Makala hii imechapishwa katika jarida la Raia Mwema toleo la wiki hii lililotoka tarehe 25/11/2015, lakini kwa sababu nisizoelewa tovuti ya jarida hilo haijawa-updated kwa wiki kadhaa sasa. Kwa vile makala ninazotuma gazetini hufanyiwa uhariri kabla ya kuchapishwa, yawezekana makala iliyopo gazetini ikawa na tofauti kidogo na hii.
MAKALA YA RAIA MWEMA
TOLEO LA NOVEMBA 25, 2015
“Hotuba hii ya Rais Magufuli ni moja ya hotuba bora kabisa katika
historia ya siasa za Tanzania.” Hili lilikuwa hitimisho langu katika
mtandao wa kijamii wa Twitter mara
baada ya Rais John Magufuli kumaliza kulihutubia Bunge wiki iliyopita, huko
Dodoma.
Na kwa hakika watu
kadhaa waliafikiana na hitimisho hilo.
Kilichovutia wengi waliosikia hotuba hiyo, katika shughuli ya ufunguzi
wa Bunge la 11, sio tu mpangilio wa hotuba yenyewe bali pia jinsi kila
alilotamka lilivyoonyesha bayana kuwa lilitoka moyoni mwake kwa dhati kabisa.
Rais alianza hotuba yake
hiyo kwa kuorodhesha matatizo mbalimbali aliyobaini wakati wa kampeni zake
Urais ambapo alizunguka takriban Tanzania nzima. Alitoa uchambuzi wa kina wa
matatizo hayo kabla ya kuelezea kwa undani ni kwa jinsi gani serikali yake
itayashughulikia. Ilikuwa ni zaidi ya hotuba ya kisiasa, na pengine ingeweza
kabisa kuwa mhadhara wa kitaaluma uliofanyika katika lugha nyepesi na ya
kueleweka.
Moja ya vitu
vilivyonivutia sana katika hotuba hiyo ni jinsi Rais Magufuli alivyoweza kutupatia
jibu la swali ambalo kwa miaka kadhaa lilionekana kuwatatiza viongozi wetu
mbalimbali: “Kwanini Tanzania ni masikini
licha ya utajiri lukuki wa raslimali ilionao.” Alieleza bayana na kwa
kirefu jinsi ufisadi, rushwa na uhalifu vinavyochangia kukwamisha maendeleo ya
taifa letu. Kadhalika, alifafanua, kwa kutumia takwimu halisi, jinsi mabilioni
ya fedha yalivyotumika visivyo kwa matumizi yasiyo muhimu na yaliyo nje ya
uwezo wa taifa letu masikini.
Kwa hakika ilikuwa
hotuba ya kihistoria iliyofunika kabisa utovu wa nidhamu wa hali ya juu
ulioonyeshwa awali na wabunge wa upinzani ambao walitumia muda mwingi kabla ya
hotuba hiyo kuzomea na baadaye kuamiriwa
kutoka nje ya ukumbi huo.
Lakini kwa vile sio
rahisi kumridhisha kila mtu, baadhi ya wenzetu waliosikiliza hotuba hiyo walidai kuwa eti “haina tofauti na
hotuba nyingine kadhaa zilizokuwa nzuri kuzisikiliza lakini zikaishia kuwa
maneno matamu tu.” Wengine walikwenda mbali zaidi na kudai kuwa hata mtangulizi
wa Rais Magufuli, Rais Mstaafu Jakaya Kikwete naye pia alianza urais wake kwa
hotuba za kutia moyo kama hizo lakini mengi ya aliyoahidi, hususan lile la ‘Maisha
Bora kwa Kila Mtanzania,’ yaliishia kuwa ahadi tu.
Sikubaliani kabisa na
wakosoaji hao, japo hoja zao zinaweza kuwa na mantiki kidogo. Ni kweli kwamba
ukosefu wa hotuba za kuvutia si moja ya matatizo yanayoikabili nchi yetu. Wengi
wa wanasiasa na viongozi wetu ni mahiri sana wa maneno lakini tatizo huwa
katika kutafsiri maneno yao kuwa vitendo.
Wakosoaji hao hawapo
sahihi kwa sababu, kama nilivyoeleza awali, hotuba hiyo ilikuwa ya kutoka
moyoni.Ilikuwa hotuba ya kiongozi anayeguswa na yanayoisibu nchi yake, kiongozi
mwenye uelewa wa changamoto zinazoukabili uongozi wake, na mwenye dhamira
thabiti ya kukabiliana na changamoto hizo.
Kuna mbinu moja muhimu
ya kubaini iwapo mtu anaongea ukweli au anahadaa, nayo ni kumwangalia usoni.
Tangu kuanza kwa kampeni zake za urais na hadi wakati wa hotuba hiyo ya wiki
iliyopita, uso wa Rais Magufuli wakati anaongea unaonyesha bayana kuwa kila
neno linalotoka mdomoni mwake ni la dhati, linatoka moyoni na si sehemu ya
porojo tulilozowea kutoka kwa wengi wa wanasiasa na viongozi wetu. Mtaalam
yeyote wa kubaini ukweli na uongo hatoshindwa kuafikiana nami kuwa uthabiti wa
kauli za Magufuli upo wazi kwa yeyete anayemwangalia usoni wakati anaongea.
Lakini pia, hotuba hiyo
ilikuwa mwendelezo wa ishara nzuri zilizoanza kujitokeza siku moja tu tangu
Rais Magufuli aingie ofisini, ambapo alifanya ziara ya kushtukiza Wizara ya
Fedha, kabla ya kufanya ziara nyingine kama hiyo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Na siku ya uzinduzi wa Bunge, alitukumbusha enzi za (Waziri Mkuu wa zamani)
hayati Edward Sokoine, aliyesifika kwa uchungu wa mali za umma, baada ya
kuamuru zaidi ya shilingi milioni 200 zilizochangwa kwa ajili ya hafla ya
mchapalo ya sherehe za uzinduzi wa Bunge jipya zielekezwe kwenye ununuzi wa
vitanda katika hospitali ya Muhimbili, na kiasi kidogo tu kitumike kwa ajili ya
hafla hiyo.
Kimahesabu, chini ya
wiki tatu tangu aingie madarakani, Rais Magufuli ameshaokoa jumla ya shilingi
milioni 900 kutokana na hatua alizochukua dhidi ya matumizi yasiyo ya lazima.
Kwa kasi hii, tuna kila sababu ya kutarajiwa kuiona nchi yetu ikipaa kiuchumi,
na hatimaye Watanzania kunufaika na neema lukuki ambayo nchi yetu imejaaliwa
kuwa nayo.
Sina shaka kuhusu
uwezekano wa mafanikio ya hatua za Rais Magufuli huko serikalini. Licha ya kuwa
na Waziri Mkuu mchapakazi mzoefu, Majaliwa Kassim Majaliwa, kuna kila dalili
kuwa baraza la mawaziri ambalo hadi wakati ninaandaa makala hii lilikuwa
halijatangazwa, litasheheni wachapakazi kama yeye. Kwahiyo, kazi ya kurejesha
nidhamu serikalini, kupunguza matumizi yasiyoendana na umasikini wetu na
kupambana na ufisadi ina dalili kubwa za mafanikio.
Eneo ambalo Rais
Magufuli hawezi kufanikiwa peke yake pasipo ushirikiano wa Watanzania wote ni
nje ya serikalini na huko ‘mtaani.’ Mara kadhaa nimekuwa nikisisitiza umuhimu
wa wananchi kujenga kasumba ya kudai haki na stahili zao badala ya kuona
haki/stahili hizo ni kama fadhila au upendeleo flani. Wenzetu huku Ughaibuni
wamejenga desturi ya kutokubali huduma au bidhaa inayotolewa chini ya kiwango
wanachostahili. Haki na stahili za mpokea huduma ni miongoni mwa vitu
vinavyopewa umuhimu mkubwa huku tulipo.
Haitokuwa rahisi kwa
Rais Magufuli au wasaidizi wake kwenda kila sehemu kuwezesha au kuharakiasha
upatikanaji wa huduma. Jukumu hilo linapaswa kusaidiwa na wananchi wenyewe
ambao mara nyingi ndio wahanga wakubwa wa huduma mbovu. Kadhalika, watoa huduma
nje ya serikali wanapaswa kutambua kuwa hizi ni zama mpya, na asiyeweza
kuendana na kasi ya Rais Magufuli na ajiweke kando.
Lakini mchango mkubwa
zaidi wa wananchi wote unahitajika zaidi katika kupambana na ufisadi, rushwa na
uhalifu mwingine nje ya serikali. Wakati Rais ameahidi kukabiliana na ‘mapapa’
wa uhalifu kama kwenye biashara hatari ya madawa ya kulevya, pasipo wananchi
kumsaidia kwa kuwatenga wahusika na kuwaripoti - badala ya kuwasujudia na kuwapa majina ya
heshima kama ‘wazungu wa unga’ au ‘mapedejee’ – basi tutamkwamisha, na nchi
yetu itaendelea kuumizwa na vitendo hivyo viovu.
Kadhalika, ili
kauli-mbiu ya ‘Hapa Ni Kazi Tu’ iweze kuleta matokeo kusudiwa na kuwa ya
ufanisi ni muhimu kwa kila Mtanzania kuachana na dhana fyongo ya kusaka
mafanikio kwa njia za mkato, turejee zama za Ujamaa na Kujitegemea ambapo
waliokula bila kuvuja jasho tuliwaita ‘kupe.’ Sote tuchape kazi, tuache kufanya
‘ujanja ujanja,’ tuone fahari kuwa na shughuli halali badala ya kuamini kuwa
ufisadi, rushwa, uhalifu,nk ndio njia rahisi na sahihi za kufikia mafanikio kwa
haraka.
Baada ya kumpoteza Baba
wa Taifa Marehemu Mwalimu Julius Nyerere aliyetujengea misingi imara ya taifa
letu, japo sasa inamong’onyoka kwa kasi, na mzalendo wa daraja la kwanza, Marehemu
Sokoine, sala/dua zetu katika wimbo wetu wa taifa katika maneno “Mungu Ibariki
Tanzania…” zimesikika, na Mwenyezi Mungu ametuletea ‘Nyerere na Sokoine mpya’
kupitia kwa Rais wetu mpya Dkt Magufuli. Tusijiangushe wenyewe kwa kutotumia
ipasavyo fursa hii adimu.
Nimalizie makala hii
kwa wito ‘wa kitaalamu’ kwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa, ambao
pamoja na majukumu mengine, wana dhamana ya ulinzi wa Rais wetu na viongozi
wengine wakuu kitaifa. Kama alivyosema mwenyewe, vita aliyoanzisha dhidi ya
kila vitendo na kasumba zinazolikwaza taifa letu ni nzito na inawagusa watu
wazito. Kwa vile yayumkinika kusema kuwa vitendo vya rushwa,ufisadi na uhalifu
vimefikia hatua ya ‘kimafia,’ basi ni muhimu kuimarisha ulinzi wa Rais wetu (na
viongozi wengine wanaopatiwa ulinzi) kwa sababu ‘tupo vitani.’
Simaanishi kuwa ulinzi
uliopo una mapungufu lakini angalizo hili linazingatia ukweli kwamba ‘vita’
hiyo inagusa maslahi ya wengi, maslahi ya ‘kupe’ lukuki walioigeuza Tanzania
yetu kuwa ni ‘shamba la bibi,’ la kuvuna wasichopanda, sambamba na wahalifu
wanaoingiza, kuuza na kusafirisha madawa ya kulevya kana kwamba ni bidhaa
iliyoidhinishwa na Shirika la Viwango la Taifa (TSB), majangili wanaoshindana
kuua wanyamapori wetu na kusafirisha nyara za serikali, na wahalifu wengineo.
Rais Magufuli ameahidi
kutotuangusha, basi nasi tusimwangushe.
Hapa Ni Kazi Tu!
Raia mwema halipatikani mtandaon labda wameona mapato yanapungua kwenye hard cpy......mawazo ni yangu binafsi
ReplyDeleteRaia mwema halipatikani mtandaon labda wameona mapato yanapungua kwenye hard cpy......mawazo ni yangu binafsi
ReplyDelete