12 Oct 2012



Watanidharau, watanicheka, watapambana lakini nitashinda

JOHNSON Mbwambo ameandika katika Gazeti la Raia Mwema la Oktoba 3, mwaka huu, kuhusu dhihaka za Zitto kwa Prof. Muhongo (Waziri wa Nishati na Madini). Nimesoma na nimemuelewa. Kwanza naomba radhi iwapo tafsiri ya taarifa yangu niliyoitoa kwa vyombo vya habari na kuwekwa kwenye blogu yangu (zittokabwe.com) ilikuwa ina dhihaka.
Nimefundishwa kutodhihaki watu na hasa watu wanaonizidi umri na siasa zangu sio za dhihaka bali za masuala (issues). Kupitia kwa ndugu Mbwambo naomba radhi kwa wote walioona kuna dhihaka katika andiko langu. Sikuwa na nia ya kumdhihaki Waziri Muhongo. Nia yangu ni kuonyesha kuwa Waziri Muhongo alichokifanya ni kuwacheza shere Watanzania, kwa kuwaambia maneno ambayo yeye mwenyewe alikuwa anaamini kuwa hayawezekani.
Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara yake, Eliakim Maswi, ilithibitisha kauli yangu siku chache tu baada ya kuitoa. Mbwambo kaandika makala yake kana kwamba hapakuwa na kauli ya kufuta maneno ya Waziri. Ninaamini Mbwambo aliiona kauli ile lakini aliamua kupuuza ili kujifurahisha na imani yake kwa Prof. Muhongo na mawaziri aliowataja kwenye makala yake kwamba ni mawakala wa mabadiliko. Mbwambo anaamini kabisa kwamba ndani ya utawala wa CCM, kuna mawaziri wenye nia ya dhati ya kuleta mabadiliko.
Nieleze wazi kwamba nilishtuka sana kuona toleo moja la Gazeti la Raia Mwema likiwa na makala tatu, zote dhidi ya Zitto Kabwe. Wakati makala ya ndugu Mbwambo ilikuwa inahusu suala nyeti sana la rasilimali za taifa na ni makala nzuri yenye mafundisho, makala mbili nyingine zilikuwa ni za siasa dhidi ya Zitto. Mwandishi Mayage Mayage aliandika makala yenye kichwa cha habari “Zitto, Urais 2015 kwa chama gani?” na Mwanasafu wa gazeti hili la Raia Mwema, Evarist Chahali aliandika makala yenye kichwa cha habari “Rais Kikwete anapofikiri kama Kabwe Zitto.”
Namwambia Mayage akasome vizuri historia ya ujenzi wa CHADEMA. Yeye anadhani CHADEMA imeanza mwaka 2010. CHADEMA kimejengwa na watu, si mtu mmoja. Wanaoamua mgombea wa chama si watu wachache anaowadhani yeye Mayage bali ni wanachama wa CHADEMA kutoka sehemu mbalimbali za Tanzania, ikiwamo Munanila, mkoani Kigoma anapotoka Mayage.
Huyu Chahali anasema ananijua sana. Inawezekana ananijua kuliko mimi ninavyojijua. Lakini mimi simjui na wala sijawahi kumwona ana kwa ana, nimekuwa nikimwona tu kwenye mitandao ya kijamii akinizushia, kunitukana na kunisema. Sikushangaa kusoma makala yake ya wiki iliyopita. Wote wawili nawakumbusha msemo wa Mahatma Gandhi aliposema; “Kwanza wanakudharau, kisha wanakucheka, kisha wanapambana na wewe, kisha unashinda".
Sasa nirejee kwenye makala ya ndugu Mbwambo. Prof. Muhongo simjui, licha ya kwamba nimekuwa mmoja wa wabunge walioko mstari wa mbele kuhakikisha utajiri wa nchi unatumika kwa manufaa ya nchi, sikuwahi kumsikia Prof. Muhongo mpaka alipoteuliwa kuwa Waziri wa Nishati na Madini.
Sikuwahi kusikia akipaza sauti yake dhidi ya mikataba mibovu ya madini licha ya kwamba yeye ni msomi aliyebobea katika masuala ya miamba. Wakati Bunge la tisa, chini ya Spika Samuel Sitta, likiwa limecharuka kutaka mikataba mibovu ipitiwe na kubadilishwa tulitarajia sana kupata ushauri wa wataalamu wetu lakini hawakuonekana, "walikwina"?
Walikuwa waoga kusema maana wangeharibu uhusiano kati yao na watawala. Tulihangaika wenyewe bila maarifa yoyote kuhusu sekta ya madini. Wengine ilibidi kuacha kazi za ubunge na kwenda masomoni ili kuongeza ujuzi wa masuala ya kisheria na kiuchumi kuhusu sekta ya rasilimali (madini na mafuta).
Wasomi wetu hawakuwa nasi. Walichague kuendelea kufanya kazi za ushauri kwa kampuni za utafutaji madini nchini. Leo Mbwambo anawaona hawa ndiyo mawakala wa mabadiliko. Labda anasema kweli. Ila mimi nimekata tamaa na mabadiliko kuletwa na watu waliomo serikalini, kwa sababu kadhaa.
Moja, kama alivyosema ndugu Mbwambo, nilipigia kelele sana mkataba wa Buzwagi na mikataba mingine ya madini. Niliendelea kupiga kelele mpaka sheria mpya ya madini ilipopitishwa na Bunge. Nimuulize Mbwambo kwamba, licha ya sheria mpya kuandikwa imechukua miaka mingapi kampuni za madini kufanya kazi zao kwa kutumia sheria hiyo mpya? Je, mikataba mingapi iliyopitiwa imerekebishwa au hata kuvunjwa? Pengine niwasaidie kuwakumbusha taarifa kwamba, hakuna kilichofanyika kwa mujibu wa sheria mpya, licha ya kufuatilia kwa kina bungeni kupitia michango na hata maswali bungeni sambamba na makala mbalimbali.
Tangu Waziri Prof. Muhongo na timu yake waingie ofisini ni maneno tu tunayosikia bila matendo. Hata suala la mgawo wa umeme ambalo ndugu Mbwambo analisema kama mfano, yeye anajua namna ambavyo wananchi wanalalamikia umeme kukatika hovyo, tena bila taarifa wala maelezo. Muhongo alifanikiwa sana kuaminisha watu wenye mawazo huru kama Mbwambo wakamwona yupo sahihi kiasi hata cha kufumbia macho mgawo wa umeme usio na maelezo, unaoendelea nchini.
Siwaamini mawaziri kwa sababu wanasema lolote linalowajia midomoni mwao hata kama wanaamini kuwa wanalosema haliwezekani kutekelezwa. Waziri wa Nishati na Madini alisema kuhusu mikataba ya mafuta na gesi ili kufurahisha watu. Huo ni msingi wa kwanza wa kauli yangu ambayo ndugu yangu Mbwambo ameitafsiri kuwa ni dhihaka. Nilikuwa nasema ukweli mchungu kwamba, serikali haiwezi kufanya lolote kuhusu mikataba. Nilitoa changamoto kuwa kama serikali kweli imedhamiria, iweke mikataba hii wazi. Je, wameiweka wazi?
Pili, Waziri wa Nishati na Madini anataka umma umwone kwamba anajua sana masuala ya sekta kuliko Mtanzania mwingine yeyote. Nitatoa mfano mmoja unaonihusu moja kwa moja. Katika mkutano wa Bunge uliopita, Tanzania ilitembelewa na Waziri Mkuu mstaafu wa Urusi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Kirusi iliyonunua leseni ya kutafuta uranium kule Selous. Kampuni ya UraniumOne iliyonunua leseni hii ya Mkuju River Project kutoka Kampuni ya Mantra ya Australia, kwa dola za Marekani milioni 980.
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilitaka ilipwe kodi ya ongezeko la mtaji (capital gains tax) kampuni hii ilikataa. TRA wakaenda mahakamani kudai malipo ya kodi yenye thamani ya dola za Marekani milioni 116 ambazo ni sawa na asilimia 20 ya thamani ya mauzo na kesi inaendelea. Kwa mujibu wa sheria zetu kampuni zinapouziana leseni, lazima Waziri wa Nishati na Madini atoe idhini ya mauzo hayo. Mgeni huyo kutoka Urusi alikuja nchini kupigia debe idhini hii, ili itolewe leseni maalumu ya uchimbaji (special mining licence).
Nikasimama kutoa taarifa bungeni kwamba mawaziri wanakutana na huyu Waziri Mkuu mstaafu wa Urusi kuhusu leseni ya Mkuju River Project na kuweka wazi kwamba Kampuni ya UraniumOne hawajalipa kodi ya capital gains. Nilisimama kutoa taarifa baada ya majibu ya Waziri Muhongo kwamba, kilichouzwa si kampuni ya Tanzania bali Australia na hivyo hakuna kodi.
Kwa makusudi kabisa niliacha habari ya kesi ya TRA dhidi ya kampuni hii ili kuona umakini wa mawaziri wetu wapya kabla ya kukutana na lobbyists (washawishi) wa kampuni hizi za madini. Waziri Muhongo aliposimamishwa na Naibu Spika, Job Ndugai, akasema “Sisi tunajua zaidi kuliko Zitto" Kwanza Waziri hakuwa anajua.
Ni makosa kabisa kujadili suala ambalo mamlaka mojawapo ya nchi wamelipeleka mahakamani na linasubiri uamuzi. Lakini suala la Waziri kutokuwa na taarifa lilidhibitishwa na ujio wa Naibu Waziri George Simbachawene, aliponifuata na kuomba "details" kuhusu taarifa niliyotoa. Kulikuwa na haja gani kwa Waziri kusema bungeni yeye anajua zaidi na baadaye kumtuma Naibu wake kutafuta taarifa?
Huu ni udhaifu mkubwa sana wa uongozi. Kutojua si makosa, inawezekana kuwa wengine hatukusomea miamba lakini tumesomea masuala ya kodi kwenye madini na mafuta. Waziri makini anayejali nchi yake anawezaje kukutana na mwekezaji anayekataa kukulipa kodi yako bila wewe hata kuulizia utalipwa lini?
Unaulizwa bungeni unasema "ninajua zaidi" na Mwandishi mahiri kama Mbwambo anasema "mpeni nafasi atende"!
Nilipomsikia Waziri anasema ameagiza TPDC (Shirika la Maendeleo la Mafuta) kupitia mikataba nikajua na hili nalo hajui. Amesema tu ili watu wafurahi kwamba mikataba inapitiwa. Kupitia mikataba bila kuchukua hatua dhidi ya mikataba mibovu ni nini kama sio kutafuta umaarufu tu? Unapitia mikataba ili iwe nini kama huwezi kuchukua hatua?
Kuna mikataba ambayo imeingiwa kwa rushwa, sheria zetu zinasema kuwa mikataba iliyoingiwa kwa rushwa ni sawa na haipo. Hata sheria za kimataifa za mikataba zinatambua hivyo. Waziri anaposema kuwa tunapitia mikataba ili kuhakikisha kuwa mikataba ijayo inakuwa mizuri ni kichekesho. Hivi tunajua vitalu vingapi vimegawiwa na vingapi vimebaki? Hivi sasa kuna mikataba 29 na leseni 26. Vitalu vilivyobaki hivi sasa ni tisa tu.
Wizara inatuambia tunaangalia hii mikataba 29 ili kuboresha 9. Haya si mapitio bali ni kuangalia tu kama nilivyosema katika sentensi iliyotangulia. Mapitio bora zaidi ni uwazi wa mikataba yote tuliyoingia mpaka sasa na kuzuia kabisa mikataba mipya wala kugawa vitalu vipya vya kutafuta mafuta na gesi.
Uporaji wa rasilimali ni wa namna mbili, moja ni watu wachache na kampuni zao kupora kwa kupitia mikataba mibovu na pili ni kizazi kimoja kunyonya rasilimali zote bila kujali kizazi kijacho. Katika maandiko yangu nimeshauri kuwa tusigawe vitalu vipya mpaka tuone mafanikio ya mikataba hii 29 na leseni 26 tulizonazo hivi sasa. Wito wangu ni mmoja tu, uwazi wa mikataba. Kutaka uwazi si dhihaka. Uwazi ni uwajibikaji.
Suala la mapitio ya mikataba kwa jicho la juu juu ni suala la kuunga mkono. Lakini ukitazama historia ya nchi yetu katika masuala haya utabaini kwamba tunapaswa kufanya zaidi ya mapitio ya mikataba.
Tunapaswa kufanya jambo ambalo hatujawahi kulifanya nalo ni kuiweka wazi mikataba hii kwa umma. Hii ndiyo hoja yangu.
Inawezekana kabisa kwamba maneno niliyotumia yameudhi watu fulani lakini ikumbukwe mimi ni Mbunge wa Upinzani na ni wajibu wangu kukosoa serikali kila inapowezekana. Bahati nzuri miaka yangu saba bungeni hivi sasa imetumika kwa kiasi kikubwa sana katika kufuatilia kwa karibu sekta ya madini, mafuta na gesi. Ni rahisi sana mimi kuweza kuona suala linalosemwa na serikali linasemwa tu au serikali inamaanisha? Katika suala la mapitio ya mikataba kwenye sekta ya madini na mafuta kwa kweli serikali haipo makini. Watu wajuvi wa mambo kama kina Mbwambo wanapaswa kwenda zaidi ya mapitio na kutaka mikataba iwekwe wazi na kuchambuliwa kwa uwazi kabisa.
Waziri Muhongo anayo nafasi ya kufanya kazi yake, afanye kazi yake bila bugudha. Mbwambo ajue kuwa Mbunge Zitto pia anayo kazi yake kwa mujibu wa Katiba ibara ya 63 nayo ni "kuisimamia" serikali. Niacheni nami nifanye kazi yangu.
Makala hii iliyoandikwa na Kabwe Zitto, Mbunge wa Kigoma Kaskazini ni majibu kwa makala iliyoandikwa na Mwanasafu wetu, Johnson Mbwambo, katika toleo lililopita la gazeti hili la Raia Mwema, kupitia safu yake ya Tafakuri Jadidi.
MAONI: NI KWELI ZITTO HANIJUI, NA KATIKA MAKALA HUSIKA NILIANDIKA "NAMJUA ZITTO VIZURI" NA SIO "TUNAJUANA VIZURI." NA KIMSINGI, HAKUPASWA KUNIJUA WAKATI NILIPOKUWA NAMJUA (KINYUME CHA HIVYO,JUKUMU ZIMA LA KUMJUA LISINGEKUWA NA MAANA). BY THE WAY, HIVI ZITTO ANAMJUA KILA MPIGA KURA KATIKAJIMBO LAKE, LET ALONE MIE AMBAYE SIKUMPIGIA KURA?

SIKUANDIKA KUWA NAMJUA ZITTO VIZURI KWA MINAJILI YA KUSAKA SIFA AU KUJIKOMBA KWAMBA "NINAMFAHAMU VIZURI RAIS MTARAJIWA" BALI NILIANDIKA HIVYO KUPIGIA MSTARI KUWA MWANASIASA NINAYEMZUNGUMZIA NI MTU NINAYEMFAHAMU (KIVIPI,WAPI...NAOMBA NISIZUNGUMZIE HILI KWA MUDA HUU).

SITAKI KUMWITA MHESHIMIWA ZITTO MBABAISHAJI LAKINI MAKALA YAKE HII INANISHAWISHI KUFIKIRIA HIVYO.ZITTO ANAZUNGUMZIA MIE KUMJUA, ANADAI NINAMTUKANA (HIVI RAIS MTARAJIWA HATAMBUA KUWA MTU AKIKUTUKANA KWENYE TWITTER UNAPASWA KUMRIPOTI KWA WAMILIKI WA MTANDAO HUO BADALA YA KULALAMIKA KWENYE MAKALA?).HUYU ANAYEDAI NINAMTUKANA NDIYE SAME PERSON ALIYEANDIKA HAYA  ni upumbavu kufikiri kwa misingi wa kidini. Huna haki kuleta ubaguzi wako wa kidini hapa. 3 out of 15 muslims, unaita ubaguzi? (chanzo: http://goo.gl/8MLDO

Mwanasiasa huyu mbabaishaji alinilaumu kwa "kuleta ubaguzi" lakini yeye si mbaguzi anapodai watu waliozaliwa kabla ya uhuru hawawezi kutuletea maendeleo ya kiuchumi.

NIMALIZIE KWA KUWAACHIA WASOMAJI FURSA YA KUAMUA WENYEWE IWAPO MHESHIMIWA ZITTO AMEJIBU HOJA (NINAZOZIONA) ZA MSINGI KATIKA MAKALA HII







0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.