17 Apr 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Kabla ya yote sina budi kuanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kutimiza siku 100 tangu achaguliwe kuwa Rais wa serikali ya awamu ya nne huko nyumbani.Si huko nyumbani tu ambako wananchi wengi wameridhika na utendaji wa Mheshimiwa na serikali yake bali hata huku Ughaibuni.Kuna dalili nyingi zinazoonyesha kwamba nchi yetu inaweza kurudisha heshima yake ambayo kwa kiwango kikubwa ilikuwa imepotea ndani na nje ya nchi.

Siku moja nikiwa kibaruani hapa napoishi nilikutana na jamaa mmoja ambaye nilipomfahaisha kuwa mimi ni Mtanzania alionyesha kuwa na shauku ya kuongea nami.Huyo jamaa alinifahamisha kuwa yeye ni Mskotishi ambaye miaka michache alipata fursa ya kutembelea Tanzania kufanya mchanganuo wa mradi flani uliokuwa ufadhiliwe na wahisani wa kimataifa.Jamaa alianza kwa kuniuliza kwanini Tanzania ni nchi masikini wakati ina utajiri kibao wa asili.Nikajifanya kama sikulielewa swali lake na kumtaka anifafanulie huo anaoita utajiri.Akanitolea mlolongo wa vitu:madini,misitu,ardhi yenye rutuba,maziwa na mito kadhaa,mbuga za wanyama (na hapo akaniambia kuwa Selous ni mojawapo ya mbuga za asili kubwa kabisa duniani),mlima Kilimanjaro,na kikubwa zaidi ya vyote,AMANI.Sio siri,nilibaki nang’ang’aa macho tu bila ya kuwa na jibu la haraka la swali lake la msingi:kwanini Tanzania ni miongoni mwa nchi masikini sana duniani wakati ina utajiri lukuki?

Jamaa akaendelea kunikalia kooni.Akanipa mfano hai wa uzoefu wake kuhusu Tanzania.Nilisema hapo mwanzo kuwa huyo jamaa alikuja hapa kwa ajili ya mradi flani.Alidai kuwa wakati yeye na wenzake wakiwa wanaandaa mambo flani kuhusu mradi huo,wakakumbana na mambo ambayo yeye aliyaona ya ajabu sana kwa mtizamo wake.Alieleza kuwa katika ofisi zaidi ya moja walikutana na watendaji wa serikali ambao waliwaomba “ma-TX” hao kuongeza gharama halisi za mradi huo kwa makubaliano ya “teni pasenti” pindi fungu la fedha likitoka.Huyo jamaa na wenzake walionekana kushangazwa sana na tabia ya watendaji hao wa serikali walioonekana kuwa hawakuwa na uchungu wowote na nchi yao wala kujali umuhimu wa mradi huo kwa Taifa lao.Jamaa anadai wao walikataa ofa hizo (kama ni kweli au la mimi sijui) na picha aliyobaki nayo ni kwamba wabomoaji wa Tanzania kwa kiasi kikubwa ni Watanzania wenyewe.

Nimeelezea stori ya Mskotishi huyo kubainisha jambo ambalo haliitaji mtu kutoka nje kutuelezea.Ni wangapi tunaojua kwamba wapo watendaji ambao kwa teni pasenti wanatoa vibali vya kazi kwa wageni wasiostahili kuwepo bila kujali kuwa wanaweza kuwa magaidi?Au wale wanaotoa vibali vya ujenzi kwa makandarasi wasio na sifa na hatimaye kuhatarisha maisha ya watuamiaji wa majengo hayo?Au wale wanaruhusu bidhaa mbovu,ikiwa ni pamoja na chakula,kuingia nchini bila kujali athari kwa afya za watumiaji?Orodha ni ndefu.

Ndio maana Watanzania wengi walio huku Ughaibuni walifurahishwa sana na kauli ya Mheshimiwa Kikwete kuwa atakula sahani moja na watu wanaofanya kazi za umma na kutanguliza maslahi yao binafsi badala ya ya yale ya Taifa ikiwa pamoja na wale wanaosaini mikataba bomu zaidi ya ile ya baadhi ya machifu wetu enzi za ukoloni.Ni dhahiri kuwa nchi yetu iko katika nafasi ambayo haistahili kuwepo.Nchi yetu haipaswi kuwa masikini wa kutupwa wakati tuna rasilimali kibao.

Salamu za wabongo walioko huko kwenda kwa Mheshimiwa Kikwete ni kwamba akaze uzi na kutowalea wazembe kama ilivyokuwa huko nyuma.Mtu akiboronga atimuliwe mara moja.Kuunda tume kuichunguza tume iliyofanya ubadhirifu wakati inachunguza ubadhirifu wa fedha uliofanywa na tume nyingine ni kupoteza fedha tu.Wazembe watimuliwe na ikiwezekana wafikishwe kwenye vyombo vya sheria haraka iwezekanavyo.Historia inaonyesha kuwa binadamu tuna tabia ya kuogopa mambo yanayoweza kuhatarisha nafasi zetu nzuri.Kiongozi anaeteuliwa kuchukua nafasi ya mwenzie alietimuliwa kutokana na utendaji mbovu ana nafasi kubwa ya kuwa mtendaji mzuri kwa vile anajua akiboronga yatamkumba yaliyompata aliyemtangua.

Mwisho,wabongo walioko huku “wanakupa tano” Mheshimiwa Kikwete na serikali yako huku wakitarajia kuwa dhamira yako ya kurudisha heshima ya nchi yetu itatimia.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.