17 Sept 2009


HIZI SIO HARAKATI ZA SIASA BALI NI UTOTO.NA UTOTO HUU UNAENDELEA KWA VILE CHAMA TAWALA KINA IMANI YA KUTOSHA KUWA WANAOCHEZEWA SHERE (WAPIGA KURA) BADO WAKO USINGIZINI,NA KINACHOENDELEA (UTOTO HUO) NI SAWA NA NJOZI.

HEBU SOMA HII,KISHA TAFAKARI:

Makamba amfuata Spika Sitta Urambo, ampigia magoti

*ASEMA HANA UGOMVI NAYE, ASEMA ALIKUWA MLEZI WA NDOA ZA WANAYE

Na John Dotto, Tabora

KATIKA kile kilichoelezwa kwamba, ni kujisafisha mbele ya Spika wa Bunge, Samuel Sitta, CCM imesema ipo pamoja naye katika kutekeleza majukumu yake kama Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu Mkuu wa CCM, Yusufu Makamba; ikiwa ni siku chache baada ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kuondoa utata uliotokana na maazimio ya Halmashauri Kuu ya chama hicho ulioonyesha kuwa wabunge wanaopiga kelele dhidi ya ufisadi, wanakichafua chama na serikali yake.

Akizungumza na viongozi wa CCM wilaya ya Urambo kwenye mkutano wa ndani uliohudhuriwa na Spika Sitta, Makamba, alitumia muda mwingi kumsifia Sitta kwamba ni mtu muelewa, asiyetetereka na wala kuyumbishwa na mtu yeyote na kwamba anachokifanya ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya chama hicho.

Makamba aliwaambia wanaCCM hao kwamba, hana chuki na Sitta, kwani hata alipokuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alimkaribisha katika ndoa za wanawe na akapewa nafasi ya kuzungumza kama baba mlezi, heshima ambayo alisema hataisahau katika maisha yake.

Alisema wana CCM wanatakiwa kupuuza maneno ya watu wanaodai chama kina mgogoro na Spika, kwasababu hakuna kitu kama hicho na yote anayoyatekeleza kwenye Bunge ni kwa niaba ya chama chake.

Hata hivyo, baada ya kikao cha NEC, Makamba alikuwa mstari wa mbele kudai kuwa kikao kile kina uwezo wa kumuhoji mbunge yoyote hata Sitta kama anakwenda tofauti na chama.

Makamba alinukuliwa akisema NEC ni mama na akina Spika ni watoto hivyo ina mamlaka ya kuhoji mienendo yao.

Mara baada ya kikao cha NEC, Sitta alifanya ziara mkoani Tabora na kulalamika kwamba, CCM makao makuu wamewakataza viongozi wa chama hicho mkoani kumpokea.

Hatua ya Makamba kwenda Urambo kuhutubia na Sitta, inatafsiriwa kama njia ya kuweka mambo sawa na kufuta makovu ya huko nyuma baina yake na Spika.

Kwa upande wake, Sitta alimshukuru Makamba kwa kutembelea jimboni kwake na mkoa wa Tabora kwa ujumla.

Katika mkutano wa hadhara uliofanyika baada ya kikao cha ndani kumalizika, Makamba aliwahakikishia wananchi wa Urambo kwamba CCM kipo pamoja na mbunge wao Sitta, ndiyo maana wanatekeleza ahadi zote ikiwemo ujenzi wa barabara ya Urambo Kaliua mpaka Tabora Mjini.

Akizungumzia suala la ufisadi, Makamba alisema kuwa wanaCCM wote kuanzia ngazi ya matawi wanapaswa kuungana na wabunge wanaopiga vita ufisadi, kwani vita dhidi ya rushwa ni ya wanaCCM wote.

Alisema anakerwa na watu wanaosema CCM ni chama cha mafisadi kwani ufisadi wa mtu mmoja si wa CCM na akatoa mfano kuwa dhambi ya Mkatoliki mmoja si dhambi ya Askofu Kilaini wala kanisa lote.

Makamba alimaliza ziara yake jana mkoani Tabora na juzi alipokuwa akizungumza na viongozi wa CCM wakiwemo makatibu wote wa wilaya za Tabora kwenye ukumbi wa mikutano wa CCM mkoa, aliwalaumu viongozi hao kukaa kimya wakati wapinzani wanakishambulia chama hicho kwa kukipakazia maneno machafu.

Aliwataka waamke na kukipigania chama na kuacha kukaa kimya na kusubiri makao makuu ama Makamba kujibu mashambulizi.

Baada ya kikao cha Nec kilichofanyika Dodoma mwezi uliopita, Makamba na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chilligati kwa nyakati tofauti walisema CCM imeunda kamati ya watu watatu, inayoongozwa na Rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi kuwachunguza wabunge wenye tabia ya kuishambulia serikali nje ya vikao vya chama.

Habari za ndani ya kikao hicho ambazo baadaye zilivuja kwa vyombo vya habari, zilieleza kuwa Nec ilimweka kitimoto Spika Sitta kwa madai kuwa anaruhusu mijadala inayokichafua chama na serikali, huku baadhi ya wajumbe wakishinikiza anyang'anywe kadi ya CCM kwa madai kuwa anawapa uhuru bungeni watu wanaoishambulia serikali kwa ufisadi.

Hata hivyo, mwanzoni mwa wiki hii baada ya hotuba ya Rais, Chilligati alisema chama hicho hakina ugomvi wala uadui na wabunge wake wanaoongoza vita dhidi ya mafisadi nchini.

Kabla ya hapo, Mwenyekiti wa Mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita ambaye alisemekana kumwandama Spika Sitta katika kikao cha NEC na akamwita faru aliyejeruhiwa anayetakiwa kumalizwa kabla hajasababisha madhara zaidi, naye alibadili msimamo na kuwaunga mkono wapiganaji wa ufisadi pamoja na Spika Sitta kwamba, wanatekeleza ilani ya CCM, hivyo wanastahili kuungwa mkono.

Mabadiliko haya ya siasa ndani ya chama hiki tawala na mfululizo wa matukio ya aina hiyo likiwemo la Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, John Mwakipesile ambaye amekaririwa katika vyombo vya habari akisema hana ugomvi na Mbunge wa Kyela, Dk Harrison Mwakyembe, anayesemekana kuwa ni hasimu wake kisiasa.

CHANZO: Mwananchi


NA HAWA NDIO TUNAOTARAJIA WAREJEE KUTUTAWALA 2010!

1 comment:

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.