Showing posts with label YANGA. Show all posts
Showing posts with label YANGA. Show all posts

26 Feb 2017








DK 1. Mpira umeanza

DK 3: Yanga wanapata penati baada ya Chirwa kuangushwa na mlinzi wa Simba eneo la Penati.

DK 4: Mathew Akrama anamlamba kadi ya njano Lufunga kwa kumuangusha Chirwa

DK 5 - GOOOAAL: Simon Msuva anawaandikia Yanga bao la kwanza kwa mkwaju wa penati.



DK 10: Simba wanaonesha kumiliki mpira, Yanga wanakuwa makini.

DK 13: Mavugo anapokea pasi nzuri lakini anakuwa butu na kupoteza mpira ule muhimu langoni mwa Yanga, Dida anaudaka.

DK 15: Mchezo sasa upo balanced huku mipango ya Simba ikiwa haijakaa vizuri, wanashindwa kujiamini.

DK 16: Juma Luizio anaotea.

DK 17: Simba wanafanya mashambulizi lakini Dida anawahi na kudaka, Yondani yupo chini baada ya kugongwa katika purukushani hiyo.

DK 19: Kamusoko anapiga krosi murua kutokea kulia, Chirwa anaunganisha kwa kichwa na Agyei anadaka.

DK 20: Yanga wanafanya shambulizi lakini Niyonzima anapiga shuti la kitoto Agyei anaudaka.

DK 22: Kotei anafanya kazi ya ziada kuokoa mpira miguuni kwa Msuva

DK 23: Krosi safi ya Juma Abdul, Zimbwe anaokoa na kuwa kona ya kwanza

DK 23: Niyonzima anachonga kona nzuri hapa lakini Agyei anaruka na kupangua

DK 25: Kamusoko anapokea pasi murua kutoka kwa Chirwa, anapiga shuti lakini mpira haujai vizuri mguu hivyo kuwa dhaifu, Agyei anaudaka.

DK 26 - Sub: Simba wanafanya mabadiliko ya mapema, Anaingia Ndemla na kutoka Luizio.

DK 28: Zuru anapoteza pasi muhimu sana ambayo ingewapa Yanga goli la pili muhimu

DK 29: Nafasi nzuri zaidi kwa Simba, Mavugo akiwa amebaki yeye peke yake na kipa Dida, anapiga mpira wa kichwa dhaifu na unatoka nje.

DK 32: Mavugo anawachambua kama karanga mabeki wa Yanga, Yondani anazuia shuti la Mavugo na Munishi anaudaka.

DK 34: Munishi analeta mbwembwe baada ya kudaka mpira baada ya kukaa na mpira mkononi kwa zaidi ya muda unaoruhusiwa. Simba wanapiga mpira wa adhabu ndogo ndani ya eneo la 18.

DK 35: Said Mdemla anapiga shuti linapaa aka mnazi.

DK 37: Yanga wanafanya shambulizi lakini Agyei anauwahi mpira. Ndemla anapiga shuti maridadi lakini linatoka nje ya lango la goli.

DK 40: Mo Ibrahim anaachia shuti kali sana lakini Munishi anaupoza mpira kwanza na kuudaka.

DK 41: Simba wanaonekana kuzinduka wakati huu wa kuelekea mapumziko. Wanapiga moja mbili lakini Dida anaudaka mpira.

DK 42: Kamusoko anapiga shuti tena lakini mpira haujai mguu, mpira unatoka nje na kuwa goal kick

DK 42: Kamusoko yuko chini baada ya kugongana na Muzamiru

DK 44: Mo Ibrahim analazwa chini karibu na eneo la boksi, anajirusha hadi kwenye 18, wachezaji wa Simba wanadai penati ila refa anasema ni kwenye ukingo wa boksi.

DK 45: Hajibu anapiga mpira wa adhabu, inakuwa goli kick.

DK 45+1: Kamusoko anaonekana hali yake haijatengamaa, analala chini na refa anaita huduma ya kwanza na kumtoa nje ya uwanja

DK 45+3 - Sub: Kamusoko anatoka, anaingia Said Juma Makapu

DK 45+4: Mpira ni mapumzikooooooooo

DK 46: Mpambano wa mahasimu unarejea tena kipindi cha Pili huku Yanga wakiwa kifua mbele kwa bao moja la Msuva.

DK 46: Simba wanafanya mashambulizi ya mfululizo mara mbili lakini umakini wa Munishi anaweza kuokoa hatari zote.

DK 48: Simba wanafanya mashambulizi karibu kabisa na lango la Yanga, Mavugo anamfanyia madhambi mchezaji wa Yanga.

DK 50 -SUB: Anatoka Lufunga anaingia Shiza Kichuya.

DK 52: Mavugo anachezewa madhambi, refa anampa kadi ya njano Vincent wa Yanga

Dk 53: Banda analazimika kufanya kazi ya ziada na kuwa kona
KADI Dk 52, Vicent analambwa kadi ya njano kwa kumfanyia madhambi Mavugo

Dk 53: Msuva anageuka vizuri kwenye boksi la Simba na kuachia mkwaju mkali kabisa, GOAL KICK

DK 55- RED CARD: Boukungu anamuangusha Chirwa akiwa amebaki peke yake nje ya eneo la hatari, anatolewa nje kwa kadi nyekundu

DK 56: Anapiga faulu nzuri lakini Agyei anauona mpira na kuudaka.

DK 57: Simba wanafanya shambuli na kupata kona, Kichuya anaenda kuchonga kona.

DK 57- SUB: Simba wanamtoa Mo Ibrahim na nafasi yake inachukuliwa na Jonas Mkude

DK 63: Yanga wanafanya shambulizi lakini Agyei anatokea na kuondosha hatari

DK 64: Hajibu anapiga shuti kimo cha sungura na Munishi anaudaka kwa umaridadi

DK 66- GOOOOAAL: Mavugo anaisawazishia Simba kwa goal la kichwa kwa pasi Murua ya Shiza Kichuya.

DK 68: Simba pamoja na kuwa pungufu wanaonesha kurudi mchezoni na sasa mchezo ni vuta nikuvute.

DK 70- SUB: Anaingia Deus Kaseke kuchukua nafasi ya Hamis Tambwe, Tambwe leo katiwa kibindoni hafurukuti.

DK 72: Yanga wanakwenda vizuri na krosi ya MSuva inazuliwa na Kichuya na kuwa kona

Simba wanaonesha kupambana huku Yanga wakiwa hawajui walifanyalo, Yanga wanapoteza mipira muhimu ambayo ingeweza kuleta madhara.

DK 77: Haruna Niyonzima anaoneshwa kadi ya njano kwa kucheza ndivyo sivyo

DK 78- SUB: Yanga wanafanya mabadiliko, anaingia Mahadhi na kutoka Zuru

DK 81- GOOOOOAL: Shiza Kichuya akitokea upande wa kulia anaingia vizuri na katikati na kumtungua Munishi goal la kiwango, Munishi hakuwa na ujanja wowote wa kuufikia mpira ule.

DK 83: Defence ya Yanga inaonesha kuchoka kabisa, haina tena maelewano.

DK 85: Mavugo anawachambua kama karanga mabeki wa Yanga wasiopungua watatu, anapiga shuti kali sana na linagonga nguzo ya goli.

DK 90: Zinaongezwa dakika 4 za lala salama, Yanga wanaonesha kuchanganyikiwa. Wachezaji wa Simba Kichuya na Mavugo wanajiangusha ili kupoteza muda.

DK 90+1: Hatari langoni mwa Simba lakini inakuwa goal kick, Agyei anachelewesha mpira Msuva anaukimbilia na kumtengea kipa.

DK 90+4: Mpiraaa umekwishaaaaaa, Simba wanaondoka kidedea na point tatu.

18 Aug 2011


Sosthenes Nyoni
SIMBA, Simba ndio ulikuwa wimbo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam baada vijana hao wa mtaa wa Msimbazi kulipinza kisasi kwa ukifunga Yanga mabao 2-0 kwenye mchezo wa Ngao ya Jamii.

Simba waliofungwa kwenye Kombe la Kagame na Ngao ya Jamii mwaka jana vijana hao wa Mganda Moses Basena walizinduka na kupata mabao ya mapema kupitia kiungo Haruna Moshi 'Boban' dakika 15 na penalti ya Felix Sunzu dakika 38.

Simba iliyoanza kwa kasi mchezo huo ilifanikiwa kupata bao la kuongoza kupitia kwa Moshi 'Boban' aliyemalizia vizuri krosi ya kutoka upande wa kushoto iliyopigwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Sunzu aliyekuwa na ushirikiano mkubwa na Emmanuel Okwi.

Mshambuliaji Sunzu alifungia Simba bao la pili kwa mkwaju wa penalti baada ya Nadir Haroub kumchezea vibaya Moshi 'Boban', kwenye eneo la hatari dakika 35. Sunzu alilazimika kuonyesha ueledi wake pale alipotakiwa kurudia penalti hiyo baada ya mwamuzi Israel Mjuni kusema Kado alitokea kabla ya kupigwa kwa penalti ya kwanza pamoja na kuwa alikuwa amefunga.

Kocha Moses Basena aliyeonekana kujifunza kwa makosa alitumia mfumo wa 4:2:3:1 na kutoa nafasi kubwa kwa Okwi, Haruna na Sunzu kutawala sehemu kubwa ya kiungo tofauti na ilivyokuwa kwenye fainali ya Kombe la Kagame.

Okwi alifanya atakalo mbele ya mabeki wa Yanga walionekana kuwa kama watu waliozidiwa na mazoezi na kukosa unyumbulifu mchezoni, huku safu ya ulinzi wa Simba chini ya mkongwe Victor Costa aliweza kuwapoteza mchezoni kabisa mshambuliaji Keneth Asamoah na Jerry Tegete.

Kiungo Haruna Niyonzima alijitahidi kuonyesha uwezo mkubwa wa kutawala mpira na kujaribu kutafuta goli kwenye mechi yake ya kwanza ya watani wa jadi, lakini alikosa msahada kutoka kwa wenzake.

Simba ilianza mashambulizi kwa kasi na dakika kwanza Okwi alikosa bao baada ya shuti lake kumgonga Haroub na kupaa juu ya goli.

Okwi alipoteza nafasi nyingine dakika 8 baada ya kuwalamba chenga mabeki wa Yanga, lakini aliugonga mpira mbele zaidi na kipa Shaaban Kado akauwahi.

Beki wa Yanga, Chacha Marwa, nahodha Shadrack Nsajigwa alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Okwi. Naye Juma Nyoso wa Simba alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Asamoah.

Haruna Niyonzima alipiga shuti la umbali wa mita 25 baada ya kumchungulia Juma Kaseja kwa bahati mpira huo ulipaa juu ya goli.

Kipindi cha pili Yanga iliamka baada ya kuingia Hamisi Kiiza na Rashid Gumbo lakini walishindwa kuipenya ngome ya Simba.

Yanga waliendeleza sera yao ya kugomea jezi za wadhamini wa ligi Vodacom zenye nembo nyekundu kwa kuvaaa jezi za mdhamini wao TBL tofauti na Simba wenyewe walivaa zile walizopewa na Vodacom

Vikosi Yanga; Shaaban Kado, Shadrack Nsajigwa, Oscar Joshua, Nadir Haroub, Chacha Marwa, Juma Seif, Godfey Taita, Haruna Niyonzima, Keneth Asamoah/ Gumbo, Jerry Tegete, Kigi Makasi/ Kiiza.

Simba: Juma Kaseja, Said Nasoro, Amir Maftah, Juma Nyoso, Victor Costa, Partick Mafisango, Salum Machaku/ Kiemba, Jerry Santo, Felix Sunzu, Haruna Moshi/ Gervais Kago, Emmanuel Okwi/ Kapombe.

CHANZO: Mwananchi

16 May 2011



Yanga wampa uchifu Manji 
Sunday, 15 May 2011 20:54

Clara Alponce
WAZEE wa klabu ya Yanga jana walimkabidhi Mkuki, Ngao na Kigoda kama alama ya cheo cha uchifu kwa aliyekuwa mfadhili wao Yussuf Manji.Manji alikabidhiwa heshima hiyo na kamati ya wazee ya muafaka wa Yanga chini ya kiongozi wake Mzee Yahaya Akilimali.

Akizungumza kwenye hafla hiyo mama Shadia Karume alisema Manji amejifunza mengi Yanga na amerejea rasmi kwa ajili ya kufanya kazi ya kuijenga Yanga mpya.Mama Karume alisema," Manji anatakiwa kujua hasira, jazba hazifai namtaka asahau yote yaliyopita."

Mama Karume aliongeza kuwa kuna watu wengi waliofanya mambo makubwa na mazuri Yanga huko nyuma na Manji ni moja wao."Mume wangu ndiye aliyejenga jengo la Yanga hapa Dar es Salaam, lakini angejisikia vibaya kama lingeachwa na kuharibika bila ya kufanyiwa ukarabati kama aliousimamia Manji,"alisema Mama Karume ambaye pia alimtaka Manji kujenga jengo lingine la Yanga huko Zanzibar kwa sababu uwanja umeshapatikana.

Tukio hilo lilishuhudiwa na viongozi wa serikali akiwemo Jamal Rwambo, Mbunge Mussa Zungu, Mudhihir Mudhihir pamoja na wachezaji wa Yanga huku burudani ikitolewa na bendi za Msondo, Sikinde na Tanzanite

CHANZO: Mwananchi.

11 May 2011




Africa here we come! Birmingham set to tour Tanzania ahead of new season

By Sportsmail Reporter

Last updated at 11:11 AM on 11th May 2011

Birmingham are planning a pre-season trip to Tanzania in July.

The details have not yet been finalised but first-team coach Andy Watson and chief medical officer Ian McGuinness have travelled to Africa to inspect facilities

Birmingham are expected to undertake a four-day trip, with Tanzanian top-flight sides Simba or Yanga, or possibly both, providing the opposition at the National Stadium in Dar-es-Salaam.

Watson told the club's website: 'The people of Tanzania that we have met have been very hospitable and kind, and from what we've seen of the country so far it looks an amazing place.
'We have been made aware of just how much the Tanzanian people love their football - especially the Barclays Premier League - and when everything is fully in place we look forward to coming back in July and playing.'

SOURCE: The Daily Mail

1 Nov 2008

Picha kwa hisani ya SPOTI NA STAREHE

Ubabaishaji unakwamisha sana maendeleo ya taifa letu.Lakini hapa nataka nizungumzie ubabaishaji kwenye uongozi na uendeshaji wa vilabu vya Simba na Yanga.Hebu soma kwanza hapa chini kabla hatujaendelea na mada hii ya kupotezea muda.
MWENYEKITI wa klabu ya Simba Hassan Dalali amemteua Mkurugenzi wa Kampuni ya Aurora Security, Ally Suleiman kuwa mshauri wake atakayesaidia kumshauri kuhusiana na mambo yote yanayohusu masuala ya uongozi wa Simba. 

Akizungumza Dar es Salaam jana, Dalali alisema ameamua kuwa na mshauri ili aweze kuiendesha klabu yake kwa umakini na kufuata mwongozo ambao utaisadia klabu hiyo. 

Dalali alisema Suleiman amekuwa mtu wa karibu, ambaye ametoa mchango mkubwa ndani na nje ya klabu, hivyo ameona ni muhimu na kuwa uteuzi huo ni kujenga Simba yenye umoja na mshikamano.
Alisema klabu yake ipo katika mikakati ya kuhakikisha Simba inakuwa klabu kubwa, huku ikiimarisha timu yake na kuwa mfano wa kuigwa. 

"Uteuzi wa mshauri wangu umezingatia vigezo vingi ikiwemo ukaribu wake katika mambo ya msingi yanayoihusu klabu yetu," alisema Dalali.

Akizungumzia uteuzi huo, Suleiman alisema amefurahi kupata wadhifa huo na kuahidi kuisaidia klabu hiyo kwa hali na mali lengo likiwa ni kujenga Simba imara
CHANZO:Majira
Baada ya kufungwa na Yanga ndio Dalali anakumbuka umuhimu wa kuwa na mshauri!?Kwa tafsiri nyingine ni kwamba kwa muda wote tangu apate uenyekiti wa Simba m-babaishaji huyu amekuwa akiongoza kwa kubahatisha.Ndio!Kama sio hivyo,mshauri wa nini muda huu? Yaani ni ubabaishaji juu ya ubabaishaji.

Mimi ni mpenzi wa Simba.Zamani Simba ikifungwa basi ni majonzi makubwa.Katika familia yetu,watoto wote wanane tunaipenda Simba.Marehemu Mama (Mungu Amlaze Mahali Pema Peponi) alikuwa mpenzi wa Pan Africa,kwa sababu mpwae,Gordian Mapango,alikuwa mchezaji wa timu hiyo.Baba aliamua kuisapoti Yanga,sio kwa vile anaipenda bali kuleta "usawa" ndani ya familia.

Kwa miaka kadhaa sasa,nimebaki kuwa mpenzi-jina tu,it doesnt really make any difference Simba ikishinda au ikifungwa.Sababu kuu ya kupoteza mapenzi kwa Simba,na soka ya Tanzania kwa ujumla,ni ubabaishaji uliopita kiasi wa viongozi wa klabu hiyo kongwe.Ubabaishaji huo umepelekea timu hiyo kukimbiwa na wafadhili kibao na kupoteza udhamini mbalimbali.Nani mwenye akili timamu atawekeza kwenye biashara kichaa?Ukiona mtu anapanda mpunga jangwani basi hicho sio kilimo bali tambiko.Ndo maana nashawishika kuamini kwamba uwepo wa Manji hapo Yanga unaweza kuwa ni "zaidi ya mambo ya soka".

Nirudi kwenye title ya post hii.Nilitegemea Simba ingefungwa na Yanga.Na nilitegemea kipigo kikubwa zaidi ya hilo bao moja.Kama Toto Africa waliweza kutufunga bao 4-1,tungetegemea nini katika mechi na Yanga?Anyway,kipigo ni kipigo.Mategemeo yangu ya kipigo yametimia,japo kwa idadi tofauti na niliyokuwa naitarajia.Kingine nilichadhani kingeandamana na kipigo hicho ni kuutimua uongozi mzima wa Simba.Hilo halijatokea lakini naamini viongozi hao wamekalia kuti kavu.By the way,uongozi wa Simba na Yanga ni zaidi ya kukalia kuti kavu;ni sawa na kibonge cha mtu kuning'inia kwenye utando wa buibui.Mtu mwenye mtizamo makini hawezi kutamani kuongoza timu hizi za kibabaishaji,ambazo lugha wanayoelewa "wanachama" ni ushindi tu.

Of course,timu inatakiwa ishinde kila mechi.Lakini timu itashinda vipi ikiwa haina vyanzo vya mapato zaidi ya kutembeza bakuli kama ombaomba?Hao wachezaji wanakula nini kabla ya kujituma uwanjani?Au ni timu za kiroho ambapo Neno la Mungu linashinda mahitaji ya fedha na vifaa?Kwanini wachezaji wasipokee rushwa iwapo viongozi wanawaibia mishahara yao kiduchu inayopatikana kwa migomo?Wanachama wababaishaji wa klabu hizi wanajua kupiga majungu tu lakini hawana mchango wowote kwa ustawi wa klabu hizi.Ndio maana akiondoka mfadhili mmoja timu inakuwa hohehahe.Na ndio maana Manji amekuwa mungu-mtu hapo Yanga (na mwenyekiti Madega amegeuka kuwa msemaji wa familia ya mfadhili kuhusu ugonjwa wa mfadhili huyo!)

Je kuna ufumbuzi wa tatizo hili la ubabaishaji wa viongozi na wanachama wa Simba na/au Yanga?Kwa mtizamo wangu nadhani ufumbuzi upo lakini unahitaji udikteta wa aina flani.Unajua kuna udikteta kwa ajili ya watu na udikteta dhidi ya watu.Udikteta kwa ajili ya watu ni kama ule wa Sokoine:kwa wahujumu wa uchumi Sokoine alikuwa dikteta,lakini kwa wananchi wengi kiongozi huyo alikuwa ni shujaa na mkombozi.Sihitaji kuelezea dikteta dhidi ya watu ni wa aina gani,lakini anaweza kuwa hata anayethamini haki za binadamu za mafisadi wachache badala ya walalahoi walio wengi.Je udikteta kwa ajili ya watu unawezaje kuokoa vilabu vyetu na soka la Tanzania kwa ujumla?Ni kwa serikali kutumia sheria kali katika kuleta mageuzi ya kudumu katika vilabu vya soka.Najua kuna ishu za watu kwenda mahakamani kupinga maamuzi flani,lakini ukweli unabaki kwamba sheria zikiandaliwa na kusimamiwa vizuri basi wahuni wanaokimbilia mahakamani watafyata mkia.Njia nyepesi ya kuvibana vilabu hivyo ni kutunga sheria inayovitaka kujisajili upya,kwa mfano.Pia sheria hiyo inaweza kutamka bayana aina ya viongozi,namna ya uendeshaji wa vilabu unavyopaswa kuwa na hata aina za wanachama.FIFA itatufungia kwa vile serikali imeingilia mambo ya soka?Why care!kwani sasa hatujafungiwa na tumeendelea kuwa kichekesho kila mwaka?Bora tu tufungiwe ili tuweze kujipanga vyema kuliko kuendeleza ubabaishaji huu.Au msomaji unasemaje?

22 Oct 2008


HII ya Yanga haijapata kutokea kwenye historia ya soka ya Ligi Kuu Tanzania Bara. Ndio kauli nyepesi unayoweza kuitumia kama ukipata nafasi ya kupita karibu na kambi ya Yanga jijini Dar es Salaam.

Yanga imeweka kambi kwenye Hoteli ya Lamada Ilala, jijini Dar es Salaam chini ya ulinzi mkali wa askari ambao haujapata kutokea kwa timu yoyote ya Tanzania pengine tangu Ligi Kuu Bara ianzishwe.

Ulinzi huo ambao wachezaji wa Yanga wamesema kwamba hawajapata kuuona, unadaiwa kuwekwa na mdhamini mkuu wa klabu hiyo, Yusufu Manji kutokana na kikosi hicho kukabiliwa na pambano gumu dhidi ya Simba Jumapili kwenye Uwanja Mkuu wa Tanzania jijini Dar es Salaam.

Walinzi hao wengine wakiwa na silaha ambao wametapakaa kila kona mpaka kwenye korido za kwenda vyumbani, walimwagwa hotelini hapo juzi Jumapili jioni wakati mechi baina ya Yanga na Polisi Dodoma ikiendelea kwenye Uwanja wa Taifa. Yanga ilishinda 3-1.

"Tuliporudi tu ile jioni tukashangaa mazingira yamebadilika ghafla, kila kona ina walinzi na wengine wamebeba silaha na wengine wana virungu pamoja na baadhi ya wanachama ambao walikuwa wanapitapita huku na huko kutulinda," alidokeza mchezaji mmoja.

"Sijapata kuiona hali hii, mpaka wachezaji tunashangaa kwa jinsi walinzi walivyomwagwa huku nje wapo kama 12, kwenye korido za vyumbani wapo na kwenye ngazi za kushukia pia wapo.

"Huruhusiwi kutoka nje ya geti na hata ukikaa nje mazungumzo yako yanafuatiliwa kila hatua, yaani mpaka wageni wanaoingia wanaulizwa maswali kama ni mtu mwenye chumba chake lazima waende mpaka chumbani wakahakikishe kama kweli ana chumba.

"Sisi wenyewe wakati unatoka chumbani unaulizwa unakwenda wapi, ukitoka nje kwenye ngazi unawakuta pia hawa walinzi wanafanana na wale wa ile kampuni inayolinda kule ofisni kwa Manji."

Mchezaji mwingine alisema; "Huku ni mitutu tu kila upande bwana, hata kama unaenda nje kununua vocha au kitu chochote kuna walinzi.

"Kwa jinsi palivyo huku utafikiri tunacheza fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika tena na Real Madrid, ni kasheshe tupu ndugu yangu lakini ndio soka," alisema mchezaji mwingine.

Mwanaspoti ilipojiri kwenye kambi ya timu hiyo jana, askari hao walicharuka mithili ya mbogo wenye njaa na hawakutaka kusikiliza chochote.

"Unakwenda wapi? Wewe ni mteja hapa au unakwenda kuwaona wachezaji wa Yanga?" Walisema walinzi hao wakiwazuia waandishi wa Mwanaspoti kuingia ndani ya hoteli hiyo.

"Huwezi kuingia humu hotelini mpaka upate kibali cha Yanga, wasiliana na mwenyekiti au meneja wa timu," alisema askari mmoja wa kampuni ya Group 7 Security aliyekuwa ameshika rungu.

"Ondokeni eneo hili haraka, usije ukatusababishia matatizo makubwa au tukakufanya chochote baadaye ikawa matatizo, ondoka bwana kwa usalama wako," alisema mlinzi mwingine aliyekuwa amekunja sura.

Waandishi wa Mwanaspoti wamekuwa wakienda mara kwa mara katika hoteli hiyo kufanya mahojiano na wachezaji wa timu hiyo, lakini kila kitu sasa kimebadilika na mawasiliano pekee yaliyobaki ni kwa njia ya simu.

Yanga ambayo imekuwa ikinyanyaswa na Simba kwenye Ligi Kuu Bara kwa takribani miaka saba sasa, inaonekana kujizatiti na kutaka kulipiza kisasi na hasa kutokana na hali kutokuwa shwari ndani ya Simba.

Viongozi wa Yanga wameapa kufanya mauaji makubwa Jumapili kwa madai kuwa dalili za kuimaliza Simba zilianza mwishoni mwa wiki wakati Toto wenye urafiki na Yanga walipoifunga Simba mabao 4-1

CHANZO: Mwanaspoti

28 Oct 2007

Asalam aleykum,

Kwanza nianze kwa salamu za rambirambi kwa familia,ndugu,jamaa na marafiki wa marehemu Salome Mbatia,aliyetutoka hivi majuzi kutokana na ajali ya gari.Sote ni wasafiri,mwenzetu ametutangulia tu,Bwana ametoa Bwana ametwaa,jina lake lihimidiwe milele.Baada ya rambirambi hizo naomba kuzungumzia suala moja ambalo kwa naona kwa namna flani linaathiri umoja wetu wa kitaifa.Jambo hilo ni kuendekeza itikadi za chama kwenye matukio ambayo kimsingi ni ya kitaifa zaidi kuliko kichama.Katika picha mbalimbali kuhusu msiba wa marehemu Mbatia nimeona “makada” lukuki wa chama tawala wakiwa katika magwanda yao ya kijani na nyeusi.Nikabaki najiuliza,hivi waungwana hao wangevaa mavazi yao ya kawaida wangeonekana hawana majonzi ya msiba huo?Au walivaa mavazi hayo kwa maagizo ya kiongozi flani?Kama ni maagizo kutoka ngazi za juu,mbona viongozi wakuu wa chama hicho walikuwa kwenye mavazi yao ya kawaida tu (hasa suti nyeusi)?JK,Malecela,Karume,Makamba,nk wote walikuwa wamevalia suti nyeusi na wala sio magwanda ya kijani na nyeusi,pengine kwa sababu msiba huo ulikuwa wa kitaifa,na hata jeneza la marehemu halikuvikwa bendera ya CCM bali ya Taifa.

Nafahamu marehemu Mbatia alikuwa mwanachama,kada na kiongozi wa chama dume,lakini marehemu pia alikuwa naibu waziri wa serikali ambayo japo inaongozwa na CCM lakini inawatumikia Watanzania wote bila kujali itikadi zao.Katika utekelezaji wa majukumu yake ya unaibu waziri,marehemu Mbatia alikuwa akigusa maisha ya kila Mtanzania,awe mwanachama wa CUF,TLP,Chadema,au kama sie tusio memba wa chama chochote.Nafahamu waliovaa magwanda ya CCM watasema kuwa walitinga mavazi hayo kutokana na nafasi ya marehemu katika chama,lakini sote tunafahamu kuwa alama za chama (mfano bendera,vipeperushi,mavazi,nk) zina tabia ya kuvuta hisia hasi katika mikusanyiko ya isiyo ya kichama.Nafahamu pia kwamba kila mwombolezaji alikuwa na haki ya kuvaa vyovyote atakavyo lakini pia naamini wengi wetu tunapojiandaa kwenda kwenye misiba huwa tunatafakari nini cha kuvaa,na kuepuka mavazi ambayo yanaweza kuleta hisia tofauti.

Hakuna dhambi kuweka maslahi ya chama mbele ya chama kingine lakini ni dhambi kubwa kuweka maslahi ya chama mbele ya maslahi ya taifa.Chama cha siasa kinaweza kufa lakini taifa lazima liendelee kuwa hai.Mtu anaweza kuamua kuhama chama kimoja na kuingia kingine kadri apendavyo,lakini ni mbinde kwelikweli kuhama utaifa wako na kuchukua mwingine kirahisi namna hiyo.Nafahamu kuna watakaopingana nami,lakini binafsi naamini kwamba kuna wenzetu wamekuwa wakituletea “politiki” hata pale pasipostahili.Yaani matukio kadhaa ya kitaifa yamekuwa yakiporwa na hao wanaotaka kutuonyesha namna gani walivyo wakereketwa kwenye siasa.Na katika hili sio wanachama wa kawaida tu bali hata baadhi ya viongozi wenye nyadhifa serikalini.Kuweka kando mambo ya chama na kuzungumzia masuala ya kitaifa hakumfanyi kiongozi wa serikali kukosa sifa za uongozi.Kuna vikao na mikutano ya chama,na huko ndiko mahala pa kupiga propaganda za vyama.

Kwa kawaida huwa naanza makala zangu na habari za ughaibuni lakini niliona ni vema katika makala hii nikaanza na mada hiyo ya msiba wa marehemu Mbatia,na “kuwananga” wale walioleta mambo ya siasa kwenye msiba huo wa kitaifa.Huku ughaibuni,duru za kisiasa zinaelekea zaidi eneo la Ghuba ambapo kwa upande mmoja hali ya usalama ni ya wasiwasi huko kaskazini mwa Irak kwani majeshi ya Uturuki yameripotiwa kufanya mashambulizi kadhaa dhidi ya Wakurd.Waturuki wanadai kuwa lengo la mashambulizi hayo ni kuwadhibiti wapiganaji wa kikundi cha PKK kinachipigania kuunda kwa taifa huru la Wakurd.Kwa upande mwingine,kuna dalili kwamba Marekani inajiandaa kuivamia Iran.Majuzi,Marekani ilitangaza vikwazo kadhaa dhidi ya Iran,lakini zaidi ya hapo kuna taarifa kwamba jeshi la anga (US air force) limeomba fedha za dharura dola milioni 88 kwa ajili ya kufanya marekebisho kwenye ndege za kivita ziitwazo B2 ili ziweze kuhimili uzito wa mabomu yanayojulikana kama “Big Blu” au “the Mother of All Bombs” (mama wa mabomu yote).Mabomu hayo yana uzito wa takriban tani 13 kila moja,na yana uwezo mkubwa zaidi wa kupenya vizuizi (ardhi,miamba,nk).Inasemekana kuwa majengo ya kituo cha nyuklia cha Iran huko Natanz yapo futi 75 chini ya ardhi,Inaelezwa pia kwamba tayari Marekani imeshatambua “targets” 1000 nchini Iran ambazo zitakuwa za kwanza kushambuliwa pindi mambo yatapokuwa mambo.

Mahesabu ya kisiasa yanaashira pia kwamba wazo la mkutano kati ya Israel na Palestina utakaofanyika hivi karibuni huko Annapolis,Marekani (ambao unatarajiwa “kuzaa” taifa la Palestina) ni miongoni mwa dalili za Marekani kujipanga kuivamia Iran.Yaani mantiki hapo ni kwamba kwa kuunda taifa la Palestina,kelele za mataifa ya Waarabu wa Sunni kama Saudi Arabia na Misri zitakuwa sio kubwa sana pindi Iran itakaposhambuliwa na Marekani.Hata hivyo,wazo la kuishambulia Iran linaangaliwa kwa wasiwasi na baadhi ya wajuzi wa siasa za kimataifa na diplomasia.Kuna wanaodhani kwamba ni vema Marekani ikamaliza kibarua ilichojipachika huko Irak na Afghanistan kabla ya kukimbilia kuivamia Iran.Pia wanaonya kwamba uvamizi dhidi ya Iran unaweza kuzua wimbi kubwa la ugaidi wa kimataifa (pengine kutokana na madai kwamba Iran imekuwa ikivisaidia baadhi ya vikundi vinavyodaiwa kuwa vya kigaidi,mfano Hizbollah),kukongoroa kabisa hali ya usalama nchini Irak na pengine kusababisha bei ya mafuta kupanda zaidi ya dola 100 kwa pipa.

Sababu zinazotolewa na Marekani kuhusu umuhimu wa kuidhibiti Iran ni pamoja na kwamba dunia itakuwa mahala salama zaidi iwapo Iran haitakuwa na uwezo wa kutengeneza au kumiliki silaha za nyuklia (ilishasemwa huko nyuma kuwa dunia itakuwa salama zaidi pindi Saddam Hussein atapong’olewa madarakani).Ukweli ni kwamba Iran yenye uwezo wa kinyuklia ni tishio kwa swahiba mkuu wa Marekani,Israel.Pia kuna wanaotaka Bush aingie kwenye vitabu vya historia kwa “kuiadhibu na kuidhibiti Iran na hivyo kuepusha madhara yanayoweza kutokea pindi nchi hiyo ikiweza kutengeneza na kumiliki silaha za maangamizi”.Waumini wa mawazo haya wanatambua kuwa Bush amebakiwa na muda mchache kabla hajafungasha virago vyake kutoka jengo lilipo namba 1600 Pennsylvania Avenue (makazi ya rais,White House),na wanadhani kwamba asipotumia muda huu kuishikisha adabu Iran,basi inaweza kuwa vigumu mno kufanya hivyo mbeleni hususan iwapo mgombea yoyote wa chama cha Democrats atamrithi Bush.

Nirejee tena huko nyumbani.Hapa nina mawili.Kwanza,katika kikao kilichopita cha Bunge tulisikia namna baadhi ya watendaji katika Wizara ya Maliasili na Utalii wanavyoendeleza ufisadi.Waziri alieleza kuwa ameshakabidhi orodha ya wahusika mahala panapostahili,na akaahidi kuendelea kuwabana mafisadi katika wizara hiyo.Tukio la hivi karibuni ambapo magogo kadhaa yalikamatwa yakiwa tayari kusafirishwa nje,limezuia “mchezo wa kuigiza” ambapo wakati Waziri anasema hivi baadhi ya watendaji wake wanadiriki kumpinga hadharani kwa kusema vinginevyo.Hivi hawa wanaompinga Waziri wanapata jeuri hiyo wapi?Nimeona kwenye gazeti la “Habari Leo” ambapo Waziri Maghembe alieleza kwamba amejipanga vizuri kukabiliana na matatizo yote ndani ya wizara yake,ikiwa ni pamoja na tatizo la ufisadi.Yayumkinika kutabiri kuwa dhamira yake nzuri inaweza isifanikiwe kutokana na kiburi kilichojengwa na baadhi ya anaowaongoza katika wizara hiyo ambapo bila kujali protokali au nidhamu wanadiriki kupinga hadharani na kauli halali ya serikali (kupitia waziri wake).Hivi jeuri,kiburi na kujiamini kwa “wazalendo” hao inatoka wapi?

Mwisho,ni ushindi wa Simba dhidi ya Yanga.Mwenye kununa na anune,lakini ndio hivyo tena,milioni 50 hazikufanikiwa kumaliza uteja wa watani wetu wa mtaa wa Jangwani.Nilishatabiri katika makala za nyuma kuwa atakaefungwa kwenye mapambano wa watani wa jadi ataingia kwenye mgogoro.Mie nadhani kufungwa huko ni sehemu ndogo tu ya tatizo linaloikabili Yanga.Ukiangalia maelezo aliyotoa Mwenyekiti wa klabu hiyo pale mfadhili wao alipojitoa (kwa muda!?) ambapo alieleza kwa undani na kwa kuzingatia vipengele vya sheria kuhusu utata uliopo kwenye suala zima la klabu hiyo kugeuzwa kampuni.He!!muda si mrefu Mwenyekiti huyohuyo alisikika tena akipita huku na kule kuomba radhi.Je ina maana yale maelezo aliyotoa awali hayakuwa sahihi?Mie naamini yalikuwa,bado yako na yataendelea kuwa sahihi kama kweli Yanga (na Simba pia) wanataka wafike sehemu wakajiendesha wenyewe kwa mafanikio na kuachana na utegemezi.Yote yanawekana iwapo kila mmoja atatimiza wajibu wake.

Alamsiki

27 Aug 2007

Asalam aleykum,


Kuna habari flani nimeiona gazetini imeniacha nakenua meno kwa kicheko.Kwa mujibu wa gazeti moja la Daily Mail la hapa Uingereza eti inadaiwa kwamba wanawake warefu “wanawazimia sana” wanaume wafupi.Kilichopelekea madai hayo ni maswali wanayojiuliza wafuatiliaji wa mambo ya watu (wambeya?) eti kwanini mwanamitindo wa kimataifa Sophia Dahl “amekolea” kwa mwanamuziki “andunje” wa midundo ya jazz,Jamie Callum.Gazeti hilo linadai kwamba wanaume wafupi huwa wanafanya jitihada sana kuhakikisha kuwa wanafidia “pengo” la urefu wao kwa kujituma kwenye maeneo mengine.Hoja nyingine ya kuchekesha ni ile inayodai kuwa watu wafupi ni “vipotabo” kwa wanawake warefu,na hata wakialikwa kwenye nyumba za watu warefu basi ni rahisi kwa “masoti chesisi” hao kufiti kwenye makochi pasipo kulalamika kuwa miguu inauma iwapo kochi lenyewe ni la kujibana.Sijui habari hiyo inawahusu wanaume wafupi wa nchi za Magharibi pekee au dunia nzima lakini lililo wazi ni kwamba suala la mwanamke kumzimia mwanaume au mwanaume kumzimia mwanamke ni la mtu binafsi,na ufupi,urefu,wembamba au unene sio kigezo muhimu sana japo sote tunafahamu kwamba wengi wetu tuna “mapendezeo” yetu.


Wiki iliyopita nilipata nafasi ya kushuhudia mchezo wa kirafiki wa soka kati ya timu ya taifa ya Scotland dhidi ya ile ya Afrika Kusini (Bafana Bafana),mechi iliyofanyika kwenye uwanja wa Pittodrie hapa Aberdeen.Ilipendeza kuona Waafrika wachache wanaoishi hapa wakiwa wametinga jezi za Bafana kuonyesha sapoti yao kwa timu hiyo.Japo mechi hiyo iliisha kwa Scotland kuibuka na ushindi kiduchu wa bao moja kwa bila, “sie” tuliofungwa (Waafrika wote siku hiyo tuligeuka kuwa Wasauzi) tulifarijika kuiona timu ya “nyumbani” ikitandaza kabumbu la kuvutia.Unajua mara nyingi hawa watu weupe wanakupa heshima pale utapowaonyesha una uwezo sawa nao au pengine zaidi yao.

Na wikiendi nilipata fursa ya kuangalia (kwenye runinga) michuano ya kimataifa ya riadha kutoka huko Osaka,Japan.Kama kawaida,Waethiopia na Wakenya wametesa vilivyo.Nimesoma kwenye magazeti yahuko nyumbani kuwa nasi tunawakilishwa na wanariadha kadhaa.Sijui tutaambulia chochote au itaendelea kuwa hadithi ile ile ya kuwa wasindikizaji wa kudumu.Lakini naamini kwamba kama Wakenya na Waethiopia wanaweza kutawala kwenye anga hizo,basi nasi pia tunaweza kabisa kufanya vizuri.Ni lini tutapata akina Filbert Bayi na Suleiman Nyambui wengine?Upeo wangu mdogo wa Jiografia unanishawishi kuamini kwamba hali ya hewa ya mkoa kama Arusha unatupatia mazingira mazuri ya kuzalisha wanariadha ya viwango vya kimataifa.Na ushahidi upo kwa kuangalia “perfomance” ya baadhi ya mashujaa wetu wa miaka ya nyuma.Penye nia pana njia,na kama tutawekeza vya kutosha basi kwa hakika tutaweza kurejesha historia ambayo kwa sasa imeshaanza kusahaulika.

Kuna dalili za mafanikio huko mbele ya safari kwenye soka letu. “Uchawi wa Kibrazil” wa Maximo na mwenzie Tinoco unaelekea kuzaa matunda.Ukichanganya na sapoti ya kutosha kutoka kwa JK mwenyewe basi si ajabu nasi tukajikuta tunaingia kwenye ramani ya soka ulimwenguni.Kinachonipa shaka ni matatizo ya uongozi kwenye vilabu vyetu vya soka.Maana kila kukicha utasikia wanachama Simba wanataka kupindua uongozi,au wenzao wa Yanga wanamkalia kooni kiongozi flani,au mara usikie kocha flani kabwaga manyanga kwa vile hajalipwa stahili zake,na vioja vingine visivyo na mwisho.Katika makala yangu iliyopita niliwausia viongozi wa Simba kutumia vizuri mkataba walioingia na kampuni moja kupromoti “chata” ya Adidas.Hee!haujapita muda mrefu nasikia baadhi ya wanachama wanapania kuung’oa uongozi ulio madarakani.Na hapohapo nasikia kocha Twalib Hilal anasema anarejea umangani kwa vile hajakamilishiwa malipo yake.Kiongozi mmoja anang’aka jukumu la kumlipa kocha huyo kwa kudai kwamba aliletwa na Friends of Simba.Ok,tuseme kuwa mapenzi ya Friends of Simba kwa klabu yao yaliwasukuma kumtafuta kocha mwenye uwezo wa kuipeleka mbali klabu ya Simba,na wakamsomesha Twalib hadi akakubali kusamehe mshahara mnono huko Umangani.Sasa,viongozi hawakupaswa kubweteka na kuliacha jukumu la mshahara kwa Frienda of Simba pekee.Kwanza,msaada uliotolewa na kikundi hicho unaweza kutafsiriwa kama msaada kwa uongozi kwani sote tunajua “politiki” za Simba na Yanga:matokeo yakiwa mabaya basi uhai wa viongozi kuwa madarakani unakuwa unaning’inia kwenye utando wa buibui.

Ni kama kichekesho vile kwa sababu miezi michache iliyopita,uongozi huohuo wa Simba uliweka msimamo thabiti dhidi ya kundi la Friends of Simba wakidai kundi hilo linaihujumu klabu hiyo.Navyoelewa mimi ni kwamba kwa vile klabu hiyo inajiendesha “Kiswahili” ni lazima wawepo watu wa kuikwamua kifedha pale inapokwama,na kwa namna mambo yalivyo,kila wakati uchumi wa vilabu vyetu ni wa kusuasua kama suala la amani huko Somalia.Ufumbuzi wa matatizo sio Mapinduzi,kwani yameshafanyika mengi tu na hakuna lolote la msingi lililopatikana.Wala kukimbilia mahakamani sio ufumbuzi wa matatizo.Na kuwa na mahusiano mazuri na vipoba hakuwezi kuwa ufumbuzi wa kudumu wa matatizo ya klabu kama Simba.Ufumbuzi pekee ni kwa vilabu hivyo kujiendesha kibiashara.Soka ni zaidi ya burudani kwani ikiendeshwa kisasa inaweza kuwa chanzo kizuri cha mapato.Unaposikia Manchester United,Chelsea au Liverpool zinavutia wawekezaji kutoka nje ya Uingereza sio kwamba matajiri hao ni wakereketwa sana wa soka (ingekuwa ni ukereketwa basi wangenunua vilabu katika nchi zao) bali wanajua bayana kwamba soka ni biashara yenye faida.

Twanga Pepeta wako ziarani hapa Uingereza,na wametapisha kumbi walizotembelea.Hivi kwa mfano Simba au Yanga wangefanya ziara sehemu mbalimbali duniani wasingeweza kujichumia mapato mkubwa pengine zaidi ya hayo wanayopata Twanga?Na kwa kufanya ziara nje ya nchi vilabu vyetu vingeweza kuua ndege wawili kwa jiwe moja:kutengeneza mapato ya kutosha na kuitangaza vipaji vya wanasoka wao,ambao wakipata timu huku nje inamaanisha mapato zaidi kwa vilabu hivyo.Najua wapo wanaoniona kama nimechanganyikiwa kwa kutoa mawazo kama haya.Siwalaumu kwani kwa jinsi wanavyofahamu ubabaishaji uliokithiri kwenye vilabu vyetu,hata ziara za mikoani zinahitaji mitulinga ili ziwe na mafanikio.

Mwisho,ningependa kutumia fursa hii kuwapongeza marais wa nchi za Afrika Mashariki kwa kuzingatia maoni ya wananchi wao kuhusu suala la kuharakisha Muungano wa nchi hizo.Mimi ni muumini wa hekima ya umoja,yaani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.Lakini umoja kati ya watu wenye “backgrounds” zinazotofautiana unaweza usizae matokeo yanayokusudiwa.Nilisoma sehemu flani ambapo DCI Manumba aliweka bayana kuwa kuongezeka kwa wimbi la ujambazi huko nyumbani kunachangiwa kwa kiasi kikubwa na wageni wanaoingiza nchini pasipo kufuata taratibu za uhamiaji.Ni ukweli usiopingika kuwa hali ya amani iliyopo Tanzania ni kivutio kizuri kwa “watu wa shari” kutoka nchi jirani.Unadhani hali itakuwaje pindi “washari” hao watakuwa wanaweza kuingia Tanzania kirahisi kama vile mtu anavyotoka Ilala kwenda Temeke hapo Muungano huo utakapokuwa umekamilika.Lakini hoja hiyo ya uhalifu ni ndogo tu ukilinganisha na ukweli kwamba tuna mambo yetu kadhaa ya muhimu tunayopaswa kuyashughulikia kwanza kabla ya kufikiria kujitanua.Na miongoni mwa mambo hayo muhimu ni suala la Muungano kati ya “Tanganyika” na Zanzibar.Halafu kuna hii “lulu” yetu ya amani na utulivu.Najua kila mtu ana tafsiri yake ya neno “amani na utulivu” lakini naamini sote tunakubaliana kuwa hatuwezi kulinganisha nchi yetu na mbinde za Wahutu na Watutsi huko Rwanda na Burundi au tatizo la ukabila huko Kenya (bila kusahau Mungiki).Na yayumkinika kusema kuwa “uwekezaji” wa wenzetu hapo nyumbani ni mkubwa zaidi ya wetu huko kwao.Mazingira yaliyoiua jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki bado yapo,na ni vema yakarekebishwa kabla ya kufikiria wazo la Muungano mpya.

Alamsiki






13 Jul 2007

Asalam aleykum,

Baada ya matukio ya hivi karibuni yaliyotuweka matumbo moto kufuatiwa mahayawani flani kuamua kuendesha kampeni yao ya kishetani ya kutaka kulipua mabomu huko London na hapo Glasgow (Waskotishi bado hawaamini kuwa ugaidi umeingia kwenye ardhi yao) sio wazo baya kuanza makala hii kwa habari “nyepesi nyepesi.” Gazeti la Daily Mail la hapa liliripoti hivi karibuni kuhusu matokeo ya utafiti yaliyoonyesha kuwa wanaume wenye aibu wana nafasi kubwa ya kupata magonjwa ya moyo kuliko wale wasio na aibu!Hizi tafiti nyingine…we acha tu.Kwa mujibu wa gazeti hilo,utafiti huo ulifanyika kwa kipindi cha miaka 30 uliwahusisha maelfu ya wanaume ambapo watafiti kutoka chuo kikuu cha Northwestern cha Chicago,Marekani walipokuwa wanafanya ufuatiliaji wa wawaliowahoji kwenye utafiti huo walibaini kuwa asilimia 60 kati yao (waliohojiwa) walikuwa wameshafariki,huku chanzo kikuu cha vifo kikiwa “heart attack” (nadhani kwa Kiswahili sahihi ni msongo wa moyo).Mambo hayo!

Na ukisikia duniani kuna mambo usidhani ni utani.Mzembe mmoja amekamatwa huko New Hampshire (Manchester) baada ya kushindikana kwa jaribio lake la kutaka kufanya uporaji benki huku akiwa amejivika matawi ya miti kama “camouflage” (kificho) yake.Jamaa huyo,James Coldwell,aliingia kwenye tawi la benki ya ushirika ya Citizens,huku akiwa amejivika majani na kuwatisha wahudumu wa benki hiyo kabla ya kufanikiwa kuondoka na kitita cha fedha,lakini alinaswa na polisi muda mfupi baadaye kwani triki yake ya “uninja wa majani” haikumsaidia kwa vile majani hayo hayakufunika sura yake,na wanausalama waliweza kuitambua vizuri kwenye CCTV.

Jumuiya ya Ulaya (EU) nayo ilijikuta kwenye wakati mgumu hivi karibuni baada ya kutoa filamu fupi kwa ajili ya promosheni ya kuhamasisha Jumuiya hiyo ambapo wahusika kwenye filamu hiyo ya sekunde 44 yenye jina “Let’s Come Together” walikuwa wakifanya “ngono nyepesi” (soft porn).Wapinzani wa wazo la Muungano wa nchi za Ulaya waliishambulia EU kwa kupoteza fedha za walipa kodi kwa kutengeneza filamu hiyo waliyoiona kuwa ni mwendelezo wa ubabaishaji wa Jumuiya hiyo.Nilipomtumia rafiki yangu flani habari hiyo kutoka gazetini alitania kwa kusema labda na sie tunahitaji “kampeni chafu” kama hiyo ya EU “kuuza” wazo la Muungano wa Afrika Mashariki ambao unaelekea kuwakera wadau wengi.

Nae mwanamama Amy Beth Ballamura amaepigwa marufuku kutia mguu kwenye pwani yoyote ya Uingereza baada ya kufanya majaribio zaidi ya 50 ya kujiua kwa kurusha baharini.Miongoni mwa sababu zilizopelekea kuchukuliwa kwa hatua ya kumdibiti mwanamama huyo ni pamoja na kuzitia huduma ya uokoji (emergency services) gharama ya zaidi ya pauni milioni 1 (zaidi ya shilingi bilioni mbili za huko nyumbani) kila wanapoitwa kwenda kumuokoa.Lakini pamoja na “tamaa” yake ya kujitoa roho,askari mmoja aliambulia tuzo ya ushujaa mwaka 2003 baada ya kusikia kelele za kuomba msaada kutoka baharini na kuamua kujitosa majini kufuata kelele hizo,ambapo alifanikiwa kumuokoa mwanamama huyo mwenye umri wa miaka 44.Cha kushangaza ni kwamba kama kweli alikuwa na nia ya kujitoa uhai sasa hizo kelele za kuomba msaada zilikuwa za nini?

Enewei,baada ya "nyepesi nyepesi" hizo (zote ni habari za kweli na wala sio kuwa “nawapiga fiksi” wasomaji wangu wapendwa) sasa tuangalie mambo ya muhimu zaidi huko nyumbani.Kwanza niseme siafikiani na hoja za Waziri wa Sheria Mama Nagu kwamba Bunge halipaswi kufanya kazi ya kupitia mikataba kabla ya kutiwa saini ili libaki na uhalali wake wa kuiwajibisha Serikali kwa mujibu wa dhamana ya mgawanyo wa mamlaka, kuchunguzana na kuwajibishana.Siafikiani naye kwa sababu hoja za baadhi ya wabunge kuwa mikataba hiyo ifikishwe kwao kabla ya kusainiwa zilizingatia ukweli kwamba kuna mapungufu makubwa yanayoendelea katika suala zima la kusaini mikataba mbalimbali.Mantiki nyepesi (simple logic) inaweza kutueleza kwamba maslahi ya nchi ni muhimu zaidi ya huo mgawanyiko wa madaraka.Hivi kwa mfano wazo la mikataba kuletwa bungeni lingekubaliwa,halafu nchi inufaike kwa kuingia mikataba yenye maslahi kwa Taifa,tatizo linakuwa wapi?Hivi kipi bora,kulinda mgawanyiko wa madaraka huku mikataba ya ajabu ajabu ikiendelea kuwepo au “kupindisha sheria” kwa kuileta mikataba hiyo bungeni kabla haijasainiwa halafu nchi ikanufaika nayo?

Pia nimesoma kwenye gazeti moja la huko nyumbani kwamba lile tishio la wafugaji huko wilayani Kilombero limerejea tena.Nitamke bayana kuwa hili linanihusu binafsi kwa vile mie ni “mwana wa pakaya” naetokea mitaa ya huko.Hawa wafugaji ni wakorofi,watovu wa nidhamu na wavunja sheria wakubwa.Maagizo kadhaa yameshatolewa kuwataka waheshimu sheria za nchi lakini wameamua kuweka pamba masikio.Mamlaka husika zinapaswa kuliangalia suala hili kwa makini zaidi kwani wanachofanya wafugaji hao sio tu kinahatarisha amani (mifugo yao inakula mazao ya wakulima,na hilo pekee linatosha kuzusha ugomvi) lakini pia hawawatakii mema wakulima kwani kwa kuswaga mifugo yao kwenye mashamba wanamaanisha kuwa wanataka wakulima hao wakose chakula na hela wanazojipatia kwa kuuza akiba ya mavuno yao.Hili ni bomu la wakati (time bomb) kwani japo hakuna bondia wa Kindamba (kama yupo basi samahani kwani sijamsikia) lakini hiyo haimaanishi kuwa mtu atakaeswaga mifugo yake kwenye mashamba ataachwa afanye anavyotaka.Hapo itakuwa kuchukua sheria mkononi,na japo mie ni mpinzani mkubwa wa kuchukua sheria mkononi,natambua dhahiri kuwa mtu “anapoletewa za kuleta” anaweza kabisa kuiweka sheria kando,hususan pale haki yake inapopuuzwa kwa makusudi.Kwa vile mkoa wa Morogoro umebahatika kuwa na RC ambaye ni “mjeshi” mstaafu basi hapana shaka Brigedia Jenerali Kalembo huyo atatumia “mbinu za medani” kuwadhibiti wafugaji hao wenye uhaba wa nidhamu.

Kikao cha Bunge kinaelekea ukingoni na miongoni mwa hoja nilizovutiwa nazo ni ile ya Mheshimiwa Shabiby (wa Gairo) kuhusu ujanja unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi makubwa ya abiria.Alieleza kuwa mengi ya mabasi yanayotumika sasa yamefanyiwa “usanii” kwa kuweka mabodi mapya kwenye “chasis” na injini za malori au za kale.Kuna jina moja tu linalowafaa “wasanii” hawa nalo ni “WAUAJI.” Wanathamini sana kukwepa gharama za kununua mabasi mapya lakini hawajali hata chembe madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na vitendo vyao vya “kuunda mabasi feki.” Kwa upande mwingine tuseme bila kuonekana aibu kwamba mabasi ya namna hiyo yanafahamika hata bila kuwa na ujuzi wa umakanika kwani ulifika pale stendi ya mabasi Ubungo unaweza kukutana na basi ambalo linaonekana dhahiri kuwa bodi yake “imepachikwa” sehemu isiyostahili.Trafiki yeyote aliyehitimu mafunzo yake vyema na mwenye uchungu na maisha ya Watanzania wenzie hawezi kuliruhusu basi “lililovimba mbavuni utadhani lina ujauzito” liendelee na safari,na mabasi ya namna hiyo yako mengi tu.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kuwa wanavunja sheria na kuhatarisha maisha ya abiria wao lakini hawajali kwa vile hakuna aliyechukuliwa sheria hadi leo.Si ajabu tukisikia kuwa baadhi ya mabasi hayo yanatumia injini za matrekta au hata za mashine za kusaga….(nashindwa kumalizia,nimekabwa na kicheko japo jambo hili sio la kuchekesha hata chembe.)

Mwisho,wakati Gavana wetu keshatamka bayana kuwa hatojiuzulu (utadhani alijichagua mwenyewe kwenye posti hiyo),sie wapenzi wa Simba tunajipoza kwa kusherehekea ubingwa wetu ambao kidogo umetibuliwa na hizi habari za viongozi kugombea mapato ya mechi huko Morogoro.Wito kwa watani wetu wa jadi Yanga ni huu:Micho akirudi (kama kweli atarudi) ashauriwe kukutana na Twalib Hilal apewe darasa kuwa ukocha sio sawa na ukatibu mwenezi wa klabu: ukocha ni vitendo vingi maneno machache lakini Mserbia Micho kila siku “anachonga” kuhusu hili au lile lakini matunda ya kazi yake kwenye dimba ni haba.Enewei,asilaumiwe sana kwani alishawahi kusema kuwa wachezaji wake hawafundishiki,na katika mechi ya juzi anaweza kuongeza sababu kuwa “lile tumbo la kuendesha” limechangia kukosa ushindi.

Alamsiki






18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Leo tuzungumize michezo,hususan soka.Kwa takriban wiki nzima sasa habari ya soka iliyotawala katika vyombo vya habari vya hapa Uingereza ni kuhusu suala la mchezaji mahiri wa klabu ya Manchester United na timu ya Taifa,Wayne Rooney.Ishu yenyewe ni kwamba ilidaiwa kuwa Rooney alikuwa na madeni yanayofikia pauni 700,000 (takribani shilingi milioni 140 za huko nyumbani) aliyokuwa akidaiwa na makampuni ya kamari (betting).Inasemekana tayari amemalizana na wadai wake.Wapo waliomlaumu mchezaji huyo kwa kutumia vibaya fedha zake,lakini wengine wamemtetea kwamba haikuwa ubaya kutumia kipato chake kinachotokana na ajira yake.

Ndio,soka huku Ughaibuni na hata katika baadhi ya nchi za huko Afrika ni ajira.Ni ajira ambayo inamwezesha mtu kama Rooney kutumbukiza zaidi ya shilingi milioni 100 kwenye kamari.Pointi yangu sio uhusiano wa soka na kamari bali soka kama ajira.Tukirudi huko nyumbani,siku chache zilizopita klabu kongwe za Simba na Yanga zilichimba mkwara kuwa zingesusia ligi kuu ya Bara iwapo mgao wa mapato ungeendelea kuwanufaisha zaidi wengine badala ya wao wanaovuja jasho dakika 90.Binafsi niliguswa sana na hoja za klabu hizo japokuwa kwa bahati mbaya nasikia wakongwe hao wamenywea katika kutimiza azma yao ya kutaka “kieleweke.”Sijui kuufyata huko ni kwa vile viongozi wa klabu hizo walitoa hoja hiyo kama kutingisha kiberiti,au sijui ni ubabe wa vyama vyetu vya michezo huko nyumbani!Lakini naamini klabu hizo zilikuwa na hoja ya msingi kabisa.

Pambano lao la mwisho liliingiza milioni 98 kama sijakosea.Lakini kila klabu ikaambulia shilingi milioni 23.6 tu.Kwa kweli huo ni sawa na uonevu.Mapato hayo yalitokana na umaarufu wa klabu hizo,hivyo zenyewe ndio zilipaswa kunufaika zaidi na mapato hayo.Nadhani klabu hizo zilistahili kupata kiwango kikubwa zaidi ya hicho hasa ikizingatiwa kuwa timu hizo kwa sasa ni kama za kulipwa kutokana na kuwa na wachezaji kadhaa wa kigeni ambao mishahara yao ni ya juu.Jitihada za kuzigeuza klabu hizo kuwa kampuni zimekuwa zikikwama mara kwa mara.Kwa hiyo tofauti na klabu kubwa za huku Ughaibuni ambazo zinaendeshwa kwa mfumo wa kampuni hivyo kutotegemea sana mapato ya uwanjani,chanzo kikuu cha mapato kwa vilabu vyetu vya nyumbani ni mapato yanayotokana na watu wanaoingia uwanjani kushuhudia mechi zao.

Imenisikitisha sana kuona hoja ya klabu hizo imekufa kienyeji.Lakini sikushangaa sana kwa vile sio siri kwamba vilabu vyetu huko nyumbani vinaendeshwa kwa ubabaishaji sana.Kwanza kwa Simba na Yanga hawapaswi kutegemea mapato ya uwanjani kama chanzo pekee cha mapato.Japo hoja ya klabu hizo kugeuzwa kuwa kampuni bado ni ya muhimu sana ingawaje wenyewe wanapuuzia,vipo vyanzo vingine kadhaa vya mapato ambavyo vimetelekezwa.Kwa mfano,kwa kutengeneza kalenda 100,000 zenye picha za wachezaji ambazo zingekuwa katika ubora unaostahili na kuziuza angalau kwa shilingi 500 kila moja,klabu ingejiingizia shilingi milioni 50.Hilo linawezekana kabisa hasa kwa vile gharama za utengenezaji wa kalenda sio kubwa sana na kuna uwezekano wa kupatikana wadhamini wa kugharamia mradi wa aina hiyo.
Kwa mtizamo wangu,watu wanaopaswa kubeba lawama zaidi katika suala zima la ubabaishaji kwenye vilabu vyetu ni hao wanaoitwa wanachama.Hao ndio wanaochagua viongozi wabovu,na ni haohao ambao hawakawii kwenda mahakamani kupinga uongozi ambao wao wenyewe waliuweka madarakani.Wanang’ang’ania kujiita wanachama wakati mchango wao mkubwa katika kuendesha klabu hizo ni kwenda kwenye vyombo vya habari kutaka uongozi wa klabu ujiuzulu,au kocha hafai au wakati mwingine kusema lolote tu ili wasikike hewani.Kama kweli wanachama wa Simba na Yanga wangekuwa wenye mwamko unaostahili basi naamini wangetumia nguvu za wingi wao kuhakikisha hoja zilizotolewa na viongozi wao kuetetea maslahi ya klabu hizo zinashinda.Badala ya hoja hizo kuonekana ni ajenda binafsi za Wambura au Kifukwe zingekuwa ni hoja za klabu na wanachama wa Simba na Yanga.

Kulalamika bila kutoa ufumbuzi wa tatizo ni sawa na kulikuza tatizo.Kwa hiyo,nawajibika kutoa mchango wangu katika kupata ufumbuzi.Nadhani Tenga na wenzie wa TFF wanapaswa kuliangalia upya suala la mgao wa mapato kwa klabu,na sio kwa Simba na Yanga pekee bali vilabu vyote.Vilabu vina haki ya kudai ziada ya wanachokipata kutokana na jitihada zo uwanjani.Kuhusu uendeshaji wa vilabu,Serikali inapaswa kuingilia kati kwa kutengeneza sera ambayo haitotota fursa ya uababishaji,iwe wa viongozi au wanachama.

Alamsiki.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.