyo haikuweza kupata taarifa za mipango ya mapinduzi hayo mapema.


Na kama ni kweli ilivyosema Serikali ya Zanzibar, kwamba mpango wa mapinduzi ya 1972 uli­buniwa tangu mwaka 1968, ilikuwaje JWTZ na Usalama wa Taifa, achilia mbali kikosi cha Us­alama wa Ndani cha Karume (Gestapo), kilichoongozwa na Kanali Seif Bakari kisibaini mapema hadi siku ya kupoteza uhai wa Kiongozi wa.taifa hilo?  Je, si kweli kwamba historia ya 1964 ilikuwa ikijirudia?


Haya yanaweza kuwa maoni ya wengi, wakiwamo wachunguzi wa mambo ya siasa. Mwanazuoni mahiri barani Afrika, Ali Mazrui anabainisha katika kitabu chake 'Africa's International Relations' (uk. 11); "ukizingatia jinsi Sheikh Abeid Karume alivyoitawala Zanz­ibar kwa ukatili na ubaguzi mkubwa, lolote lilitarajiwa kutokea kwake; hakuna aliyetarajia kwam­ba angedumu kwa miaka minane madarakani. Ndiyo maana hati­maye wengi hawakushangaa alipouawa mwaka 1972."

30 Dec 2007

Hatimaye Mwai Kibaki ametangazwa mshindi katika uchaguzi mkuu nchini Kenya.Ni rahisi kuhisi Raila Odinga ameporwa ushindi kutokana na namna matokeo ya uchaguzi huo yalivyochukua muda mrefu kuliko ilivyopaswa.Wakati matokeo haya yanaweza kuwaacha watu wengi,hususan wafuasi wa Raila,wakiwa hawaamini kinachoendelea,binafsi naona ni mwendelezo wa "kanuni isiyo rasmi" ya siasa za Afrika ambapo mara nyingi CHAMA TAWALA HAKISHINDWI UCHAGUZI ISIPOKUWA PALE KINAPOLEWA MADARAKA NA KUJIONDOA CHENYEWE KWA UZEMBE.KANU haikushindwa uchaguzi na NARC (enzi hizo) kwa vile wapinzani walikuwa na nguvu sana au wananchi walikuwa wameichoka sana,bali ilijifunga "own goal" kwa kusimamisha mgombea butu.Vyama pinzani vinaweza kufanya kila jitihada kukiondoa chama tawala madarakani lakini tatizo linabaki kuwa katika chaguzi nyingi za Afrika,vyama pinzani ni sawa na mshtakiwa aliyeko mahakamani ambapo hakimu,mwendesha mashtaka na baraza la wazee wanatoka upande wa mshtaki (ni dhahiri hapo hakutakuwa na haki kwa mshtakiwa).Na katika soka,mkiwa mnashindana na timu ambayo refa,kamisaa na washika vibendera ni manazi wa wapinzani wenu,basi hapo ni kipigo tu hata mtumie mbinu za Brazil.

Kwanini vyama tawala vya Afrika vipo tayari kufanya lolote linalowezekana kuhakikisha vinabaki madarakani?Well,jibu jepesi ni kwamba viongozi wengi wa vyama hivyo ni mafisadi wanaojua bayana kwamba wakiondoka madarakani wanaweza kujikuta wanaishia jela kwa maovu yao.Japo kwa ujumla siasa ni mchezo mchafu,kwa Afrika siasa ni zaidi ya mchezo mchafu,na pengine sio mchezo at all bali mazingaombwe.

3 Sept 2007

Asalam aleykum,

Nianze na nyepesi nyepesi.Majuzi,kibibi kimoja kilisherehekea “bethdei” yake ya 100 (karne hiyo!!) kwa kuvuta sigara yake ya 170,000 (naomba kusisitiza,laki moja na alfu sabini).Kikongwe hicho,Anne Langley,mkazi wa Croydon,kusini mwa jiji la London,alianza kuvuta sigara siku chache baada ya kuibuka kwa vita kuu ya kwanza ya dunia mwezi Juni mwaka 1914,wakati huo akiwa na miaka mitano tu.Na aliadhimisha kutimiza karne moja tangu azaliwe kwa kuwasha “mche” wake (sigara) kwenye mshumaa ulopandikizwa kwenye keki yake ya kumtakia “hepi bethdei.”Anne,aliyepachikwa jina la utani la “mstaafu mwenye mapafu ya chuma (iron-lunged pensioner)” anasema alianza “kubobea” kwenye vutaji sigara siku tano tu tangu aanze kuvuta na tangu wakati huo hajafikiria kuacha fegi licha ya kampeni kali kabisa zinazoendeshwa kumshawishi wavutaji watundike madaluga (majuzi serikali ya hapa imetangaza kwamba kuanzia mwakani pakti zote za sigara zitakuwa na picha “za kutisha” kuonyesha madhara ya sigara kwenye mwili wa mvutaji).Alipoulizwa siri yake ya kuvuta sigara kwa muda mrefu namna hiyo pasipo kudhurika,kibibi huyo alidai kwamba siri yake pekee ni kuwa katika muda wote ambo amekuwa mvuta sigara hajawahi kumeza moshi.Mie nadhani pengine siri yake kuu ni hayo “mapafu ya chuma”,na chuma chenyewe ni kile kisichishika masizi au kutu,au chuma cha pua.

Tukiendelea kucheza kwenye mada hiyo hiyo “ya hovyo hovyo” ya fegi,mwanamama mmoja huko Sweden amepigwa stop kuvuta sigara uwani kwake kwa vile jirani wanayepakana ana “allergy” na moshi wa sigara.Mahakama ya mazingira katika mji wa Arkapin uliopo kusini mwa Sweden,ilimwamuru Ingela Olofsson ku-stop mara moja kuvuta sigara awapo uwani kwani jirani yake,mwanasheria Richard Berggren,alidai kuwa huwa analazimika kuvaa “oxygen mask” kila asubuhi wakati anapokwenda kwenye gari lake analilipaki uwani karibu na jirani yake huyo,na kila anaporejea jioni kutoka kazini,.Vita kati ya majirani hao imedumu kwa kitambo sasa kabla ya kufikishwa mahakamani ambapo mwanzoni suluhu ilitafutwa kwa njia za kidiplomasia pasipo na mafanikio.Ingela ameishutumu mahakama hiyo kwa uamuzi huo aliouita kuwa ni “wa kichaa.” Wanasheria wa Michael waliowahi kumwandikia barua Ingela wakidai kwamba mteja wao amelazimika kutofungua baadhi ya madirisha ya nyumba yake kwa zaidi ya miaka miwili sasa kwani anapofungua tu moshi mkuuubwa wa sigara mithili ya ule wa treni za kale unaingia kutoka kwa jirani yake, na kumsababishia matatizo ya kupumua.Ni ujirani wa gubu,kunyimana uhuru au vituko vya ughaibuni?Hilo nakuachia wewe msomaji wangu mpendwa uamue.

Hebu sasa tuongelee mambo “siriaz.” Wiki chache zilizopita zimekuwa sio nzuri kwa Rais Joji Bush.Ilianza kwa tangazo la kujiuzulu kwa mshirika wake wa karibu na mpanga mikakati (strategist) wake wa muda mrefu,Karl Rove,ikafuatia tangazo jingine la kujiuzulu kwa mwanasheria mkuu na swahiba wa Bushi,Albert Gonzalez,na majuzi tena likaja “soo” la nguvu:seneta mkongwe wa jimbo la Idaho,Larry Craig alilazimika kujiuzulu baada ya kukumbwa na kashfa ya kuzengea “shoga” kwenye choo cha wanaume katika uwanja wa ndege wa Minneapolis.Skandali la seneta huyo ambaye amekuwa madarakani mihula matatu mfululizo lilitokea mwezi Juni mwaka huu ambapo askari kanzu mmoja aliyekuwa akiwinda watu wanaozengea mashoga kwenye vyoo alipominywa mguu na seneta huyo katika namna ambayo mashoga wanaitumia kuonyesha dhamira ya kutaka mapenzi.Inaelezwa kuwa vyoo vya umma ni sehemu maarufu za mawindo ya wanaotafuta mapenzi ya jinsia moja,na mara kwa mara askari kanzu “hujichanganya” katika maeneo hayo ili kuwanasa wenye malengo ya “kumendeana.” Baada ya kukamatwa na askari huyo,seneta Larry alikiri kufanya kosa wakati wa mahojiano katika kituo cha polisi (ambapo baadae alijitetea kwamba aliamua kukiri kosa hilo ili suala hilo lipotee kimyakimya).Na inaelekea kama mbinu hiyo ilikuwa linaelekea kufanikiwa hadi majuzi zilipoibuka habari kwamba alikamatwa takriban miezi miwili iliyopita.Awali alishikilia msimamo wake kwamba yeye siyo shoga,na alighafilika tu kukiri kosa mbele ya polisi,na ana mpango wa kuwasiliana na mwanasheria wake ili kurekebisha mambo.Kwa seneta kukiri mbele ya mamlaka ya sheria kwamba amefanya kosa,kisha kudai kuwa hakufanya kosa hilo,ilimaanisha kuwa alidanganya,ambalo ni kosa kubwa zaidi pengine zaidi ya hilo la kufumaniwa chooni.

Haikuwa habari mbaya kwa Bushi pekee bali kwa chama kizima cha Republican ambacho kwa upande mmoja kinakabiliwa na shinikizo la mwenendo mbaya wa vita huko Iraki,na upande mwingine kinahangaika kutengeneza mazingira mazuri ya ushindi katika uchaguzi mkuu wa Marekani hapo mwakani.Dalili kwamba seneta huyo “angebana lakini mwishowe angeachia” (angebadili msimamo wake wa kudai hana hatia) ilianza kujitokeza pale baadhi ya maseneta wenzie akiwemo anayewania kupitishwa na chama hicho kugombea urais mwakani,seneta John McCain wa jimbo la Arizona,walipotamka bayana kwamba ni muhimu kwa Craig “kuachia ngazi” (kujiuzulu).Ni skendo ambayo kwa namna flani imegusa kwenye “moyo” wa mtizamo wa kisiasa wa chama cha Republican,ambacho kinasisitiza maadili mema katika familia na kina upinzani mkali dhidi ya mahusiano ya kimapenzi ya jinsia moja.Pia seneta Craig alikuwa mpinzani mkali wa suala la ndoa za mashoga (same-sex marriage) na anafahamika kama mtetezi mzuri wa maadili ya kifamilia.Baadhi ya wajuzi wa siasa za ndani za Marekani wanatabiri kuwa huo ndio mwisho wa maisha ya kisiasa ya seneta huyo.

Tukirejea huko nyumbani,nimevutiwa sana na mjadala kuhusu Miss Tanzania “mpya.” Kwanza nimpatie pongezi zake na kumsisitiza kwamba safari yake ya kulitangaza jina la Tanzania ndio imeanza.Mijadala inayoendelea kwenye mtandao (na pengine huko nyumbani,japo sina uhakika na hilo) ni kuhusu “uasia” wa binti huyo.Naomba nitofautiane na wanaoleta hoja ya ubaguzi.Mwalimu Nyerere alitusisitiza tuepuke kuhukumiana kwa misingi ya rangi au asili zetu.Sijui kwanini binafsi nilihisi huyo binti angeibuka mshindi,na nikashiriki kwenye “shindano” la bloga Shamim Mwasha la kutabiri nani angeibuka Miss Tanzania mwaka huu,ambapo kura yangu nilimpa mshindi huyo.Ubaguzi wa rangi sio suala zuri na binti huyo asihukumiwe kwa asili yake bali ushiriki wake kwenye mashindano yajayo ya Miss World.Tukubali kwamba kwa vile nchi yetu ina “pasenteji” flani ya Watanzania wenye asili ya Asia na mabara mengine basi kuna uwezekano wa kuwa na Miss Tanzania ambaye ni Mtanzania mwenye asili ya Asia,kama vile tulivyo na wabunge wenye asili ya Kiasia.Kwa Miss Tanzania mpya,namna ya kuwanyamzisha wapinzani wako ni kufanya kile Waingereza wanachoita “proving them wrong.” Ni kama ukiwa mwanafunzi halafu wazushi wanadai wewe ni “kilaza” (shule haiendi vyema),cha kufanya hapo sio kubishana nao bali “kufaulu kwa rangi zinazopepea” (passing with flying colours).

Mwisho,nashawishika kuhoji kuhusu wimbi la wasomi wanaokimbilia kwenye siasa.Nimesoma kwenye gazeti flani ambapo maprofesa flani wamebwagwa kwenye mchakato wa kugombea uongozi wa CCM katika mkoa flani.Na sio kwamba walibwagwa na maprofesa wenzao.Pengine hoja itakuwa ni kuutumikia umma ndani ya chama cha siasa,lakini nadhani hoja hiyo inapingana na ukweli kwamba kwa kufanya kazi “ya wito” ya kufundisha,msomi anautumikia umma mkubwa zaidi ya ule anaotaka kuutumikia ndani ya chama.Natambua bayana kwamba kila raia ana uhuru wa kujihusisha na siasa alimradi kwa kufanya hivyo hakinzani na sheria za nchi,za uchaguzi au za chama husika,lakini kwa vile sote tunatambua umuhimu wa wasomi wetu kubaki kwenye taaluma zao (kutokana na uhaba wa wasomi tulionao sambamba na mahitaji halisi ya taifa letu “changa”) ingekuwa vizuri kwa wataaluma kuendelea kulitumikia taifa huko mashuleni na vyuoni badala ya hili wimbi la kukimbilia kwenye siasa.Na iwapo taasisi za elimu hazitoi mazingira mwafaka ya kuutumikia umma kwa namna msomi angependa basi pengine si vibaya kwa wasomi kuja na mawazo kama kuanzisha “think-tanks” ambazo zikiendeshwa kiufanisi zinaweza kuwa za umuhimu kama au hata zaidi ya vyama vya siasa.

Alamsiki


2 Aug 2007

Asalam aleykum,

Wanasema kuwa siasa inahitaji kuwa na mvuto (appeal).Lakini mvuto wa mwanamama Myra Bushell,mshindi wa uchaguzi mdogo wa kanseli kwa tiketi ya chama cha Liberal Democrats cha hapa Uingereza,ni zaidi ya mvuto wa kawaida unaohitajika kwenye siasa.Myra aligombea na kushinda nafasi ya uwakilishi kwenye kanseli ya Bideford huko Devon,huku akiwa ni mcheza-uchi/nusu uchi kwenye vilabu (stripper) na mwendesha huduma ya ngono-kwa-simu (phone-sex-line) ambayo anachaji pauni 1.50 kwa dakika (takriban shilingi 3500 za huko nyumbani).Yeye anajitetea kuwa hayo ni maisha yake binafsi nje ya siasa,lakini tayari wajumbe watatu wa kanseli hiyo wameshajiuzulu kupinga vitendo vya mwanasiasa huyo ambaye pia ana tovuti yake ya huduma za ngono.Myra anajitetea kwamba wakati anautumikia umma kama mwanasiasa,anapaswa pia kumudu gharama za maisha,na ndio maana amekuwa akijihusisha na shughuli hizo “nyeti.” Habari njema kwake ni kwamba katibu (clerk) wa kanseli hiyo,George McMauchlan,ametamka bayana kuwa Myra hajavunja sheria yoyote ya maadili ya kazi ya ujumbe wa kanseli kwa vile “shughuli zake binafsi nje ya siasa” haziathiri utendaji wake wa kazi.Kaazi kweli kweli!!


Tukiachana na habari hizo za mwanasiasa “stripper”, kwa takriban wiki nzima iliyopita,medani za sera za nje za Marekani ilikuwa imetawaliwa na habari kwamba taifa hilo lilikuwa linajiandaa kutekeleza mpango wa kuziuzia silaha baadhi ya nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati.Wanufaika wakubwa wa mpango huo ni pamoja na Saudi Arabia,Misri,na kama ilivyo ada,Israel.Hata hivyo,mpango huo umezaa mvutano wa namna flani kwenye duru za siasa za ndani za Marekani kwani wapo wanaodhani kwamba hoja ya serikali ya Bush kuwa inaziuzia silaha nchi kama Saudi Arabia na Misri ili,pamoja na mambo mengine,kudhibiti kujitanua kijeshi kwa Iran,inaweza kupingana na ukweli kuwa rafiki wa leo anaweza kuwa adui wa kesho,na silaha unazompatia leo kujilinda zinaweza kutumika kesho kukudhuru.Na mpango huu umekuja wakati wachambuzi wa siasa za kimataifa wanaoona kuna kuyumba kwenye urafiki wa muda mrefu kati ya Marekani na Saudi Arabia.Hivi karibuni,Saudi iliweka bayana mtizamo wake kuhusu vita ya Irak kwa kusema kuwa uvamizi wa Marekani nchini Irak unachochea machafuko na suluhisho pekee ni kwa majeshi ya kigeni kuondoka nchini Irak.Pia kumekuwepo shutuma za hapa na pale kwamba Saudi Arabia inavisapoti vikundi vya madhehebu ya Sunni nchini Irak ili kuvikabili vikundi vya madhehebu ya Shia ambavyo inadaiwa vinapata sapoti ya Iran.Kitakwimu na kujiografia,Saudi ni taifa la ki-Sunni wakati Iran ni la ki-Shia,na mahusiano kati ya nchi hizo mbili sio mazuri.Saudi kwa upande wake inahofia sana kukua kwa nguvu za kijeshi za Iran,hasa kwa vile hadi sasa,ukitoa Israel,Saudi ni taifa lenye nguvu kubwa katika eneo la Ghuba na Mashariki ya Kati.

Wakati mwingine ni vigumu kuzielewa sera za nje za Marekani kwani kwa jinsi flani ilipaswa kujifunza kutokana na maamuzi yake ya zamani ambayo kwa namna moja au nyingine yamekuwa yakiiumiza kichwa katika kipindi hiki tulichonacho,kwa mfano msaada wake wa silaha kwa Irak wakati Saddam alipokuwa rafiki wa nchi hiyo,na misaada yake kwa mujahidina wa Afghanistan wakati wa vita dhidi ya Muungano wa nchi za Kisovieti (USSR).Tawala za nchi nyingi za Kiarabu na Ghuba sio za kidemokrasia (kwa vipimo vya nchi za magharibi),na miongoni mwa sababu zinazodaiwa kuchangia kuibuka kwa siasa za msimamo mkali wa kidini katika nchi hizo kushindwa kwa tawala hizo kuleta mabadiliko ya manufaa ya kisiasa,kiuchumi na kijamii.Lakini katika kukoroga zaidi mambo,baadhi ya tawala hizo zimekuwa zikuvikumbatia na kuvifadhili vikundi vyenye msimamo mkali wa kidini ili tawala hizo ziendelee kuwa madarakani.Kwa uchambuzi mwepesi,yayumkinika kusema kuwa hatma ya tawala hizo kwa muda mrefu sio ya kuaminika sana,na Marekani inaweza kujutia huko mbeleni kwa kuzilinda tawala hizo kwa misaada ya kijeshi.

Na taarifa zaidi kutoka Irak zinaeleza kuwa “picha haziivi” kati ya mkuu wa majeshi ya Marekani nchini humo,Jenerali David Petraeus,na Waziri Mkuu wa Irak,Nour al-Maliki.Inasemekana kuwa Maliki alishamuomba Rais Bush amwondoe Jenerali huyo msomi mwenye shahada ya kwanza katika sayansi (Bachelor of Science),shahada ya uzamili katika Utawala wa Umma (M.A in Public Administration) na shahada ya uzamifu kwenye siasa za kimataifa (PhD in International Relations) na alishakuwa (assistant) Professor kwenye US Military Academy. “Bifu” (kupingana) kati ya Maliki na Jen Petraeus kunatokana na baadhi ya maamuzi yanayopingana kati ya watu hao muhimu kwa mafanikio au kutofanikiwa kwenye sera ya Bush kuhusu Irak.Inaelezwa kuwa Maliki haafikiani na mpango majeshi ya Marekani unaoelekea kuasisiwa na Jen Petraeus wa kuvipatia silaha vikundi vya madhehebu ya Sunni ili vipambane na wapiganaji wa Al-Qaeda nchini humo.Maliki ambaye ni muumini wa madhehebu ya Shia anaelekea kuhofia kuwa silaha hizo zinaweza kutumika dhidi ya vikundi vya madhehebu ya Shia,au kwa mtizamo wa muda mrefu,kuchangia vita vya wenyewe kwa wenyewe pindi majeshi ya Marekani yatakapoondoka (kama kuna kuondoka kweli).

Baada ya mjadala wa siasa za kimataifa,hebu tegeukie mambo mengine ya huko nyumbani.Nitahadharishe kuwa naamini baadhi ya ntakayoandika hapa yatawaudhi watu flani lakini kuudhika kwao kutakuwa na maana moja tu kwangu:kwamba ujumbe umefika na wabadilike badala ya kununa.Binafsi,nadiriki kusema kuwa mzazi makini hawezi kumrushusu binti yake kuingia kwenye mambo ya u-Miss.Kwanini?Kwa sababu inaelekea wengi wa mabinti wanaotafuta u-miss huwa aidha wanarubunika kuwa wenye tabia mbovu baada ya kupata majina au pengine fani nzima ya u-miss ni kichocheo cha umalaya (samahani kwa maneno makali).Yaani kila kukicha utaskia sijui Miss nanihii katembea na mume wa mtu,au Wema Sepetu kapigwa picha za utupu,au Faraja Kotta kalibwaga buzi lake lililoiba fedha wapi sijui,na vituo vingine mia kidogo.Kuna kasoro kwenye fani ya u-miss lakini jamii inaelekea imelifumbia macho suala hilo.Lundenga,Chipungahelo na wadau wengine wa fani ya u-miss wana jukumu la kuithibitishia jamii kuwa tatizo haliko kwenye fani hiyo bali ni kwa baadhi tu ya washiriki.Na kama tatizo ni washiriki basi watuambie bayana inakuwaje wanaweza kupenya katika ngazi mbalimbali hadi kifikia levo ta taifa na kuanza kutuonyesha madudu yao.Rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari aliwahi kunidokeza kuwa fani hiyo imetawaliwa sana na viongozi,wadhamini na mapromota walafi wa kula uroda ambao wanarahisishiwa kazi na mabinti wenye tamaa ya umaarufu wa chapchap,ambao kwao sio ishu kuvua “makufuli” yao ili wakwae u-miss.Ujumbe wangu kwenu ni simpo:msipokuwa makini mtaondoka kwa kilo mbili,na kwa vile mnathamini sana umaarufu,basi kudhoofika kwa afya zenu kutatawala sana kurasa hizohizo zinazoripoti kila siku namna mnavyoibemenda Amri ya Sita kama hamna akili nzuri.Mkikasirika shauri yenu lakini mmezidi kufanya mambo ya aibu.

Halafu kuna mambo mawili yamenisikitisha sana.La kwanza ni hii tabia ya ubabe inayoelekea kumkolea msanii TID.Binafsi,nazipenda sana kazi za kijana huyu,na mwanzoni nilikuwa namtofautisha na wasanii wengine wa bongo kwa vile amewahi kukaa ugahibuni kwa muda wa kutosha na amekuwa akipata mialiko ya nje mara kwa mara.Lakini pengine kwa kutotambua kuwa taswira (image) ya msanii ni muhimu katika kumuweka au kumporomosha kwenye chati,ameendelea kushika vichwa vya habari kwa matukio yasiyopendeza.Wimbo wake naoupenda sana unaitwa “chagua moja”,nami ujumbe wangu kwake ni mfupi:chagua moja kati ya kujiporomosha wewe mwenyewe kwa matendo yasiyofaa au jirekebishe tabia zako ili uendelee kubaki kuwa “Top In Dar.” Usikasirike,ni somo jepesi tu hilo.

Jingine lililonikera ni gazeti la RISASI ambalo katika toleo lake la Julai18-20 lilikuwa na habari kwamba “Warembo TZ wapiga picha za X tupu…zasambazwa mitaani,baadhi yao ni washiriki wa kusaka mataji ya u-miss.” Kinachosikitisha sio kama iwapo habari hiyo ni ya kweli au ya kubuni bali ni picha zilizotumika kwenye habari hiyo.Rafiki yangu mmoja aliyeko Marekani amenifahamisha kuwa wasichana walioko kwenye picha hizo ni wacheza filamu za ngono (porn stars) wa Marekani na wala sio Watanzania.Kwa kuthibitisha alichokuwa anasema,alinipatia tovuti ambazo zina picha za Wamarekani hao weusi.Kama picha zilizotumiwa na RISASI ni feki basi yayumkinika kusema kuwa hata habari yenyewe ni feki.Hivi ni uzembe wa mhariri kucheki ukweli wa habari husika au ndio kuwafanya Watanzania wajinga kwa kuwapa habari “sensational” ambazo hazina ukweli?Nyie ni watu wazima ambao mmeshatengeneza faida ya kutosha kwa kuandika udaku lukuki wa kweli,sasa tamaa ya nini hadi mfikie hatua ya kunyofoa mapicha kwenye mtandao na kuzusha habari?Shame on you!

Alamsiki

18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Habari za huko nyumbani

Mojawapo ya tofauti kubwa kati ya jamii ya hawa wenzetu na huko nyumbani ni namna uhuru wa kujieleza (freedom of expression) unavyothaminiwa.Of course,uhuru huo unaambatana na wajibu,kwa sababu kama wanataaluma wa kanuni za maisha wanavyosema,uhuru bila wajibu ni sawa na kukaribisha vurugu.Kadhalika,uhuru huo sio wa asilimia 100 (absolute),kwa vile hakuna kitu kama hicho duniani.Lakini ukilinganisha na huko nyumbani,yayumkinika kusema kwamba hawa wenzetu wana uhuru mkubwa zaidi wa kujieleza.Sambamba na hilo ni uhuru wa taasisi zinazopaswa kuujulisha umma nini kinaendelea katika jamii yao na hata nje ya jamii hiyo.Hapa nalenga zaidi kwenye taasisi za habari:hususan magazeti na vituo vya radio na runinga.

Kuna magazeti hapa ambayo ni mithili ya hayo yanayoitwa “ya udaku” huko nyumbani.Magazeti kama The Sun,News of the World,Daily Mirror,nk yamebobea sana katika kuibua skandali mbalimbali hapa Uingereza.Inapotokea kwamba habari flani imepotoshwa basi hao walioguswa na habari hiyo wataamua aidha kukanusha au kukimbilia mahakamani kudai fidia.Wakati mwingine watajwa kwenye habari hizo hulazimika kukiri makosa yao hadharani.Kwa mfano,juzijuzi iliripotiwa kuna Naibu Waziri Mkuu John Prescott alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na katibu muhtasi wake Tracey Temple.Katika sekeseke hilo ambalo bado halijatulia ilimzalimu Bwana Prescott kukiri kuwa yaliyosemwa na magazeti ni kweli.

Nakumbuka mwanataaluma mmoja huko nyumbani aliwahi kuvitaka vyombo vya habari kuwa na ujasiri wa kutaja majina ya watuhumiwa bila kuwa na hofu ya kuburuzwa mahakamani,iwapo vyombo hivyo vina uhakika na walinachoripoti.Hebu chukulia mfano wa habari kama hii: “kiongozi wa chama kimoja cha siasa kinachoanzia na herufi C anadaiwa kuwa na uhusianowa kimapenzi na mtangazaji flani ambaye jina lake linaanzia na herufi D…”Hivi habari kama hiyo si ni sawa na chemsha bongo kwa msomaji?Hali ilikuwa mbaya sana miaka ya nyuma kwa sababu ilikuwa ni vigumu mno kujua ni mtuhumiwa gani hasa anazungumziwa katika stori husika.Hata hivyo,kuna dalili kwamba mambo huenda yakabadilika hasa baada ya ujio wa magazeti jasiri ambayo yako tayari kwa lolote.Ukweli ni kwamba kama ushahidi upo wa kutosha hakuna haja ya kuficha jina la mhusika (labda ithibitike kuwa kumtaja kutaathiri uchunguzi,au kwa sababu za kimaadili).

Siyalaumu magazeti yanayoshindwa kutaja majina ya wahusika katika skendo flani japokuwa nayapa changamoto kufanya hivyo.Siyalaumu kwa sababu sio kosa lao,sio uoga,bali ni mazingira yaliyopo.Siasa za nchi yetu baada ya uhuru hadi mwanzoni mwa miaka ya 1990 zilikuwa zimegubikwa na usiri mkubwa.Kutaja madhambi ya kiongozi ilikuwa dhambi,na hapa tunazungumzia kuanzia ngazi ya mtaa hadi taifa.Usiri sio mbaya kama unatumiwa kwa manufaa ya wengi,lakini kwa bahati mbaya baadhi ya watu walikuwa wanautumia kuficha maovu yao.Waliofilisi mashirika ya umma walinufaika sana na siasa za usiri.Viongozi hawakuwa tayari kusikia kauli nyingine zaidi ya sifa,na kuwakosoa ilikuwa ni kujichimbia kaburi.Kwa hiyo,hali tuliyonayo sasa ni matokeo ya miongo kadhaa ya kuishi katika siasa za kusifia na si kukosoa.

Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni miongoni mwa maeneo ambayo yameathiriwa sana na kutokuwepo uhuru wa kutoa mawazo sambamba na uoga wa kuadhibiwa unapoongea kinyume na matakwa ya wakubwa.Nilikuwa sijazaliwa wakati mataifa haya yanaungana,na sijafanya utafiti wa kutosha iwapo Muungano huo ulifanywa kwa ridhaa ya wadau (wananchi) au yalikuwa ni maamuzi tu ya viongozi.Miaka nenda miaka rudi watu wamekuwa wakiongea “chini ya uvungu” kwamba Muungano huu una matatizo mengi tu japokuwa yanaweza kutatuliwa pale penye nia.Baadhi ya viongozi wamekuwa wanakwepa kuzungumzia matatizo yaliyopo kwa madai ya “kukwepa jinamizi la Muungano.”

Hivi karibuni kumekuwa na harakati za kisheria na kisiasa kuhusu Muungano.Kundi la Wazanzibari limefungua kesi kuhusu Muungano,Mchungaji Mtikila nae anaonekana kuukalia kooni Muungano,na viongozi wa serikali kutoka Bara walikutana na wale wa viswani kujadiliana kuhusu suala la Muungano.Juu ya hayo serikali ya awamu ya nne ina waziri anaeshughulikia suala la Muungano.Hata hivyo,kauli za Waziri Kiongozi wa Zanzibar Samsi Vuai Nahodha kuwa suala la mafuta ni la kisiwa hicho pekee,sio kitu cha kukiacha kipite hivihivi tu.Scotland,sehemu ya muungano unaounda United Kingdom (Uingereza) ina utajiri mkubwa wa mafuta.Lakini japokuwa kumekuwa na kelele za hapa na pale kuhusu muungano huo,utajiri wa mafuta haujawahi kuipa kiburi Scotland ifikirie kujitoa katika muungano huo au itumie mapato yote ya mafuta peke yake.Sasa kelele zimeanza hata kabla hayo mafuta hayajapatikana huko Zanzibar,je yakipatikana si ndio itakuwa mshikeshike!

Mimi nadhani suala la Muungano linazungumzika.Ikibidi kufanya kura ya maoni kujua matakwa ya sasa ya wananchi kuhusu Muungano,basi na ifanyike bila kuogopa matokeo yake.Siasa za kuogopana na kubembelezana zimepitwa na wakati,na iwapo itathibitika kuwa upande mmoja wa Muungano hauridhiki na muundo au kuwepo kwake,basi jitihada za dhati zifanyike kupata ufumbuzi.Tukiendelea na siasa za usiri na kujidanganya kwamba kila kitu kinakwenda vizuri,si ajabu siku moja Muungano huu ukavunjikia mahakamani.Hiyo itakuwa aibu sana hasa kwa wale wanaodai kukwepa “jinamizi la kuvunjikiwa na Muungano.”Inatokea huko Serbia-Montenegro,inaweza pia kutokea huko nyumbani iwapo wanasiasa wetu hawatafanya jitihada za makusudi.

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.