Duru
za siasa za Uingereza zimevamiwa na mwanasiasa hatari lakini mahiri kwa
ushawishi, ndivyo wanavyoeleza baadhi ya wachambuzi wa siasa nchini hapa
kufuatia kuibuka kwa kasi kwa Nigel Farage na chama chake ‘cha kibaguzi’ cha
United Kingdom Independence Party (UKIP).
Pamoja
na kauli zake za kukera na pengine za ubaguzi wa waziwazi, Farage ana kipaji
muhimu kwa mwanasiasa: kutumia mapungufu
ya vyama vikuu – Conservatives, Labour na Liberal Democrats – kuwavuta wananchi
wakiunge mkono chama chake. Na anafanikiwa kwa kiasi kikubwa, hasa baada ya
chama hicho kushinda kiti cha ubunge katika uchaguzi mdogo wa jimbo la uchaguzi
la Clacton huko England.
Matokeo
hayo yamekipatia chama hicho mbunge wa kwanza, Douglas Carswell, ambaye alihama
kutoka Conservatives hivi karibuni. Taratibu duru za kisiasa nchini hapa
zinaanza kuiona UKIP kama chama makini licha ya sera zake zenye mwelekeo wa
ubaguzi.
Ajenda
kuu ya UKIP ni kuitaka Uingereza ijiondoe kwenye Umoja wa nchi za Ulaya
(European Union). Kadhalika, chama hicho kinapinga vikali ujio wa wageni nchini
hapa, huku kikidai kuwa serikali ya chama tawala (Conservatives)
inayoshirikiana na Liberal Democrats, imeshindwa kama ilivyokuwa kwa serikali
iliyotangulia ya Labour kutatua tatizo hilo.
Suala
la uhamiaji ni moja ya turufu muhimu kila unapojiri uchaguzi katika nchi hii,
na UKIP wanaitumia ajenda hiyo kwa ufanisi mkubwa. Hata hivyo, baadhi ya
wachambuzi wanatahadharisha kuwa Farage ni mtu hatari kwa sababu ya mrengo wake
mkali wa kulia ambao unakaribiana na ule wa chama cha wazi cha kibaguzi cha
British National Party. Baadhi ya wachambuzi wanaiona UKIP kama mchanganyiko wa
Conservatives na BNP, lakini wanatambua kuwa mvuto wake unachangiwa na kuongea
yale yanayowagusa wapiga kura wengi.
Laiti
UKIP ikiendelea kufanya vema, na dalili zipo za kutosha, kuna uwezekano wa chama
hicho kuweza kuunda serikali ya umoja na Conservatives baada ya uchaguzi mkuu
ujao. Laiti hilo likitokea, ni wazi kuwa Uingereza itakuwa taifa tofauti kwa
kiasi kikubwa na hilo tulilonalo hivi sasa.
Lengo
la makala hii sio kumzungumzia Farage au chama chake cha UKIP bali kuangalia
haja ya kuwa na ‘akina Nigel Farage wa siasa za Tanzania.’ Hapo simaanishi kuwa
na wanasiasa wenye sera za kibaguzi bali wenye kutambua matatizo yanayoikabili
Tanzania yetu na sio tu kuyatumia kupata sapoti bali kuyatafutia ufumbuzi. Kwa
sasa hatuna mwanasiasa wa aina hiyo.
Sijui
hadi muda huu ni Watanzania wangapi wanatambua kuwa tuna chini ya mwaka mmoja
kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu hapo mwakani. Sintofahamu ya Bunge la
Katiba na hatimaye kupatikana kwa Katiba pendekezwa kumewachanganya wananchi
vya kutosha. Na katika kukoroga mambo zaidi, yayumkinika kuhitimisha kuwa ni
Watanzania wachache tu wanaofahamu iwapo kutakuwa na kura ya maoni ya kupitisha
au kukataa Katiba pendekezwa. Tayari Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeshatamka kuwa
haiwezi kuharakisha kura hiyo, japo Rais Jakaya Kikwete ameendelea
kuwahakikishia Watanzania kuwa Katiba mpya itapatikana hivi karibuni.
Tupate
Katiba mpya au la, mwaka mmoja kutoka sasa tutamchagua mrithi wa Rais Kikwete,
awe ni kutoka CCM au chama kingine. Mazingira yalivyo hadi sasa hayatoi
mwelekeo wa nani anayeweza kushika wadhifa huo muhimu kwa Tanzania yetu.
Binafsi, ninaamini kuwa mrithi wa Kikwete atakuwa ‘mtu wake wa karibu,’ chaguo
lake ambalo kwa mbinu za wazi na zisizo wazi atapigiwa upatu hadi kushika
wadhifa huo.
Sababu
ya Kikwete kuuhitaji ‘mtu wake’ ipo wazi. Vipindi vyake viwili vya utawala
vimetawaliwa na mlolongo wa kashfa mbalimbali za ufisadi. Pasipo kuwa na mtu
‘wa kuaminika,’ si ajabu tukashuhudia yaliyomkumba Rais wa zamani za Zambia
Frederick Chiluba. Na hata kama haistahili kwa Rais aliye madarakani kumwandama
mrithi wake, mantiki ya kawaida tu inatosha kueleza kuwa hakuna mtu anayetaka
kustaafu huku hajui hatma yake itakuwa vipi. Moja ya kanuni isiyo rasmi ya
siasa ni hii: “kamwe usimkabidhi madaraka adui yako. Atakuangamiza hata kabla
hajaizowea ofisi uliyomkabidhi.” Ni wazi Kikwete analitambua hilo.
Mengi
yanaongelewa kuhusu ‘watu wa karibu na Kikwete’ lakini ni vigumu kujua ukweli.
Kama kuna mwanasiasa ambaye amefanikiwa sana kuonekana kama mrithi asiye rasmi
wa Kikwete ni Edward Lowassa. Lakini taarifa zinakanganya kuhusu mahusiano ya
wanasiasa hao ambao walikuwa marafiki wakubwa. Kuna wanaodai urafiki wao
umevurugika, lakini uzoefu wa kisiasa waonyeshe kuwa hakuna maadui (au
marafiki) wa kudumu katika siasa. Kwa vile Lowassa (Akishirikiana na mwanasiasa
mwingine Rostam Aziz) alimsaidia sana Kikwete kuingia madarakani, yawezekana
‘deni’ hilo likapelekea Kikwete kumsaidia Lowassa kuwa mrithi wake, hasa endapo
(Lowassa) atamhakikishia Kikwete ‘usalama wake’ baada ya kustaafu.
Kuna
wanaosema Bernard Membe, mwanasiasa mwingine aliye karibu na Kikwete ni
miongoni mwa wanaoweza kupewa nafasi hiyo. Nilishawahi kuongelea vikwazo dhidi
ya Membe lakini kwa vile ni vigumu kwa nchi ya Kiafrika kupata Rais kinyume na
matakwa ya Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi husika, na kwa vile Membe ni
shushushu mstaafu, basi hakuna lisilowezekana iwapo atapata sapoti ya kutosha
kutoka kwa ‘mashushushu wenzake.’
Lipo
suala la Zanzibar ambalo kwa akina sie tunaochimbachimba mambo tunaona ni kama
bomu la wakati (time bomb) linalosubiri kulipuka kuhusiana na hatma ya
Muungano. Sahau kuhusu Katiba pendekezwa, hatma ya Muungano itategemea uwezo wa
aliyepo madarakani kulazimisha matakwa ya watawala. Na kwa minajili hiyo, naona
uwezekano wa Dkt Ali Shein kupigiwa chapuo amrithi Kikwete. Na kwa vile Shein
amekuwa Makamu wa Rais wa Kikwete kwa miaka 10, si vigumu kumpatia ‘bosi wake
wa zamani’ uhakika wa ustaafu wake.
Kuhusu
Waziri Mkuu Mizengo Pinda, binafsi ninashindwa kuelewa malengo yake kuhusu
kuwania urais. Labda yawezekana ni kile kinachoitwa ‘Plan B’ yaani iwapo kila
‘mrithi mtarajiwa wa Kikwete’ akishindikana, basi Pinda anakuwa ‘mchezaji wa
akiba’ wa kuokoa jahazi. Katika mazingira ya kawaida, ni miujiza tu ndiyo
inayoweza kumwingiza Pinda Ikulu. Sababu ni nyingi, nitaziongelea katika makala
zijazo. Hata hivyo, kama alivyo Membe, Pinda ni shushushu mstaafu, na hilo
laweza kuwa turufu kwake.
Wakati
takriban yote niliyoyaongelea hapo juu ni ya kufikirika zaidi kwa maana
hayajiri waziwazi, mwanasiasa pekee ambaye tangu aitangaze nia yake ya kutaka
urais hapo mwakani ameendelea kuwaaminisha Watanzania kuwa yupo ‘serious’ ni
January Makamba. Ninaomba kukiri kwamba awali nilipomsikia January akitangaza
nia hiyo nilidhani anatania. Siku kadhaa baadaye, kwa kutumia mitandao ya
kijamii hasa Twitter, mwanasiasa huyo kijana amejitanabaisha kama mtu anayetaka
kwa dhati kuliongoza taifa hili.
Hivi
ninavyoandika makala hii, January ameanzisha utaratibu wa maswali na majibu
(question and answer session) huko Twitter kwa kutumia ‘hashtag’ #askJanuary
yaani ‘Muulize January.’ Japo ninatambua kuwa ni vigumu kuhitimisha ‘mafanikio’
ya mwanasiasa kwa kuangalia ‘anavyojichanganya na watu’ katika mtandao wa
kijamii, hasa kwa kuzingatia ukweli kwamba bado Watanzania wengi si watumiaji
wa mitandao ya jamii, January amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kujenga sio tu
kuaminika kuwa yupo ‘serious’ katika dhamira yake ya kutaka urais mwakani lakini
pia amejiweka karibu na watu wengi wanaotumia mitandao hiyo ya kijamii.
Sasa
kama Rais ajaye atatokana na kutambulika kwake kwa angalau baadhi ya wapiga kura,
basi hadi muda huu January anaongoza katika hilo- pasi haja ya kufanya opinion
poll. Alitangaza anataka urais, ameendelea kuwaaminisha wananchi kuwa anataka
urais, anaendelea kueleza atafanya nini akiwa Rais, na kwa sie tunaoamini kuwa
mitandao ya kijamii ni moja ya nyenzo muhimu kufikisha ujumbe kwa wananchi
(angalau huku nchi za Magharibi), basi lolote linawezekana kwa mwanasiasa huyo
kijana.
Nihitimishe
makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu wa wagombea urais ambapo
katika moja ya makala zijazo nitazungumzia ‘muungano wa UKAWA kumsimamisha
mgombea mmoja’ nikielemea zaidi kwenye vikwazo kutoka kwa ‘nguvu za giza’,
sambamba na kuwachambua wanasiasa wengine wanaotajwatajwa. Kwa mfano, kuna
anayedhani Ridhiwani Kikwete anaweza kuingia katika mbio za kurithi nafasi inayoshikiliwa
na baba yake hivi sasa?
Mwisho
kabisa, kama tahadhari, uchambuzi wangu unaelemea zaidi katika kile tunachoita’
hali halisi mtaani,’ kufuatilia matokeo kadri yanavyojiri, upepo wa kisiasa
unavyovuma, na ninajitahidi kuepuka kutumia uelewa wangu wa stadi za siasa au
taaluma nyinginezo kuniongoza katika uchambuzi huu. Kwa kifupi, ninaongozwa na hali halisi.
MUNGU
IBARIKI TANZANIA
0 comments:
Post a Comment