Showing posts with label UNDP. Show all posts
Showing posts with label UNDP. Show all posts

5 Aug 2010

SHIRIKA la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), limesema rushwa iliyojitokeza katika mchakato wa kura za maoni za CCM, ni hatari kwa mustakabali wa taifa.

Kufuatia hali hiyo shirika hilo limewataka Watanzania hasa vijana, kutokubali kununuliwa katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.
“Katika vitu vya kushangaza ni jinsi wagombea ubunge na udiwani wa CCM walivyokuwa wakishindana kutoa rushwa ili wachaguliwe na wananchi,” alisema Meneja Mradi wa Kusaidia Uchaguzi wa UNDP, Oskar Lehner.

Lehner alisema hayo jana jijini Dar es Salaam katika kongamano la siku mbili lililowakutanisha zaidi ya vijana 140 kutoka mashirika mbalimbali yasiyokuwa ya kiserikali na wale wa vyuo vikuu.

Kwa mujibu wa Lehner, uuzaji wa shahada za kupigia kura katika uchaguzi, ni sawa na kuuza malengo ya baadaye katika maisha ya watu hivyo ni vyema Watanzania wakafahamu kwamba mustakabali wa maendeleo ya nchi upo katika kipindi hiki cha Uchaguzi Mkuu.

UNDP inatoa kauli hiyo baada ya vyombo mbalimbali vya habari kuripoti rushwa katika mchakato mzima wa kura za maoni za CCM kuwapata wabunge na madiwani watakaogombea katika uchaguzi ujao.

“Angalieni jinsi matendo ya rushwa yalivyoripotiwa katika mchakato wa kampeni na upigaji kura za maoni ya kuchagua mgombea ubunge na udiwani wa CCM," alisema na kuongeza.

“Wananachi na hasa vijana mjihadhari na kujiepusha na rushwa katika uchaguzi, eleweni kuwa, kuuza shahada yako ya kupigia kura, ni sawa na kuuza malengo ya baadaye katika maisha yako,"

“Mafanikio na maendeleo ya baadaye ya nchi, yapo katika mikono yenu hasa katika kipindi hiki cha Uchaguzi Mkuu.”

CHANZO: Mwananchi

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.