18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Leo tuzungumize michezo,hususan soka.Kwa takriban wiki nzima sasa habari ya soka iliyotawala katika vyombo vya habari vya hapa Uingereza ni kuhusu suala la mchezaji mahiri wa klabu ya Manchester United na timu ya Taifa,Wayne Rooney.Ishu yenyewe ni kwamba ilidaiwa kuwa Rooney alikuwa na madeni yanayofikia pauni 700,000 (takribani shilingi milioni 140 za huko nyumbani) aliyokuwa akidaiwa na makampuni ya kamari (betting).Inasemekana tayari amemalizana na wadai wake.Wapo waliomlaumu mchezaji huyo kwa kutumia vibaya fedha zake,lakini wengine wamemtetea kwamba haikuwa ubaya kutumia kipato chake kinachotokana na ajira yake.

Ndio,soka huku Ughaibuni na hata katika baadhi ya nchi za huko Afrika ni ajira.Ni ajira ambayo inamwezesha mtu kama Rooney kutumbukiza zaidi ya shilingi milioni 100 kwenye kamari.Pointi yangu sio uhusiano wa soka na kamari bali soka kama ajira.Tukirudi huko nyumbani,siku chache zilizopita klabu kongwe za Simba na Yanga zilichimba mkwara kuwa zingesusia ligi kuu ya Bara iwapo mgao wa mapato ungeendelea kuwanufaisha zaidi wengine badala ya wao wanaovuja jasho dakika 90.Binafsi niliguswa sana na hoja za klabu hizo japokuwa kwa bahati mbaya nasikia wakongwe hao wamenywea katika kutimiza azma yao ya kutaka “kieleweke.”Sijui kuufyata huko ni kwa vile viongozi wa klabu hizo walitoa hoja hiyo kama kutingisha kiberiti,au sijui ni ubabe wa vyama vyetu vya michezo huko nyumbani!Lakini naamini klabu hizo zilikuwa na hoja ya msingi kabisa.

Pambano lao la mwisho liliingiza milioni 98 kama sijakosea.Lakini kila klabu ikaambulia shilingi milioni 23.6 tu.Kwa kweli huo ni sawa na uonevu.Mapato hayo yalitokana na umaarufu wa klabu hizo,hivyo zenyewe ndio zilipaswa kunufaika zaidi na mapato hayo.Nadhani klabu hizo zilistahili kupata kiwango kikubwa zaidi ya hicho hasa ikizingatiwa kuwa timu hizo kwa sasa ni kama za kulipwa kutokana na kuwa na wachezaji kadhaa wa kigeni ambao mishahara yao ni ya juu.Jitihada za kuzigeuza klabu hizo kuwa kampuni zimekuwa zikikwama mara kwa mara.Kwa hiyo tofauti na klabu kubwa za huku Ughaibuni ambazo zinaendeshwa kwa mfumo wa kampuni hivyo kutotegemea sana mapato ya uwanjani,chanzo kikuu cha mapato kwa vilabu vyetu vya nyumbani ni mapato yanayotokana na watu wanaoingia uwanjani kushuhudia mechi zao.

Imenisikitisha sana kuona hoja ya klabu hizo imekufa kienyeji.Lakini sikushangaa sana kwa vile sio siri kwamba vilabu vyetu huko nyumbani vinaendeshwa kwa ubabaishaji sana.Kwanza kwa Simba na Yanga hawapaswi kutegemea mapato ya uwanjani kama chanzo pekee cha mapato.Japo hoja ya klabu hizo kugeuzwa kuwa kampuni bado ni ya muhimu sana ingawaje wenyewe wanapuuzia,vipo vyanzo vingine kadhaa vya mapato ambavyo vimetelekezwa.Kwa mfano,kwa kutengeneza kalenda 100,000 zenye picha za wachezaji ambazo zingekuwa katika ubora unaostahili na kuziuza angalau kwa shilingi 500 kila moja,klabu ingejiingizia shilingi milioni 50.Hilo linawezekana kabisa hasa kwa vile gharama za utengenezaji wa kalenda sio kubwa sana na kuna uwezekano wa kupatikana wadhamini wa kugharamia mradi wa aina hiyo.
Kwa mtizamo wangu,watu wanaopaswa kubeba lawama zaidi katika suala zima la ubabaishaji kwenye vilabu vyetu ni hao wanaoitwa wanachama.Hao ndio wanaochagua viongozi wabovu,na ni haohao ambao hawakawii kwenda mahakamani kupinga uongozi ambao wao wenyewe waliuweka madarakani.Wanang’ang’ania kujiita wanachama wakati mchango wao mkubwa katika kuendesha klabu hizo ni kwenda kwenye vyombo vya habari kutaka uongozi wa klabu ujiuzulu,au kocha hafai au wakati mwingine kusema lolote tu ili wasikike hewani.Kama kweli wanachama wa Simba na Yanga wangekuwa wenye mwamko unaostahili basi naamini wangetumia nguvu za wingi wao kuhakikisha hoja zilizotolewa na viongozi wao kuetetea maslahi ya klabu hizo zinashinda.Badala ya hoja hizo kuonekana ni ajenda binafsi za Wambura au Kifukwe zingekuwa ni hoja za klabu na wanachama wa Simba na Yanga.

Kulalamika bila kutoa ufumbuzi wa tatizo ni sawa na kulikuza tatizo.Kwa hiyo,nawajibika kutoa mchango wangu katika kupata ufumbuzi.Nadhani Tenga na wenzie wa TFF wanapaswa kuliangalia upya suala la mgao wa mapato kwa klabu,na sio kwa Simba na Yanga pekee bali vilabu vyote.Vilabu vina haki ya kudai ziada ya wanachokipata kutokana na jitihada zo uwanjani.Kuhusu uendeshaji wa vilabu,Serikali inapaswa kuingilia kati kwa kutengeneza sera ambayo haitotota fursa ya uababishaji,iwe wa viongozi au wanachama.

Alamsiki.

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.